Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 8/15 kur. 10-13
  • Falsafa ya Kigiriki—Je, Iliboresha Ukristo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Falsafa ya Kigiriki—Je, Iliboresha Ukristo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Dini ya Kiyahudi Iliyogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki”
  • “Utamaduni wa Kigiriki Uliogeuzwa Kufuata Ukristo”
  • “Ukristo Uliogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki” na “Falsafa ya Kikristo”
  • Wachafuzi Wenye Kufisidi
  • Kweli
  • Wazo Hilo Laingia Dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu
    Ni Nini Hutupata Tunapokufa?
  • Je, Mababa wa Kanisa Walikuwa Watetezi wa Kweli ya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Plato
    Amkeni!—2013
  • Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 8/15 kur. 10-13

Falsafa ya Kigiriki—Je, Iliboresha Ukristo?

“Ingawa Ukristo ulipinga utamaduni wa kipagani wa Ugiriki na Roma, ulikubali hasa falsafa nyingi za kitamaduni.”—The Encyclopedia Americana.

“MTAKATIFU” Augustine alikuwa na fungu muhimu kati ya wale waliokuwa na uvutano hususa juu ya mawazo ya “Kikristo.” Kulingana na The New Encyclopædia Britannica, “mawazo ya [Augustine] ndiyo yaliyotumiwa kuchanganya kabisa dini ya Agano Jipya na mapokeo ya Kiplato ya falsafa ya Kigiriki; na ndiyo pia yaliyotumiwa kupitisha matokeo ya mchanganyiko huo kwa Jumuiya za Wakristo za Katoliki ya Kiroma na Mfufuo wa Harakati za Uprotestanti wa enzi za kati.”

Urithi wa Augustine unadumu kwelikweli. Akiongea kuhusu kadiri ambavyo falsafa ya Kigiriki imeathiri Jumuiya ya Wakristo, Douglas T. Holden alisema: “Theolojia ya Kikristo imechanganyikana sana na falsafa ya Kigiriki hivi kwamba imetokeza watu ambao maoni yao yameathiriwa kwa asilimia 90 na mawazo ya Kigiriki, na kwa asilimia 10 na mawazo ya Kikristo.”

Wasomi fulani wanaamini kwa dhati kwamba uvutano huo wa kifalsafa uliboresha Ukristo pale mwanzoni, ukaboresha mafundisho yake, na kuufanya uwe wenye kusadikisha zaidi. Je, ndivyo ilivyokuwa? Uvutano wa falsafa ya Kigiriki ulianza lini na jinsi gani? Je, kweli huo uliboresha au ulichafua Ukristo?

Ni jambo linaloelimisha kufuata matukio kuanzia karne ya tatu K.W.K. hadi karne ya tano W.K., kwa kuchunguza mitajo minne ya kipekee: (1) “Dini ya Kiyahudi Iliyogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki,” (2) “Utamaduni wa Kigiriki Uliogeuzwa Kufuata Ukristo,” (3) “Ukristo Uliogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki,” na (4) “Falsafa ya Kikristo.”

“Dini ya Kiyahudi Iliyogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki”

Mtajo wa kwanza, “Dini ya Kiyahudi Iliyogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki,” ni kinyume kabisa. Dini ya awali ya Waebrania, iliyoanzishwa na Mungu wa kweli, Yehova, haikupaswa kuchafuliwa na mawazo ya dini zisizo za kweli. (Kumbukumbu la Torati 12:32; Mithali 30:5, 6) Hata hivyo, tangu mwanzo, usafi wa ibada ulitishwa na mazoea na mawazo ya kidini yaliyoizunguka—kama vile uvutano kutoka Misri, Kanaani, na Babiloni. Yasikitisha kwamba Israeli iliruhusu ibada yake ya kweli ichafuliwe sana.—Waamuzi 2:11-13.

Karne kadhaa baadaye, Palestina ya kale ilipopata kuwa sehemu ya Milki ya Ugiriki chini ya Aleksanda Mkuu katika karne ya nne K.W.K., uchafuzi huo ukawa mbaya zaidi, ukaacha nyuma hali ya kudumu yenye kuharibu. Aleksanda aliandikisha Wayahudi katika jeshi lake. Uhusiano kati ya Wayahudi na mshindi wao mpya uliathiri sana mawazo ya kidini ya Wayahudi. Elimu ya Kiyahudi ikapenywa na mawazo ya Kigiriki. Yasoni, Kuhani wa Cheo cha Juu, anajulikana kwa kuanzisha chuo cha Kigiriki jijini Yerusalemu mwaka wa 175 K.W.K. ili kuendeleza uchunguzi wa Homer.

Kwa kupendeza, Msamaria aliyeandika katika nusu ya pili ya karne ya pili K.W.K., alijaribu kuonyesha kwamba historia ya Biblia ni uandishi wa historia ya Kigiriki. Vitabu vya kiapokrifa vya Kiyahudi, kama vile Yudithi na Tobiti, vyagusia hekaya za kiashiki za Kigiriki. Kulitokea wanafalsafa kadhaa Wayahudi waliojaribu kupatanisha mawazo ya Kigiriki na dini ya Kiyahudi na Biblia vilevile.

Filo, Myahudi wa karne ya kwanza W.K., ndiye mtu anayetambuliwa zaidi kuhusiana na hilo. Alitumia isivyo haki mafundisho ya Plato (karne ya nne K.W.K.), ya Wapithagorea, na Wastoa. Wayahudi waliathiriwa sana na maoni ya Filo. Akitoa muhtasari juu ya kupenyeza huku kwa mawazo ya Kigiriki katika utamaduni wa Kiyahudi kulikofanywa na wasomi, mwandishi Myahudi Max Dimont, asema: “Wakiwa wameongezewa mawazo ya Kiplato, mantiki ya Aristotle, na sayansi ya Euclid, wasomi Wayahudi walitafuta kuielewa Torati kwa kutumia vifaa vipya. . . . Walianza kuongeza kusababu kwa Kigiriki juu ya ufunuo wa Kiyahudi.”

Baadaye, Waroma walitwaa Milki ya Ugiriki pamoja na Yerusalemu. Hilo lilitoa fursa kwa mabadiliko makubwa hata zaidi. Kufikia karne ya tatu W.K., mafundisho ya kifalsafa na ya kidini ya watu wenye kufikiri waliojitahidi kusitawisha na kuunganisha mawazo ya Plato, yakachukua muundo hususa, unaojulikana kijumla leo kuwa Uplato Mambo Leo. Umoja huo wa kauli ni lazima ungeathiri sana Ukristo ulioasi imani.

“Utamaduni wa Kigiriki Uliogeuzwa Kufuata Ukristo”

Katika karne tano za kwanza za wakati wetu wa kawaida, wasomi fulani walijaribu kuonyesha uhusiano kati ya falsafa ya Kigiriki na kweli iliyofunuliwa ya Biblia. Kitabu A History of Christianity chasema: “Wakristo wenye kuchunguza asili ya uhai walionyesha kwamba Wagiriki walioishi miongo kadhaa kabla ya Kristo ni kama watu wanaojitahidi sana kumjua Mungu lakini pasipo mwelekezo, wakijitahidi kumtunga Yesu kwa kutumia falsafa yao isiyo na maana na kubuni Ukristo kutokana na kufikiri kwao duni.”

Plotinasi (205-270 W.K.), aliyetangulia watu hao wenye kufikiri, alitokeza mfumo ambao hasa ulitegemea nadharia ya mawazo ya Plato. Plotinasi alitokeza dhana ya nafsi iliyo tofauti na mwili. Profesa E. W. Hopkins alisema hivi kuhusu Plotinasi: “Theolojia yake . . . iliathiri sana viongozi wa maoni ya Kikristo.”

“Ukristo Uliogeuzwa Kufuata Utamaduni wa Kigiriki” na “Falsafa ya Kikristo”

Kuanzia karne ya pili W.K., “Wakristo” wenye kufikiri walijitahidi sana kuwavutia wasomi wapagani. Licha ya onyo dhahiri la mtume Paulo dhidi ya “semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu,” na “mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli,” walimu hao walichanganya katika mafundisho yao falsafa fulani zilizotokana na utamaduni wa Kigiriki uliowazunguka. (1 Timotheo 6:20) Mfano wa Filo ulionekana kudokeza kwamba ingewezekana kupatanisha Biblia na mawazo ya Kiplato.—Linganisha 2 Petro 1:16.

Bila shaka, kweli ya Biblia ndiyo hasa iliyoathiriwa sana. Walimu “Wakristo” walijaribu kuonyesha kwamba Ukristo ulipatana na falsafa ya Waroma na Wagiriki. Clement wa Alexandria na Origen (karne ya pili na ya tatu W.K.) walifanya Uplato Mambo Leo uwe msingi wa kile kilichokuja kuitwa “falsafa ya Kikristo.” Ambrose (339-397 W.K.), askofu wa Milan, alikuwa “amekubali mafunzo ya karibuni zaidi ya Kigiriki, ya Kikristo na ya kipagani vilevile—hasa vitabu . . . vya Plotinasi, mpagani aliyefuata Uplato Mambo Leo.” Alijaribu kuwapa Waroma wenye elimu Ukristo uliofuata utamaduni wa Kigiriki na Waroma. Augustine naye akafanya vivyo hivyo.

Karne moja baadaye, Dionisio wa Areopago, yamkini mtawa Msiria (aliyeitwa pia Dionisio-bandia), alijaribu kupatanisha Uplato Mambo Leo na “theolojia ya Kikristo.” Kulingana na ensaiklopedia moja, “maandishi [yake] yalianzisha mwelekeo hususa wa kufuata Uplato Mambo Leo katika mafundisho mengi ya Kikristo na pia hali ya kiroho ya enzi za kati . . . ambao umetokeza namna mbalimbali za mafundisho [ya Kikristo] ya kidini na ujitoaji hadi wakati wa sasa.” Hilo ni dharau dhahiri kama nini kwa onyo la mtume Paulo dhidi ya “falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu”!—Wakolosai 2:8.

Wachafuzi Wenye Kufisidi

Imeonekana kwamba “Waplato Wakristo walizingatia sana ufunuo na kuiona falsafa ya Plato kuwa kifaa bora zaidi cha kusaidia kuelewa na kutetea mafundisho ya Maandiko na mapokeo ya kanisa.”

Plato mwenyewe alikuwa amesadiki kwamba kuna nafsi isiyoweza kufa. La muhimu ni kwamba kutokufa kwa nafsi ni mojawapo ya mafundisho maarufu yasiyo ya kweli yaliyojipenyeza katika “theolojia ya Ukristo.” Kukubali fundisho hili hakuwezi kuhalalishwa eti kwa sababu kufanya hivyo kuliufanya Ukristo uvutie zaidi umma. Alipokuwa akihubiri huko Athene, kitovu hasa cha utamaduni wa Kigiriki, mtume Paulo hakufundisha fundisho la Kiplato la nafsi. Badala yake, alihubiri fundisho la Kikristo la ufufuo, hata ingawa wasikilizaji wengi Wagiriki waliliona kuwa jambo gumu kukubali aliyosema.—Matendo 17:22-32.

Kinyume cha falsafa ya Kigiriki, Maandiko yaonyesha wazi kwamba nafsi si kile mtu anacho bali ni kile yeye alicho. (Mwanzo 2:7) Wakati wa kufa, nafsi hukoma kuwapo. (Ezekieli 18:4) Mhubiri 9:5 hutuambia: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa.” Fundisho la kutokufa kwa nafsi halifundishwi katika Biblia.

Fundisho jingine la udanganyifu lilihusu cheo cha Yesu kabla ya kuwa mwanadamu, wazo la kwamba alikuwa sawa na Baba yake. Kitabu The Church of the First Three Centuries chaeleza: “Fundisho la Utatu . . . lilipata awali yalo katika chanzo cha kigeni kabisa kilicho tofauti na Maandiko ya Kiyahudi na ya Kikristo.” Ni chanzo gani hicho? Fundisho hilo “lilikua, na likapandikizwa juu ya Ukristo, kupitia mikono ya Mababa wenye kufuata mawazo ya Plato.”

Kwa kweli, kadiri wakati ulivyopita nao Mababa wa Kanisa wakazidi kuathiriwa na Uplato Mambo Leo, ndivyo Wanautatu walivyozidi kupata wafuasi wengi zaidi. Yaonekana kuwa falsafa ya Uplato Mambo Leo ya karne ya tatu iliwawezesha kupatanisha kisichoweza kupatanishwa—kufanya Mungu mwenye sehemu tatu aonekane kuwa Mungu mmoja. Kwa kusababu kifalsafa, walidai kwamba watu watatu wanaweza kuwa Mungu mmoja huku wakibaki kuwa mtu mmoja-mmoja!

Hata hivyo, kweli ya Biblia yaonyesha wazi kwamba Yehova peke yake ndiye Mungu Mweza Yote, Yesu Kristo ni Mwana Wake aliyeumbwa, mwenye cheo cha chini kidogo, nayo roho takatifu ni kani Yake ya utendaji. (Kumbukumbu la Torati 6:4; Isaya 45:5; Matendo 2:4; Wakolosai 1:15; Ufunuo 3:14) Fundisho la Utatu humfedhehesha Mungu wa pekee wa kweli na kutatanisha watu, likiwaondosha kwa Mungu wasiyeweza kumwelewa.

Tumaini lenye kutegemea Maandiko la milenia ni fundisho jingine lililoathiriwa vibaya na uvutano wa Uplato Mambo Leo juu ya mawazo ya Kikristo. (Ufunuo 20:4-6) Origen alijulikana kwa kuwashutumu wamilenia. Kwa nini alipinga sana fundisho hili la kweli la Biblia juu ya utawala wa Kristo wa miaka elfu moja? Kichapo The Catholic Encyclopedia chajibu: “Kwa kuzingatia Uplato Mambo Leo uliotegemeza mafundisho yake . . . , [Origen] hangeweza kuwaunga mkono wamilenia.”

Kweli

Matukio yaliyotajwa juu hayakuhusiana kwa vyovyote na kweli. Kweli hii ni mkusanyo wa mafundisho yote ya Kikristo yapatikanayo katika Biblia. (2 Wakorintho 4:2; Tito 1:1, 14; 2 Yohana 1-4) Biblia ndiyo chanzo pekee cha kweli.— Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16.

Hata hivyo, adui wa Yehova, wa ile kweli, wa wanadamu, na wa uhai udumuo milele—Shetani Ibilisi, “muua-binadamu” na “baba ya uwongo”—ametumia mbinu mbalimbali za ujanja ili aighushi kweli. (Yohana 8:44; linganisha 2 Wakorintho 11:3.) Mafundisho ya wanafalsafa wapagani Wagiriki ni mojawapo ya mbinu yenye nguvu zaidi ambayo ametumia—yakidhihirisha hasa mawazo yake mwenyewe—katika jitihada ya kubadili maudhui na namna ya mafundisho ya Kikristo.

Kuchanganya huku kusiko kwa asili kwa mafundisho ya Kikristo na ya falsafa ya Kigiriki ni jaribio la kughushi kweli ya Biblia, kukipunguza uwezo na uvutio wake kwa watafutaji kweli walio wapole, wanyofu, na wenye kufundishika. (1 Wakorintho 3:1, 2, 19, 20) Pia kunaelekea kuchafua usafi wenye kutakata wa mafundisho ya Biblia, kukifanya tofauti baina ya kweli na lisilo kweli isiwe wazi.

Leo, chini ya mwelekezo wa Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, mafundisho ya kweli ya Kikristo yamerudishwa. Pia, watafutaji kweli walio wanyofu wanaweza kutambua kwa urahisi kutaniko la kweli la Kikristo kwa matunda yake. (Mathayo 7:16, 20) Mashahidi wa Yehova wako tayari na wana hamu ya kusaidia watu hao wapate maji ya kweli yasiyoghushiwa na kuwasaidia wapate kushika imara urithi wa uhai wa milele unaotolewa na Yehova Baba yetu.—Yohana 4:14; 1 Timotheo 6:19.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Augustine

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Maandishi ya Kigiriki: From the book Ancient Greek Writers: Plato’s Phaedo, 1957, Ioannis N. Zacharopoulos, Athens; Plato: Musei Capitolini, Roma

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki