Maswali Kutoka kwa wasomaji
Mtume Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa ‘akiyasahau yaliyo nyuma, akiyachuchumilia yaliyo mbele’? (Wafilipi 3:13) Je, mtu aweza kusahau jambo fulani kimakusudi?
La, katika visa vingi hatuwezi kuondoa kimakusudi jambo fulani akilini mwetu. Uhakika ni kwamba, sisi husahau mengi ambayo tungependa kukumbuka na kukumbuka mambo mengi ambayo ni afadhali tungeyasahau. Basi, Paulo alimaanisha nini alipoandika maneno ya Wafilipi 3:13? Muktadha hutusaidia kuelewa.
Katika Wafilipi sura ya 3, Paulo afafanua “sababu [yake] ya kuutumainia mwili.” Yeye asema juu ya malezi yake bora ya Kiyahudi na bidii yake kwa ile Sheria—mambo ambayo yangeweza kumpa faida nyingi katika taifa la Israeli. (Wafilipi 3:4-6; Matendo 22:3-5) Hata hivyo, alikataa faida hizo, akiziondosha, kwa kusema kitamathali. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa amepata kitu kizuri zaidi—“uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu.”—Wafilipi 3:7, 8.
Lengo kubwa la Paulo lilikuwa kupata, si cheo katika ulimwengu huu, bali “ufufuo wa mapema kutoka kwa wafu.” (Wafilipi 3:11, 12, NW) Hivyo, yeye aandika hivi: “Nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:13, 14) Paulo aliposema kwamba alikuwa ‘akiyasahau yaliyo nyuma,’ hakumaanisha kwamba kwa njia fulani alikuwa amefuta kutoka akilini mambo “yaliyo nyuma.” Bila shaka bado alikuwa akiyakumbuka, kwa kuwa alikuwa ametoka tu kuyaorodhesha. Isitoshe, katika Kigiriki cha awali, yeye atumia namna ya kitenzi kionyeshacho kitendo kinachoendelea, si kilichomalizika. Yeye asema “nikiyasahau,” si “nikiwa nimeyasahau.”
Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “sahau” (e·pi·lan·thaʹno·mai) lina maana tofauti-tofauti, moja yazo ni “kutoshughulikia,” au “kupuuza.” Kulingana na Exegetical Dictionary of the New Testament (iliyohaririwa na Horst Balz na Gerhard Schneider), hilo ndilo linalomaanishwa na “kusahau” katika Wafilipi 3:13. Paulo hakuendelea kufikiri juu ya vitu alivyokuwa ameacha. Alijifunza kuviona kuwa visivyo na umaana. Vilikuwa kama “takataka” vikilinganishwa na tumaini la kimbingu.—Wafilipi 3:8, HNWW.
Maneno ya Paulo yanaweza kutumikaje leo? Naam, huenda Mkristo, kama Paulo, alikuwa amedhabihu mambo fulani ili kumtumikia Mungu. Huenda aliacha kazi-maisha yenye mapato makubwa ili ajiunge na utumishi wa wakati wote. Au huenda ni wa familia yenye utajiri ambayo iliacha kumtegemeza kifedha kwa sababu haikubali kweli. Dhabihu kama hizo ni zenye kupongezwa, lakini si jambo la kuhangaikia daima. Mkristo ‘husahau,’ huacha kuhangaikia, mambo “yaliyo nyuma” akitazama wakati ujao mtukufu unaomngojea.—Luka 9:62.
Labda kanuni kuu iliyo katika maneno ya Paulo yaweza kutumiwa kwa njia nyingine. Namna gani juu ya Mkristo aliyejihusisha katika mwenendo mbaya kabla ya kujifunza juu ya Mungu? (Wakolosai 3:5-7) Au tuseme, baada ya kuwa Mkristo, alitenda dhambi nzito na kutiwa nidhamu na kutaniko. (2 Wakorintho 7:8-13; Yakobo 5:15-20) Ikiwa ametubu kikweli na kubadili njia zake, yeye ‘ameoshwa.’ (1 Wakorintho 6:9-11) Kilichotendeka ni jambo lililopita. Huenda asisahau kihalisi kile alichofanya—kwa kweli, angekuwa mwenye hekima kujifunza kutokana na yale aliyojionea ili asirudie dhambi. Hata hivyo, yeye ‘husahau’ katika maana ya kutojidhulumu daima. (Linganisha Isaya 65:17.) Akiwa amesamehewa kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, yeye hujitahidi kutohangaikia wakati uliopita.
Kwenye Wafilipi 3:13, 14, Paulo ajifafanua kuwa mkimbiaji katika mbio, ‘akikaza mwendo’ afikie lengo. Mkimbiaji hutazama mbele, si nyuma. Vivyohivyo, Mkristo apaswa kutazama baraka zilizo mbele, si mambo aliyoacha nyuma. Paulo pia asema: “Hata mkiwaza mengine katika jambo lo lote, Mungu atawafunulia hilo nalo.” (Wafilipi 3:15) Hivyo, sali kwa Mungu akusaidie kusitawisha maoni haya. Jaza akili yako kwa mawazo ya Mungu kama yapatikanavyo katika Biblia. (Wafilipi 4:6-9) Tafakari juu ya upendo wa Yehova kwako na juu ya baraka unazofurahia kwa sababu ya huo. (1 Yohana 4:9, 10, 17-19) Kisha, kupitia roho takatifu Yehova atakusaidia usihangaikie kile ulichoacha nyuma. Badala ya hivyo, kama Paulo, utatazamia wakati ujao mtukufu ulio mbele.—Wafilipi 3:17.