Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 9/1 kur. 25-28
  • Kumtumikia Mungu Mwenye Kutumainika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Mungu Mwenye Kutumainika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukua Katika Ugiriki
  • Katikati ya Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe
  • Kupata Tumaini Lenye Kutegemeka
  • Kukamatwa na Kufungwa Gerezani
  • Kushtakiwa kwa Ajili ya Kugeuza Imani ya Watu
  • Kifo cha Mwana Wangu
  • Kusaidia Wengine Wamtumaini Yehova
  • Urithi Mkubwa
  • Kuazimia Kumtumaini Yehova
  • Kutumikia Chini ya Mkono Wenye Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Nilipata Utajiri wa Kweli Katika Australia
    Amkeni!—1994
  • Kumpa Yehova Kile Anachostahili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 9/1 kur. 25-28

Kumtumikia Mungu Mwenye Kutumainika

Kama ilivyosimuliwa na Kimon Progakis

Ilikuwa jioni yenye baridi sana katika 1955. Mke wangu, Giannoula, nami tukaanza kuwa na wasiwasi kwa sababu mwana wetu George, mwenye umri wa miaka 18, hakurudi kutoka kioski alikokuwa akifanya kazi. Bila kutazamia, polisi mmoja alibisha kwenye mlango wetu. “Mwana wenu aligongwa na gari alipokuwa akiendesha baiskeli kurudi nyumbani,” yeye akasema, “na amekufa.” Kisha akainama mbele na kunong’ona hivi: “Watakuambia ilikuwa aksidenti, lakini kwa kweli, aliuawa kimakusudi.” Kasisi wa hapo na viongozi fulani wa kikosi cha kijeshi walikuwa wamekula njama ya kumuua.

KATIKA miaka hiyo, Ugiriki ilipokuwa ikirudia hali nzuri baada ya nyakati za mapambano na ugumu, lilikuwa jambo la hatari kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilijionea mamlaka ya Kanisa Othodoksi la Kigiriki na mashirika ya vikosi vya kijeshi kwa sababu kwa zaidi ya miaka 15, nilikuwa nimekuwa mshiriki wayo mwenye bidii. Acha nikuambie juu ya mambo yaliyoongoza kwenye msiba huo katika familia yetu zaidi ya miaka 40 iliyopita.

Kukua Katika Ugiriki

Nilizaliwa mwaka wa 1902 kwa familia yenye utajiri katika kijiji kidogo karibu na mji wa Chalcis, Ugiriki. Baba yangu alikuwa mwenye bidii katika siasa za mahali hapo, na washiriki wa familia yetu walikuwa wachaji wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Nikawa msomaji mwenye bidii wa vitabu vya kisiasa na vya kidini wakati ambapo walio wengi wa wananchi wenzangu hawakujua kusoma wala kuandika.

Umaskini na udhalimu ulioenea sana mwanzoni mwa karne ya 20 ulitokeza ndani yangu hali ya kutamani ulimwengu wenye hali bora. Nilifikiri kwamba dini, ingeweza kuboresha hali ya kuhuzunisha ya wananchi wenzangu. Kwa sababu ya mwelekeo wangu wa kidini, viongozi wa kijiji changu walitoa shauri kwamba niwe padre wa kanisa Othodoksi la Kigiriki katika jumuiya yetu. Hata hivyo, ingawa nilikuwa nimetembelea makao mengi ya watawa wa kiume na nilikuwa na mazungumzo marefu pamoja na maaskofu na abati, sikuhisi nikiwa tayari wala kuwa na nia ya kukubali daraka la aina hiyo.

Katikati ya Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe

Miaka kadhaa baadaye, katika Aprili 1941, Ugiriki ilishambuliwa na kutwaliwa na majeshi ya Nazi. Hilo lilianzisha kipindi chenye huzuni cha machinjo, njaa kuu, hali ya kunyimwa mahitaji, na kuteseka kwingi sana kwa binadamu. Harakati ya ukinzani yenye nguvu ilitokea, na nikajiunga na kimojawapo vikundi vya wapiganaji wa kuvizia vilivyopigana na wale washambulizi Wanazi. Likiwa tokeo, nyumba yangu iliteketezwa mara kadhaa, nilipigwa risasi, na mavuno yangu yaliharibiwa. Mapema katika 1943 familia yangu nami hatukuwa na la kufanya ila kukimbilia ile milima ya mawe-mawe. Tuliendelea kukaa huko mpaka mwisho wa kutwaliwa kwa nchi na majeshi ya Ujerumani katika Oktoba 1944.

Mapambano ya wenyewe kwa wenyewe ya kisiasa na ya kiraia yalitokea baada ya Wajerumani kuondoka. Kikundi changu cha ukinzani cha wapiganaji wa kuvizia kikawa mojawapo majeshi makuu yaliyopigana katika vita ya wenyewe kwa wenyewe. Ingawa matazamio ya Kikomunisti ya haki, usawa, na uandamani yalinivutia, hatimaye uhalisi wa hali ukaniacha nikiwa nimekata tamaa kabisa. Kwa kuwa nilikuwa na wadhifa wa juu katika kikundi hicho, nilijionea kwamba mamlaka huelekea kuwafisidi watu. Zijapokuwa nadharia na matazamio zilizoonekana kuwa bora, ubinafsi na kutokamilika kunaharibu makusudi ya kisiasa hata yawe ni mazuri kama nini.

Jambo lililonishangaza hasa ni kwamba kwenye pande mbalimbali za pambano hilo la wenyewe kwa wenyewe, makasisi wa kanisa Othodoksi walikuwa wakitumia silaha kuwaua watu wa dini yao wenyewe! Nilijiuliza, ‘Makasisi hawa wanaweza kusemaje kwamba wanamwakilisha Yesu Kristo, aliyeonya: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga”?’—Mathayo 26:52.

Katika vita ya wenyewe kwa wenyewe, mwaka wa 1946, nilikuwa nikijificha karibu na mji wa Lamia, katikati ya Ugiriki. Nguo zangu zilikuwa zimechakaa kabisa, kwa hiyo nikaamua kujigeuza sura na kwenda kwa mshoni jijini ili anishonee nguo mpya. Mjadala mkali ulikuwa ukiendelea nilipowasili, na upesi nikajipata nikisema, si juu ya siasa, bali juu ya jambo nililopenda tangu zamani, dini. Kwa sababu ya kuona maoni yangu yenye maarifa, wasikilizaji walidokeza kwamba niseme na ‘profesa fulani wa theolojia.’ Wakaenda kumleta mara moja.

Kupata Tumaini Lenye Kutegemeka

Katika mazungumzo yaliyofuata, “profesa” huyo aliniuliza ni nini kilichokuwa msingi wa itikadi zangu. “Baba Watakatifu na Sinodi za Maaskofu,” nikajibu. Badala ya kunipinga, alifungua Biblia yake ndogo kwenye Mathayo 23:9, 10, akaniomba nisome maneno ya Yesu: “Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.”

Hilo lilinielimisha! Nilihisi kwamba mtu huyu alikuwa akisema kweli. Alipojitambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nilimwomba baadhi ya fasihi ili nisome. Aliniletea kitabu Light, ambacho ni ufafanuzi wa kitabu cha Biblia cha Ufunuo, kisha nikarudi nacho hadi maficho yangu. Kwa muda mrefu sana, wale hayawani-mwitu wanaorejezewa katika Ufunuo walikuwa wamekuwa fumbo kwangu, lakini sasa nilijifunza kwamba hao waliwakilisha mashirika ya kisiasa yaliyoko katika karne yetu ya 20. Nikaanza kuelewa kwamba Biblia ina maana yenye kutumika kwa nyakati zetu na kwamba napaswa kujifunza hiyo na kupatanisha maisha yangu kulingana na kweli zayo.

Kukamatwa na Kufungwa Gerezani

Muda mfupi baadaye, askari-jeshi waliingia maficho yangu kwa mshindo wakanikamata. Nilitupwa katika seli ya chini ya ngome. Kwa kuwa nilikuwa nimekuwa mhalifu aliyetafutwa sana kwa muda fulani, nilitazamia kuuawa. Humo, katika seli yangu, nilitembelewa na yule Shahidi aliyekuwa amesema nami kwa mara ya kwanza. Alinitia moyo kumtumaini Yehova kikamili, jambo ambalo nilifanya. Nilihukumiwa kifungo cha uhamisho cha miezi sita kwenye kisiwa cha Ikaria cha Bahari Aegea.

Mara nilipowasili, nilijitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova, si Mkomunisti. Wengine waliokuwa wamejifunza kweli za Biblia walitumwa uhamishoni huko pia, kwa hiyo niliwatafuta, na tulijifunza Biblia pamoja kwa ukawaida. Walinisaidia kupata ujuzi zaidi kutoka Maandiko na uelewevu bora juu ya Mungu wetu mwenye kutumainika, Yehova.

Katika 1947, kifungo changu cha gerezani kilipoisha, niliitwa kwenye ofisi ya wakili wa mashtaka wa umma. Aliniambia kwamba alivutiwa na mwenendo wangu, akasema kwamba ningeweza kutumia jina lake iwapo ningetumwa uhamishoni tena. Nilipowasili Athene, ambako familia yangu ilikuwa imehamia nilipokuwa uhamishoni, nilianza kushirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova na upesi nikabatizwa, ukiwa ufananisho wa wakfu wangu kwa Yehova.

Kushtakiwa kwa Ajili ya Kugeuza Imani ya Watu

Kwa miongo kadhaa, Ugiriki iliwashtaki Mashahidi wa Yehova chini ya sheria zilizopitishwa katika 1938 na 1939 zilizokataa kugeuzwa imani kwa watu. Hivyo, kutoka 1938 hadi 1992, kulikuwa na visa 19,147 vya kukamatwa kwa Mashahidi katika Ugiriki, na mahakama zilitoa hukumu mbalimbali zilizojumlika kuwa miaka 753, ambayo 593 ilitumika kihalisi. Mimi binafsi, nilikamatwa zaidi ya mara 40 kwa sababu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, na kwa ujumla nilikaa miezi 27 katika magereza mbalimbali.

Wakati mmoja nilikamatwa kwa sababu ya barua niliyokuwa nimemwandikia kasisi fulani wa kanisa Othodoksi la Kigiriki katika Chalcis. Katika 1955, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalikuwa yamesihiwa sana kutuma kwa makasisi wote kijitabu Christendom or Christianity—Which One Is “the Light of the World”? Mmoja wa makasisi mwenye cheo cha juu niliyekuwa nimemwandikia alinishtaki mahakamani kwa tendo la kugeuza imani. Wakati wa kesi hiyo, wakili wa Mashahidi na pia yule mwanasheria wa mahali hapo walitoa utetezi wenye ustadi, wakieleza wajibu ambao Wakristo wa kweli wanao wa kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

Hakimu msimamizi wa mahakama alimuuliza yule mwenye cheo cha pili baada ya askofu hivi: “Je, ulisoma ile barua na kile kijitabu?”

“La,” yeye akajibu kwa nguvu, “nilivirarua na kuviondolea mbali mara tu nilipofungua bahasha!”

“Basi waweza kusemaje kwamba mtu huyu alikugeuza imani?” hakimu msimamizi akauliza.

Halafu wakili wetu akataja vielelezo vya maprofesa na wengine waliotolea maktaba za umma vitabu vingi sana. “Je, ungesema kwamba watu hao walijaribu kugeuza imani ya wengine?” akauliza.

Kwa wazi, utendaji huo haukuwa kugeuza imani ya wengine. Nilimshukuru Yehova niliposikia hukumu: “Hakuna hatia.”

Kifo cha Mwana Wangu

Mwana wangu George alisumbuliwa pia daima, hasa kwa uchochezi wa makasisi wa kanisa Othodoksi. Yeye alikamatwa pia mara nyingi sana kwa sababu ya bidii yake ya ujana katika kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Hatimaye, wapinzani wakaamua kumuua na, wakati uleule, kutuma ujumbe wenye kutisha kwa sisi wengine ili tuache kuhubiri.

Yule polisi aliyekuja nyumbani kwetu kuripoti kifo cha George alisema kwamba padre wa mahali hapo wa kanisa Othodoksi la Kigiriki na viongozi fulani wa kikosi cha kijeshi walikuwa wamekula njama ya kumuua mwana wetu. “Aksidenti” hizo zilikuwa kawaida katika nyakati hizo za hatari. Ijapokuwa huzuni ambayo kifo chake kilisababisha, azimio letu la kuendelea kuwa wenye bidii katika kazi ya kuhubiri na kumtumaini Yehova kikamili liliimarishwa tu.

Kusaidia Wengine Wamtumaini Yehova

Katikati ya miaka ya 1960, mke na watoto wangu walikuwa wakipisha miezi ya kiangazi katika kijiji cha pwani cha Skala Oropos, karibu kilometa 50 kutoka Athene. Wakati ule, hakuna Mashahidi walioishi huko, kwa hiyo tuliwatolea majirani ushahidi wa vivi hivi. Wakulima fulani wa huko waliitikia vizuri. Kwa kuwa wanaume walifanya kazi muda mrefu katika mashamba yao wakati wa mchana, tuliongoza mafunzo ya Biblia pamoja nao usiku sana, na baadhi yao wakawa Mashahidi.

Tukiona jinsi Yehova alivyokuwa akibariki jitihada zetu, kwa miaka 15 hivi, tulisafiri kwenda huko kila juma ili kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wale wenye kupendezwa. Watu wapatao 30 tuliojifunza nao huko wamefanya maendeleo kufikia hatua ya ubatizo. Mwanzoni, kikundi cha funzo kilifanyizwa, nami nikapewa mgawo wa kuongoza mikutano. Baadaye hicho kikundi kikawa kutaniko, na leo zaidi ya Mashahidi mia moja kutoka eneo hilo hufanyiza Kutaniko la Malakasa. Twashangilia kwamba wanne kati ya wale tuliowasaidia wanatumikia sasa wakiwa wahudumu wa wakati wote.

Urithi Mkubwa

Upesi baada ya kuweka wakfu maisha yangu kwa Yehova, mke wangu alianza kufanya maendeleo kiroho akabatizwa. Wakati ule mgumu wa mnyanyaso, imani yake iliendelea ikiwa thabiti naye akaendelea akiwa imara na bila kusita katika uaminifu-maadili wake. Hakulalamika kamwe juu ya yale magumu mengi aliyopata kwa sababu ya kufungwa kwangu gerezani mara nyingi.

Miaka hii yote, tuliongoza mafunzo mengi ya Biblia pamoja, naye alisaidia wengi kwa matokeo kwa mfikio wake sahili na wenye idili. Kwa sasa, yeye ana njia ya kupelekea watu wengi sana Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida.

Kwa sababu hasa ya utegemezo wa mwenzi wangu mwenye upendo, watoto wetu watatu walio hai pamoja na familia zao, zinazotia ndani wajukuu sita na vitukuu wanne, wote ni wenye bidii katika utumishi wa Yehova. Ingawa hawajalazimika kukabiliana na mnyanyaso wala upinzani mkali ambao mke wangu na mimi tulikabili, wao wameweka tumaini lao kamili katika Yehova, na wanaendelea kutembea katika njia zake. Itakuwa shangwe kama nini kwetu sote kuunganishwa tena na George wetu mpendwa arudipo katika ufufuo!

Kuazimia Kumtumaini Yehova

Miaka hii yote, nimeona roho ya Yehova ikitenda kazi juu ya watu wake. Tengenezo lake lenye kuelekezwa kwa roho limenisaidia kuona kwamba hatuwezi kuweka tumaini letu katika jitihada za wanadamu. Ahadi zao za kuwa na wakati ujao bora hazina thamani, hizo ni uwongo mtupu tu.—Zaburi 146:3, 4.

Ujapokuwa umri wangu wenye kuongezeka na matatizo mabaya ya afya, macho yangu yamekazwa juu ya uhalisi wa tumaini la Ufalme. Kwa kweli najuta ile miaka niliyotolea dini isiyo ya kweli na nikijaribu kuleta hali bora kupitia njia za kisiasa. Ikiwa ningeishi maisha yangu tena, bila shaka ningeamua tena kumtumikia Yehova, Mungu mwenye kutumainika.

(Majuzi Kimon Progakis alilala katika kifo. Alikuwa na tumaini la kidunia.)

[Picha katika ukurasa wa 26]

Picha ya karibuni ya Kimon na mke wake, Giannoula

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki