Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 5/1 kur. 25-29
  • Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ugonjwa Wawa Baraka
  • Naponea Chupuchupu
  • Maendeleo ya Kiroho
  • Kukamatwa Kwingi na Vifungo
  • Mtihani wa Aina Tofauti
  • Kutahadhari
  • Kupata Mwenzi Mwaminifu
  • Utumishi wa Betheli
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • “Badala ya Dhahabu, Nilipata Almasi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kumpa Yehova Kile Anachostahili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kumtumikia Mungu Mwenye Kutumainika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 5/1 kur. 25-29

Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA LAMBROS ZOUMBOS

Nilikabili uamuzi mgumu: kukubali toleo la baba mdogo wangu tajiri niwe meneja wa nyumba zake nyingi—kwa kufanya hivyo ningesuluhisha matatizo ya kifedha ya familia yangu—au niwe mhudumu wa wakati wote wa Yehova Mungu. Acheni nieleze mambo yaliyochochea uamuzi niliofanya hatimaye.

NILIZALIWA katika mji wa Volos, Ugiriki, katika 1919. Baba yangu alikuwa muuza nguo za wanaume, nasi tulifurahia ufanisi wa kimwili. Lakini likiwa tokeo la mshuko wa kiuchumi mwishoni mwa miaka ya 1920, baba alifilisika na kupoteza duka lake. Nilihuzunika kila wakati nilipoona baba akiwa na uso wa kukata tamaa.

Kwa muda fulani familia yangu iliishi katika ufukara. Kila siku nilitoka shuleni saa moja mapema ili nipange mstari wa kupata chakula. Bado, licha ya umasikini wetu tulifurahia maisha ya familia matulivu. Nilitamani kuwa daktari, lakini katikati ya utineja wangu nililazimika kuacha shule na kuanza kufanya kazi ili kuisaidia familia yangu isalimike.

Kisha, wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, Wajerumani na Waitalia wakateka Ugiriki, na kukawa na njaa kuu. Mara nyingi niliona marafiki na watu niliowajua wakifa kwa njaa mitaani—maono ya kuogofya sana ambayo sitasahau kamwe! Wakati mmoja familia yetu ilikaa siku 40 bila kuwa na mkate uliokuwa chakula kikuu katika Ugiriki. Ili kusalimika, ndugu yangu mkubwa zaidi nami tulienda kijiji cha karibu na kupata viazi kutoka kwa marafiki na watu wa ukoo.

Ugonjwa Wawa Baraka

Mapema katika 1944, nikawa mgonjwa sana nikiwa na aina ya mchochota wa mapafu. Wakati wa miezi mitatu niliyokuwa hospitalini, binamu yangu mmoja aliniletea vijitabu viwili na kusema: “Soma hivi; nina hakika utavipenda.” Hivyo vijitabu, Who Is God? na Protection, vilitangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Baada ya kuvisoma, nilishiriki yaliyomo na wagonjwa wenzangu.

Nilipoondoka hospitali, nilianza kushirikiana na Kutaniko la Volos la Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, kwa mwezi mmoja niliendelea kukaa nyumbani nikiwa mgonjwa wa nyumbani, na kwa muda wa saa sita hadi nane kila siku, nilisoma matoleo ya zamani ya Mnara wa Mlinzi, pamoja na vichapo vinginevyo vya Watch Tower Society. Likiwa tokeo, nilifanya maendeleo ya kiroho upesi sana.

Naponea Chupuchupu

Siku moja katikati ya mwaka wa 1944, nilikuwa nimeketi kwenye benchi ya bustani huko Volos. Kwa ghafula kikundi cha askari kilichokuwa kikiunga mkono majeshi ya Kijerumani yaliyomiliki kilizingira sehemu hiyo na kukamata kila mmoja aliyekuwapo. Tuliokamatwa tukiwa karibu 24 tuliongozwa barabarani hadi kwenye makao makuu ya Gestapo, yaliyokuwa katika bohari la tumbaku.

Dakika chache baadaye, nilisikia mtu akiita jina langu na jina la yule mtu niliyekuwa nikiongea naye katika bustani. Ofisa wa kijeshi Mgiriki alituita na kutuambia kwamba mmoja wa watu wangu wa ukoo alipoona tukiandamana na askari, alimwambia kuwa sisi tulikuwa Mashahidi wa Yehova. Kisha huyo ofisa Mgiriki akasema kwamba tulikuwa huru kwenda nyumbani, naye akatupa kadi yake rasmi ili tuitumie ikiwa tungekamatwa tena.

Siku iliyofuata tuligundua kuwa Wajerumani walikuwa wamewaua wengi wa wale waliokuwa wamekamatwa ili kulipiza kisasi cha mauaji ya wanajeshi wawili Wajerumani yaliyofanywa na kikundi cha wapiganiaji ukombozi Wagiriki wa upinzani. Zaidi ya kule kuokolewa kutokana na kifo, pindi hiyo nilijifunza umuhimu wa kutokuwamo kwa Kikristo.

Katika vuli ya 1944, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Wakati wa kiangazi kilichofuata, Mashahidi walifanya mipango kwa ajili yangu ili nishirikiane na Kutaniko la Sklithro kwenye milima, ambapo ningeweza kupona kabisa. Vita ya wenyewe kwa wenyewe iliyofuata umiliki wa Wajerumani ilikuwa ikipamba moto katika Ugiriki wakati huo. Ikatukia kwamba kijiji nilichokuwa nikiishi kilitumika kikiwa kitovu cha majeshi ya wapiganaji wa kuvizia. Kasisi wa huko na mtu mwingine mkatili walinishtaki kuwa mpelelezi wa majeshi ya serikali nao wakanihoji katika mahakama yao wenyewe ya kijeshi ya wapiganaji wa kuvizia.

Aliyekuwapo katika hiyo kesi ya mahakama bandia alikuwa kiongozi wa wapiganaji hao wa kuvizia wa hilo eneo. Nilipomaliza kueleza sababu za kukaa kwangu kijijini na kuonyesha kwamba nikiwa Mkristo sikushiriki kamwe katika vita ya wenyewe kwa wenyewe, kiongozi aliwaambia wengine: “Mtu yeyote akimgusa huyu, ataniona!”

Baadaye nilirudi mji wa nyumbani Volos nikiwa na nguvu hata zaidi katika imani yangu kuliko katika afya yangu ya kimwili.

Maendeleo ya Kiroho

Upesi baadaye niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa hesabu wa kutaniko la kwetu. Licha ya matatizo yaliyotokezwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe—kutia ndani kukamatwa mara nyingi kwa sababu ya mashtaka ya kugeuza imani za watu yaliyochochewa na makasisi—kushiriki katika huduma ya Kikristo kulikuwa chanzo cha shangwe kubwa kwangu mimi na kwa kutaniko lote.

Kisha mapema mwaka wa 1947, tulitembelewa na mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Hiyo ilikuwa ziara ya kwanza ya aina hiyo baada ya Vita ya Ulimwengu 2. Wakati huo kutaniko letu lililokuwa likikua katika Volos liligawanywa ili kufanyiza makutaniko mawili, nami nikawekwa rasmi kuwa mwangalizi-msimamizi wa mojawapo makutaniko hayo mawili. Wakati huo matengenezo ya kijeshi na kitaifa yalikuwa yakitia watu hofu. Makasisi waliitumia hali hiyo kwa faida yao. Walichochea wenye mamlaka dhidi ya Mashahidi wa Yehova kwa kueneza uvumi wa uwongo kwamba tulikuwa Wakomunisti au vikundi vyenye siasa kali.

Kukamatwa Kwingi na Vifungo

Mnamo 1947, nilikamatwa mara kumi hivi na kufanyiwa kesi tatu mahakamani. Kila wakati niliachiliwa. Katika masika ya 1948, nilihukumiwa kifungo cha miezi minne kwa ajili ya kugeuza imani za watu. Nilifungwa katika gereza la Volos. Wakati huohuo idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika kutaniko letu iliongezeka maradufu, nao mioyo ya akina ndugu ilijawa na shangwe na furaha.

Katika Oktoba 1948, nilipokuwa mkutanoni na wengine sita waliokuwa wakiongoza kutanikoni, polisi watano waliingia kwa fujo na kutukamata kwa kutisha kutupiga risasi. Walitupeleka kituo cha polisi bila kueleza sababu ya kutushika, na huko tukapigwa. Nilipigwa ngumi usoni na polisi aliyekuwa bondia mbeleni. Kisha tukatupwa kwenye seli.

Baadaye ofisa msimamizi aliniita niende ofisini mwake. Nilipoufungua mlango alinirushia chupa ya wino, iliyonikosa na kupasuka ukutani. Alifanya hilo ili kujaribu kuniogopesha. Kisha akanipa karatasi na kalamu na kuamuru: “Andika majina yote ya Mashahidi wa Yehova katika Volos, kisha uniletee hiyo orodha asubuhi. Usipofanya hivyo, utaona cha mtema kuni!”

Sikujibu, lakini niliporudi kwenye seli, ndugu waliosalia nami tulisali kwa Yehova. Niliandika jina langu tu kwenye hiyo karatasi na kusubiri niitwe. Lakini sikusikia lolote tena kutoka kwa huyo ofisa. Wakati wa usiku, majeshi ya upinzani yalikuwa yamekuja, naye alikuwa ameongoza watu wake dhidi yayo. Katika mapigano yaliyofuata, aliumia vibaya, ikawa lazima kukata mguu wake mmoja. Hatimaye, kesi yetu ikasikizwa, nasi tulishtakiwa kwa kuwa na mkutano usio halali. Sote tukiwa saba tukahukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani.

Kwa kuwa nilikataa kuhudhuria Misa ya Jumapili gerezani, nilifungwa peke yangu. Siku ya tatu, niliomba kuongea na mkurugenzi wa gereza. “Tafadhali niruhusu niseme,” nikamwambia, “yaonekana hakuna sababu ya kumwadhibu mtu aliye tayari kukaa miaka mitano gerezani kwa ajili ya imani yake.” Alifikiria kwa uzito juu ya hilo, na mwishowe akasema: “Kuanzia kesho, utakuwa ukifanya kazi hapa pamoja nami ofisini mwangu.”

Hatimaye, nilipata kazi ya kuwa msaidizi wa daktari katika gereza. Likiwa tokeo, nilijifunza mengi juu ya utunzaji wa afya, jambo ambalo limethibitika kuwa lenye faida sana katika miaka ya baadaye. Nilipokuwa gerezani, nilikuwa na fursa nyingi za kuhubiri, na watu watatu waliitikia na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Hatimaye, baada ya karibu miaka minne gerezani, niliachiliwa katika 1952 na kuwa mfungwa wa nje. Baadaye, nililazimika kwenda mahakamani katika Corinth kwa ajili ya suala la kutokuwamo. (Isaya 2:4) Huko nilifungwa kwa muda mfupi kwenye gereza la kijeshi, na zamu nyingine ya kutendwa vibaya ikaanza. Maofisa fulani walikuwa na vitisho vya ajabu, wakisema: “Nitauzidua moyo wako vipande vipande kwa kutumia jisu,” au, “Usitarajie kifo cha upesi kutokana na risasi sita tu.”

Mtihani wa Aina Tofauti

Hata hivyo, baada ya muda mfupi nilirudi nyumbani na kutumikia tena pamoja na Kutaniko la Volos na kufanya kazi ya kimwili isiyo ya wakati wote. Siku moja nilipokea barua kutoka ofisi ya Watch Tower Society iliyoko Athens, ikinialika niende kupata mazoezi kwa majuma mawili halafu nianze kutembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Wakati huohuo, baba mdogo wangu, ambaye hakuwa na mtoto yeyote na aliyekuwa na nyumba nyingi, akaniomba niwe meneja wa mali zake. Familia yangu ingali ilikuwa maskini, nayo kazi hii ingeweza kusuluhisha matatizo yao ya kiuchumi.

Nilimtembelea baba mdogo wangu ili kuonyesha shukrani zangu kwa ajili ya toleo lake, lakini nikamjulisha kwamba nilikuwa nimeamua kukubali mgawo wa pekee katika huduma ya Kikristo. Basi aliinuka na kunitazama kwa macho makavu, na kuondoka mara moja chumbani. Alirudi na kiasi kikubwa cha fedha ambacho kingeweza kuiruzuku familia yangu kwa miezi kadhaa. Yeye alisema: “Chukua hizi, ufanye chochote utakacho nazo.” Hata kufikia leo, siwezi kueleza zile hisia nilizokuwa nazo pindi hiyo. Ni kana kwamba nilisikia sauti ya Yehova ikiniambia, ‘Umefanya uchaguzi mzuri. Mimi niko pamoja nawe.’

Kwa kibali cha familia yangu, nilielekea Athens Desemba 1953. Ingawa ni mama tu aliyekuja kuwa Shahidi, wale washiriki wengine wa familia hawakupinga huduma yangu ya Kikristo. Nilipoenda kwenye ofisi ya tawi katika Athens, jambo lingine nisilotazamia liliningoja. Kulikuwa na telegramu kutoka kwa dada yangu, ikisema kwamba jitihada za baba za miaka miwili za kupata malipo ya uzeeni zilifanikiwa. Ni nini zaidi ningetaka? Nilihisi kana kwamba nilikuwa na mabawa, nikiwa tayari kuruka juu sana katika utumishi wa Yehova!

Kutahadhari

Katika miaka yangu ya kwanza-kwanza ya kazi ya mzunguko, nilihitaji kuwa mwangalifu sana kwa kuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiteswa sana na mamlaka za kidini na kisiasa. Ili kutembelea ndugu zetu wa Kikristo, hasa wale waliokuwa wakiishi katika miji midogo na vijiji vidogo, nilikuwa nikitembea kwa muda wa saa nyingi za usiku. Ndugu waliokuwa wakijihatarisha kukamatwa, waliokuwa wakikusanyika na kuningoja kwa subira. Ziara hizo zilikuwa kitia-moyo kama nini kwetu sote!—Warumi 1:11, 12.

Ili kuepuka kugunduliwa, nyakati nyingine nilijibadili. Wakati mmoja nilivalia kama mchungaji ili kupita kizuizi cha barabarani ili kufika kwenye mkusanyiko wa ndugu waliohitaji sana uchungaji wa kiroho. Kwenye pindi nyingine, katika 1955, Shahidi mwenzangu nami tulijifanya kuwa wauzaji wa kitunguu saumu ili kuepuka kushukiwa na polisi. Mgawo wetu ulikuwa kuwasiliana na ndugu Wakristo waliokuwa wamekuwa wasiotenda katika mji mdogo wa Árgos Orestikón.

Tulianika bidhaa zetu kwenye soko la umma la huo mji. Hata hivyo, polisi mmoja mchanga aliyekuwa akishika doria akaanza kushuku, na kila wakati alipopita, alitukodolea macho kwa udadisi sana. Hatimaye, akaniambia: “Wewe huonekani kama muuzaji wa kitunguu saumu.” Wakati huohuo, wanawake wachanga watatu walitufikia na kutaka kununua vitunguu saumu. Nikiashiria bidhaa zangu, nikasema hivi: “Polisi huyu mchanga hula vitunguu saumu kama hivi, tazameni jinsi alivyo mwenye nguvu na mwenye kupendeza!” Hao wanawake wakamwangalia huyo polisi na kucheka. Yeye pia akatabasamu na kuondoka.

Alipoondoka nilichukua fursa ile kwenda kwenye duka ambalo ndugu zetu wa kiroho walifanya kazi ya kushona. Nilimwomba mmoja wao kushonelea kifungo cha koti langu nilichong’oa mwenyewe. Alipokuwa akifanya hili, niliinama na kumnong’onezea: “Nimekuja kutoka kwa ofisi ya tawi ili kukuona.” Kwanza akina ndugu waliogopa kwa kuwa hawakuwa wamewasiliana na Mashahidi wenzao kwa miaka mingi. Niliwatia moyo kwa kadiri ambavyo niliweza na kufanya mipango ili kukutana nao baadaye kwenye makaburi ya huo mji ili tuwe na mazungumzo zaidi. Kwa kufurahisha, ziara hiyo ilikuwa yenye kutia moyo, nao tena wakawa wenye bidii katika huduma ya Kikristo.

Kupata Mwenzi Mwaminifu

Katika 1956, miaka mitatu baada ya kuanza kazi ya kusafiri, nilikutana na Niki, mwanamke mchanga Mkristo aliyependa sana kuhubiri na aliyetamani kutumia maisha yake katika huduma ya wakati wote. Tulipendana na kuoana Juni 1957. Nilikuwa na shaka ikiwa Niki angeweza kukabili mahitaji ya kazi ya mzunguko chini ya hali ngumu zilizowakumba Mashahidi wa Yehova wakati huo katika Ugiriki. Kwa msaada wa Yehova aliweza, hivyo akawa mwanamke wa kwanza kuandamana na mume wake katika kazi ya mzunguko katika Ugiriki.

Tuliendelea pamoja katika kazi ya mzunguko kwa miaka kumi, tukitumikia mengi ya makutaniko katika Ugiriki. Mara nyingi tulijibadili na tukiwa na sanduku mikononi, tulikuwa tukitembea usiku kwa muda wa saa nyingi ili kufika kwenye kutaniko. Licha ya upinzani mkubwa tuliokabili mara nyingi, tulisisimka sana kujionea wenyewe ongezeko la ajabu la idadi ya Mashahidi.

Utumishi wa Betheli

Katika Januari 1967, Niki nami tulialikwa kutumikia katika Betheli, kama iitwavyo ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Mwaliko huo ulitushangaza sote wawili, lakini tuliukubali, tukiwa na uhakika kwamba Yehova alikuwa akielekeza mambo. Kadiri muda ulivyopita, tulikuja kuthamini jinsi lilivyokuwa pendeleo kubwa kutumikia katika kitovu cha utendaji wa kitheokrasi.

Miezi mitatu baada ya kuingia utumishi wa Betheli, kikosi cha kijeshi kikanyakua mamlaka, na Mashahidi wa Yehova wakalazimika kuendelea na kazi yao kwa njia ya kichinichini. Tulianza kukutana katika vikundi vidogo-vidogo, na kufanya makusanyiko yetu msituni, tukahubiri kwa busara, na kuchapisha na kugawanya fasihi za Biblia kisiri. Haikuwa vigumu kuzoea hali hizo, kwa kuwa tulikuwa tu tumerudia upya zile njia tulizotumia miaka iliyopita za kufanya utendaji wetu. Licha ya vizuizi, idadi ya Mashahidi iliongezeka toka chini ya 11,000 katika 1967 na kufikia zaidi ya 17,000 katika 1974.

Baada ya karibu miaka 30 katika utumishi wa Betheli, Niki nami twaendelea kufurahia baraka za kiroho licha ya vizuizi vya kiafya na umri. Kwa zaidi ya miaka kumi, tuliishi katika majengo ya tawi yaliyoko kwenye Kartali Street katika Athens. Katika 1979 tawi jipya liliwekwa wakfu katika Marousi, kiunga cha Athens. Lakini tangu 1991 tumefurahia tawi kubwa jipya lililo Eleona, kilometa 60 kaskazini mwa Athens. Hapa natumikia katika mahali pa kutunzia wagonjwa pa Betheli, ambapo yale mazoezi niliyopata nikiwa msaidizi wa daktari wa gereza yamekuwa msaada sana.

Wakati wa kile kipindi cha zaidi ya miongo minne katika utumishi wa wakati wote, sawa na Yeremia, nimetambua ukweli wa ahadi ya Yehova: “Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.” (Yeremia 1:19) Ndiyo, Niki nami tumefurahia kikombe kilichojaa baraka kutoka kwa Yehova. Twashangilia daima kwa vile ametujali kwa upendo mwingi sana na kwa fadhili zisizostahiliwa.

Kitia-moyo changu kwa vijana walio katika tengenezo la Yehova ni kwamba wafuatie utumishi wa wakati wote. Kwa kufanya hivyo ndipo tu wataukubali mwaliko wa Yehova ili kumjaribu na kuona ikiwa atatimiza ahadi yake, ‘kufungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’ (Malaki 3:10) Kutokana na mambo niliyojionea, naweza kuwahakikishia enyi vijana kuwa Yehova kwelikweli atawabariki ninyi nyote mmtumainio kikamili.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Lambros Zoumbos na mke wake, Niki

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki