Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Nguvu Yenye Kugeuza ya Neno la Mungu
KWA kukiri mwenyewe, alikuwa “mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri.” (1 Timotheo 1:13) Lakini alibadilika! Kugeuka kwa mtume Paulo kulikuwa kukubwa hivi kwamba baadaye alitangaza hivi: “Niigeni mimi kama nami ninavyomwiga Kristo.”—1 Wakorintho 11:1, HNWW.
Leo, mamia ya maelfu ya waabudu wanyoofu ulimwenguni wanafanya mabadiliko kama hayohayo. Ni nini huwawezesha kufanya hivyo? Wanatwaa ujuzi wa Neno la Mungu na kuutumia katika maisha zao. Jambo lililoonwa lifuatalo lakazia nguvu ya Neno la Mungu ya kugeuza.
Katika Slovenia wenzi wa ndoa wazee-wazee waliishi peke yao nje ya kijiji kimoja. Mume aitwaye Jože, alikuwa na umri wa karibu miaka 60 naye alikuwa na tatizo kubwa la uraibu wa kileo. Ingawa hivyo, alimtunza mke wake mgonjwa, Ljudmila. Siku moja Jože alifikiwa na wapiga-mbiu wawili wa Ufalme. Aliwakaribisha Mashahidi hao ndani ya nyumba yake, ambapo walimkuta mkeye. Aliposikia ujumbe wa Ufalme, Ljudmila alitiririkwa na machozi ya shangwe. Jože pia alifurahia aliyosikia akauliza maswali mengi. Baada ya kuwaachia wenzi hao wa ndoa fasihi za Biblia, Mashahidi hao waliondoka.
Mwezi mmoja baadaye Mashahidi hao waliweza kurudi, na waliona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani mezani. Alipoulizwa alikitoa wapi, Jože alisema: “Niliona tangazo nyuma ya mojawapo magazeti mliyoniachia. Basi nikaandikia ofisi yenu katika Zagreb na kuomba kitabu hicho.” Kwa kufikiria kupendezwa kwake, alialikwa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliofuata ambao ungefanyiwa katika Jumba la Ufalme. Mashahidi hao waliona shangwe alipofika!
Upesi funzo la Biblia likaanzishwa, na maendeleo mazuri yakafanywa. Kwa kielelezo, Jože alipoonyeshwa katika Biblia kwamba “usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala . . . usivisujudie wala kuvitumikia,” mara moja alikusanya mifano yote ya kidini iliyokuwa katika nyumba yake, kutia ndani picha za mifano, na kuzitupa.—Kutoka 20:4, 5.
Kiu ya Jože ya kiroho ilikuwa ikizimwa. Hata hivyo, kwa kusikitisha, bado alikuwa na kiu nyingine. Kwa miaka 18 hivi, alikuwa amekunywa lita saba za divai kila siku. Kwa sababu ya tatizo lake la kunywa, hakutunza sura yake binafsi. Lakini baada ya kujifunza maoni ya Mungu kuhusu matumizi mabaya ya alkoholi, aliazimia kubadilika.
Alijitahidi kushinda tatizo lake la kunywa polepole, akiweka rekodi ya kiwango alichokuwa akinywa kila siku. Upesi akaacha kuwa mtumwa wa divai. Katika mafundisho yake ya Biblia, pia alijifunza kwamba Wakristo wa kweli wanatakiwa kudumisha usafi wa kibinafsi. Hivyo, akawapa wale Mashahidi pesa na kuwaambia: “Haya, nendeni mnunue nguo zozote ninazohitaji ili nivalie vizuri kwenye mikutano ya Kikristo na katika utumishi wa shambani!” Wale Mashahidi walirudi na nguo za ndani, soksi, viatu, shati, suti, tai, na mkoba.
Baada ya kujifunza Biblia kwa mwaka mmoja, Jože na Ljudmila walistahili kuandamana na Mashahidi katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Miezi mitatu baada ya hapo walionyesha wakfu wao kwa Mungu kupitia ubatizo wa maji kwenye mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Japo uzee na afya iliyodhoofika, Jože alishiriki kwa ukawaida katika kuhubiri habari njema na baadaye, hadi kifo chake katika Mei 1995, alikuwa akitumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko. Matunda mazuri yaliyotokezwa katika maisha za mtu huyu mnyenyekevu na mke wake hutoa ushuhuda kwa nguvu za kugeuza za Neno la Mungu!