Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 6/1 kur. 20-23
  • Kutimiza Ahadi Yangu ya Kumtumikia Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutimiza Ahadi Yangu ya Kumtumikia Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukulia Lithuania
  • Kutimiza Ahadi Yangu
  • Majaribu ya Mapema ya Imani
  • Marufuku na Kukamatwa Tena
  • Kudumisha Imani Gerezani
  • Kurudia Huduma ya Wakati Wote
  • Kurekebisha Hali Zifaane na Mahitaji
  • Nilichochewa na Uaminifu-Mshikamanifu wa Familia Yangu kwa Mungu
    Amkeni!—1998
  • Kumngojea Yehova kwa Subira Tangu Ujana Wangu na Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Imani Katika Mungu Ilinitegemeza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 6/1 kur. 20-23

Kutimiza Ahadi Yangu ya Kumtumikia Mungu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA FRANZ GUDLIKIES

Ni askari wanne tu katika kikosi changu cha askari zaidi ya mia moja, waliobaki hai. Nikiwa nimekabiliwa na kifo, nilipiga magoti, nikamwahidi Mungu, ‘Nikinusurika vita hii, nitakutumikia sikuzote.’

NILITOA ahadi hiyo miaka 54 iliyopita, katika Aprili 1945, nilipokuwa askari katika jeshi la Ujerumani. Ilikuwa muda mfupi kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kwisha, nalo jeshi la Sovieti lilikuwa likishambulia kwa nguvu zote likielekea Berlin. Askari wetu walikuwa karibu na mji wa Seelow kwenye Mto Oder, kilometa zinazopungua 65 kutoka Berlin. Hapo, tulipigwa kwa mizinga mfululizo, nacho kikosi changu kilikuwa kikiangamizwa.

Ndipo, kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nilipolia na kusali kwa Mungu. Nilikumbuka andiko la Biblia ambalo mama yangu mwenye kumhofu Mungu alitaja mara nyingi: “Ukaniite siku ya mateso; nitakuokoa, na wewe utanitukuza.” (Zaburi 50:15) Nikiwa katika mahandaki huku nikihofia uhai wangu, nilitolea Mungu ahadi iliyotajwa juu. Niliweza kuitimizaje? Na nilipataje kuwa askari wa jeshi la Ujerumani?

Kukulia Lithuania

Katika mwaka wa 1918, wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Lithuania ilijitangazia uhuru na kuanzisha mfumo wa serikali ya kidemokrasia. Nilizaliwa mwaka wa 1925 katika wilaya ya Memel (Klaipėda) karibu na Bahari ya Baltiki. Wilaya hiyo ilikuwa imetoka tu kuunganishwa na Lithuania mwaka mmoja kabla sijazaliwa.

Maisha yangu ya utotoni, pamoja na ya dada zangu watano, yalikuwa yenye furaha. Baba alikuwa kama rafiki wa karibu, akifanya mambo sikuzote pamoja nasi watoto. Wazazi wetu walikuwa washiriki wa Kanisa la Kievanjeli, lakini hawakuwa wakihudhuria mikutano ya ibada kwa sababu Mama alichukizwa na unafiki wa kasisi wa kanisa hilo. Hata hivyo, yeye alimpenda Mungu na Neno lake, Biblia, ambalo alisoma kwa bidii.

Katika mwaka wa 1939, Ujerumani ilinyakua sehemu ya Lithuania ambapo tuliishi. Kisha nikaitwa kutumikia katika jeshi la Ujerumani mapema mwaka wa 1943. Nilijeruhiwa katika mojawapo ya mapigano, lakini baada ya kupona majeraha, nikarudi kwenye Eneo la Mashariki la Mapigano. Kufikia wakati huu, mkondo wa vita ulikuwa umebadilika nao Wajerumani walikuwa wakilikimbia jeshi la Sovieti. Basi, ni wakati huo nilipoponea chupuchupu kuuawa, kama inavyosimuliwa katika utangulizi.

Kutimiza Ahadi Yangu

Wakati wa vita, wazazi wangu walihamia Oschatz, Ujerumani, kusini-mashariki ya Leipzig. Baada ya vita, ilikuwa vigumu sana kujua walikokuwa. Lakini tulifurahi kama nini tulipokutana tena hatimaye! Muda mfupi baadaye, katika Aprili 1947, niliandamana na Mama kwenda kusikiliza hotuba ya watu wote iliyotolewa na Max Schubert, mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mama aliamini kwamba alikuwa amepata dini ya kweli, nami pia nikaamini vivyo hivyo baada ya kuhudhuria mikutano michache.

Muda mfupi baadaye, Mama alianguka kutoka ngazini, na kupata majeraha yaliyomwua miezi kadhaa baadaye. Akiwa hospitalini kabla ya kifo chake, alinitia moyo kwa uchangamfu: “Nimesali mara nyingi kwamba angalau mmoja wa watoto wangu aweze kumjua Mungu. Sasa ninaona kwamba sala zangu zimejibiwa, na ninaweza kufa kwa amani.” Ninatazamia kwa hamu kama nini wakati ambapo Mama atafufuka na kujua kwamba sala zake zilitimizwa!—Yohana 5:28.

Katika Agosti 8, 1947, miezi minne tu baada ya kusikiliza hotuba ya Ndugu Schubert, nilibatizwa kwenye kusanyiko lililokuwa Leipzig, kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu. Hatimaye, nilikuwa ninachukua hatua za kutimiza ahadi yangu kwa Mungu. Punde si punde nikawa painia, kama wanavyoitwa wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Wakati huo kulikuwa mapainia wapatao 400 walioishi katika ile ambayo baadaye ilikuja kuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani, au Ujerumani Mashariki.

Majaribu ya Mapema ya Imani

Jirani mmoja huko Oschatz alijaribu kunivutia nipendezwe na Umaksi, akinitolea fursa ya kupata elimu katika chuo kikuu ambayo ingedhaminiwa na Serikali ikiwa ningejiunga na Chama cha Muungano wa Kisoshalisti cha Ujerumani (SED). Nilikataa toleo hilo, kama vile Yesu alivyokataa toleo la Shetani.—Mathayo 4:8-10.

Siku moja katika Aprili 1949, polisi wawili walikuja mahali nilipofanya kazi, wakataka niandamane nao. Nilipelekwa kwenye ofisi ya mahali hapo ya shirika la ujasusi la Sovieti ambapo nilishtakiwa kwa kuwafanyia ujasusi wabepari wa Magharibi. Walisema ningeweza kuthibitisha kutokuwa na hatia, kwa kuendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba lakini niripoti kwao mtu yeyote aliyezungumza isivyofaa kuhusu Muungano wa Sovieti au SED, au yeyote aliyezuru mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilipokataa kushirikiana nao, nilifungiwa ndani ya seli. Baadaye, nilipelekwa mbele ya ile iliyoonekana kuwa mahakama ya kijeshi. Hukumu yangu: Miaka 15 ya kazi ngumu Siberia!

Nilibaki mtulivu, na hilo likawavutia maofisa hao. Ndipo wakaniambia kwamba hukumu yangu ingeendelea kutumika, lakini ingetosha kwangu kuripoti mara moja kwa juma hadi wakati ambapo ningekuwa tayari kushirikiana nao. Kwa kuwa nilitaka mashauri kutoka kwa Mashahidi waliokomaa zaidi, nilisafiri hadi Magdeburg, mahali ilipokuwa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society wakati huo. Safari hiyo haikuwa rahisi kwa sababu nilikuwa nikipelelezwa. Ernst Wauer, aliyekuwa akifanya kazi katika Idara ya Sheria Magdeburg, aliniambia hivi: “Pambana na utashinda. Ridhiana na utashindwa. Tulijifunza hayo kwenye kambi za mateso.”a Shauri hilo lilinisaidia kutimiza ahadi yangu ya kumtumikia Mungu.

Marufuku na Kukamatwa Tena

Nilipendekezwa kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye katika Julai 1950. Hata hivyo, polisi walivamia makao yetu huko Magdeburg Agosti 30, na kazi yetu ya kuhubiri ikapigwa marufuku. Kwa hiyo, mgawo wangu ukabadilishwa. Mimi na Paul Hirschberger tungefanya kazi na makutaniko yapatayo 50, tukikaa siku mbili au tatu na kila kutaniko, huku tukiwasaidia akina ndugu wawe na mpango wa kuendelea na huduma yao chini ya marufuku. Katika miezi iliyofuata, nilinusurika kukamatwa na polisi mara sita!

Mtu fulani alikuwa amejipenyeza katika kutaniko moja naye alitusaliti kwa Stasi, Shirika la Usalama la Serikali. Kwa hiyo, katika Julai 1951, mimi na Paul tukakamatwa barabarani na wanaume watano wakiwa na bunduki tayari kufyatua risasi. Tunapokumbuka, tungeweza kuona kwamba hatukuwa tumelitegemea tengenezo la Yehova kadiri tulivyopaswa. Tulikuwa tumeshauriwa na ndugu zetu wa zamani zaidi tusisafiri pamoja wakati wowote. Kujitumaini kupita kiasi kulifanya tukose uhuru wetu! Isitoshe, hatukuwa tumezungumzia kimbele yale ambayo tungesema tukikamatwa.

Nikiwa peke yangu katika seli, nilimsihi Yehova kwa machozi anisaidie nisiweze kusaliti ndugu zangu au kuridhiana imani yangu. Baada ya kulala, niliamshwa ghafula na sauti ya rafiki yangu Paul. Juu tu ya seli yangu palikuwa chumba ambapo alikuwa akihojiwa na Stasi. Kwa kuwa usiku huo ulikuwa wenye joto na unyevunyevu, mlango wa roshani uliachwa wazi, na kwa umbali ningeweza kusikia kila kitu. Baadaye, nilipohojiwa, nilitoa majibu yaleyale, jambo lililoshangaza maofisa hao. Nilikumbuka tena na tena andiko la Biblia ambalo Mama alipenda sana, “Ukaniite siku ya mateso; nitakuokoa, na wewe utanitukuza,” na kutiwa moyo sana.—Zaburi 50:15.

Baada ya kuhojiwa, mimi na Paul tulikaa kwa muda wa miezi mitano katika kizuizi kabla ya kushtakiwa kwenye gereza la Stasi la Halle na baadaye Magdeburg. Nikiwa Magdeburg, mara kwa mara nilitupia jicho majengo ya ofisi yetu yaliyokuwa yamefungwa wakati huo. Laiti ningelikuwa nikifanya kazi huko badala ya kuwa gerezani! Hukumu yetu ilitangazwa katika Februari 1952: “Miaka 10 gerezani na miaka 20 ya kutokuwa na haki za raia.”

Kudumisha Imani Gerezani

Mashahidi wa Yehova waliokuwa wamehukumiwa kifungo cha angalau miaka kumi walivaa kitambulisho cha pekee kwa muda fulani wakiwa gerezani. Utepe mwekundu ulishonelewa kwenye mguu mmoja wa suruali na mkono mmoja wa jaketi. Pia, kipande kidogo cha mviringo cha kadibodi nyekundu kiliwekwa upande wa nje wa mlango wa seli yetu ili kutahadharisha walinzi kwamba tulikuwa wahalifu hatari.

Kwa kweli, wenye mamlaka walituona kuwa wahalifu wabaya sana. Hatukuruhusiwa kuwa na Biblia kwa sababu kama mlinzi mmoja alivyoeleza: “Shahidi wa Yehova mmoja akiwa na Biblia mkononi ni kama mhalifu akiwa na bunduki mkononi.” Ili kukusanya vipande vya Biblia, tulisoma vitabu vya mwandishi Mrusi, Leo Tolstoy, ambaye mara nyingi alinukuu maandiko ya Biblia katika vitabu vyake. Tulikariri maandiko hayo ya Biblia.

Kabla ya kukamatwa mwaka wa 1951, nilikuwa nimemchumbia Elsa Riemer. Alinitembelea gerezani mara nyingi iwezekanavyo na kuniletea kifurushi cha chakula mara moja kila mwezi. Yeye pia alificha chakula cha kiroho katika vifurushi vyake. Wakati mmoja, alijaza makala za Mnara wa Mlinzi ndani ya soseji kadhaa. Mara nyingi walinzi walikata soseji ili kuchunguza ikiwa kulikuwa na kitu kilichofichwa ndani, lakini wakati huu kifurushi hicho kilifika muda mfupi kabla ya siku ya kazi kwisha, na hakikuchunguzwa.

Wakati huo, mimi na Karl Heinz Kleber tulikaa katika seli ndogo pamoja na wafungwa watatu wasio Mashahidi. Tungesomaje Mnara wa Mlinzi bila kuonekana? Tulijifanya tunasoma kitabu lakini ndani tulificha makala za Mnara wa Mlinzi. Pia tulipitisha chakula hiki cha kiroho chenye thamani kwa Mashahidi wenzetu waliokuwa gerezani.

Tulipokuwa gerezani, tulitumia fursa mbalimbali ili kujulisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Nilisisimka kuona mmoja wa wafungwa wenzangu akipata kuwa mwamini likiwa tokeo la kufanya hivyo.—Mathayo 24:14.

Kurudia Huduma ya Wakati Wote

Baada ya takriban miaka sita gerezani, niliachiliwa Aprili 1, 1957. Baada ya muda unaopungua majuma mawili, nilimwoa Elsa. Wakati shirika la Stasi lilisikia juu ya kuachiliwa kwangu, lilitafuta kisingizio cha kunirudisha gerezani. Ili kuepuka uwezekano huo, mimi na Elsa tulivuka mpaka kwenda kuishi Berlin Magharibi.

Tulipofika Berlin Magharibi, Sosaiti ilitaka kujua mipango yetu. Tuliwaeleza kwamba mmoja wetu angepainia na yule mwingine aajiriwe.

“Mngeonaje nyote wawili mkiwa mapainia?” tukaulizwa.

“Ikiwa hilo linawezekana,” tukajibu, “tutaanza mara moja.”

Hivyo tulipewa ujira kidogo kila mwezi wa kutusaidia kujitegemeza, nasi tukaanza kutumikia tukiwa mapainia wa pekee mwaka wa 1958. Tulipata shangwe iliyoje kuona watu tuliojifunza nao Biblia wakirekebisha maisha yao na kuwa watumishi wa Yehova! Miaka kumi iliyofuata tukiwa mapainia wa pekee ilitufunza kufanya kazi pamoja karibu-karibu tukiwa mume na mke. Elsa aliniunga mkono sikuzote, hata nilipokuwa nikirekebisha gari. Pia tulisoma, tukajifunza, na kusali pamoja.

Katika mwaka wa 1969 tulipewa mgawo wa kazi ya kusafiri, tukizuru kutaniko tofauti kila juma ili kuhudumia mahitaji ya washiriki wake. Josef Barth, mwanamume mwenye uzoefu katika kazi ya kusafiri, alinitolea shauri hili: “Ukitaka kufanikiwa katika mgawo wako, pendezwa tu na akina ndugu.” Nilijaribu kutumia shauri hilo. Matokeo yakawa kwamba, tulikuwa na uhusiano mchangamfu sana na wenye upatano na Mashahidi wenzetu, ambao ulifanya iwe rahisi kutoa shauri lilipohitajika.

Katika mwaka wa 1972, Elsa alibainika kuwa na ugonjwa wa kansa na kufanyiwa upasuaji. Baadaye, aliugua baridi-yabisi. Ingawa alikuwa na maumivu mengi, bado aliandamana nami kila juma katika kutumikia makutaniko, akishiriki katika huduma pamoja na akina dada kadiri alivyoweza.

Kurekebisha Hali Zifaane na Mahitaji

Katika mwaka wa 1984 wakwe zangu walihitaji utunzaji wa wakati wote, kwa hiyo tuliacha kazi ya kusafiri ili kusaidia kuwatunza hadi walipokufa miaka minne baadaye. (1 Timotheo 5:8) Kisha, Elsa akawa mgonjwa sana mwaka wa 1989. Kwa kufurahisha, amepona kwa kiasi fulani, lakini imenibidi kufanya kazi zote za nyumbani. Ningali ninajifunza kushughulika na mtu mwenye maumivu yasiyokoma. Hata hivyo, licha ya mkazo na kuhangaika kihisia-moyo, tumedumisha upendo wetu kwa mambo ya kiroho.

Tunashukuru kwamba, leo tungali katika orodha ya mapainia. Hata hivyo, tumekuja kufahamu kwamba kile cha maana si madaraka tuliyo nayo au yale tuwezayo kufanya, bali ni kudumu tukiwa waaminifu. Tunataka kumtumikia Mungu wetu Yehova, si kwa miaka michache tu, bali kwa umilele. Yaliyotupata yametuzoeza vizuri kwa ajili ya wakati ujao. Naye Yehova ametupa nguvu za kumsifu hata chini ya hali zenye majaribu makali zaidi.—Wafilipi 4:13.

[Maelezo ya Chini]

a Masimulizi ya maisha ya Ernst Wauer yapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1991, ukurasa wa 25 hadi 29.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nilitiwa gerezani hapa Magdeburg

[Hisani]

Gedenkstätte Moritzplatz Magdeburg für die Opfer politischer Gewalt; Foto: Fredi Fröschki, Magdeburg

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tulipooana mwaka wa 1957

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Elsa leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki