Kitabu Cha Mithali—Kimejaa Hekima Katika Maneno Machache
JE! UNA maisha yasiyokuwa na matatizo na kukata tamaa? Ni wachache wanaoweza kusema ndiyo. Na mara nyingi jitihada za kusuluhisha matatizo hushindwa, na kuacha watu wakiwa katika matatizo mabaya zaidi kuliko hali zao za kwanza. Je! kuna chanzo cha mashauri ambacho watu wanaweza kutegemea wapate kufanya mambo yawe nafuu (afadhali)?
Kuna chanzo kizuri sana cha uongozi kama huo katika kitabu cha Biblia cha Mithali. Ijapokuwa kiliandikwa katika Mashariki ya Kati zaidi ya miaka 2,500 iliyopita, maneno hayo machache ya hekima ya Mithali yanapasa watu wote na yangali ni ya kisasa.
Biblia inaonyesha kwamba sehemu kubwa ya mithali ilitokana na Mfalme Sulemani. (Mit. 1:1; 10:1; 25:1) Ingawa maandishi ya Kimaandiko hayasemi moja kwa moja kwamba Sulemani aliziandika, yanaonyesha sana kwamba alifanya hivyo. Yanasema kwamba alizungumza maelfu ya mithali na kwamba ‘alitafakari, akatafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi.’—1 Fal. 4:32; Mhu. 12:9.
Namna ya usemi katika kitabu hicho cha Biblia ni mashairi ya Kiebrania ambayo si vifungu vyenye maneno yenye kutamkwa kwa sauti inayofanana bali mawazo yenye kufanana. Mara nyingi sana mistari inayofanana inatofautisha, kama ilivyo katika Mithali 10:28, Inayosema hivi: “Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha; bali kutaraji kwa wasio haki kutapotea.” Katika nyinginezo, semi zenye kufanana zinaonyesha jambo lile lile, kama ilivyo katika maneno ya Mithali 18:15: “Moyo wa mwenye [ufahamu] hupata maarifa; na sikio la mwenye hekima hutafuta maarifa.”
KUSUDI KUU
Kusudi la kitabu cha Mithali linaelezwa mwanzoni mwake kabisa, ambapo tunasoma hivi: “Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli. Kujua hekima na adabu; kutambua maneno na ufahamu [“maneno yenye maana ya ndani-ndani,” The Jerusalem Bible] kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili. Kuwapa wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari.”—Mit. 1:1-4.
Kitabu cha Mithali kinaelekeza mashauri mengi kwa vijana, watu ‘wasio na ujuzi’ (NW) ambao mioyo yao inaingiwa na kila namna ya uvutano na ambao wanakengeushwa kwa urahisi. Lazima wapate kuthamini “hekima,” ambayo inatia ndani kuona mambo kama yalivyo hasa na kujua namna ya kutumia maarifa hayo. Vilevile, “adabu” ni ya lazima, kama kitu cha mtu mwenyewe kujizuia na kama adhabu inayotolewa na wengine.—Mit. 1:1-4; 2:7, 10-13; 4:1, 5-7, 13.
Mithali hizo zinatoa msaada wa pekee wa kusitawisha uwezo wa akili katika njia inayofaa. Kuna vitia-moyo vingi vya kupata ufahamu na “werevu,” yaani, ujuzi na kufanya maamuzi mazuri katika sehemu zote za maisha. (Mit. 1:4; 8:5) Elimu hiyo haimaliziki kamwe. “Mwenye hekima [atasikiliza] na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia. Kufahamu mithali na kitendawili, na maneno ya wenye hekima na mafumbo yao.” (Mit. 1:5, 6) Mara nyingi mithali za Kibiblia zinakuwa kama misemo migumu kufahamika na kama ‘vitendawili,’ vyenye kufadhaisha, semi zenye mafumbo zinazohitaji kufumbuliwa. Ili kuzifahamu inachukua wakati na kutafakari. Hekima nyingi ya Mithali inapatikana na wale tu walio na nia ya kuitafuta sana. Jambo hilo linaonekana wazi katika maneno haya ya Mithali 2:1-5:
“Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate ufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate kufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyosititika; ndipo utakapofahamu kumcha [Yehova], na kupata kumjua Mungu.”
Ebu tuchunguze mifano kadha wa kadha ya mashauri yenye hekima yanayopatikana katika kitabu cha Mithali.
MAMBO ANAYOCHUKIA MUNGU
Watu wanaotaka kujua yaliyo haki na yasiyo haki wanaelekeana na maoni mengi yenye kuvuruga yaliyo tofauti. Mithali zinaweza kusaidia kuondoa mvurugo huo. Kwa mfano, katika mistari minne tu mifupi inayofuata, twajifunza juu ya maoni fulani ya akili na matendo yanayofanana nayo ambayo Mungu anachukia:
“Kuna vitu sita anavyovichukia [Yehova]; naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”—Mit. 6:16-19.
Kuzidisha namba kwa ile inayofuata iliyo kubwa zaidi kunatumiwa mara nyingi na waandikaji wa Biblia. (Ayubu 5:19; 33:29; Mit. 30:15, 16, 18, 19, 21-31; Isa. 17:6; Amosi 1:3, 6, 9, 11, 13; 2:1, 4, 6) Katika Mithali 6:16-19, namba hizo hazipaswi kufahamika kwa njia halisi, kama kwamba ni kusema Mungu anachukia vitu sita au saba peke yake. Sehemu hizo saba ni za msingi nazo zatia ndani namna zote za matendo mabaya. Ya kwanza sita yanakaza fikira juu ya sehemu tatu za mabaya—katika kufikiri (“macho yenye kiburi,” “moyo uwazao mawazo mabaya”), katika kusema (“shahidi wa uongo,” “apandaye mbegu za fitina”) na katika kutenda (“mikono imwagayo damu isiyo na hatia,” “miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu”). Mwenye kuchukiza sana ni mtu wa saba anayetajwa. Anapendezwa sana na kutokeza ugomvi kati ya watu ambao kama asingefanya hivyo wangeishi pamoja kwa amani. Kuongezeka kutoka sita mpaka saba kunadokeza kwamba wanadamu wakati wote wanaongeza matendo yao maovu.
Mtu anapofahamu kwa kuthamini kwamba Muumba huona kiburi, fitina na kusema uongo kwa kadiri ile ile kama umwagaji wa damu na vitendo vingine vya kutumia jeuri, anapaswa kuchochewa afanye mabadiliko ya lazima ndani yake mwenyewe. Matokeo yake yatakuwa uhusiano mzuri zaidi pamoja na wengine na furaha nyingi zaidi katika maisha ya kila siku.
KUSHINDANA NA HASIRA
Kimoja cha visababishaji vya taabu kati ya watu ni hasira isiyozuiliwa. Wengine huenda wakadhani kwamba kufoka kwa hasira ni wonyesho wa nguvu. Walakini Neno la Mungu linasema kinyume kabisa cha jambo hilo, kwa kusema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” (Mit. 16:32) Ingawa mashujaa wanaoteka mji wanaonyesha ujasiri mwingi, kuzuia hasira ya mtu kunahitaji nguvu na ujasiri mwingi zaidi.
Mtu anawezaje kufanya maendeleo ya kuzuia hasira yake? Mithali inatoa maagizo haya mazuri:
“Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi? wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi; usije ukajifunza njia zake; na kujipatia nafsi yako mtego.”—Mit. 22:24, 25.
“Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.”—Mit. 15:1.
“Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; basi acheni ugomvi kabla haujafurika.”—Mit. 17:14.
Semi zote hizo zinatia moyo kukimbia hali zenye kutokeza hasira mara tu inapoanza. Sababu yenyewe inatajwa vizuri katika maneno haya yanayofuata: “Ikiwa umefanya kipumbavu kwa kujikuza; au ikiwa umewaza mabaya [“iwapo umetunga hila,” An American Translation], basi weka mkono wako juu ya kinywa chako. Kwa maana kupiga maziwa huleta siagi; na kupiga pua hutokeza damu; kadhalika kuchochea hasira hutokeza ugomvi.”—Mit. 30:32, 33.
Pindi fulani watu wote huwa na maelekeo ya kipumbavu ya kujikuza. Huenda wakadai wengine mambo yasiyofaa au pengine kusema au kufanya jambo la kuudhi. Nyakati kama hizo mtu anapaswa ‘kuweka mkono juu ya kinywa,’ akizuia maneno mengine au matendo mengine yanayoweza kumkasirisha zaidi yeye aliyeudhika. Kama vile tu siagi inavyohitaji kupigwa-pigwa na sikuzote ili pua itokwe na damu inahitaji kufinywa, ugomvi uliositawi kabisa hutokea wakati tu watu wanaachilia maoni yenye hasira na kuendelea kuchocheana kwenye hasira.
EPUKA UVIVU
Kitabu cha Mithali kinasifu kazi ya bidii na hakitii moyo uvivu. Mwandikaji huyo aliyeongozwa na Mungu anaandika hivi: “Mtu mvivu husema, Simba yuko nje; nitauawa katika njia kuu.” (Mit. 22:13) Ili aepuke kufanya kazi mtu mvivu anabuni visababu vya kuwazia tu kama vile kudai kwamba simba ameingia mjini naye huenda akamwua akienda nje. Mithali nyingine tatu zinakazia namna mtu asiyekuwa na nia ya kufanya kazi anavyoleta matokeo juu yake mwenyewe na juu ya wengine:
“Mtu mvivu anajionyesha kuwa anatamani, bali nafsi yake haina kitu. Walakini, nafsi za wenye juhudi zitanoneshwa.”—Mit. 13:4, NW.
“Mtu mvivu hataki kulima wakati wa baridi; hivyo wakati wa mavuno ataomba, hana kitu.”—Mit. 20:4.
“Kama siki menoni, na kama moshi machoni, ndivyo alivyo mtu mvivu kwao wamtumao.”—Mit. 20:26.
UHITAJI WA KUTIWA ADABU
Kwa kuwa wanadamu hawajakamilika nao wana maelekeo ya kufuata njia yenye vizuizi vichache zaidi, watu wengi hukataa kutiwa adabu. Kitabu cha Mithali kinatia moyo nia tofauti na hiyo, kikisema hivi: “Elekeza moyo wako kusikiliza [kutiwa adabu] tega masikio yako kusikia maneno ya maarifa.” (Mit, 23:12) Hapa adabu inamaanisha kujizuia na kusahihishwa na wengine. Mara nyingi inatolewa kupitia kwa “maneno ya maarifa,” yaani, maneno yanayotokana na mtu mwenye maarifa nayo yanatumika kuwaarifu wengine, Nyakati nyingine, hata hivyo, adabu inapaswa kuwa imara zaidi kuliko maneno matupu. “Machubuko ya fimbo husafisha uovu, na mapigo hufikilia ndani ya mtima.” (Mit. 20:30) Inapokubaliwa katika roho inayofaa, adabu iliyo imara si kwamba inazuia vitendo vibaya tu bali inachochea watu wafanye mbadiliko yo kindani kwa faida.
Kwa habari ya watoto kutiwa adabu na wazazi, twasoma hivi: “Usimnyime mtoto wako [adabu]; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na [Kaburi].” (Mit. 23:13, 14) “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi mapema.”—Mit. 13:24.
Bila shaka, adabu inapaswa kutolewa kwa kujiweza wala si kwa kutoka kwa hasira. Wala haitakuwa lazima kutumia adhabu ya kupiga nyakati zote. Katika visa vingi, maneno machache tu ya shauri la hekima yanatosha. “[Kemeo] hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu, kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu.”—Mit. 17:10.
EPUKA UASHERATI
Kitabu cha Mithali ‘kinalaani uasherati. Fikiria, kwa mfano, maneno haya ya kuonya:
“Maana maagizo hayo ni taa, na sheria hiyo ni nuru, na maonyo ya [kumtia adabu] mtu ni njia ya uzima. Yakulinde na mwanamke mwovu, asikupate, na kukuponya na ubembelezi wa mgeni. Usiutamani uzuri wake moyoni mwako; wala usikubali akunase kwa kope za macho yake. Maana kwa malaya mtu hutiwa katika hali ya kuhitaji kipande cha mkate; na kahaba humwinda mtu anase nafsi yake iliyo ya thamani.” (Mit. 6:23-26)
Wale wanaofanya vitendo vya uasherati mara nyingi wanaingia katika umaskini. Watu wanaotafuta anasa ya ngono pamoja na “malaya” au wale ambao kwa njia yo yote wanafanya uasherati wanaweza kulipa bei kwa kupoteza afya wanapoangukia maradhi yenye kuumiza na yenye kulemaza ya kisonono na kaswende. Hatari hiyo ni kubwa hata zaidi wakati mtu anapofanya ngono na mtu asiyekuwa mwenzi wake wa ndoa. Mzinzi anahatirisha ‘nafsi iliyo na thamani,’ au uzima, wa mwenzi wake wa haramu. Kuhusu jambo hilo, mwandikaji huyo aliyeongozwa na Mungu anaongeza hivi:
“Je! mtu aweza kutia moto kifuani pake, na nguo zake zisiteketezwe? Je! mtu aweza kukanyaga makaa ya moto, na nyayo zake zisiungue? Ndivyo alivyo aingiaye kwa mke wa jirani yake; kila mtu amgusaye huyo atakuwa na hatia. . . . Mtu aziniye na mwanamke [amepungukiwa na moyo]; afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake. Atapata jeraha na kuvunjwa heshima; wala fedheha yake haitafutika. Maana wivu ni ghadhabu ya mtu; wala hatahurumia siku ya kujilipiza kisasi. Hatakubali ukombozi uwao wote; wala hatakuwa radhi, ujapomlipa vitu vingi.” (Mit. 6:27-35)
Kukosa uaminifu katika ndoa kwaweza kutokeza umizo lisiloweza kuondoleka kwa watu na jamaa zenye kuhusika.
JIHADHARI NA ‘MAISHA MATAMU’
Katika historia yote jambo kubwa la kufuatia maishani kwa watu wengi limekuwa ni kutafuta anasa. Ingawa Biblia haikatazi kuwa na wakati mzuri, inakazia uhitaji wa kupata maoni yaliyosawazika ya matendo ya anasa. “Je! umeona asali? Kula kadiri ya kukutosha; usije ukashiba na kuitapika.” (Mit. 25:16) Kama vile tu kula kupita kiasi asali ya halisi kunavyoweza kumfanya mtu awe mgonjwa mwilini, ndivyo kujitia kupita kiasi katika ‘maisha matamu’ ya anasa kunavyoweza kuongoza kwenye ugonjwa wa kimwili na vilevile wa kiroho. Pamoja na hayo, kukazia anasa kupita kiasi mara nyingi kunaongoza kwenye hali zenye msiba za umaskini. “Mtu apendaye anasa atakuwa maskini; apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri.”—Mit. 21:17.
Namna gani jitihada ya kukusanya mali? Kitabu cha Mithali kinaonya kwamba utajiri hautegemeki nao unaweza kutokomea (kupotea) ghafula. Twasoma hivi: “Usijitaabishe ili kupata utajiri; acha kuzitegemea akili zako mwenyewe: Je! utavikazia [mali] macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.” (Mit. 23:4, 5) Kwa kuwa utajiri mwingi unaweza kupotezwa haraka kwa ajili ya kuangaliwa vibaya au hali zisizotangulia kuonwa, Maandiko yanaonya watu waelekeze jitihada zao kwenye jambo lenye kutegemeka zaidi kuliko kufuatia utajiri. Angalia sana shauri hili:
“Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; na kuwaangalia sana ng’ombe zako. Kwa maana mali haziwi za milele; na taji je! yadumu tangu kizazi hata kizazi? Manyasi huchukuliwa, na majani mabichi huonekana, na maboga ya milimani hukusanyika. Wana-kondoo hufaa kwa mavazi yako; na mbuzi ni thamani ya shamba: Tena yatakuwapo maziwa ya mbuzi, ya kukutosha kwa chakula chako, na chakula cha watu wa nyumbani mwako, na posho la vijakazi vyako.”—Mit. 27:23-27.
Wala mali (“hazina”) wala cheo cha umaarufu (“taji”) havitoi uhakikisho wa usalama wa kweli. Wakati, jitihada na fedha zinazotumiwa katika mapatano ya biashara mara nyingi hupotezwa kwa ajili ya kuanguka kwa mpango huo. Matukio yasiyotazamiwa yanaweza kufanya mali na cheo cha heshima vitokomee ghafula. Kwa upande mwingine, jitihada zinazotolewa za kuangalia wanyama wa kufugwa hazitokezi upungufu, bali sikuzote hutokeza ongezeko kwa mwenyewe. Mungu hutoa bure “manyasi” ya kulishia wanyama wa kufugwa. Katika historia yote ya kibinadamu uangalizi wa bidii wa wanyama wa kufugwa wakati wote umejionyesha kuwa wenye kutegemeka zaidi kama njia ya kupata chakula, mavazi mshahara kuliko kuwa na utajiri wala umaarufu. Ndiyo sababu ya shauri hili lenye hekima: “Fanya bidii kujua hali ya makundi yako.” Kanuni iliyoko katika maneno haya inaweza kutumiwa kwa habari ya kazi ya bidii katika jambo lo lote lile lenye kutegemeka kufanya kazi leo.
Kitabu cha Mithali, ingawa kiliandikwa maelfu mengi ya miaka iliyopita, kina uongozi usiozeeka kwa watu walio hai leo. Yasome kwa ukawaida maneno hayo yaliyoongozwa na Mungu. Tafakari masomo yake. Ingawa kila mithali ina maneno machache tu, hekima yake nyingi yaweza kufanya maisha yako yawe salama na yenye furaha kwa umilele.