Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 10/1 kur. 22-25
  • Kumpa Yehova Kile Anachostahili

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumpa Yehova Kile Anachostahili
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutenda kwa Kupatana na Yale Niliyojifunza
  • Kuhubiri Japo Vizuizi
  • Huduma Yetu Katika Aidhonochori
  • Mnyanyaso Mkatili
  • Ukuzi Japo Upinzani
  • Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Nilipata Utajiri wa Kweli Katika Australia
    Amkeni!—1994
  • “Badala ya Dhahabu, Nilipata Almasi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 10/1 kur. 22-25

Kumpa Yehova Kile Anachostahili

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA TIMOLEON VASILIOU

Nilikuwa nimekamatwa kwa sababu ya kufundisha watu Biblia katika kijiji cha Aidhonochori. Polisi walinivua viatu, wakaanza kupiga nyayo zangu. Walipoendelea kunipiga, miguu yangu ikawa imekufa ganzi nisiweze tena kuhisi maumivu. Kabla ya kusimulia jambo lililofanya nipigwe vibaya hivyo, ambalo lilikuwa kawaida nchini Ugiriki wakati huo, ebu niwasimulie jinsi nilivyopata kuwa mwalimu wa Biblia.

PUNDE tu baada ya kuzaliwa mwaka wa 1921, familia yetu ilihamia mji wa Rodholívos, kaskazini mwa Ugiriki. Nilipokuwa kijana, niliishi maisha ya ukaidi. Nilianza kuvuta sigareti nikiwa na umri wa miaka 11. Baadaye nikawa mnywaji wa pombe wa kupindukia na mcheza kamari, nikawa naenda kwenye karamu za ulevi karibu kila usiku. Nilikuwa na kipawa cha kupiga muziki, basi nikajiunga na bendi fulani ya kwetu. Kwa muda wa mwaka mmoja hivi niliweza kucheza ala nyingi za bendi hiyo. Lakini, kwa upande mwingine nilipenda kusoma na nilipenda haki.

Mapema katika mwaka wa 1940, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa ikiendelea, bendi yetu ilialikwa ipige muziki kwenye maziko ya msichana mmoja mdogo. Kando ya kaburi, watu wa ukoo na marafiki walikuwa wakilia sana kwa huzuni. Niliathiriwa sana na hali yao ya kukosa tumaini kabisa. Nikaanza kujiuliza, ‘Kwa nini tunakufa? Je, kuna uhai mwingine mbali na uhai wetu mfupi wa sasa? Naweza kupata majibu wapi?’

Siku chache baadaye, niliona nakala moja ya Agano Jipya kwenye rafu nyumbani kwangu. Nikaichukua, nikaanza kuisoma. Niliposoma maneno ya Yesu katika Mathayo 24:7 kuhusu vita yenye kuenea kuwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake, nikatambua kwamba ni lazima maneno yake yanatimizwa wakati wetu. Katika majuma yaliyofuata, nilisoma mara kadhaa nakala hiyo ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Kisha mnamo Desemba 1940, nilizuru familia moja jirani—mwanamke mmoja mjane na watoto wake watano. Katika chumba chao cha juu nilipata rundo la vijitabu, na kimojawapo kilikuwa na kichwa A Desirable Government, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Nilibaki huko kwenye chumba cha juu na kusoma kijitabu hicho chote. Nikasadiki kabisa mambo niliyosoma kwamba kwa kweli twaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho” na kwamba hivi karibuni Yehova Mungu atakomesha mfumo huu wa mambo na kuweka ulimwengu wake mpya wenye uadilifu mahali pake.—2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:13.

Jambo ambalo lilinivutia zaidi ni uthibitisho wa Kimaandiko wa kwamba waaminifu wataishi milele kwenye paradiso duniani na kwamba mateseko na kifo hazitakuwapo tena katika huo ulimwengu mpya chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. (Zaburi 37:9-11, 29; Ufunuo 21:3, 4) Nilipokuwa nikisoma, nilimshukuru Mungu kupitia sala kwa sababu ya mambo hayo, nikamwomba anionyeshe matakwa yake. Ikawa wazi kwamba Yehova Mungu astahili ujitoaji wangu wa nafsi yote.—Mathayo 22:37.

Kutenda kwa Kupatana na Yale Niliyojifunza

Tokea wakati huo, niliacha kuvuta sigareti, nikaacha ulevi, nikaacha kucheza kamari. Nikawakusanya wale watoto watano wa yule mjane pamoja na ndugu yangu mmoja na dada zangu wawili waliokuwa wachanga, nikawafafanulia yale niliyokuwa nimejifunza kwenye kile kijitabu. Upesi sote tukaanza kuelezea wengine yale machache tuliyokuwa tunayafahamu. Tukajulikana katika jumuiya hiyo kuwa Mashahidi wa Yehova, ijapokuwa bado hatukuwa tumepata kukutana na Shahidi yeyote. Tangu mwanzoni kabisa, nilikuwa nikitumia zaidi ya muda wa saa mia moja kila mwezi nikiwaeleza wengine mambo ya ajabu niliyokuwa nimejifunza.

Mmojawapo wa makasisi wa kanisa la Othodoksi la Kigiriki alimwendea meya akimlalamikia juu yetu. Kumbe siku kadhaa awali, bila sisi kujua, Shahidi mmoja mchanga alipata farasi aliyepotea akawarudishia wenyewe. Kwa sababu ya unyoofu huo, meya huyo aliwaheshimu Mashahidi, akakataa kumsikiliza kasisi huyo.

Siku moja mnamo Oktoba 1941, nilipokuwa nikitoa ushahidi sokoni, mtu mmoja alitaja kwamba kuna Shahidi wa Yehova anayeishi katika mji mmoja ulio karibu. Zamani Shahidi huyo aitwaye Christos Triantafillou alikuwa polisi. Nilimtembelea nikapata kujua kwamba alikuwa amekuwa Shahidi tangu mwaka wa 1932. Nilifurahi kama nini aliponipa vichapo vingi vya zamani vya Watch Tower! Vichapo hivyo vilinisaidia sana nifanye maendeleo ya kiroho.

Mnamo 1943, nilionyesha wakfu wangu kwa Mungu kupitia ubatizo wa maji. Kufikia wakati huo nilikuwa nikiongoza mafunzo ya Biblia katika vijiji vitatu vilivyokuwa karibu—Dhravískos, Palaeokomi, na Mavrolofos. Nilikuwa nikitumia kitabu The Harp of God kwenye funzo la Biblia. Hatimaye, nilipata pendeleo la kuona makutaniko manne ya Mashahidi wa Yehova yakianzishwa katika eneo hili.

Kuhubiri Japo Vizuizi

Mnamo 1944, Ugiriki iliwekwa huru kutoka mikononi mwa Ujerumani, na muda fulani baadaye, mawasiliano yalianzishwa na ofisi ya tawi ya Watch Tower Society jijini Athens. Ofisi ya tawi iliniomba nihubiri katika eneo ambako hakuna mtu aliyekuwa amepata kujua ujumbe wa Ufalme. Baada ya kuhamia huko, nilikuwa nikifanya kazi kwenye shamba moja kwa miezi mitatu kisha nihubiri muda wote uliobakia katika mwaka.

Nilibarikiwa mwaka huo kwa sababu mama yangu alibatizwa, na vilevile yule mwanamke mjane pamoja na watoto wake, ila binti yake kitinda mimba, Marianthi, aliyebatizwa mwaka wa 1943 na kuwa mke wangu mpendwa Novemba mwaka huo. Miaka 30 baadaye, mnamo 1974, baba yangu pia akawa Shahidi aliyebatizwa.

Mapema mwaka wa 1945 tulipokea nakala ya kwanza iliyorudufishwa ya Mnara wa Mlinzi kutoka kwenye ofisi ya tawi. Makala yake kuu ilikuwa na kichwa “Enendeni, Mkawafanye Mataifa Yote Kuwa Wanafunzi.” (Mathayo 28:19, The Emphatic Diaglott) Basi mara moja mimi na Marianthi tukaondoka nyumbani tukahubiri katika maeneo ya mbali yaliyo mashariki ya Mto Strymon. Baadaye Mashahidi wengine walijiunga nasi.

Mara nyingi tulitembea miguu mitupu kufikia kijiji kimoja, tukitembea kwa maili nyingi kuvuka mabonde na milima. Tulitembea miguu mitupu ili tuhifadhi viatu vyetu kwa sababu kama vingalikwisha, hatungaliweza kupata viatu vingine. Katika miaka ya 1946 hadi 1949, vita ya wenyewe kwa wenyewe ilikuwa imekumba Ugiriki, na ilikuwa hatari sana kusafiri. Ilikuwa kawaida kuona maiti zilizotapakaa barabarani.

Badala ya kuvunjika moyo kwa sababu ya magumu hayo, tuliendelea kutumikia kwa bidii. Mara nyingi nilihisi kama mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami, gongo lako na fimbo yako vyanifariji.” (Zaburi 23:4) Katika kipindi hicho mara nyingi tulikuwa tukiondoka nyumbani tusirudi huko kwa majuma kadhaa, na nyakati nyingine nilikuwa nikitumia muda wa saa 250 kwa mwezi katika huduma.

Huduma Yetu Katika Aidhonochori

Kimojawapo cha vijiji tulivyozuru mwaka wa 1946 kilikuwa Aidhonochori, nacho kilikuwa juu mlimani. Tulimkuta mtu mmoja huko ambaye alituambia kwamba kuna watu wawili kijijini humo waliotaka kusikia ujumbe wa Biblia. Lakini, kwa sababu ya kuhofu majirani wake, mtu huyo hakutaka kutuonyesha wanakoishi. Hata hivyo, tulipata nyumba za watu hao, tukakaribishwa. Na kwa dakika chache tu sebule ikajaa watu pomoni! Wao walikuwa ama watu wa ukoo ama marafiki wa karibu. Nilishangaa sana kuona umakini wao walipokuwa wameketi wakitusikiliza. Upesi tukapata kujua kwamba wao walikuwa wakingoja kwa hamu kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova, lakini wakati Ujerumani ilipotwaa eneo hilo, hakukuwa na Mashahidi. Upendezi wao ulichochewa na nini?

Watu hao wawili wenye familia walikuwa mashuhuri katika chama cha Ukomunisti cha eneo hilo, nao walikuwa wakiwafundisha watu dhana za Kikomunisti. Lakini wakapata kitabu kiitwacho Government, kilichochapishwa na Watch Tower Society. Walipokisoma kitabu hicho, wao walisadiki kwamba tumaini la pekee la serikali kamilifu na yenye uadilifu ni Ufalme wa Mungu.

Tukaketi kuongea na watu hao na marafiki zao hadi usiku wa manane. Waliridhishwa kabisa na majibu yenye kutegemea Biblia kwa maswali yao. Lakini, kumbe upesi baadaye Wakomunisti wa kijiji hicho wakapanga njama ya kuniua kwa sababu waliniona kuwa niliwageuza viongozi wao wa zamani kuacha Ukomunisti. Ikatukia kwamba miongoni mwa watu waliohudhuria usiku huo wa kwanza alikuwa mtu yule aliyeniambia juu ya watu waliopendezwa katika kijiji hicho. Hatimaye alifanya maendeleo kupata ujuzi wa Biblia, akabatizwa, na baadaye akawa mzee Mkristo.

Mnyanyaso Mkatili

Muda mfupi baada ya kukutana na wale watu ambao zamani walikuwa Wakomunisti, polisi wawili waliingia kwa kishindo kwenye nyumba tulimokuwa tukiongoza mkutano. Walitukamata sisi tukiwa wanne huku wakitutisha kwa bunduki, wakatupeleka kwenye kituo cha polisi. Huko, luteni mmoja wa polisi, ambaye alikuwa rafiki ya makasisi wa Othodoksi ya Kigiriki, alitushutumu sana. Hatimaye akauliza, “Sijui niwafanyie nini?”

“Acha tuwaonyeshe cha mtema kuni!” wale polisi waliokuwa wamesimama nyuma yetu wakasema kwa pamoja.

Tayari ilikuwa usiku sana. Polisi hao wakatufungia kwenye chumba cha chini kisha wakaenda kwenye baa iliyokuwa ujiranini. Walipokuwa wamelewa chakari, wakarudi na nikatolewa kutoka chumba cha chini.

Nilipoona hali yao, nikatambua kwamba wangeweza kuniua wakati wowote. Basi nikasali kwa Mungu anipe nguvu ya kuvumilia chochote ambacho wangenifanyia. Walichukua fimbo na kama nilivyosimulia mwanzoni, wakaanza kupiga nyayo zangu. Baadaye wakaanza kunipiga mwili wote kisha wakanitupa tena kwenye chumba cha chini. Kisha wakamtoa mwingine, wakaanza kumpiga.

Wakati uo huo, nilitumia fursa hiyo kuwatayarisha wale Mashahidi wengine wawili wachanga wakabiliane na jaribu lililokuwa mbele yao. Lakini polisi hao wakaamua kunirudisha kwenye chumba cha juu. Walinivua nguo, na watano wakanipiga kwa muda wa saa moja, wakinikanyaga-kanyaga kichwa kwa viatu vyao vya majeshi. Kisha wakanitupa kwenye chumba cha chini ambako nilipoteza fahamu kwa muda wa saa 12.

Hatimaye tulipoachiliwa, familia moja katika kijiji hicho ilituandalia mahali pa kulala usiku huo na kututunza. Siku iliyofuata, tuliondoka, tukarudi nyumbani. Tulikuwa hoi sana kutokana na mapigo hayo hivi kwamba safari hiyo, ambayo kwa kawaida huchukua muda wa saa mbili, ilituchukua muda wa saa nane. Mwili wangu ulivimba sana kwa sababu ya mapigo hayo hivi kwamba Marianthi karibu ashindwe kunitambua.

Ukuzi Japo Upinzani

Mwaka wa 1949, vita ya wenyewe kwa wenyewe ilipokuwa ikiendelea, tulihamia Thessalonica. Nilipewa mgawo wa kutumikia nikiwa msaidizi wa mtumishi wa kutaniko katika mojawapo ya makutaniko manne ya jijini. Baada ya mwaka mmoja kutaniko lilikua sana hivi kwamba tukafanyiza kutaniko jingine, nikapewa mgawo wa kuwa mtumishi wa kutaniko hilo, au mwangalizi-msimamizi. Mwaka mmoja baadaye hilo kutaniko jipya likakua kwa karibu mara mbili, na kutaniko jingine tena likafanyizwa!

Wapinzani walikasirishwa na ukuzi wa Mashahidi wa Yehova katika Thessalonica. Siku moja mwaka wa 1952 niliporudi nyumbani kutoka kazini, nilipata nyumba yetu imeteketezwa kabisa. Marianthi aliponea chupuchupu. Kwenye mkutano usiku huo, ilibidi tueleze ni kwa nini tulihudhuria mikutano kwa mavazi machafu—tulikuwa tumepoteza kila kitu. Ndugu na dada zetu Wakristo walituhurumia sana na kututegemeza.

Mwaka wa 1961, nilipewa mgawo wa kazi ya kusafiri, tukizuru makutaniko tofauti-tofauti kila juma ili kuwaimarisha ndugu kiroho. Kwa miaka 27 iliyofuata, mimi na Marianthi tulizuru mizunguko na wilaya katika Makedonia, Thrace, na Thessaly. Japo mke wangu mpendwa Marianthi alikuwa karibu kipofu tangu mwaka wa 1948, kwa ujasiri ametumikia pamoja nami, akivumilia majaribu mengi ya imani. Yeye pia alikamatwa, akapelekwa mahakamani, na kufungwa mara nyingi. Kisha afya yake ikaanza kudhoofika, akafa mwaka wa 1988 baada ya kupambana na kansa kwa muda mrefu.

Mwaka uo huo, niliwekwa rasmi nitumikie nikiwa painia wa pekee katika Thessalonica. Sasa, baada ya zaidi ya miaka 56 ya kumtumikia Yehova, bado naweza kujitahidi na kushiriki katika sehemu zote za huduma. Nyakati nyingine, nilikuwa nikiongoza mafunzo 20 ya Biblia na watu wanaopendezwa kila juma.

Nimejifunza kwamba kweli tumo mwanzoni mwa programu kubwa ya ufundishaji ambayo itaendelea hadi ulimwengu mpya wa Yehova na kuendelea kwa miaka elfu moja. Lakini, nahisi kwamba huu si wakati wa kupunguza mwendo, wa kutochukua mambo kwa uzito, au wa kuridhisha tamaa zetu za kimwili. Namshukuru Mungu kwa kunisaidia kuweka ahadi ambayo nilitoa mwanzoni kwa sababu kwa kweli Yehova astahili ujitoaji wetu na utumishi wa nafsi yote.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikitoa hotuba wakati tulipigwa marufuku kuhubiri

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na mke wangu, Marianthi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki