Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ijwyp makala 84
  • Kwa Nini Sikuzote Ninasema Jambo Lisilofaa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Sikuzote Ninasema Jambo Lisilofaa?
  • Vijana Huuliza
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa nini ninasema jambo lisilofaa?
  • Kudhibiti ulimi
  • Onyesha Upendo na Heshima kwa Kuzuia Ulimi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kwa Sababu Gani Yakupasa Uzuie Ulimi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Tumia Vizuri Nguvu za Ulimi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Kwa Nini Nilisema Jambo Hilo?
    Amkeni!—2012
Pata Habari Zaidi
Vijana Huuliza
ijwyp makala 84
Kijana akijaribu kuyakamata maneno ambayo yametoka mdomoni mwake

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Sikuzote Ninasema Jambo Lisilofaa?

“Wakati mwingine ninaweza kudhibiti ulimi wangu, lakini wakati mwingine inaonekana ni kana kwamba mdomo unasema bila msaada wowote wa ubongo!”​—James.

“Ninapokuwa na mkazo ninazungumza bila kufikiri, na nisipokuwa na mkazo ninazungumza kupita kiasi. Hivyo, kwa ujumla ninakosea kila wakati.”​—Marie.

Biblia inasema kwamba: “Ulimi ni . . . moto” na, “Jinsi moto mdogo unavyoweza kuteketeza msitu mkubwa!” (Yakobo 3:​5, 6) Je, maneno yako yanakusababishia matatizo mara nyingi? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia.

  • Kwa nini ninasema jambo lisilofaa?

  • Kudhibiti ulimi

  • Vijana wenzako wanasema nini

Kwa nini ninasema jambo lisilofaa?

Kutokamilika. Biblia inasema hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Sisi si wakamilifu na kwa sababu hiyo ni rahisi kwetu kusema jambo lisilofaa tunapozungumza.

“Kwa kuwa nina ubongo na ulimi ambao si mkamilifu, itakuwa upumbavu kwangu kusema kwamba ninaweza kuvidhibiti kikamili vitu hivyo.”​—Anna.

Kuzungumza kupita kiasi. Biblia inasema hivi: “Maneno yanapokuwa mengi, makosa hayawezi kuepukwa.” (Methali 10:19) Watu wanaozungumza kupita kiasi​—na kusikiliza kidogo​—wanaweza kuwaudhi wengine kwa urahisi kwa kusema mambo yasiyofaa.

“Kwa kawaida watu wenye akili zaidi si wale wanaozungumza sana. Yesu alikuwa mtu mwenye akili zaidi kuwahi kuishi duniani, lakini wakati mwingine alikaa kimya.”​—Julia.

Kejeli. Biblia inasema hivi: “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga.” (Methali 12:18) Mfano mmoja wa maneno yanayosemwa bila kufikiri ni kejeli​—maneno yanayoumiza yanayowashushia hadhi wengine. Watu wanaokejeli wanaweza kusema, “Nilikuwa nikitania tu!” Lakini kuwaaibisha wengine si jambo la kuchekesha. Biblia inatuambia tuache kabisa “matusi, na mambo yote yanayodhuru.”​—Waefeso 4:​31.

“Mimi ni mcheshi sana, na ninapenda vichekesho​—sifa zinazoongoza kwenye kejeli, ambazo mara nyingi zinafanya niingie kwenye matatizo.”​—Oksana.

Kijana akijaribu kurudisha dawa ya meno kwenye tyubu

Ukisema jambo huwezi kulirudisha mdomoni kama usivyoweza kurudisha dawa ya meno uliyoifinya kutoka kwenye tyubu yake

Kudhibiti ulimi

Si rahisi kujifunza kudhibiti ulimi wako, lakini kanuni za Biblia zinaweza kusaidia. Kwa mfano, fikiria kanuni zifuatazo.

“Zungumza moyoni mwako, . . . na unyamaze kimya.”​—Zaburi 4:4.

Wakati mwingine jambo bora ni kukaa kimya. Kijana anayeitwa Laura anasema hivi: “Jinsi ninavyohisi ninapokuwa na hasira ni tofauti na jinsi ninavyohisi baada ya hasira kwisha. Ninapotulia, kwa kawaida ninashukuru kwamba sikusema jambo nililotaka kusema.” Hata kutulia kwa sekunde chache, kunaweza kukuzuia usizungumze jambo lisilofaa.

“Je, sikio halipimi maneno kama ulimi unavyoonja chakula?”​—Ayubu 12:11.

Unaweza kujiepusha na huzuni kubwa ikiwa utapima jambo unalotaka kusema kwa kufikiria maswali haya:

  • Ni jambo la kweli? Je, ni jambo la fadhili? Je, ni lazima niliseme?​—Waroma 14:19.

  • Nitahisije mtu mwingine akiniambia jambo hilo?​—Mathayo 7:​12.

  • Nitakuwa nimeonyesha ninaheshimu maoni yake?​—Waroma 12:10.

  • Je, hapa ni mahali panapofaa kusema jambo hili?​—Mhubiri 3:7.

“Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.”​—Wafilipi 2:3.

Ushauri huo utakusaidia kufikiria sifa nzuri za wengine, ambazo zitakusaidia kudhibiti ulimi wako na kufikiri kabla ya kusema. Hata ikiwa ni kuchelewa mno na umeshasema jambo fulani lenye kuumiza, unyenyekevu utakusaidia kuomba msamaha​—na utafanya hivyo haraka iwezekanavyo! (Mathayo 5:​23, 24) Kisha azimia kudhibiti ulimi wako kwa kiwango kikubwa zaidi.

Vijana wenzako wanasema nini

Taylor

“Ninapokuwa na msisimuko wa mazungumzo, kwa kawaida mimi husema mambo ambayo ninajutia baadaye. Lakini nikitulia hata kwa sekunde kumi na kufikiria jinsi maneno yangu yatakavyowaathiri wengine au jinsi yatakavyochangia jambo fulani lenye kujenga katika mazungumzo, hapo ninaweza kuudhibiti ulimi wangu vizuri zaidi.”​—Taylor.

Brandon

“Mtu akisema jambo linalokuudhi, ni vizuri kufikiria hali. Mara nyingi, yanakuwa maneno anayoropoka tu na yanaweza kusahaulika. Nyakati nyingine, kile kilichosemwa kinaweza kuwa si cha haki kwa maoni yako, lakini huenda kina ukweli fulani ndani yake. Mawasiliano mazuri na matulivu ni njia ya kusuluhisha hali hizo.”​—Brandon.

Jessica

“Ni rahisi kuepuka kusema maneno ya kuumiza ikiwa hufikirii mambo hayo. Wakati mwingine tunahitaji kufanyia kazi jinsi tunavyoona hali na mtazamo wetu kuelekea watu. Ikiwa tutafanya hivyo, hatutashawishiwa kwa urahisi kusema jambo ambalo linaweza kuwaumiza wengine.”​—Jessica.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki