Matendo Yetu Yanakuwa na Matokeo Juu ya Kundi
Katika Mithali 11:11 twasoma hivi: “Mji hutukuzwa kwa mbaraka wa mwenye haki; bali mji hupinduliwa kwa kinywa cha mwovu.”
Wenyeji wa mji wanaofuata mwendo wa unyofu husaidia sana kuleta amani pamoja na hali njema nao wanajenga wengine, nao mji husitawi. Wale wanaosema mambo mabaya yenye kuvunjiana heshima wanaleta msukosuko, ukosefu wa furaha, kutokuwa na umoja na taabu. Hasa inakuwa hivyo ikiwa watu hao wana vyeo vyenye mamlaka. Mji wa namna hiyo huwa na ghasia, upotovu nayo hali ya kiadili na ya kiuchumi huendelea kuharibika.
Kanuni hiyo ambayo imetajwa hapo inahusu (inatumika) kati ya mashahidi Wakristo wa Yehova, kwa kuwa ‘wanaishi’ katika makundi yao yaliyo kama miji. Kundi ambalo watu wa kiroho wanaofikiria Maandiko huwa na uvutano, linajikuta likiwa na furaha, lenye kutenda, likiwasaidia washiriki wake na kumletea Mungu sifa. Mungu anafurahi wa kulisitawisha kiroho kundi hilo. Lakini wale wasioridhika, wasiotosheka, wanaotafuta makosa na kusema kwa uchungu juu ya namna mambo yanavyofanywa wanakuwa kama “shina la uchungu,” (“shina lenye sumu,” NW) liwezalo kutambaa na kuwaambukiza wengine ambao hapo kwanza hawakuwa wamehusika. (Ebr. 12:15) Mara nyingi hao wenye matata huwa wanataka kupata mamlaka na kujulikana zaidi. Wanaleta migawanyiko kwa kuchochea uvumi wakisema kwamba mambo yanakawia kufanywa, au kwamba hakuna haki ya hukumu, au kwamba kuna chuki ya kikabila, na vivyo hivyo, katika kundi au kati ya wazee.
Mithali nyingine inashughulika na kanuni hiyo kwa habari ya mtu mmoja mmoja, ikisema hivi: “Ulimi wenye utulivu ni mti wa uzima, bali ukiwa na upotovu unaleta kuvunjika katika roho.” (Mit. 15:4, NW) Ulimi unaosema vizuri na kusema kweli na kwa upole, kwa fadhili na kwa unyenyekevu huwa na matokeo mazuri juu ya msikilizaji. Unamwinua na kumjenga kiroho, na kwa hiyo, unasaidia sana kuleta afya njema ya kiroho kundini mwote. Bali ulimi wenye upotovu unaumiza na kuvunja roho ya wasikilizaji, pasipo kuwapa mawazo yo yote mema na yenye kuwajenga ya kuwasaidia waendelee katika njia ya uzima. Ina kuwa kama kwamba, ulimi mbaya unaelekea kuleta uharibifu wa kiroho na kifo kwa wengine.