Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 11/15 kur. 4-7
  • Namna Malaika Wanavyoweza Kukusaidia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namna Malaika Wanavyoweza Kukusaidia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukutana na Malaika
  • Je, Twapaswa Kuwaomba Malaika Watusaidie?
  • Kumwomba Mungu Atusaidie
  • Malaika na Maadili
  • Malaika Walinzi
  • Ujumbe Ambao Malaika Hubeba
  • Malaika—Jinsi Wanavyohusika Katika Maisha Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Malaika—Je! Wao Wanaathiri Maisha Yako Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Malaika Ni Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 11/15 kur. 4-7

Namna Malaika Wanavyoweza Kukusaidia

NENO la Mungu huthibitisha kuwako kwa malaika. Hilo hutuambia kwamba kuna mamilioni ya viumbe hawa wa kiroho. Mtumishi wa Yehova Mungu Danieli alipata ono la vitu vya kimbingu ambavyo aliandika juu yake hivi: “Maelfu elfu wakamtumikia [Mungu], na elfu kumi mara elfu kumi wakasimama mbele zake.”—Danieli 7:10.

Ona kwamba taarifa ya Danieli hutupatia habari zaidi juu ya malaika kuliko idadi yao tu. Hiyo pia huonyesha kwamba malaika humtumikia Mungu. Wao ni watumishi wake. Kwa kupatana na hilo, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mhimidini BWANA, enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini BWANA, enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.”—Zaburi 103:20, 21.

Biblia pia hueleza kwamba maisha ya malaika hayakuanzia duniani wakiwa wanadamu. Yehova aliwaumba malaika mbinguni hata kabla hajaiumba dunia. Wakati Mungu ‘alipoiweka misingi ya dunia, wana wote wa Mungu walipiga kelele kwa furaha.’—Ayubu 38:4-7.

Malaika ni viumbe wa kiroho—wasioonekana, wenye nguvu, wenye akili. Katika Biblia, neno la Kiebrania mal·ʼakhʹ na neno la Kigiriki agʹge·los yanatafsiriwa “malaika” wakati kiumbe wa kiroho anaporejezewa. Maneno haya hupatikana karibu mara 400 katika Biblia. Yote mawili yana maana moja, yaani, “mjumbe.”

Kukutana na Malaika

Malaika kwa wazi ni wajumbe. Huenda wafahamu simulizi la Biblia juu ya malaika Gabrieli alipomtokea Mariamu. Alimwambia kwamba ijapokuwa alikuwa bikira, angezaa mwana ambaye angeitwa Yesu. (Luka 1:26-33) Malaika mmoja pia aliwatokea wachungaji fulani waliokuwa malishoni. Yeye alitangaza hivi: “Kumezaliwa kwenu leo Mwokozi, ambaye, ni Kristo Bwana.” (Luka 2:8-11) Vivyo hivyo, malaika walipeleka ujumbe kwa Hagari, Abrahamu, Loti, Yakobo, Musa, Gideoni, Yesu na watu wengine wanaorekodiwa katika Biblia.—Mwanzo 16:7-12; 18:1-5, 10; 19:1-3; 32:24-30; Kutoka 3:1, 2; Waamuzi 6:11-22; Luka 22:39-43; Waebrania 13:2.

Ni jambo lifaalo kuangaliwa kwamba, ujumbe wote huo uliopelekwa na malaika, ulipatana na kutimizwa kwa makusudi ya Mungu wala, si makusudi ya wanadamu waliohusika. Malaika waliwatokea wawakilishi wa Mungu, kulingana na mapenzi yake na kwa wakati wake aliouweka. Wanadamu hawakuwaomba msaada.

Je, Twapaswa Kuwaomba Malaika Watusaidie?

Je, ni sawa kuwaomba malaika watusaidie wakati wa taabu? Ikiwa ndivyo, tungependa kujua jina la malaika awezaye kutusaidia kwa njia bora zaidi. Kwa sababu hiyo, vitabu fulani vya kibiashara huorodhesha majina ya kudhaniwa ya malaika wengi pamoja na nyadhifa zao, majina yao ya vyeo, na wajibu wao. Kitabu kimoja huorodhesha kile kinachokiita wale “malaika kumi bora,” wale “malaika wanaojulikana sana katika ulimwengu wa Magharibi.” Pamoja na orodha hiyo kuna lile shauri la kufunga macho yako, kurudia-rudia jina la malaika huyo polepole mara kadhaa, kuvuta pumzi nyingi, kupumua polepole, na “kujiandaa kwa uwezekano wa kuwasiliana na malaika hao.”

Kwa kutofautisha, Biblia hutoa majina mawili tu ya malaika waaminifu wa Mungu, Mikaeli na Gabrieli. (Danieli 12:1; Luka 1:26) Yawezekana, sababu ya kuandaa majina hayo ilikuwa kuonyesha kwamba kila malaika ni mtu halisi wa kiroho wa kipekee mwenye jina, si nguvu fulani tu au kani isiyo na utu.

Ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba malaika fulani walikataa kuwaambia wanadamu majina yao. Yakobo alipomwuliza malaika ajitambulishe kwa jina lake, yeye alikataa kufanya hivyo. (Mwanzo 32:29) Alipoombwa kujitambulisha, malaika aliyekuwa amemtokea Yoshua alisema tu kwamba yeye alikuwa “amiri wa jeshi la BWANA.” (Yoshua 5:14) Wazazi wa Samsoni walipomwuliza malaika fulani jina lake, yeye alisema hivi: “Kwani wewe kuniuliza jina langu, kwa kuwa jina hilo ni la ajabu?” (Waamuzi 13:17, 18) Kwa kutoandaa orodha ya majina ya malaika, Biblia hutulinda dhidi ya kuwapa malaika heshima na ibada isiyostahili. Na jinsi tutakavyoona, hiyo pia haitufundishi tuwaombe watusaidie.

Kumwomba Mungu Atusaidie

Biblia hutuambia yote tunayopaswa kujua juu ya mambo yanayohusu milki ya kiroho. Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha . . . ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Ikiwa Mungu alitaka tujue majina ya malaika wengi, yeye angewafunua hao katika Neno lake, Biblia. Na ikiwa Mungu alitaka kutufundisha namna ya kuwasiliana na malaika na kuzungumza nao katika sala, yeye angeandaa habari hizo katika Maandiko.

Badala ya hivyo, Yesu Kristo alifundisha hivi: “Usalipo ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye katika siri . . . lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.’” (Mathayo 6:6, 9) Maoni ya Kimaandiko ni haya: Hatupaswi kuomba malaika watusaidie au kuwatolea sala, lakini twapaswa kumfikia Muumba wa malaika kwa njia ya sala, Mungu mwenyewe. Jina lake si fumbo, na hakuna haja ya kupata ono ili kulifunua. Ijapokuwa jitihada zimefanywa ili kulificha jina la Mungu, hilo hupatikana katika rekodi ya Biblia zaidi ya mara 7,000. Kwa mfano, ilikuwa kwa kumrejezea Baba wa kimbingu kwamba mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”—Zaburi 83:18.

Yehova si mwenye shughuli mno asiweze kutusikiliza tukimwendea katika sala. Biblia hutuhakikishia hivi: “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

Malaika na Maadili

Kinyume na yale yanayoonyeshwa mara nyingi na vyombo vya habari, malaika hawahukumu watu. Hilo lafaa, kwani malaika hawajaruhusiwa kuwahukumu wanadamu. Yehova ndiye “Hakimu wa wote,” ingawa “amekabidhi kuhukumu kote kwa Mwana,” Yesu Kristo. (Waebrania 12:23; Yohana 5:22) Hata hivyo, lingekuwa kosa kudhani kwamba malaika hawajali namna tunavyoishi maisha yetu. Yesu alisema hivi: “Shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.”—Luka 15:10.

Hata hivyo, malaika si wasimama-kando tu. Nyakati zilizopita, wao walikuwa wafishaji, wakitekeleza hukumu za Mungu. Kwa mfano, Mungu aliwatumia malaika dhidi ya Wamisri wa kale. Kulingana na Zaburi 78:49, “a[li]wapelekea ukali wa hasira yake, ghadhabu, na uchungu, na taabu, kundi la malaika waletao mabaya.” Hali kadhalika, Biblia yaripoti kwamba kwa usiku mmoja malaika mmoja aliwaangamiza askari Waashuri 185,000.—2 Wafalme 19:35.

Vivyo hivyo, wakati ujao, malaika watawaangamiza wale ambao kwa kukataa kujipatanisha na viwango vya Mungu vya uadilifu, hutisha hali njema ya wengine. Yesu atakuja “pamoja na malaika zake wenye nguvu katika moto wenye kuwaka mwali, aletapo kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.”—2 Wathesalonike 1:7, 8.

Hivyo, Maandiko huonyesha kwamba malaika waaminifu wa Mungu hufanya mapenzi yake kwa kutimiza maagizo yake wakishikilia viwango vyake vya haki. Kwa wazi, ikiwa tunataka malaika za Mungu watusaidie, twahitaji kujua mapenzi ya Mungu ni nini na kujitahidi kwa bidii kuyafanya.

Malaika Walinzi

Je, malaika huwajali watu na kuwalinda? Mtume Paulo aliuliza hivi: “Je, wao [malaika] wote si roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuwahudumia wale watakaorithi wokovu?” (Waebrania 1:14) Kwa wazi, jibu la swali la Paulo ni ndiyo.

Kwa sababu ya kukataa kwao kuiinamia sanamu ya dhahabu iliyosimamishwa na Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, wale Waebrania watatu Shadraka, Meshaki, na Abednego walitupwa ndani ya tanuru lenye moto mkali sana. Hata hivyo, watumishi hao waaminifu wa Mungu hawakuchomwa na moto huo. Mfalme alipoangalia ndani ya tanuru, aliona “watu wanne,” akasema kwamba “sura yake yule wa nne [ilikuwa] mfano wa mwana wa miungu.” (Danieli 3:25) Miaka kadhaa baadaye, Danieli alijipata kwenye shimo la simba kwa sababu ya uaminifu wake. Yeye pia hakupatwa na dhara lolote na kutangaza hivi: “Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba.”—Danieli 6:22.

Kutaniko la wafuasi wa Kristo lilipoanzishwa katika karne ya kwanza W.K., malaika walitokea tena, wakiwafungua huru mitume kutoka gerezani. (Matendo 5:17-24; 12:6-12) Na maisha ya Paulo yalipohatarishwa baharini, malaika fulani alimhakikishia kwamba angefika Roma salama.—Matendo 27:13-24.

Watumishi wa siku hizi wa Yehova Mungu wamesadikishwa kabisa kwamba majeshi ya Mungu ya kimalaika wasioonekana ni halisi na wanaweza kulinda, sawa na walivyomlinda Elisha na mtumishi wake. (2 Wafalme 6:15-17) Kwa kweli, “malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.”—Zaburi 34:7; 91:11.

Ujumbe Ambao Malaika Hubeba

Ingawa malaika huhangaikia hali njema ya wale wanaomtumikia Yehova Mungu, wao pia wanahusika katika kuhakikisha kwamba watu wanajifunza juu yake na makusudi yake. Mtume Yohana aliandika hivi: “Nami nikaona malaika mwingine akiruka katika mbingu ya kati, naye alikuwa na habari njema idumuyo milele ili aitangaze kuwa taarifa za mteremo kwa wale wakaao juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu, akisema kwa sauti kubwa: ‘Hofuni Mungu na kumpa utukufu.’”—Ufunuo 14:6, 7.

Je, wewe wataka kujua yaliyomo katika ‘habari njema hii idumuyo milele’? Ikiwa ndivyo, waulize Mashahidi wa Yehova. Wao watafurahi kukujulisha.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Malaika akiruka katika mbingu ya kati anatangaza habari njema idumuyo milele. Je, wataka kujifunza kuihusu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki