Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 10/1 kur. 26-27
  • Vitendawili na Kusudi la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vitendawili na Kusudi la Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vitendawili vya Biblia Vimejaa Tele
  • Kufumbua Siri Takatifu
  • Kufumbua “Misemo Isiyoeleweka Vizuri”
  • Kuitazama Nuru
  • Pata Hekima na Ukubali Nidhamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • ‘Ee Mungu, Utume Nuru Yako’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kitabu Cha Mithali—Kimejaa Hekima Katika Maneno Machache
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Siri Ambayo Wakristo Hawathubutu Kuweka!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 10/1 kur. 26-27

Vitendawili na Kusudi la Mungu

MTU asipojua jibu, hilo linakuwa chemsha bongo; lakini mtu ajuapo jibu, basi si chemsha bongo. Twazungumzia nini? Kitendawili.

Katika jamii za leo ambazo hufuatia mambo halisi, watu wana mwelekeo wa kuona kutega vitendawili kuwa michezo ya watoto, lakini katika nyakati za kale kitendawili kilikuwa “jaribio la hekima,” chasema The Interpreter’s Dictionary of the Bible.—Linganisha Mithali 1:5, 6.

Badala ya Yehova kusema mapenzi yake au kusudi lake kwa lugha rahisi, nyakati nyingine ameficha kimakusudi maneno yake ya kiunabii, akitumia ufananisho, “misemo isiyoeleweka vizuri” ya kimafumbo, au vitendawili vyenye kutatanisha. (Zaburi 78:2, King James Version; Hesabu 12:8, The Emphasized Bible) Hata ingawa neno la Kiebrania linalomaanisha kitendawili limetumiwa mara 17 tu katika Biblia, Maandiko yamejaa tele vitendawili na mithali.

Vitendawili vya Biblia Vimejaa Tele

Inasemekana kwamba Mfalme Solomoni aliweza kutegua hata maswali yenye kutatanisha zaidi, au vitendawili, aliyoulizwa. (1 Wafalme 10:1, kielezi cha chini cha New World Translation of Holy Scriptures With References) Bila shaka aliweza kuyatatua kwa sababu ya hekima aliyopewa na Mungu. Ikiwa zile ripoti za wanahistoria wa kale zinazosema kwamba pindi moja Mfalme Hiramu wa Tiro alimshinda Solomoni katika shindano la kutega vitendawili ni kweli, yaelekea jambo hilo lilitukia baada ya Solomoni kupoteza roho ya Yehova kwa sababu ya kuasi. Mwamuzi Samsoni vilevile alipenda sana kutega vitendawili. Pindi moja, akiwa amepewa uwezo na roho takatifu, kitendawili kilimwezesha kuwaogofya maadui wa Mungu.—Waamuzi 14:12-19.

Hata hivyo, vitendawili vingi vya Biblia vinahusika moja kwa moja na makusudi ya Yehova. Kwa mfano, fikiria Mwanzo 3:15. Unabii huo, ambao ndio msingi wa kichwa kikuu cha Biblia, wenyewe ni fumbo la aina fulani, “siri takatifu.” (Waroma 16:25, 26) Mbali na kupewa maono na ufunuo upitao uwezo wa wanadamu, mtume Paulo pia aliona sehemu fulani za kusudi la Mungu katika “njia isiyo ya waziwazi,” au kihalisi, kwa “maneno yasiyoeleweka kwa urahisi.” (1 Wakorintho 13:12; 2 Wakorintho 12:1-4) Lakini vipi juu ya makisio mengi kuhusu nambari ya fumbo la hayawani mwitu—“mia sita sitini na sita”—inayotajwa kwa ghafula na bila ufafanuzi kwenye Ufunuo 13:18? Ni nani awezaye kuvitegua vitendawili hivyo vya Mungu, navyo vina kusudi gani?

Kufumbua Siri Takatifu

Kwa wengi wetu, uwezo wa kuona ndio hisi muhimu zaidi kati ya hisi zetu tano. Lakini bila nuru, hatungeweza kuona. Tungekuwa kama kipofu. Ndivyo ilivyo na akili ya mwanadamu. Ina uwezo wa kustaajabisha wa kulinganisha mambo, kusababu, na basi kufumbua mafumbo. Lakini, mengi zaidi yanahitajika ili kufumbua siri takatifu. Ingawa wengine wanaweza kutegua vitendawili vinavyotegwa katika Biblia, ni Mtungaji wake pekee, Yehova, Mungu wa nuru, awezaye kufumbua maana aliyokusudia ya vitendawili hivyo.—1 Yohana 1:5.

Kwa kusikitisha, watu huwa na kiburi mno ama wenye kujitegemea mno wasimngoje Yehova atoe majibu. Kwa kuvutiwa na mafumbo, kuna wale waliotafuta majibu nje ya Neno la Mungu ili kuchochea akili zao tu wala si kutafuta kweli hasa. Kwa mfano, mambo ya mafumbo ya Kiyahudi katika Cabala yalifikiria umuhimu wa kimizungu wa tarakimu na herufi za alfabeti ya Kiebrania. Kwa upande mwingine, Waagnosti wa karne ya pili walitumia Maandiko ya Kiebrania na Kigiriki katika jitihada za kufumbua kama yana maana za siri.

Lakini kutafuta huko kuliwaingiza zaidi katika desturi au ushirikina wa kipagani na kuwatenga mbali na ukweli wa Mungu. ‘Ikiwa ulimwengu umejaa maovu,’ Waagnosti wakasababu, ‘basi Muumba wake, Yahweh, hawezi kuwa Mungu mzuri.’ Je, huo ndio mkataa bora ambao wangeweza kuufikia? Mwanadamu ana akili ndogo kama nini! Si ajabu kwamba mtume Paulo alionya vikali katika barua zake alipokuwa akipinga mawazo ya uasi ambayo yaliendelezwa na mafarakano ya Kiagnosti: “Msiyapite mambo ambayo yameandikwa”!—1 Wakorintho 4:6.

Kufumbua “Misemo Isiyoeleweka Vizuri”

Lakini, kwa nini Mungu wa nuru atumie “misemo isiyoeleweka vizuri”? Vitendawili vyenyewe huyajaribu mawazo ya mtu na uwezo wake wa kufikiri. Basi, vikiwa vimenyunyizwa hapa na pale kama vikolezo vitamu kwenye chakula, nyakati nyingine vilitumiwa kuamsha tu upendezi wa wasikilizaji au kukazia ujumbe unaowasilishwa. Katika hali hizo, ufafanuzi ulitolewa punde tu baadaye.—Ezekieli 17:1-18; Mathayo 18:23-35.

Yehova hutoa hekima kwa wingi lakini haitoi kamwe kiholela. (Yakobo 1:5-8) Ebu ona kitabu cha Mithali, ambacho ni mkusanyo uliopuliziwa wa misemo mingi yenye mafumbo ambayo wengine huenda wakaiona kuwa vitendawili. Inachukua muda kuielewa na kuitafakari. Lakini ni watu wangapi ambao wako tayari kufanya jitihada hiyo? Ni wale tu walio tayari kuchimba ndio wanaoweza kupata hekima ya misemo hiyo.—Mithali 2:1-5.

Vilevile Yesu alitumia vielezi ili kufichua mtazamo wa moyoni wa wasikilizaji wake. Umati ulimsonga. Ukafurahia hadithi zake. Ukapenda miujiza yake. Lakini ni wangapi waliokuwa tayari kubadili maisha yao ili wamfuate? Walikuwa tofauti kama nini na wanafunzi wa Yesu, ambao walijaribu tena na tena kuelewa mafundisho ya Yesu, wakajikana kwa hiari ili wawe wafuasi wake! —Mathayo 13:10-23, 34, 35; 16:24; Yohana 16:25, 29.

Kuitazama Nuru

Kitabu kimoja chasema kwamba, “yaonekana upendezi katika vitendawili walingana na vipindi vya kuamka kiakili.” Leo, tuna pendeleo kubwa sana la kuishi katika wakati ambapo ‘nuru imewazukia’ watu wa Mungu. (Zaburi 97:11; Danieli 12:4, 9) Je, twaweza kumngoja Yehova kwa subira ili afunue makusudi yake kulingana na ratiba yake? Jambo la maana zaidi, je, sisi huchukua hatua bila kukawia kubadili maisha yetu tunapofahamu jinsi ya kujipatanisha kikamili zaidi na kusudi la Mungu lililofunuliwa? (Zaburi 1:1-3; Yakobo 1:22-25) Ikiwa ndivyo, Yehova atabariki jitihada zetu, ili kwamba kama vile miwani hurekebisha kutoona vizuri, roho takatifu itatusaidia tuone vizuri sana kusudi la Mungu katika jicho la akili yetu, na kuboresha mwono wetu wa kiroho.— 1 Wakorintho 2:7, 9, 10.

Kwa kweli, vitendawili vya Kimaandiko humtukuza Yehova kuwa ‘Mfunuaji wa siri.’ (Danieli 2:28, 29) Isitoshe, yeye pia ni Mchunguzaji wa mioyo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Basi tusishangae kujua kwamba nuru ya kweli ya kimungu imekuwa ikifunuliwa hatua kwa hatua. (Mithali 4:18; Waroma 16:25, 26) Badala ya kutafuta kujua mambo ya ndani sana ya Mungu kupitia mambo ya kimafumbo au hekima duni ya mwanadamu, ambayo inaweza kutokeza tu ubatili, na tumtegemee Yehova Mungu tukiwa na uhakika atuonyeshe nuru ya kweli ya “misemo yake isiyoeleweka vizuri,” akijulisha makusudi yake ya ajabu kwa watumishi waaminifu katika wakati wake uliowekwa rasmi. —Amosi 3:7; Mathayo 24:25-27.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Biblia Hebraica Stuttgartensia, Deutsche Bibelgesellschaft Stuttgart

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki