Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 9/1 kur. 24-28
  • Nilijifunza Kumtegemea Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nilijifunza Kumtegemea Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwanzo wa Majaribu Makali
  • Suala la Kuridhiana
  • Mnyanyaso Waongezeka
  • Kwenda Mashariki—Kisha Kutoroka
  • Uhuru Lakini Misiba Zaidi
  • Uhuru Hatimaye!
  • Imani Yajaribiwa Huko Slovakia
    Amkeni!—2002
  • Nilikuwa Mwanasiasa Lakini Sasa Mimi Ni Mkristo
    Amkeni!—2002
  • Licha ya Majaribu, Tumaini Langu Halijafifia
    Amkeni!—2002
  • Tulifanya Uamuzi Thabiti wa Kuunga Mkono Utawala wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 9/1 kur. 24-28

Nilijifunza Kumtegemea Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JÁN KORPA-ONDO

Ulikuwa mwaka wa 1942, nami nilikuwa nikilindwa na wanajeshi wa Hungaria karibu na Kursk, Urusi. Tulikuwa wafungwa wa serikali ya Ujerumani, Italia, na Japani, ambazo zilikuwa zikipigana na Urusi kwenye Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kaburi langu lilichimbwa, nami nikapewa dakika kumi za kuamua ikiwa ningetia sahihi hati iliyosema kwamba tangu wakati huo sikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kabla sijasimulia lililotukia baadaye, acheni niwaambie nilivyopata kuwa hapo.

NILIZALIWA mwaka wa 1904 katika kijiji kidogo cha Zahor, kilicho mashariki mwa Slovakia sasa. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, kijiji cha Zahor kilipata kuwa sehemu ya nchi ya Chekoslovakia, iliyotoka tu kuundwa. Kijiji chetu kilikuwa na nyumba zipatazo 200 na makanisa mawili, mojawapo ya hayo likiwa Katoliki ya Ugiriki na lile lingine likiwa kanisa la Calvin.

Ingawa nilikuwa mfuasi wa Kanisa la Calvin, niliishi maisha yaliyopita mipaka kiadili. Karibu nami paliishi mtu aliyekuwa tofauti sana. Siku moja alianzisha mazungumzo pamoja nami, naye akaniazima Biblia. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya kwanza kwangu kukishika kitabu hicho. Karibu wakati huohuo, mwaka wa 1926, nilimwoa Barbora na punde si punde tukawa na watoto wawili, Barbora na Ján.

Nilianza kuisoma Biblia, lakini kulikuwako mambo mengi ambayo sikuelewa. Kwa hiyo nilimwendea pasta wangu na kumwomba anisaidie. “Biblia ni ya watu wenye elimu peke yao,” akasema, “usijaribu hata kuielewa.” Kisha akanikaribisha tucheze mchezo wa kadi.

Baada ya hilo nilimwendea mtu aliyekuwa ameniazima Biblia hiyo. Alikuwa mmojawapo wa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa wakati huo. Alifurahi kunisaidia, baada ya muda fulani macho yangu yakaanza kufumbuka. Niliacha kunywa pombe kupita kiasi, na kuanza kuishi maisha maadilifu; hata nilianza kuongea na wengine juu ya Yehova. Kweli ya Biblia ilikuwa imesitawi huko Zahor mapema katika miaka ya 1920, na upesi kikundi chenye bidii cha Wanafunzi wa Biblia kilianzishwa.

Hata hivyo, kulikuwa na upinzani mkali wa kidini. Kasisi wa mahali hapo aliwageuza wengi katika familia yangu dhidi yangu, akidai kuwa nilikuwa nimerukwa na akili. Lakini maisha yangu yalianza kuwa na kusudi, nami nikaazimia kabisa kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova. Hivyo, mwaka wa 1930, nilijitoa wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Mwanzo wa Majaribu Makali

Mwaka wa 1938, eneo letu lilitawalwa na Hungaria, iliyounga mkono Ujerumani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kufikia wakati huo tulikuwa na Mashahidi wapatao 50 katika kijiji chetu chenye watu waliopungua elfu moja. Tuliendelea kuhubiri ingawa kufanya hivyo kulihatarisha maisha zetu na uhuru wetu.

Katika 1940, niliandikishwa katika jeshi la Hungaria. Ningefanyaje? Nilikuwa nimesoma unabii mbalimbali wa Biblia juu ya watu kubadili silaha zao za vita kuwa vyombo vya amani, na nilijua kwamba, hatimaye, Mungu angeondolea mbali vita vyote duniani. (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Hivyo, nilichukia vita, nami niliamua kutojiunga na jeshi, bila kujali matokeo.

