“Badala ya Dhahabu, Nilipata Almasi”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MICHALIS KAMINARIS
Baada ya miaka mitano katika Afrika Kusini ambako nilikuwa nimeenda kutafuta dhahabu, nilikuwa nikirudi nyumbani nikiwa na jambo lenye thamani zaidi. Acheni niwaambie juu ya mali niliyokuwa nayo sasa na ambayo nilitamani kushiriki.
NILIZALIWA katika mwaka wa 1904 katika kisiwa cha Ugiriki cha Cephalonia katika Bahari ya Ionia. Wazazi wangu walikufa upesi baadaye, kwa hiyo nilikua nikiwa yatima. Nilitamani msaada, na nilisali mara nyingi kwa Mungu. Hata ingawa nilihudhuria Kanisa Othodoksi la Kigiriki kwa ukawaida, sikuijua Biblia kabisa. Sikupata liwazo.
Katika mwaka wa 1929, niliamua kuhama na kutafuta maisha mazuri zaidi. Nikiacha kisiwa changu kikame, nilisafiri kwa meli kwenda Afrika Kusini kupitia Uingereza. Baada ya siku 17 baharini, nilifika Cape Town, Afrika Kusini, ambako niliajiriwa mara moja na mwananchi mwenzangu. Hata hivyo, sikupata liwazo katika mali za kimwili.
Jambo Lenye Thamani Zaidi
Nilikuwa nimekuwa Afrika Kusini karibu miaka miwili wakati mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipotembelea mahali pangu pa kazi, akanitolea fasihi za Biblia katika lugha ya Kigiriki. Zilitia ndani vijitabu Where Are the Dead? na Oppression, When Will It End? Nakumbuka vizuri jinsi nilivyovisoma kwa hamu, hata kukariri maandiko yote yaliyonukuliwa. Siku moja nilimwambia mfanyakazi mwenzangu hivi: “Nimepata kile nilichokuwa nikitafuta miaka hii yote. Nilikuja Afrika Kusini kutafuta dhahabu, lakini badala ya dhahabu, nilipata almasi.”
Ni kwa shangwe nyingi nilijifunza kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova, na kwamba Ufalme wake tayari umesimamishwa mbinguni, na kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. (Zaburi 83:18; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10; 24:3-12; 2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 12:7-12) Ilisisimua kama nini kujifunza kwamba Ufalme wa Yehova utaleta baraka zisizo na mwisho kwa jamii zote za wanadamu! Jambo lingine hakika lililonivutia lilikuwa kwamba kweli hizo zenye thamani zilikuwa zikihubiriwa ulimwenguni pote.—Isaya 9:6, 7; 11:6-9; Mathayo 24:14; Ufunuo 21:3, 4.
Upesi nilipata anwani ya ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Cape Town na kupata fasihi za Biblia zaidi. Nilipendezwa hasa kupata nakala ya kibinafsi ya Biblia. Nilichokisoma kilinichochea kutaka kutoa ushahidi. Nilianza kwa kutuma vichapo vya Biblia kwa watu wa ukoo wangu, marafiki, na watu niliofahamiana nao huko katika mji wangu wa nyumbani wa Lixoúrion. Kutokana na mafunzo yangu, nilikuja kuelewa hatua kwa hatua kwamba ili kumpendeza Yehova lazima mtu aweke wakfu maisha yake kwake. Kwa hiyo nilifanya hivyo mara moja katika sala.
Katika pindi moja, nilihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, lakini kwa kuwa sikujua Kiingereza, sikuelewa chochote. Nilipopata kujua kwamba kulikuwa na Wagiriki wengi walioishi Port Elizabeth, nilihamia huko, lakini nilikosa kupata Mashahidi wowote wenye kusema Kigiriki. Kwa hiyo, niliamua kurudi Ugiriki ili kuwa mweneza-evanjeli wa wakati wote. Nakumbuka nikijiambia, ‘Nitarudi Ugiriki hata gharama iweje.’
