Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 11/1 kur. 19-23
  • Kumpendeza Yehova Ndilo Hangaikio Langu Kuu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumpendeza Yehova Ndilo Hangaikio Langu Kuu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maisha ya Utumishi wa Kujitoa
  • Majaribu ya Imani Shuleni
  • Kutokuwamo Kwangu kwa Kikristo Kwajaribiwa
  • Utendaji Uliofanywa Upya Baada ya Kuachiliwa
  • Maisha Yenye Neema na Yenye Kuthawabisha
  • Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Yatima Aliyeachwa Ampata Baba Mwenye Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Nimeazimia Kuwa Askari-Jeshi wa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 11/1 kur. 19-23

Kumpendeza Yehova Ndilo Hangaikio Langu Kuu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA THEODOROS NEROS

Mlango wangu wa seli ulifunguka, ofisa akapaaza sauti: “Neros ni nani?” Nilipojitambulisha, aliamuru hivi: “Simama. Tunaenda kukuua.” Jambo hilo lilitokea katika kambi ya kijeshi huko Korintho, Ugiriki, 1952. Kwa nini maisha yangu yalikuwa mashakani? Kabla sijaeleza hayo, acheni niwaambie kuhusu malezi yangu.

BABA yangu alitembelewa na Wanafunzi wa Biblia (kama walivyojulikana Mashahidi wa Yehova wakati huo) katika 1925. Punde si punde akawa mmoja wao na kuwajulisha ndugu na dada zake wanane itikadi zake, wote ambao walikubali kweli ya Biblia. Vivyo hivyo na wazazi wake. Baadaye, alioa, nami nikazaliwa katika 1929 huko Agrinio, Ugiriki.

Hiyo ilikuwa miaka mibaya kama nini kwa Ugiriki! Kwanza kulikuwa na udikteta mkatili wa Jenerali Metaxas. Kisha, katika 1939, Vita ya Ulimwengu ya Pili ikalipuka, upesi baadaye Wanazi wakaitwaa nchi. Maradhi na njaa vikaenea pote. Miili iliyofura ya wafu iliondolewa kwa vigari vidogo vya kusukumia mizigo. Uovu ulimwenguni ulikuwa dhahiri sana, kama ulivyokuwa uhitaji wa Ufalme wa Mungu.

Maisha ya Utumishi wa Kujitoa

Katika Agosti 20, 1942, tulipokuwa tukifanya mkutano tukiwa kikundi nje ya Thesalonike, mwangalizi-msimamizi wetu alielekeza kwenye ndege za vita za Uingereza zilizokuwa zikiangusha mabomu jijini na kukazia jinsi tulivyolindwa kwa kutii himizo la ‘kutoachilia mbali kukusanyika pamoja.’ (Waebrania 10:25) Katika pindi hiyo, tulikutana ufuoni mwa bahari, nami nilikuwa miongoni mwa wale waliojitoa wenyewe kwa ubatizo. Tulipotoka majini, tulisimama katika foleni, na ndugu na dada zetu Wakristo waliimba wimbo uliotupongeza kwa sababu ya uamuzi tuliokuwa tumefanya. Hiyo ilikuwa siku isiyosahaulika wee!

Muda mfupi baadaye, mvulana mwingine nami tulipokuwa tukitembelea watu wakati wa huduma yetu ya nyumba hadi nyumba, polisi walitukamata na kutupeleka katika kituo cha polisi. Ili kukazia kwamba tulionwa kuwa Wakomunisti na kwamba kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imekatazwa, tulichapwa na kuambiwa hivi: “Yehova ni sawa na Stalin, nyie wajinga!”

Wakati huo vita ya wenyewe kwa wenyewe ilikuwa imechacha Ugiriki, na utendaji wa kupinga Ukomunisti ulikuwa umeongezeka sana. Siku iliyofuata tulipigishwa miguu kupita nyumbani kwetu tukiwa tumetiwa pingu, kana kwamba tulikuwa wahalifu. Lakini hayo hayakuwa ndiyo majaribu pekee niliyopata.

Majaribu ya Imani Shuleni

Mapema katika 1944, bado nilikuwa mvulana wa shule, nao Wanazi bado waliendelea kukalia Thesalonike. Siku moja shuleni, kasisi Mgiriki Mwothodoksi aliyekuwa profesa wetu wa kidini, aliniambia kwamba nilipaswa kujaribiwa kuhusu somo la siku hiyo. “Yeye si Mkristo Mwothodoksi,” wale watoto wengine wakasema.

“Yeye ni nani?” yule profesa akauliza.

“Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” nikajibu.

“Mbwa-mwitu kati ya kondoo,” akapaaza sauti, huku akinishika ghafula na kunipiga kofi usoni.

Nikafikiri, ‘Yawezekanaje mbwa-mwitu apigwe na kondoo?’

Siku chache baadaye, tukiwa karibu 350 tulikuwa tumekaa tukiwa tayari kwa chakula cha mchana. Msimamizi akasema: “Neros atasali.” Nilirudia ile iitwayo ‘Baba Yetu,’ sala ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake, kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 6:9-13. Msimamizi hakupenda hivyo, kwa hiyo akaniuliza kwa hasira kutoka mahali alipokuwa ameketi: “Kwa nini umesali hivyo?”

“Kwa sababu mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” nikasema. Kwa sababu hiyo yeye pia akanishika ghafula na kunipiga shavuni. Baadaye siku hiyo mwalimu mwingine akaniita ofisini mwake na kuniambia: “Vema, Neros, shikilia yale unayoamini, na usikate tamaa.” Usiku huo baba yangu alinitia moyo kwa maneno haya ya mtume Paulo: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.”—2 Timotheo 3:12.

Nilipomaliza shule ya sekondari, ilinipasa kuchagua kazi-maisha ambayo ningefuatia. Kwa sababu ya zogo katika Ugiriki, pia ilinibidi kukabiliana na lile swali la kutokuwamo kwa Kikristo. (Isaya 2:4; Mathayo 26:52) Hatimaye, mapema katika 1952, nilihukumiwa kifungo cha miaka 20 kwa kukataa kutwaa silaha wakati wa kipindi hicho kilichokuwa kigumu katika historia ya Ugiriki.

Kutokuwamo Kwangu kwa Kikristo Kwajaribiwa

Nilipokuwa nimezuiliwa katika kambi za kijeshi huko Mesolóngion na Korintho, nilikuwa na fursa ya kueleza makomanda wa jeshi kwamba dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia haingeniruhusu kuwa askari-jeshi katika kutegemeza mambo ya kisiasa. “Mimi tayari ni askari-jeshi wa Yesu,” nikaelezea, nikionyesha 2 Timotheo 2:3. Niliposihiwa nifikirie hilo, nilisema kwamba uamuzi wangu haukuwa umefanywa kwa ghafula tu bali ulikuwa umefanywa baada ya kufikiria kwa uzito, na kwa kuzingatia wakfu wangu kwa Mungu kufanya mapenzi yake.

Tokeo likawa kwamba, nililazimika kufanya kazi ya kulazimishwa, kukosa chakula kila baada ya siku moja kwa siku 20, na kulala kwenye sakafu ya sementi ya seli yenye ukubwa wa futi tatu kwa sita. Nilikuwa katika seli hiyo pamoja na Mashahidi wengine wawili! Wakati huo, nilipokuwa ningali katika kambi ya Korintho, ndipo nilipoitwa kutoka seli ili nikauawe.

Tulipokuwa tukienda mahali pa kuuawa ofisa aliuliza, “Je, husemi chochote?”

“La,” nikajibu.

“Hutaandikia familia yako?”

“La,” nikajibu tena. “Tayari wanajua kwamba huenda nikauawa hapa.”

Tulifika kwenye ua, nami nikaamuriwa kusimama nikiangalia ukuta. Kisha, badala ya kuamuru askari-jeshi wafyatue risasi, huyo ofisa aliagiza, “Mpelekeni ndani.” Ulikuwa uuaji wa kusingizia tu, uliokusudiwa kujaribu azimio langu.

Baadaye, nilipelekwa kwenye kisiwa kidogo cha Makrónisos, ambako sikuruhusiwa kuwa na fasihi yoyote isipokuwa Biblia. Mashahidi 13 waliwekwa katika nyumba ndogo wakitengwa na wafungwa wahalifu wapatao 500 hivi. Hata hivyo, kwa njia fulani, tulipitishiwa fasihi kisirisiri. Kwa mfano, siku moja, nililetewa sanduku la loukoúmia (peremende zipendwazo). Wakaguzi walitamani sana kuonja loukoúmia hivi kwamba walikosa kuona gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokuwa limefichwa chini yake. “Askari-jeshi walikula loukoúmia, lakini sisi ‘tulikula’ Mnara wa Mlinzi!” akasema Shahidi mmoja.

Nakala ya kitabu kilichokuwa kimetoka tu kutolewa What Has Religion Done for Mankind? kilitufikia, na Shahidi mfungwa aliyejua Kiingereza alikitafsiri. Pia tulijifunza Mnara wa Mlinzi pamoja, tukifanya mikutano yetu kwa siri. Tuliona gereza kuwa kama shule, kama fursa ya kuimarisha hali yetu ya kiroho. Zaidi ya yote, tulikuwa na furaha kwa sababu tulijua kwamba mwendo wetu wa uaminifu-maadili ulikuwa ukimpendeza Yehova.

Gereza la mwisho ambalo nilifungiwa lilikuwa Týrintha, mashariki mwa Pelopónnisos. Humo nilimgundua mlinzi aliyekuwa akiangalia kwa makini nilipokuwa nikijifunza Biblia na mfungwa mwenzangu. Nilishangaa kama nini kukutana na mlinzi huyo miaka kadhaa baadaye katika Thesalonike! Wakati huo alikuwa Shahidi. Baadaye, mmoja wa watoto wake alipelekwa gerezani, si kutumikia akiwa mlinzi bali akiwa mfungwa. Alitiwa gerezani kwa sababu ileile iliyofanya nitiwe gerezani.

Utendaji Uliofanywa Upya Baada ya Kuachiliwa

Nilitumikia miaka mitatu tu ya ile ambayo mwanzoni ilikuwa hukumu ya miaka 20. Baada ya kuachiliwa niliamua kuishi Athene. Hata hivyo, punde nikapatwa na ugonjwa wa aina ya kichomi nami nikalazimika kurudi Thesalonike. Nilikaa kitandani kwa miezi miwili. Baadaye nilikutana na msichana mrembo aitwaye Koula, nasi tukaoana Desemba 1959. Katika 1962 alianza kutumikia akiwa painia, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Miaka mitatu baadaye niliweza kujiunga naye katika kazi ya painia.

Katika Januari 1965, tulipewa mgawo wa kazi ya mzunguko, tukizuru makutaniko kuyaimarisha kiroho. Katika kiangazi cha mwaka huo pia tulikuwa na pendeleo la kuhudhuria mkusanyiko mkubwa wa wilaya kwa mara yetu ya kwanza, katika Vienna, Austria. Haukuwa kama ile tuliyofanya huko Ugiriki ambapo tulilazimika kukutana kisirisiri vichakani kwa sababu kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku. Mwishoni mwa 1965, tulialikwa kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Athene. Hata hivyo, kwa sababu ya matatizo ya afya ya baadhi ya jamaa zangu, ilitubidi turudi Thesalonike 1967.

Tulishughulikia madaraka ya familia, huku tukiendelea kuwa wenye shughuli nyingi katika kazi ya kueneza evanjeli. Wakati mmoja, nilipokuwa nikiongea na mpwa wangu Kostas, nilimfafanulia uzuri wa tengenezo la Mungu na upendo, muungano, na utii kwa Mungu ambao hupatikana humo. Yeye alisema, “Mambo hayo yangependeza sana kama tu Mungu angekuwako.” Alikubali mwaliko wangu wa kumwomba achunguze kama Mungu yuko au la. Nilimtajia kwamba tulikuwa tuhudhurie mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika Nuremberg, Ujerumani, Agosti 1969. Aliuliza kama angeweza kuandamana nasi, naye rafiki yake Alekos, ambaye alikuwa pia anajifunza Biblia nasi, alitaka kuja pia.

Mkusanyiko wa Nuremberg ulikuwa tamasha isiyo na kifani! Mkusanyiko ulifanyiwa katika stediamu kubwa ambapo Hitler alisherehekea ushindi wake wa kijeshi. Hudhurio letu lilifikia kilele cha watu 150,000, na roho ya Yehova ilionyeshwa katika mambo yote. Punde baada ya hapo Kostas na Alekos walibatizwa. Sasa wote wanatumikia wakiwa wazee Wakristo na familia zao pia ni Mashahidi.

Nilianza kujifunza na bibi mmoja mwenye kupendezwa. Mume wake alisema kwamba alitaka kuchunguza itikadi zetu, na muda mfupi baadaye akanijulisha kwamba alikuwa amealika Bwa. Sakkos, mwanatheolojia wa Othodoksi ya Ugiriki, kwa ajili ya majadiliano. Mume huyo alitaka kutuuliza maswali fulani. Bwa. Sakkos alikuja, akiwa na kasisi. Yule mwanamume tuliyekuwa tukimtembelea alianza kwa kusema, “Kwanza, ningependa Bwa. Sakkos ajibu maswali matatu.”

Akishikilia tafsiri ya Biblia ambayo tulikuwa tukiitumia katika mazungumzo yetu, mwanamume huyo aliuliza, “Swali la kwanza: Je, hii ni Biblia ya kweli, au ni Biblia ya Mashahidi?” Bwa. Sakkos alijibu kwamba ilikuwa tafsiri yenye kuaminika, na pia akawafafanua Mashahidi wa Yehova kuwa “wapenda-Biblia.”

Akiendelea, mwanamume huyo aliuliza, “Swali la pili: Mashahidi wa Yehova ni watu wenye adili?” Kwa kweli, alitaka kujua mke wake alikuwa akishirikiana na watu wa aina gani. Mwanatheolojia huyo alijibu kwamba kwa hakika ni watu wenye adili.

“Swali la tatu,” mwanamume huyo akaendelea, “Je, Mashahidi wa Yehova wanalipwa?” “La,” akajibu yule mwanatheolojia.

“Nimepata majibu ya maswali yangu, nami nimefanya uamuzi wangu,” huyo mwanamume akamalizia. Baadaye aliendelea na funzo lake la Biblia na upesi akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Maisha Yenye Neema na Yenye Kuthawabisha

Nilianza tena kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye katika Januari 1976. Miaka ipatayo sita baadaye, nilipata pendeleo la kushiriki katika kuongoza aina mpya ya kuhubiri katika Ugiriki—ushahidi wa barabarani. Kisha, katika Oktoba 1991, mke wangu nami tulianza kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Miezi michache baadaye, ilinibidi kufanyiwa upasuaji wa moyo, ambao ulifanikiwa. Sasa afya yangu ni nzuri kabisa, nami nimeweza kurudia kazi ya kuhubiri ya wakati wote. Pia natumikia nikiwa mzee katika moja ya makutaniko ya Thesalonike, na vilevile katika Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali kusaidia wale walio na mahitaji ya kitiba.

Nitazamapo nyuma maishani mwangu, natambua jinsi kufanya yampendezayo Baba yetu wa kimbingu kumekuwa jambo lenye kuridhisha. Nafurahi kwamba zamani sana nilipokea mwaliko wake wenye kuvutia: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” (Mithali 27:11) Kwa kweli moyo wangu huwa na shangwe kuona ongezeko la ulimwenguni pote la idadi ya watu wanaokuja katika tengenezo la Yehova. Kushiriki katika kuweka watu huru kupitia kweli ya Biblia na hivyo kuwafungulia tazamio la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu kwa kweli ni pendeleo wee!—Yohana 8:32; 2 Petro 3:13.

Sikuzote sisi hujaribu kutia moyo watumishi wachanga wa Yehova wawe na mradi wa huduma ya wakati wote, watoe wakati wao na nguvu zao kwake. Kwa kweli, kumtumaini Yehova na kupata furaha katika kufanya moyo wake uwe na shangwe ndiyo maisha yenye kuridhisha zaidi ambayo mtu anaweza kuwa nayo!—Mithali 3:5; Mhubiri 12:1.

[Picha katika ukurasa wa 21]

(Kutoka kushoto hadi kulia)

Kutumikia jikoni Betheli katika 1965

Nikitoa hotuba katika 1970 wakati tulipokuwa tumepigwa marufuku kuhubiri

Nikiwa na mke wangu Koula katika 1959

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu, Koulayy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki