“Shikilieni Sana Mlicho Nacho”
Kikundi cha Mashahidi kilikuwa kikihubiri katika kimoja cha visiwa vipatavyo 30, ambavyo hufanyiza Visiwa vya Cyclades vya Ugiriki. Wawili kati yao walipokuwa wakihubiri nyumba zilizokuwa kando ya barabara, walikutana na polisi aliyewaambia wamfuate hadi kwenye kituo cha polisi. Punde walipofika kwenye kituo cha polisi, simu ikalia. Kasisi wa kijiji ndiye aliyekuwa akipiga. “Nilisikia kwamba kuna Mashahidi wa Yehova kijijini,” akasema. “Ndiyo, nina wawili hapa,” polisi akajibu. “Naja sasa hivi.” Kutokana na namna ya sauti ya mazungumzo, kina ndugu wakawa wenye wasiwasi kidogo.
Hata hivyo, alipowasili, kasisi huyo alitabasamu, akawasalimu, na kuketi kando ya yule polisi. Mazungumzo yalipoendelea, yule polisi alianza kuwa mgomvi, hali kasisi aliendelea kuwa mkubalifu na mwenye heshima. Alimwambia polisi asiwadharau Mashahidi, kisha akaongeza hivi: “Wanaweza kujibu swali lolote kwa sababu wao huzoezwa kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Ingekuwa rahisi kutikisa dunia kutoka kwenye misingi yake kuliko kubadili imani ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova yeyote.”
Walipokuwa wakihubiri asubuhi iliyofuata, kina ndugu walikutana na yule kasisi tena na kumwuliza hivi: “Mbona wewe ulikuwa mwenye urafiki kwetu wakati wa mazungumzo kwenye kituo cha polisi?” Kasisi akawaambia kwamba alikuwa amewajua Mashahidi wengi katika Syros na kwamba amekuwa akisoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa miaka mingi. Kwa hakika, pindi kwa pindi amechukua gazeti la Mnara wa Mlinzi, akalificha kwenye bahasha kubwa, na kulitumia katika mahubiri yake kanisani. Alitaja hili: “Sidhani kama maisha yangekuwa na kusudi kama singekuwa na fasihi yenu. Hiyo ndiyo hunitegemeza.”
Baadaye, kasisi huyo aliwaambia Mashahidi hao hivi: “Lazima niwaambie jambo moja. Shikilieni sana mlicho nacho. Msikosee na kukiachilia. Ninayowaambia sasa ndiyo mahubiri bora zaidi ambayo nimepata kutoa, nami sisemi hilo kwa mdomo wangu tu; namaanisha hilo kwa moyo wangu wote.”