Huduma ya Wakati Wote Katika Ugiriki
Katika masika ya 1934 nilikuwa katika meli ya bahari-kuu ya Italia iliyoitwa Duilio. Nilifika Marseilles, Ufaransa, na baada ya kukaa siku kumi huko, niliondoka kwenda Ugiriki ndani ya meli ya abiria iliyoitwa Patris. Tulipokuwa baharini, meli ilipatwa na matatizo ya kiufundi, na usiku amri ilitolewa ya kuteremsha baharini mashua za kuokolea uhai. Ndipo nikakumbuka mawazo yangu juu ya kurudi Ugiriki hata gharama iweje. Hata hivyo, mashua ya Italia ya kuvuta meli ilifika hatimaye na kutuvuta hadi Naples, Italia. Baadaye tulifika hatimaye Piraiévs (Piraeus), Ugiriki.
Kutoka hapo nilikwenda Athene ambako nilitembelea ofisi ya tawi ya Watch Tower Society. Katika mazungumzo pamoja na Athanassios Karanassios, mwangalizi wa ofisi ya tawi, niliomba mgawo wa kuhubiri wakati wote. Siku iliyofuata nilikuwa njiani kwenda Peloponnisos, katika sehemu ya kusini mwa bara kuu la Ugiriki. Niligawiwa wilaya hiyo yote kuwa eneo langu la kibinafsi!
Nikiwa mwenye idili sana nilianza kazi ya kuhubiri, nikienda kutoka mji hadi mji, kutoka kijiji hadi kijiji, kutoka shamba hadi shamba, kutoka nyumba ya mbali hadi nyumba ya mbali. Upesi Michael Triantafilopoulos aliyenibatiza katika kiangazi cha 1935—zaidi ya mwaka mmoja baada ya kuwa nimeanza huduma ya wakati wote, alijiunga nami! Usafiri wa umma haukupatikana, kwa hiyo tulitembea kwenda kila mahali. Tatizo letu kubwa lilikuwa upinzani wa makasisi, ambao wangefanya chochote kutuzuia. Likiwa tokeo, tulikabili ubaguzi mwingi. Hata hivyo, vijapokuwa vizuizi, ushahidi ulitolewa, na jina la Yehova likatangazwa kotekote.
Kuvumilia Upinzani
Asubuhi moja, nilipokuwa nikihubiri katika wilaya yenye milima wa Arcadia, nilifika kijiji cha Magouliana. Baada ya muda wa saa moja wa kutoa ushahidi, nilisikia kengele za kanisa na upesi nikang’amua kwamba zilikuwa zikilia kwa sababu yangu! Umati ulikusanyika chini ya uongozi wa mwenye cheo cha chini ya askofu wa dini ya Othodoksi ya Ugiriki. Nilifunga upesi mkoba wangu wa kutoa ushahidi, nikasali kimya-kimya kwa Yehova. Yule mdogo wa askofu, pamoja na umati wa watoto ukimfuata walinijia moja kwa moja. Alianza kupiga kelele, “Ndiye huyo! Ndiye huyo!”
Hao watoto walinizingira kabisa, na kasisi akanikaribia na kuanza kunisukuma kwa tumbo lake kubwa lenye kutokeza, akisema kwamba yeye hakutaka kunigusa kwa mikono yake ‘iwapo nitachafuliwa.’ Alipiga kelele hivi, “Mpigeni! Mpigeni!” Lakini pindi hiyohiyo ofisa wa polisi akatokea na kutupeleka sisi wawili kwenye kituo cha polisi. Huyo kasisi alihukumiwa kwa kuchochea umati na akatozwa faini ya drakma 300 pamoja na gharama za mahakama. Niliachiliwa.
Tulipofika eneo jipya, tulichagua mji mkubwa zaidi kuwa kitovu cha utendaji wetu, na kutoka hapo tulihubiri eneo lote kufikia umbali wa muda wa saa nne wa kutembea kwa miguu. Hilo lilimaanisha kwamba tuliondoka asubuhi kulipokuwa na giza bado na kurudi nyumbani baada ya giza la jioni kuingia, kwa kawaida tukitembelea kijiji kimoja au viwili kila siku. Baada ya kuhubiri vijiji vilivyotuzunguka, tulihubiri katika mji uliokuwa kitovu kisha tukahamia eneo lingine. Mara nyingi tulikamatwa kwa sababu makasisi walichochea watu dhidi yetu. Katika eneo la Parnassus, katikati ya Ugiriki, nilitafutwa na polisi kwa miezi mingi. Hata hivyo, hawakupata kunikamata kamwe.
Siku moja Ndugu Triantafilopoulos nami tulikuwa tukihubiri katika kijiji cha Mouríki katika wilaya ya Boeotia. Tuligawanya kijiji katika sehemu mbili, nami nikaanza kuhubiri katika miteremko iliyo wima, kwa kuwa nilikuwa mchanga zaidi. Kwa ghafula nikasikia mayowe kutoka chini. Nilipokuwa nikikimbia kuelekea chini, nilifikiri ‘Ndugu Triantafilopoulos anapigwa.’ Wanakijiji walikuwa wamekusanyika katika mkahawa wa huko, na kasisi mmoja alikuwa akitembea kwa kishindo kwenda na kurudi kama fahali mwenye hasira. “Watu hawa hutuita ‘mbegu ya Nyoka,’” alikuwa akipiga kelele.
Huyo kasisi alikuwa tayari amevunja bakora kichwani pa Ndugu Triantafilopoulos, na damu ilikuwa ikitiririka usoni pake. Baada ya kusafisha hiyo damu, tuliweza kuondoka. Tulitembea kwa muda wa saa tatu hadi tukafika jiji la Thebes. Huko, lile jeraha lilitibiwa katika kliniki. Tuliripoti hicho kisa kwa polisi, na mashtaka yakapelekwa mahakamani. Hata hivyo, huyo kasisi alikuwa na mahusiano na wenye mamlaka, naye akaachiliwa hatimaye.
Tulipokuwa tukihubiri mji wa Leukas, wafuasi wa mmoja wa viongozi wa kisiasa wa hilo eneo “alitukamata” na kutuleta kwenye mkahawa wa kijiji, ambako tulishtakiwa katika mahakama isiyo halali. Huyo kiongozi wa siasa pamoja na wanaume wake walituzunguka-zunguka kwa zamu wakitutolea hotuba—wakifuliza kutoa maneno yenye ukali—na kututisha kwa ngumi zilizokunjwa. Wote walikuwa wamelewa. Mashutumu yao dhidi yetu yaliendelea kutoka adhuhuri hadi machweo, lakini tulibaki watulivu na kuendelea kutabasamu huku tukitangaza kutokuwa kwetu na hatia na kusali kimya-kimya kwa Yehova Mungu ili kupata msaada.
Wakati wa jioni-jioni polisi wawili walituokoa. Walitupeleka kwenye kituo cha polisi, wakatutendea vyema. Ili kutetea vitendo vyake, huyo kiongozi wa kisiasa alikuja siku iliyofuata na kutushtaki juu ya kueneza propaganda dhidi ya Mfalme wa Ugiriki. Kwa hiyo polisi walitupeleka, huku tukisindikizwa na wanaume wawili, hadi mji wa Lamia kwa uchunguzi zaidi. Tuliwekwa kizuizini kwa siku saba kisha tukapelekwa tukiwa tumetiwa pingu mikono hadi mji wa Larissa ili kuhukumiwa.
Ndugu zetu Wakristo katika Larissa, waliokuwa wamejulishwa mapema, walingojea kufika kwetu. Shauku kuu waliyotuonyesha ilikuwa ushahidi mzuri kwa walinzi. Wakili wetu, mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa kanali luteni hapo zamani, alijulikana sana mjini. Alipokwenda mbele mahakamani na kutoa hoja juu ya kesi yetu, yale mashtaka dhidi yetu yalifunuliwa kuwa yasiyo ya kweli, nasi tukaachiliwa.
Mafanikio ya ujumla ya mahubiri ya Mashahidi wa Yehova yaliongoza kwenye kuongezeka kwa upinzani. Sheria zilipitishwa katika mwaka wa 1938 na wa 1939 zilizokataza ugeuzaji wa imani, na Michael nami tulihusika katika kesi nyingi za mahakama juu ya suala hilo. Baadaye, ofisi ya tawi ilitushauri kutohubiri pamoja ili tusivute uangalifu mwingi kwenye utendaji wetu. Niliona ikiwa vigumu kutokuwa na mwandamani. Hata hivyo, nikiwa na itibari katika Yehova, nilitembea na kuhubiri wilaya za Attica, Boeotia, Phthiotis, Euboea, Aetolia, Acarnania, Eurytania, na wilaya ya Peloponnisos.
Kilichonisaidia katika kipindi hicho kilikuwa maneno haya mazuri ya mtunga-zaburi juu ya itibari katika Yehova: “Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, na kunisimamisha mahali pangu pa juu.”—Zaburi 18:29, 32, 33.
Katika mwaka wa 1940, Italia ilitangaza vita juu ya Ugiriki, na upesi baadaye majeshi ya Ujerumani yakavamia hiyo nchi. Sheria ya kijeshi ilitangazwa, na vitabu vya Watch Tower Society vikapigwa marufuku. Hizo zilikuwa nyakati ngumu kwa Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki; hata hivyo, idadi yao iliongezeka kwa kutazamisha—kutoka Mashahidi 178 katika mwaka wa 1940 hadi 1,770 kufikia mwisho wa Vita ya Ulimwengu 2 katika 1945!
Kutumikia Betheli
Katika mwaka wa 1945, nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Athene. Wakati huo, Betheli, neno limaanishalo “Nyumba ya Mungu,” ilikuwa katika nyumba ya kukodi kwenye Lombardou Street. Ofisi zilikuwa kwenye orofa ya kwanza, na mahali pa matbaa palikuwa katika chumba cha chini. Mahali hapo palikuwa na matbaa ndogo na mashine ya kukatia karatasi. Mwanzoni wafanyakazi kwenye mahali pa matbaa walikuwa watu wawili tu, lakini upesi wajitoleaji wengine walioishi nje ya Betheli walianza kuja kusaidia na kazi.
Uwasiliano pamoja na makao makuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York, ulianzishwa tena katika mwaka wa 1945, na mwaka huo tukaanza tena kuchapa Mnara wa Mlinzi kwa ukawaida katika Ugiriki. Kisha, katika mwaka wa 1947, tulihamisha ofisi yetu ya tawi hadi 16 Tenedou Street, lakini mahali pa matbaa pakabaki Lombardou Street. Baadaye hapo mahali pa matbaa palihamishwa kutoka Lombardou Street hadi kiwanda cha Shahidi mmoja kilichokuwa umbali wa kilometa tano hivi. Kwa hiyo kwa kipindi fulani tulikuwa tukisafiri kwenda na kurudi kati ya mahali patatu.
Nakumbuka nikiondoka makao yetu kwenye Tenedou Street asubuhi sana na kusafiri kwenda kwenye mahali pa matbaa. Baada ya kufanya kazi hapo hadi saa saba alasiri, nilienda Lombardou Street ambako karatasi tulizokuwa tumechapa zilipelekwa. Huko zilikunjwa kuwa magazeti, zikashonwa na kukatwa kwa mkono. Baadaye tulipeleka magazeti yaliyokamilika hadi kwenye ofisi ya posta, tukayabeba hadi orofa ya tatu, tukawasaidia wafanyakazi kuzitenganisha, na kuweka stampu juu ya bahasha ili kuzituma.
Kufikia mwaka wa 1954 idadi ya Mashahidi Ugiriki ilikuwa imeongezeka hadi zaidi ya 4,000, na majengo yaliyopanuliwa yalihitajika. Hivyo, tulihamia Betheli mpya yenye orofa tatu mjini Athene kwenye Kartali Street. Katika mwaka wa 1958, niliombwa nisimamie kazi jikoni, na hilo likawa daraka langu hadi 1983. Wakati uleule, katika mwaka wa 1959, nilimwoa Eleftheria, ambaye amethibitika kuwa msaidizi mwaminifu-mshikamanifu katika utumishi wa Yehova.
Kuvumilia Upinzani Tena
Katika mwaka wa 1967 kikosi cha kijeshi kilinyakua mamlaka, na kazi yetu ya kuhubiri ikawekewa vizuizi kwa mara nyingine tena. Hata hivyo, kwa sababu ya yale tuliyotangulia kupatwa nayo katika kukabiliana na marufuku juu ya utendaji wetu mbalimbali, tulirekebisha hali haraka na kuendelea na kazi kisiri kwa mafanikio.
Tulifanya mikutano yetu katika nyumba za faragha na kutumia uangalifu katika huduma yetu ya nyumba hadi nyumba. Hata hivyo, ndugu zetu walikamatwa kwa ukawaida, na kesi za mahakama zikaongezeka. Mawakili wetu walikuwa wenye shughuli nyingi sikuzote wakisafiri ili kushughulikia kesi zilizofanywa katika sehemu mbalimbali za nchi. Ujapokuwa upinzani, Mashahidi walio wengi waliendelea kwa ukawaida katika utendaji wao wa kuhubiri, hasa katika miisho-juma.
Katika Jumamosi au Jumapili ya kawaida baada ya mahubiri yetu kukamilika kwa siku hiyo, uchunguzi ulifanywa ili kuona ni nani waliokosekana kutoka katika vikundi vyetu. Kwa kawaida, wale waliokosekana walikuwa wakizuiliwa kwenye kituo cha polisi kilichokuwa karibu zaidi. Kwa hiyo, tuliwapelekea blanketi na chakula na kuwatolea kitia-moyo. Pia tuliwajulisha mawakili wetu, waliokuja mbele ya kiongozi wa mashtaka Jumatatu ili kutetea wale waliokuwa kizuizini. Tulikabili hali hiyo kwa furaha kwa sababu tulikuwa tukiteseka kwa ajili ya kweli!
Wakati wa marufuku utendaji wetu mbalimbali wa kuchapa kwenye Betheli ulifungwa. Kwa hiyo nyumba ambamo Eleftheria nami tuliishi katika viunga vya Athene ikawa kama mahali pa matbaa. Eleftheria alipiga chapa nakala za makala za Mnara wa Mlinzi akitumia taipureta nzito. Aliweka karatasi kumi pamoja na karatasi za kaboni ndani ya taipureta naye akalazimika kupiga chapa kwa nguvu sana ili herufi ziweze kuchapika kwenye kurasa zote kumi. Kisha nilikusanya hizo kurasa na kuzishona pamoja. Hilo liliendelea kila jioni hadi usiku wa manane. Polisi mmoja aliishi kwenye orofa ya chini, na tungali twashangaa kwa nini hakupata kamwe kuwa mwenye kushuku.
Kushangilia Katika Upanuzi Wenye Kuendelea
Demokrasia ilirudishwa Ugiriki katika mwaka wa 1974, na kazi yetu ya kuhubiri ikaendelezwa tena kwa uwazi zaidi. Hata hivyo, katika ile miaka saba ya vizuizi juu ya kazi yetu, tulifurahia ongezeko la ajabu la Mashahidi wapya zaidi ya 6,000, wakifikia jumla ya wapiga-mbiu wa Ufalme zaidi ya 17,000.
Pia tulianza tena utendaji wetu wa ukawaida wa uchapaji kwenye majengo ya tawi. Likiwa tokeo, majengo ya Betheli ya Kartali Street upesi yakawa madogo mno. Kwa hiyo, shamba la hektari moja lilinunuliwa katika kiunga cha Athene cha Marousi. Majengo mapya ya Betheli yalijengwa yaliyokuwa na vyumba 27 vya kulala, kiwanda, ofisi, na majengo mengine. Haya yaliwekwa wakfu katika Oktoba 1979.
Hatimaye tulihitaji hata nafasi zaidi. Kwa hiyo shamba la hektari 22 lilinunuliwa karibu kilometa 60 kaskazini ya Athene. Hapo mahali pako katika Eleona, kwenye upande wa kilima palipo na mandhari ya milima na mabonde yenye maji mengi. Hapo, katika Aprili 1991, tuliweka wakfu jengo kubwa zaidi lililo na nyumba 22, ambazo kila mojawapo yaweza kutosha kwa watu wanane.
Baada ya kutumia miaka zaidi ya 60 katika huduma ya wakati wote, bado nimebarikiwa kuwa na afya nzuri. Kwa kufurahisha, ‘naendelea kuzaa matunda wakati wa uzee.’ (Zaburi 92:14) Namshukuru Yehova hasa kwa vile nimeishi kuona kwa macho yangu mwenyewe ongezeko tukufu katika idadi ya waabudu wake wa kweli. Nabii Isaya alitabiri ongezeko kama hilo hivi: “Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; hayatafungwa mchana wala usiku; ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa.”—Isaya 60:11.
Jinsi lilivyo jambo la ajabu kuona mamilioni ya watu kutoka mataifa yote wakimiminika kwenye tengenezo la Yehova na kufunzwa jinsi ya kuokoka dhiki kubwa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu! (2 Petro 3:13) Naweza kusema kikweli kwamba huduma ya wakati wote imethibitika kuwa yenye thamani zaidi kwangu kuliko chochote ambacho ulimwengu huu unatoa. Ndiyo, nimepata, si hazina za dhahabu, lakini almasi za kiroho ambazo zimetajirisha maisha yangu kwa kadiri kubwa sana.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Michalis na Eleftheria Kaminaris
(Kulia) Matbaa kwenye Lombardou Street