Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 4/15 kur. 15-17
  • Je, Unajionyesha Kuwa Mwenye Shukrani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Unajionyesha Kuwa Mwenye Shukrani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Hujionyesha Kuwa Mwenye Shukrani
  • Yesu—Mtu Aliyeonyesha Shukrani Nyingi
  • Mtazamo Wenye Kuchambua wa Shetani
  • Igeni Mungu na Kristo
  • “Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”
    Huduma Yetu ya Ufalme—2008
  • Yehova Ni Mungu Anayethamini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • “Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Ni Nani Mtu wa Maana Zaidi Katika Maisha Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 4/15 kur. 15-17

Je, Unajionyesha Kuwa Mwenye Shukrani?

Kwenye makao fulani ya mishonari yaliyoko Afrika Magharibi, paliishi mbwa aitwaye Teddy. Mtu alipomtupia Teddy kipande cha nyama, alikimeza mara moja, bila hata kufurahia ladha yake wala kukitafuna. Akihemahema kwa kuchomwa na jua la kitropiki, Aijongea atupiwe kipande kingine. Nyama ilipomalizika, aligeuka na kwenda zake.

Teddy hakuonyesha shukrani hata kidogo hata kwa kwa kile alichopata. Hakuna aliyetarajia afanye hivyo. Kwa kuwa alikuwa mbwa tu.

KWA habari ya shukrani, mara nyingi sisi hutarajia wanadamu wafanye mengi zaidi kuliko wanyama. Kwa kawaida sisi hutamaushwa. Watu wengi hunyakua chochote wawezacho kupata maishani na kutafuta kupata zaidi. Jambo hilo pia halishangazi. Biblia ilitabiri kwamba katika siku za mwisho, watu wangekosa kuwa wenye shukrani.—2 Timotheo 3:1, 2.

Hata hivyo, watumishi wa Mungu wana mtazamo tofauti. Wao hutii shauri la mtume Paulo, aliyewaonya waamini wenzake kwa upole hivi: “Jionyesheni wenyewe kuwa wenye shukrani.”—Wakolosai 3:15.

Yehova Hujionyesha Kuwa Mwenye Shukrani

Yehova Mungu huweka kielelezo kikamilifu katika kuonyesha shukrani. Fikiria jinsi aonavyo watumishi wake waaminifu. Paulo alipuliziwa kuwaandikia Wakristo Waebrania hivi: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

Kuna vielelezo vingi vinavyoonyesha shukrani za Yehova kwa watumishi wake waaminifu. Alimbariki Abrahamu kwa kuzidisha uzao wake halisi, hivi kwamba walipata kuwa “kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani.” (Mwanzo 22:17) Kwa kuonyesha shukrani kwa uaminifu wa Yobu alipokuwa akijaribiwa, Yehova alirudisha mali ya Yobu iliyokuwa nyingi, na pia kuizidisha “mara mbili.” (Ayubu 42:10) Kushughulika kwa Yehova na wanadamu katika milenia zote kumethibitisha ukweli wa taarifa hii: “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

Sehemu kuu za utu wa Mungu hutia ndani kuonyesha shukrani na mwelekeo wake wa kuwathawabisha wale wanaotafuta kufanya mapenzi yake. Kutambua jambo hilo ni muhimu kwa imani ya Kikristo. Paulo aliandika hivi: “Bila imani haiwezekani kumpendeza vema, kwa maana amkaribiaye Mungu lazima aamini . . . kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Sote tungehukumiwa adhabu kama Yehova angeonyesha mtazamo mkali, wenye kuchambua. Mtunga-zaburi alitoa hoja hii zamani za kale: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Yehova hakosi kuonyesha shukrani wala si mwenye kuchambua. Yeye huwathamini sana wale wamtumikiao. Yeye hujionyesha kuwa mwenye shukrani.

Yesu—Mtu Aliyeonyesha Shukrani Nyingi

Kwa kudhihirisha kikamilifu sifa za Baba yake wa kimbingu, Yesu Kristo alijionyesha kuwa mwenye shukrani kwa mambo ambayo wengine walifanya kwa imani. Fikiria jambo lililotukia wakati mmoja kwenye hekalu huko Yerusalemu: “Sasa [Yesu] alipotazama juu aliwaona matajiri wakitumbukiza zawadi zao ndani ya masanduku ya hazina. Ndipo akaona mjane fulani mwenye uhitaji akitumbukiza sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana humo, naye akasema: ‘Nawaambia nyinyi kwa kweli, Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, alitumbukiza nyingi kuliko wao wote. Kwa maana wote hawa walizitumbukiza ndani zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani njia yote ya kujipatia riziki aliyokuwa nayo.’”—Luka 21:1-4.

Kwa kuzingatia mambo ya kifedha, mchango huo ulikuwa mdogo, hasa ukilinganishwa na michango ya matajiri. Wengi kati ya waliokuwemo hawangemtia maanani. Hata hivyo, Yesu alimwona mjane huyo. Alifahamu hali zake. Yesu alimwona na kumthamini.

Tukio jingine lilihusisha Maria, mwanamke tajiri. Yesu alipokuwa ameegama kwenye mlo, mwanamke huyo alimmwagia Yesu mafuta yenye marashi kwenye miguu yake na kichwa chake. Wengine walilichambua tendo lake, wakisababu kwamba mafuta hayo yangeweza kuuzwa kisha pesa hizo zitumiwe kusaidia maskini. Yesu aliitikiaje? Yeye alisema: “Mwacheni. Kwa nini mwajaribu kumsumbua? Alifanya kitendo bora kunielekea mimi. Kwa kweli nawaambia nyinyi, Kokote ambako habari njema yahubiriwa katika ulimwengu wote, alilofanya mwanamke huyu hakika litasimuliwa pia kuwa ukumbuko juu yake.”—Marko 14:3-6, 9; Yohana 12:3.

Yesu hakusikitika na kusema kwa kuchambua kwamba hayo mafuta yenye thamani yangetumiwa kwa njia nyingine. Alithamini ukarimu wa Maria katika kuonyesha upendo na imani. Tukio hilo limerekodiwa katika Biblia kuwa ukumbuko wa tendo lake bora. Masimulizi hayo na mengine yaonyesha kwamba Yesu alikuwa mtu aliyeonyesha shukrani nyingi.

Ikiwa wewe ni mtumishi wa Mungu, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu na vilevile Yesu Kristo ni wenye shukrani nyingi kwa jitihada zako za kuendeleza ibada safi. Ujuzi huo hutuvuta kwao na hutuchochea kuwaiga kwa kujithibitisha kuwa wenye shukrani.

Mtazamo Wenye Kuchambua wa Shetani

Sasa acheni tuchunguze kielelezo kimoja cha mtu ambaye hajionyeshi kuwa mwenye shukrani—Shetani Ibilisi. Ukosefu wa shukrani wa Shetani ulimfanya aongoze uasi wenye msiba dhidi ya Mungu.

Akiwa amesitawisha ndani yake mtazamo wenye kuchambua wa kutoridhika, Shetani alianza kuueneza kwa wengine. Fikiria yaliyotukia katika bustani ya Edeni. Yehova alimwumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, akawaweka katika bustani ya kiparadiso, akawaambia: ‘Matunda ya kila mti wa bustani mwaweza kula.’ Kulikuwa na kizuizi kimoja tu. Mungu alisema: ‘Matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya msile, kwa maana siku mtakapokula matunda ya mti huo mtakufa hakika.’—Mwanzo 2:16, 17.

Hata hivyo, punde si punde, Shetani alipinga kustahili kwa Yehova. Kwa kadiri fulani, alitaka kumfanya Hawa akose kuwa mwenye shukrani kwa Yehova sana hivi kwamba angesukumwa kuasi dhidi yake, kama vile Shetani mwenyewe alivyofanya. “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” Shetani akauliza. (Mwanzo 3:1) Jambo hilo lilidokeza wazi kwamba Mungu alikuwa akimnyima Hawa kitu chenye thamani, kitu ambacho kingemfungua macho na kumfanya awe kama Mungu mwenyewe. Badala ya kujionyesha kuwa mwenye shukrani kwa baraka nyingi alizopata kutoka kwa Yehova, Hawa alianza kutamani kilichokatazwa.—Mwanzo 3:5, 6.

Matokeo yenye msiba yanajulikana vizuri. Ingawa alipewa jina Hawa “kwa sababu alilazimika kuwa mama ya kila mwenye kuishi,” kwa maana nyingine, yeye alipata kuwa mama ya kila mwenye kufa. Kuanzia Adamu wanadamu wote wamerithi dhambi itokezayo kifo.—Mwanzo 3:20, NW; Waroma 5:12.

Igeni Mungu na Kristo

Fikiria tofauti iliyopo kati ya Shetani na Yesu. Shetani anafafanuliwa kuwa “mshtaki wa ndugu zetu . . . , ambaye huwashtaki wao mchana na usiku mbele ya Mungu wetu.” (Ufunuo 12:10) Yesu “aweza pia kuokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.”—Waebrania 7:25.

Shetani huwashtaki watumishi wa Mungu. Yesu huwathamini na kuwaombea. Wakiwa waigaji wa Kristo, Wakristo wapaswa kujitahidi kutafuta sifa nzuri kati ya mmoja na mwenzake, wakishukuru na kuthaminiana. Kwa kufanya hivyo, wanajionyesha kuwa wenye shukrani kwa yule ambaye huweka kielelezo bora kabisa katika kuonyesha shukrani, Yehova Mungu.—1 Wakorintho 11:1.

[Picha katitka ukurasa wa 17]

Yesu alionyesha shukrani kwa tendo bora la Maria

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki