“Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”
1 Yesu alipowaponya watu kumi wenye ukoma, ni mmoja tu aliyerudi na kumshukuru. Yesu aliuliza hivi: “Wale kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa?” (Luka 17:11-19) Ni jambo la maana kama nini kwetu kuonyesha uthamini na kujionyesha kuwa wenye shukrani kwa ajili ya kila tuzo kamilifu na kila zawadi njema tunayopewa na Baba yetu wa mbinguni mwenye ukarimu na mwenye upendo, Yehova Mungu!—Kol. 3:15; Yak. 1:17.
2 Tunapaswa kujionyesha kuwa wenye shukrani kwa ajili ya mambo gani? Tunathamini fidia, zawadi kubwa zaidi ambayo Mungu amewapa wanadamu. (Yoh. 3:16) Pia, tunamshukuru Yehova kwa kutuvuta kwake. (Yoh. 6:44) Tunapaswa pia kushukuru kwa sababu ya umoja wetu wa Kikristo. (Zab. 133:1-3) Labda unaweza kufikiria zawadi nyingine nyingi kutoka kwa Yehova. Hatutaki kamwe kuwa kama Waisraeli wasio na shukrani ambao walisahau kazi ambazo Yehova alifanya kwa ajili yao!—Zab. 106:12, 13.
3 Onyesha Shukrani: Ingawa huenda wale wote kumi wenye ukoma walithamini mambo ambayo Yesu aliwatendea, ni mmoja tu aliyejionyesha kuwa mwenye shukrani. (Luka 17:15) Vivyo hivyo, tunaonyesha uthamini kwa kushiriki kwa bidii katika huduma. Ikiwa tunathamini kikweli mambo yote ambayo Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo amefanya, mioyo yetu itatuchochea kuiga upendo na ukarimu wake kwa kuwaeleza wengine kumhusu. (Luka 6:45) Kadiri tunavyowaeleza wengine kuhusu ‘kazi za ajabu za Yehova na mawazo yake kutuelekea,’ ndivyo tutakavyozidi kumpenda na kumthamini.—Zab. 40:5.
4 Wachochee Wengine Waonyeshe Shukrani: Tunapaswa kutafuta njia za kuwasaidia watoto wetu na wanafunzi wetu wa Biblia kusitawisha uthamini. Wazazi wana nafasi nyingi za kufanya hivyo, kama vile wanapofurahia kutazama uumbaji wa Yehova pamoja na watoto wao. (Rom. 1:20) Tunapoongoza funzo la Biblia, tunaweza kumuuliza mwanafunzi wetu, “Jambo hili linatufundisha nini kuhusu utu wa Yehova?” Kadiri uthamini wa mwanafunzi unavyoendelea kukua, ndivyo atakavyozidi kumpenda Mungu na kuazimia hata zaidi kumpendeza.
5 Katika hizi siku za mwisho, watu wengi hawana uthamini wala shukrani. (2 Tim. 3:1, 2) Inampendeza Yehova kama nini kuwaona watumishi wake waliojitoa kwake wakionyesha shukrani kwa kushiriki kwa bidii katika huduma!—Yak. 1:22-25.