Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 4/1 kur. 9-14
  • Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Majibu Mengi, Kichwa Kilekile
  • Jinsi Fundisho Hilo Lilivyoanza
  • Milki ya Ulimwengu ya Dini Isiyo ya Kweli Yapanuka Kuelekea Mashariki
  • Namna Gani Dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu?
  • Wazo Hilo Laingia Dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu
    Ni Nini Hutupata Tunapokufa?
  • Je! Kuna Uhai Baada ya Kifo?
    Ni Nini Hutupata Tunapokufa?
  • Kutoweza Kufa kwa Nafsi—Chanzo cha Fundisho Hilo
    Ni Nini Hutupata Tunapokufa?
  • Je! Nafsi Huendelea Kuishi Baada ya Kifo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 4/1 kur. 9-14

Uhai Baada ya Kifo—Watu Huamini Nini?

“Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?”—AYUBU 14:14.

1, 2. Wengi hutafutaje faraja mpendwa wao anapokufa?

KATIKA nyumba ya mazishi huko New York City, marafiki na familia watembea kimya-kimya kando ya jeneza lililo wazi la mvulana mwenye umri wa miaka 17 ambaye amekufa kutokana na kansa. Mama ya mvulana huyo aliyevunjika moyo arudia-rudia kwa machozi hivi: “Tommy ana furaha zaidi sasa. Mungu alitaka Tommy awe mbinguni naye.” Hivyo ndivyo amefundishwa kuamini.

2 Kilometa 11,000 kutoka huko, katika Jamnagar, India, mwana mkubwa zaidi kati ya wana watatu awasha magogo moto mahali pa kuchomea maiti ya baba yao aliyekufa. Huku kelele ya moto ikiendelea, Brahman arudia-rudia maombi ya Kisanskriti hivi: “Nafsi isiyokufa kamwe na iendelee katika jitihada zake za kuwa sawa na nafsi kuu ya mwenyezi mungu.”

3. Watu wamejiuliza maswali gani kwa enzi zilizopita?

3 Uhalisi wa kifo watuzunguka. (Waroma 5:12) Ni jambo la kawaida kwetu kuwazia ikiwa kifo ndicho mwisho wa mambo yote. Akitafakari juu ya duru ya kawaida ya mimea, Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu wa kale, alionelea hivi: “Yako matumaini ya mti, ya kuwa ukikatwa utachipuka tena, wala machipukizi yake hayatakoma.” Vipi, basi, kuhusu wanadamu? “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” Ayubu akauliza. (Ayubu 14:7, 14) Katika enzi zilizopita, watu katika kila jamii wametafakari maswali haya: Je, kuna uhai baada ya kifo? Ikiwa ndivyo, ni uhai wa aina gani? Basi, watu wameamini nini? Na kwa nini?

Majibu Mengi, Kichwa Kilekile

4. Watu wa dini mbalimbali huamini nini juu ya uhai baada ya kifo?

4 Wakristo wengi wa jina tu huamini kwamba baada ya kifo, watu huenda mbinguni au motoni. Wahindu, nao, huamini katika kuzaliwa upya katika umbo jingine. Kulingana na itikadi za Kiislamu, kuna siku ya kiama baada ya kifo, wakati ambapo Allah atachanganua maisha ya kila mtu na kumpeleka kila mtu paradisoni au motoni. Katika nchi fulani, itikadi juu ya wafu ni mchanganyiko wa tamaduni za kienyeji na Ukristo wa jina. Kwa mfano, katika Sri Lanka, Wabudha na Wakatoliki huacha milango na madirisha yakiwa wazi mtu afapo nyumbani kwao, nao huweka jeneza miguu ya mfu ikielekeana na mlango wa mbele. Wao huamini kwamba kufanya hivyo hurahisisha kuondoka kwa roho, au nafsi, ya aliyekufa. Miongoni mwa Wakatoliki na Waprotestanti wengi wa Afrika Magharibi, kuna desturi ya kufunika vioo mtu afapo ili mtu yeyote asiangalie kioo na kuona roho ya mtu aliyekufa. Kisha, baada ya siku 40, familia na marafiki huadhimisha kupaa kwa nafsi kwenda mbinguni.

5. Dini nyingi hukubaliana juu ya itikadi gani iliyo kuu?

5 Yajapokuwa maoni hayo mengi, yaonekana kwamba dini nyingi hukubaliana angalau juu ya jambo moja. Huamini kwamba kitu fulani ndani ya mtu—kiwe chaitwa nafsi, roho, au mzuka—hakifi na huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Karibu mamia yote ya dini na mafarakano ya Jumuiya ya Wakristo hutetea itikadi ya kwamba nafsi haiwezi kufa. Itikadi hiyo pia ni fundisho rasmi katika dini ya Kiyahudi. Ndilo msingi wenyewe wa fundisho la dini ya Hindu la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Waislamu huamini kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Wenyeji wa Australia, Waabudu-maumbile wa Afrika, Washinto, na hata Wabudha, wote hao hufundisha namna tofauti-tofauti za fundisho hilohilo.

6. Wasomi fulani hulionaje lile wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa?

6 Kwa upande mwingine, kuna watu walio na maoni kwamba uhai wa kuweza kufahamu mambo huisha mtu anapokufa. Kwa maoni yao, lile wazo la kwamba uhai wa kihisia-moyo na wenye akili huendelea ukiwa nafsi isiyo na utu, iliyo kama kivuli ambayo imetengana na mwili, huonekana kuwa lisilopatana na akili. Mwandishi aliye pia msomi Mhispania wa karne ya 20, Miguel de Unamuno, aandika hivi: “Kuamini kwamba nafsi haiwezi kufa ni kutaka nafsi isiweze kufa, lakini ni kutaka sana iwe hivyo hivi kwamba kutaka huko kwamfanya mtu apuuze ukweli na asitumie akili.” Wengine wanaoamini hivyo hutia ndani watu wa namna mbalimbali kama vile Aristotle na Epikurasi, wanafalsafa wa kale wenye sifa, daktari Hipokrato, mwanafalsafa Mskoti David Hume, msomi Mwarabu Averroës, na aliyekuwa waziri mkuu wa kwanza wa India baada ya uhuru, Jawaharlal Nehru.

7. Ni maswali gani muhimu juu ya itikadi inayohusu kutokufa kwa nafsi ambayo lazima yachunguzwe sasa?

7 Tukiwa tunakabiliwa na mawazo na itikadi za aina hiyo zenye kupingana, lazima tuulize: Je, kweli tuna nafsi isiyoweza kufa? Ikiwa kweli nafsi yaweza kufa, basi fundisho hilo lisilo la kweli lingeweza kuwaje sehemu muhimu ya dini zilizo nyingi za leo? Wazo hilo lilianzia wapi? Ni lazima tupate majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali hayo kwa kuwa wakati wetu ujao huyategemea. (1 Wakorintho 15:19) Lakini kwanza, acheni tuchunguze jinsi fundisho hilo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilivyoanza.

Jinsi Fundisho Hilo Lilivyoanza

8. Socrates na Plato walitimiza fungu gani katika kuendeleza wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa?

8 Socrates na Plato, wanafalsafa Wagiriki wa karne ya tano K.W.K. waaminiwa kuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuendeleza ile itikadi kwamba nafsi haiwezi kufa. Lakini, hawakuwa waanzilishi wa wazo hilo. Badala yake, walilirekebisha na kulibadili liwe fundisho la kifalsafa, hivyo, wakilifanya livutie zaidi watu wenye elimu wa siku yao na kuendelea. Ukweli ni kwamba Wazoroasta wa Uajemi ya kale na Wamisri waliokuwa kabla yao waliamini katika kutokufa kwa nafsi. Basi swali ni, Ni nini chanzo cha fundisho hilo?

9. Ni nini kilichokuwa chanzo cha uvutano uliohusu tamaduni zote za kale za Misri, Uajemi, na Ugiriki?

9 “Katika ulimwengu wa kale,” chasema kitabu The Religion of Babylonia and Assyria, “Misri, Uajemi, na Ugiriki zilipatwa na uvutano wa dini ya Kibabiloni.” Kuhusu itikadi za kidini za Kimisri, kitabu hicho chaendelea kusema hivi: “Kwa sababu ya ule uhusiano wa mapema kati ya Misri na Babilonia, kama ionyeshwavyo na yale mabamba ya El-Amarna, bila shaka kulikuwa na uwezekano mkubwa kwa maoni na desturi za Kibabiloni kupenya na kuingia katika madhehebu za Misri.”a Mambo hayohayo yaweza kusemwa kuhusu tamaduni za kale za Uajemi na Ugiriki.

10. Maoni ya Wababiloni kuhusu uhai baada ya kifo yalikuwa nini?

10 Lakini, je, Wababiloni wa kale waliamini katika kutokufa kwa nafsi? Kuhusu hoja hiyo, Profesa Morris Jastrow, Jr., wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania, Marekani, aliandika hivi: “Wala watu wala viongozi wa kidini [wa Babilonia] hawakutarajia kamwe uwezekano wa kuangamizwa kabisa kwa uhai. [Kwa maoni yao] kifo kilikuwa kijia cha kuingia aina nyingine ya uhai, na kusema kwamba nafsi yaweza kufa [ya uhai wa sasa] kulikazia tu jinsi isivyowezekana kuponyoka badiliko katika maisha ambalo huletwa na kifo.” Ndiyo, Wababiloni waliamini kwamba uhai wa aina fulani, katika njia fulani, uliendelea baada ya kifo. Walionyesha hilo kwa kuzika vitu pamoja na wafu kwa matumizi katika uhai baada ya kifo.

11, 12. Baada ya Furiko, ni nini kilichokuwa chanzo cha fundisho la kutokufa kwa nafsi ?

11 Kwa wazi, fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa hurudi nyuma hadi Babiloni la kale. Je, hilo ni muhimu? Ndiyo, kwa sababu kulingana na Biblia, jiji la Babeli, au Babiloni, lilianzishwa na Nimrodi, kitukuu wa Noa. Baada ya Furiko katika siku ya Noa, watu wote walisema lugha moja na walikuwa na dini moja. Nimrodi alikuwa “katika kupingana na Yehova,” na pia yeye na wafuasi wake walitaka ‘kujifanyia jina.’ Hivyo, kwa kuanzisha jiji hilo na kujenga mnara huko, Nimrodi alianzisha dini tofauti.—Mwanzo 10:1, 6, 8-10, NW; 11:1-4.

12 Mapokeo husema kwamba Nimrodi alikufa kifo cha jeuri. Kwa kupatana na akili, baada ya kifo chake, Wababiloni wangalielekea kumstahi sana akiwa mwanzilishi, mjenzi, na mfalme wa kwanza wa jiji lao. Kwa kuwa mungu Marduk (Merodaki) alionwa kuwa mwanzilishi wa Babiloni na idadi fulani ya wafalme wa Babiloni hata waliitwa jina lake, wasomi fulani wamedokeza kwamba Marduk huwakilisha Nimrodi aliyefanywa kuwa mungu. (2 Wafalme 25:27; Isaya 39:1; Yeremia 50:2) Ikiwa ndivyo ilivyo basi, lile wazo la kwamba mtu ana nafsi ambayo huendelea kuishi baada ya kifo lazima liwe lilikuwapo angalau kufikia wakati wa kifo cha Nimrodi. Kwa vyovyote, historia hufunua kwamba baada ya Furiko, chanzo cha fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa kilikuwa Babeli, au Babiloni.

13. Fundisho la nafsi isiyoweza kufa lilieneaje usoni pa dunia yote, na tokeo lilikuwa nini?

13 Biblia yaendelea kuonyesha kwamba Mungu alitatanisha juhudi za wajenzi wa mnara huko Babeli kwa kuchafua lugha yao. Wakiwa hawawezi kuwasiliana, waliacha mradi wao na wakatawanywa “kutoka huko . . . waende usoni pa nchi yote.” (Mwanzo 11:5-9) Lazima tukumbuke kwamba ingawa usemi wa hao walionuia kujenga mnara ulibadilishwa, njia yao ya kufikiri na dhana zao hazikubadilika. Likiwa tokeo, kokote walikoenda, walienda na mawazo yao ya kidini. Kwa njia hiyo, mafundisho ya kidini ya Kibabiloni—kutia ndani lile la kutokufa kwa nafsi—yalienea usoni pa dunia yote na kuwa msingi wa dini kubwa za ulimwengu. Hivyo, milki ya ulimwenguni pote ya dini isiyo ya kweli ikaanzishwa, ambayo yafafanuliwa ifaavyo katika Biblia kuwa “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa mambo yenye kuchukiza sana ya dunia.”—Ufunuo 17:5.

Milki ya Ulimwengu ya Dini Isiyo ya Kweli Yapanuka Kuelekea Mashariki

14. Itikadi za kidini za Kibabiloni zilieneaje kuingia bara Hindi?

14 Wanahistoria fulani husema kwamba zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, mfululizo wa kuhama uliwaleta watu weupe, wa jamii ya Kiarya, kutoka kaskazini-magharibi kuingia Bonde la Indus, ambalo sasa limo hasa nchini Pakistan na India. Kutoka huko walisambaa kuingia katika nyanda za Mto Ganges na kuvuka India. Wataalamu fulani husema kwamba mawazo ya kidini ya wahamiaji hao yalitegemea mafundisho ya kale ya Wairani na Wababiloni. Basi, mawazo hayo ya kidini yakawa vyanzo vya dini ya Hindu.

15. Lile wazo kuhusu nafsi isiyoweza kufa lilikujaje kuathiri dini ya Hindu ya leo?

15 Katika India, lile wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilibadilika na kuwa fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine. Watu wenye hekima wa dini ya Hindu, waliokuwa waking’ang’ana na tatizo la ulimwenguni pote la uovu na kuteseka miongoni mwa wanadamu, walibuni ile iitwayo sheria ya Karma, sheria ya kwamba kila tokeo lina kisababishi. Wakiunganisha sheria hiyo na itikadi ya kwamba nafsi haiwezi kufa, walitokeza fundisho la kuzaliwa upya katika umbo jingine, ambamo mambo yastahiliyo na yasiyostahili yaliyofanywa katika uhai mmoja huthawabishwa au kuadhibiwa katika uhai unaofuata. Mradi wa waamini ni kufikia moksha, au kuwekwa huru kutokana na ule mzunguko wa kuzaliwa upya na kuwa kitu kimoja na yule aitwaye nafsi kuu au Nirvana. Kwa karne kadhaa, dini ya Hindu ilipokuwa ikienea, fundisho hilo la kuzaliwa upya katika umbo jingine lilienea pia. Na fundisho hilo limekuwa nguzo ya dini ya Hindu ya leo.

16. Ni itikadi gani kuhusu uhai baada ya kifo iliyokuja kutawala fikira na mazoea ya idadi iliyo kubwa zaidi ya watu wa Asia Mashariki?

16 Dini ya Hindu ilitokeza dini nyingine, kama vile Ubudha, Ujaini, na dini ya Sikh. Dini hizo huamini katika kuzaliwa upya katika umbo jingine. Isitoshe, Ubudha ulipokuwa ukipenya sehemu kubwa ya Asia Mashariki—China, Korea, Japani, na kwingineko—uliathiri sana tamaduni na dini za eneo hilo lote. Jambo hilo lilitokeza dini zenye mchanganyiko wa itikadi mbalimbali, zenye kuunga mkono mambo fulani ya Ubudha, ushirikina, na kuabudu wazazi wa kale waliokufa. Kati ya hizi, zile zenye uvutano mkubwa zaidi ni dini ya Tao, Ukonfyushasi, na dini ya Shinto. Hivyo, itikadi ya kwamba uhai huendelea kuwapo baada ya mwili kufa imekuja kutawala fikira za kidini na mazoea mbalimbali ya idadi kubwa zaidi ya watu katika eneo hilo la ulimwengu.

Namna Gani Dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu?

17. Wayahudi wa kale waliamini nini kuhusu uhai baada ya kifo?

17 Watu wanaofuata dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu wanaamini nini kuhusu uhai baada ya kifo? Kati ya dini hizo, ile ya Kiyahudi ndiyo ya kale zaidi. Vyanzo vyake vinarudi nyuma miaka ipatayo 4,000 wakati wa Abrahamu—muda mrefu kabla Socrates na Plato kubuni wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa. Wayahudi wa kale waliamini katika ufufuo wa wafu wala hawakuamini katika hali fulani ya kiasili ya kutoweza kufa kwa kibinadamu. (Mathayo 22:31, 32; Waebrania 11:19) Basi, fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa liliingiaje katika dini ya Kiyahudi? Historia yatoa jibu.

18, 19. Fundisho la kutokufa kwa nafsi liliingiaje katika dini ya Kiyahudi?

18 Mwaka wa 332 K.W.K., Aleksanda Mkubwa alishinda sehemu ya Mashariki ya Kati, kutia na Yerusalemu. Watawala waliotawala baada ya Aleksanda waliendeleza mipango yake ya kueneza Ugiriki katika milki hiyo, mchanganyiko wa tamaduni hizo mbili—wa Kigiriki na wa Kiyahudi—ukatukia. Punde si punde Wayahudi wakafahamu mawazo ya Kigiriki, hata baadhi yao wakawa wanafalsafa.

19 Filo wa Aleksandria, wa karne ya kwanza W.K., alikuwa mmojawapo wa wanafalsafa hao Wayahudi. Filo alimstahi sana Plato na alijitahidi sana kufafanua dini ya Kiyahudi kwa kutumia maneno ya falsafa ya Kigiriki, hivyo akitayarisha njia kwa ajili ya Wayahudi wenye akili wa baadaye. Talmud—muhtasari ulioandikwa wa sheria za mdomo za marabi—iliathiriwa pia na wazo la Kigiriki. “Marabi wa Talmud,” chasema kichapo Encyclopaedia Judaica, “waliamini kwamba nafsi iliendelea kuishi baada ya kifo.” Baadaye, fasihi ya kifumbo ya Kiyahudi, Cabala, hata yafundisha juu ya kuzaliwa upya katika umbo jingine. Hivyo, wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa lilipenya kisiri kupitia falsafa ya Kigiriki na kuingia dini ya Kiyahudi. Ni nini liwezalo kusemwa juu ya kuingia kwa fundisho hilo katika Jumuiya ya Wakristo?

20, 21. (a) Ni upi uliokuwa msimamo wa Wakristo wa mapema kuhusu falsafa ya Plato, au falsafa ya Kigiriki? (b) Ni nini kilichosababisha kuchanganywa kwa mawazo ya Plato na mafundisho ya Kikristo?

20 Ukristo wa kweli ulianza na Yesu Kristo. Miguel de Unamuno, aliyenukuliwa mapema, aliandika hivi kuhusu Yesu: “Aliamini hasa katika kufufuliwa kwa mwili, kulingana na njia ya Kiyahudi, wala hakuamini kwamba nafsi haiwezi kufa, kwa njia ya [Kigiriki] ya Plato.” Alimalizia kwa kusema hivi: “Kutoweza kufa kwa nafsi . . . ni fundisho la kipagani la kifalsafa.” Kwa kufikiria hilo, twaweza kuona ni kwa nini mtume Paulo aliwaonya vikali Wakristo wa karne ya kwanza dhidi ya “falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.

21 Hata hivyo, “fundisho [hilo] la kipagani la kifalsafa” lilipenya lini na jinsi gani katika Jumuiya ya Wakristo? Kichapo The New Encyclopædia Britannica chaeleza hivi: “Kuanzia katikati ya karne ya 2 [W.K.] Wakristo waliokuwa wamezoezwa falsafa ya Kigiriki kwa kiasi fulani walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kwa kutumia maneno ya falsafa za Kigiriki, ili kujiridhisha wenyewe na ili kugeuza imani ya wapagani walioelimika. Falsafa iliyowafaa kabisa ilikuwa mafundisho ya Uplato.” Wanafalsafa wawili wa mapema walioathiri sana mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo walikuwa Origen wa Aleksandria na Augustine wa Hippo. Wote wawili waliathiriwa sana na mawazo ya Plato nao waliyapenyeza katika mafundisho ya Kikristo.

22. Fundisho la kutokufa kwa nafsi limebakije kuwa fundisho muhimu katika Uislamu?

22 Ilhali wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa katika dini ya Kiyahudi na katika Jumuiya ya Wakristo lilitokea kwa sababu ya uvutano wa Plato, dhana hiyo iliingizwa katika Uislamu tangu mwanzo wake. Korani, kitabu kitakatifu cha Waislamu, hufundisha kwamba mwanadamu ana nafsi ambayo huendelea kuishi baada ya kifo. Husema kwamba hatimaye nafsi itaishi katika shamba la paradiso ya kimbingu au kuadhibiwa motoni. Hilo halimaanishi kwamba wasomi Waarabu hawajajaribu kuunganisha mafundisho ya Kiislamu na falsafa ya Kigiriki. Kwa hakika, Waarabu waliathiriwa kwa kiasi fulani na maandishi ya Aristotle. Hata hivyo, Waislamu bado huamini katika kutokufa kwa nafsi.

23. Ni maswali yapi ya lazima kuhusu uhai baada ya kifo yatakayochunguzwa katika makala inayofuata?

23 Kwa wazi, dini ulimwenguni pote zimetokeza itikadi nyingi zenye kutatanisha juu ya uhai baada ya kifo, kwa kutegemea fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa. Na itikadi hizo zimeathiri, naam, hata kutawala na kufanya mabilioni ya watu kuwa watumwa. Tukabiliwapo na hayo yote, twalazimika kuuliza: Je, kweli yawezekana kujua ni nini hutupata tunapokufa? Je, kuna uhai baada ya kifo? Biblia husema nini kuhusu hilo? Tutachunguza hilo katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a El-Amarna ni mahali pa magofu ya Akhetaton, jiji la Misri, ambalo yadaiwa lilijengwa karne ya 14 K.W.K.

Je, Waweza Kueleza?

◻ Ni kichwa kipi kinachopatikana kotekote katika itikadi za dini nyingi kuhusu uhai baada ya kifo?

◻ Historia na Biblia zaonyeshaje kwamba Babiloni la kale ndilo chanzo cha fundisho la nafsi isiyoweza kufa?

◻ Ni katika njia gani dini za Mashariki zimeathiriwa na itikadi ya Babiloni katika nafsi isiyoweza kufa?

◻ Fundisho la kutokufa kwa nafsi lilipenyaje katika dini ya Kiyahudi, Jumuiya ya Wakristo, na Uislamu?

[Picha katika ukurasa wa 12,13]

Ushindi wa Aleksanda Mkubwa ulisababisha kuchanganywa kwa utamaduni wa Kigiriki na wa Kiyahudi

Augustine alijaribu kuchanganya falsafa ya Plato na Ukristo

[Hisani]

Aleksanda: Musei Capitolini, Roma; Augustine: From the book Great Men and Famous Women

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki