Je, Waweza Kutofautisha Lililo Jema Na Lililo Baya?
“Mimi binafsi nilihusika na kuua watu wapatao 25. . . . Mimi huona mambo hayo akilini mwangu kila usiku, kila siku. Mimi huwa na jinamizi. . . . Naweza kwenda mahali fulani na nione uso unaonikumbusha watu niliowaua. Naweza kuona mambo hayo waziwazi, kama kwamba yametendeka leo, sasa hivi. . . . Nasikitika kwa yale mambo niliyofanya.”—V.S.
“Niliamuriwa kwenda humo na kuangamiza adui. . . . Sikuketi na kuwafikiria kuwa wanaume, wanawake na watoto. . . . Wakati huo nilihisi na bado nahisi kwamba nilitenda kama nilivyoamriwa, nami nilitimiza amri nilizopewa na sihisi vibaya kwa kufanya hivyo.”—W.C.
KATIKA Machi 16, 1968, wanaume wawili walionukuliwa hapo juu walishiriki katika ule ambao baadaye ungeitwa uhalifu mwovu sana. Wao, pamoja na askari-jeshi wengine, waliingia kijiji kidogo cha Vietnam na kuchinja mamia ya raia—kutia ndani wanawake, watoto, na wanaume wazee-wazee. Lakini ona maitikio yenye kutofautiana ya askari-jeshi hao wawili. Askari-jeshi wa kwanza kwa wazi anateseka kwa sababu ya yale aliyofanya. Yule wa pili anahisi kwamba matendo yake yalikuwa halali. Watu wawili wanawezaje kuitikia kwa njia tofauti hivyo jambo lilelile?
Jibu lahusu dhamiri—uwezo wa kupewa na Mungu ambao hutusaidia kujichunguza kwa unyofu na kuamua kuhusu matendo yetu na nia zetu. Dhamiri ni hisi yetu ya ndani ya kutofautisha lililo jema na lililo baya.
Watu fulani wanapofanya uamuzi, hutumia ile mithali isemayo, “Dhamiri yako na iwe mwongozo wako.” Hata hivyo, kwa kusikitisha, dhamiri si ya kutegemewa sikuzote. Kwa kweli, wengi wameruhusu na hata kufanya maovu mabaya sana, na dhamiri zao hazikuwasumbua hata kidogo. (Yohana 16:2; Matendo 8:1) Kama vile mwandishi wa riwaya Mwingereza Samuel Butler alivyoona wakati mmoja, dhamiri “punde yaacha kuitikia wale wasiokubali kuisikiliza.”
Je, waweza kuamini dhamiri yako? Jibu lategemea sana jinsi inavyozoezwa vizuri, kama vile makala ifuatayo itakavyoonyesha.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Juu mandhari ya vita: U.S. Signal Corps photo