Nilihukumiwa kifungo cha miezi 14 gerezani nami nikafungwa huko Pécs, Hungaria. Mashahidi wengine watano walikuwa katika gereza iyo hiyo, nasi tulithamini sana kuweza kushirikiana pamoja. Hata hivyo, kwa muda fulani, nilikuwa katika kifungo cha upweke nikiwa na minyororo katika miguu yangu. Tulipokataa kufanya kazi iliyohusiana na jitihada za kivita, tulipigwa. Pia, tulilazimishwa kusimama wima siku nzima, isipokuwa muda wa saa mbili wakati wa adhuhuri. Masaibu hayo yaliendelea kwa miezi kadhaa. Hata hivyo tulikuwa wenye furaha kwa sababu tulikuwa na dhamiri safi mbele za Mungu wetu.

Suala la Kuridhiana

Siku moja kikundi cha makasisi 15 Wakatoliki kilikuja ili kujaribu kutusadikisha kwamba ilikuwa muhimu tutegemeze jitihada za kivita kwa kujiunga na jeshi. Wakati wa mazungumzo hayo tulisema hivi: “Ikiwa mwaweza kuthibitisha kutoka katika Biblia kwamba nafsi haiwezi kufa na kwamba tutaenda mbinguni tukifa vitani, tutajiunga na jeshi.” Bila shaka, hawangeweza kuthibitisha hilo, nao hawakutaka kuendeleza mazungumzo hayo.

Mwaka wa 1941 kifungo changu gerezani kiliisha, nami nilikuwa nikitarajia kuungana tena na familia yangu. Badala yake, nilipelekwa nikiwa nimefungwa kwa minyororo hadi kwenye kituo cha jeshi katika Sárospatak, Hungaria. Tulipofika, nilipewa fursa ya kuachiliwa. “Unalopaswa kufanya tu,” nikaambiwa, “ni kutia sahihi ahadi hii ya kwamba utalipa pengö 200 urudipo nyumbani.”

“Hilo lawezekanaje?” nikauliza. “Mwataka fedha hizo kwa kusudi gani?”

“Ukilipa fedha hizo,” nikaambiwa, “utapokea cheti cha kusema kwamba hukupita mtihani wa kitiba wa kuingia jeshini.”

Huo ulikuwa uamuzi mgumu kwangu. Kwa zaidi ya mwaka mmoja, nilikuwa nimetendwa kinyama; nilikuwa naanza kuchoka. Sasa, kwa kulipa kiasi fulani cha fedha, ningeweza kuwa huru. “Nitafikiria hilo,” nikanong’ona.

Ningeamua nini? Nilikuwa na mke na watoto ambao nilipaswa kuwafikiria. Basi, karibu wakati uo huo, nilipokea barua kutoka kwa Mkristo mwenzangu, aliyenitia moyo katika barua hiyo. Alinukuu Waebrania 10:38, ambapo mtume Paulo anukuu maneno ya Yehova hivi: “‘Mwadilifu wangu ataishi kwa sababu ya imani,’ na, ‘ikiwa yeye ajikunyata, nafsi yangu haina upendezi katika yeye.’” Punde baadaye, maofisa wawili Wahungaria kwenye kambi wakazungumza nami, mmoja wao akisema: “Huna habari juu ya jinsi tunavyokustahi kwa sababu ya kutegemeza kanuni za Biblia kwa uthabiti hivyo! Usikate tamaa!”

Siku iliyofuata niliwaendea walionitolea uhuru wangu kwa malipo ya pengö 200 na kusema: “Kwa kuwa Yehova Mungu ameniruhusu nifungwe, atashughulikia kuachiliwa kwangu. Sitalipa fedha ili niachiliwe.” Kwa hiyo nikahukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani. Lakini huo haukuwa mwisho wa kujaribu kunifanya niridhiane. Mahakama ilikuwa tayari kunisamehe ikiwa ningekubali kutumikia katika jeshi kwa miezi miwili tu, nami hata singebeba silaha yoyote! Toleo hilo nalo nililikataa, nacho kifungo changu gerezani kikaanza.

Mnyanyaso Waongezeka

Nilipelekwa tena gerezani Pécs. Wakati huu mateso yalikuwa makali hata zaidi. Mikono yangu ilikuwa imefungwa ikiwa nyuma mgongoni, nami nilining’inizwa kwayo kwa muda wa saa mbili. Kwa sababu hiyo, mabega yangu yote mawili yaliteguka. Mateso hayo yalirudiwa-rudiwa kwa kipindi cha miezi sita hivi. Naweza kumshukuru Yehova kwamba sikukata tamaa.

Mwaka wa 1942 kikundi chetu—wafungwa wa kisiasa, Wayahudi, na Mashahidi wa Yehova 26 —kilipelekwa katika jiji la Kursk katika eneo lililokuwa limetwaliwa na vikosi vya Ujerumani. Tulichukuliwa na Wajerumani, nao wakawapa wafungwa kazi ya kubeba chakula, silaha, na mavazi na kupelekea wanajeshi kwenye mapigano. Sisi Mashahidi tulikataa kufanya kazi hiyo kwa sababu ilihalifu kutokuwamo kwetu kwa Kikristo. Kwa hiyo, tukarudishwa kwa Wahungaria.

Hatimaye, tuliwekwa katika gereza la Kursk. Kwa siku kadhaa tulichapwa kwa viboko vya mpira mara tatu kwa siku. Nilipigwa kwenye panda, nikaanguka chini. Nilipokuwa nikipigwa, nilifikiri, ‘Si vigumu sana kufa.’ Mwili wangu wote ukafa ganzi, kwa hiyo sikuweza kuhisi chochote. Kwa siku tatu hatukupewa chakula chochote. Kisha tukapelekwa mahakamani, na sita kati yetu wakahukumiwa kifo. Hukumu hiyo ilipotekelezwa, tulisalia watu 20.

Majaribu ya imani tuliyopata siku hizo huko Kursk, katika Oktoba ya mwaka wa 1942, yalikuwa ndiyo majaribu makali zaidi ambayo nimepata kukabili. Hisia zetu za moyoni zilionyeshwa vema na Mfalme Yehoshafati wa kale wakati ambapo watu wake walikabiliwa na mambo yenye kupita kiasi: “Sisi hatuna uwezo juu ya jamii kubwa hii, wanaotujia juu yetu; wala hatujui tufanyeje; lakini macho yetu yatazama kwako.”—2 Mambo ya Nyakati 20:12.

Sisi tukiwa 20 tulipelekwa nje tukachimbe kaburi la ujumla, tukilindwa na askari 18 wa Hungaria. Tulipomaliza kuchimba, tuliambiwa kwamba tulikuwa na dakika kumi za kutia sahihi hati, iliyosema hivi kwa sehemu: “Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni yenye kosa. Sitayaamini wala kuyategemeza tena kamwe. Nitaipigania nchi yangu, Hungaria . . . nathibitisha kwa kutia sahihi kwamba najiunga na Kanisa Katoliki la Kiroma.”

Baada ya dakika kumi hivi amri ikatolewa: “Geukeni kuelekea upande wa kulia! Pigeni hatua kuelekea kaburi!” Kisha, amri ikatolewa: “Mfungwa wa kwanza na wa tatu ingieni shimoni!” Hao wawili walipewa dakika nyingine kumi za kuamua kutia sahihi hati hiyo. Mmojawapo wa askari alisihi hivi: “Acheni imani yenu, mtoke kaburini!” Hakuna aliyesema lolote. Kisha ofisa msimamizi akawapiga risasi.

“Vipi waliosalia?” askari mmoja akamwuliza ofisa msimamizi.

“Wafunge,” akajibu. “Tutawatesa zaidi na kuwapiga risasi saa 12 alfajiri.”

Ghafula nikaogopa, si kwamba ningekufa, lakini kwamba singeweza kuvumilia mateso na kwamba ningeridhiana. Kwa hiyo nikajitokeza na kusema: “Bwana, tumekosea sawa na ndugu zetu ambao umetoka kuwapiga risasi. Mbona usitupige risasi pia?”

Lakini hawakutupiga risasi. Tulifungwa mikono yetu ikiwa nyuma mgongoni. Kisha tukaning’inizwa kwa mikono yetu. Tulipopoteza fahamu, walitumwagia maji. Maumivu yalikuwa makali sana kwa sababu uzito wa mwili ulitegua mabega yetu. Mateso hayo yaliendelea kwa muda wa saa tatu. Kisha, bila kutarajia, amri ya kutowapiga risasi Mashahidi wa Yehova wowote zaidi ikatolewa.

Kwenda Mashariki—Kisha Kutoroka

Majuma matatu baadaye tulipiga mwendo tukiwa kikundi kwa siku chache hadi tukafika kingo za Mto Don. Tuliambiwa na wasimamizi kwamba hatungerudishwa tukiwa hai. Siku hiyo, tulipewa kazi isiyo na kusudi, kuchimba mitaro na kuifunika tena. Jioni, tulikuwa na kiasi fulani cha uhuru wa kutembea-tembea.

Kwa maoni yangu, tungeweza kufanya mambo mawili. Tungeweza kufa papo hapo, au tungeweza kuwatoroka Wajerumani na kujiuzulu kwa Warusi. Ni watatu tu kati yetu tulioamua kujaribu kutoroka kwa kuvuka Mto Don uliokuwa umeganda. Desemba 12, 1942, tulisali kwa Yehova na kuondoka. Tulifika yalipokuwa majeshi ya Urusi na mara moja tukawekwa katika gereza la kambi pamoja na wafungwa 35,000. Kufikia masika, ni wafungwa 2,300 waliokuwa wangali hai. Wale wengine walikuwa wamekufa njaa.

Uhuru Lakini Misiba Zaidi

Niliokoka vita vilivyosalia, kutia ndani miezi kadhaa ya baada ya vita kwisha, nikiwa mfungwa wa Urusi. Hatimaye, mwezi wa Novemba 1945, nilifika nyumbani, Zahor. Shamba letu lilikuwa katika hali mbaya, kwa hiyo ilinibidi kuanza tena kulishughulikia toka mwanzo. Mke wangu na watoto wangu walikuwa wamefanya kazi katika shamba hilo wakati wa vita, lakini mwezi wa Oktoba 1944, Warusi walipokaribia, walihamishwa na kupelekwa mashariki. Mali yetu yote iliporwa.

Zaidi ya yote, niliporudi nyumbani, mke wangu alikuwa mgonjwa sana. Mwezi wa Februari 1946, akafa. Alikuwa na umri wa miaka 38 tu. Tulikuwa na kipindi kifupi sana cha kufurahia kuungana kwetu tena baada ya miaka mitano ya kutenganishwa, ambayo ilikuwa migumu sana.

Nilifarijiwa na ndugu zangu wa kiroho, kuhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Mwaka wa 1947, niliweza kuazima kiasi fulani cha fedha na kusafiri hadi Brno, safari ya karibu kilometa 400, ili kuhudhuria mkusanyiko. Humo, miongoni mwa ndugu zangu Wakristo, kutia na Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, nililiwazwa na kutiwa moyo sana.

Hatukufurahia kwa muda mrefu uhuru wetu wa baada ya vita. Mwaka wa 1948, Wakomunisti walianza kutudhulumu. Wengi wa ndugu waliokuwa wakiongoza katika kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Chekoslovakia walikamatwa katika mwaka wa 1952, nami nilipewa daraka la kutunza makutaniko. Mwaka wa 1954, mimi pia nilikamatwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka minne gerezani. Mwanangu Ján, na mwana wake Juraj walifungwa pia kwa sababu ya kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo. Nilikaa miaka miwili katika jela ya serikali iitwayo Pankrác iliyoko Prague. Msamaha ulitangazwa mwaka wa 1956, nami nikaachiliwa.

Uhuru Hatimaye!

Hatimaye, mwaka wa 1989, Ukomunisti ulishindwa kuendelea kushikilia Chekoslovakia, nayo kazi ya Mashahidi wa Yehova ikasajiliwa kisheria. Hivyo, tulikuwa huru kukutana pamoja na kuhubiri hadharani. Kufikia wakati huo kulikuwako Mashahidi wapatao mia moja katika Zahor, yaani mtu 1 kati ya kila watu 10 kijijini alikuwa Shahidi. Miaka michache iliyopita, tulijenga Jumba la Ufalme zuri na kubwa katika Zahor, linalotosha watu 200.

Afya yangu si nzuri sana kama ilivyokuwa, kwa hiyo akina ndugu hunipeleka kwenye Jumba la Ufalme kwa gari. Mimi hufurahia kuwa huko na kutoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Nina furaha hasa kuona wawakilishi wa vizazi vitatu vya familia yangu vikimtumikia Yehova, kutia ndani wajukuu kadhaa. Mmoja wao alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova katika Chekoslovakia hadi madaraka yake ya familia yalipomzuia asifanye kazi ya kuzunguka.

Namshukuru Yehova kwa kuniimarisha katika zile nyakati nyingi za majaribu yangu. Kukaza fikira zangu kwake—“kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana”—ndilo jambo ambalo limenitegemeza. (Waebrania 11:27) Ndiyo, nimeuhisi mkono wake wenye nguvu wa ukombozi. Ndiyo sababu, hata sasa, mimi hujaribu kuwapo kwenye mikutano ya kutaniko na kushiriki katika kutangaza jina lake katika huduma ya hadharani kwa kadiri niwezavyo.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Jumba la Ufalme la Zahor

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nathamini pendeleo la kutoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki