Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Kuhubiri ‘Katika Majira Yanayofaa na Katika Majira Yenye Taabu’
MAELFU ya watu walipatwa na magumu mengi wakati wa vita katika nchi ya Bosnia na Herzegovina. Katika wakati huo wenye magumu, Mashahidi wa Yehova walijitahidi sana kuwapa watu kitia-moyo na tumaini. Yafuatayo ni madondoo kutoka kwenye barua iliyoandikwa na Shahidi mmoja aliyetumikia kwa kipindi fulani katika Sarajevo.
“Ijapokuwa maisha ni magumu hapa, watu wanaitikia sana kweli ya Biblia. Mashahidi wanaoishi hapa ni kielelezo bora sana cha uvumilivu. Ijapokuwa hawana vitu vingi vya kimwili, wanadhihirisha mtazamo bora kabisa. Karibu vijana wote katika kutaniko wanafanya huduma ya wakati wote. Wahubiri wapya wanatiwa moyo wanapoona bidii yao, na kwa hiyo ni jambo la kawaida kwa wapya hawa kutumia muda wa saa 60 au zaidi kila mwezi katika huduma mara tu wanapokuwa wahubiri.
“Mbali na kuhubiri kutoka nyumba hadi nyumba, tumejaribu njia mbalimbali ili kuwafikia watu. Kwa mfano, tumekuwa na matokeo mazuri kwa kuwatolea watu vichapo vya Biblia katika maeneo mengi ya makaburi hapa mjini.
“Ushahidi pia umetolewa kwenye hospitali nyingi. Tabibu mkuu katika Idara ya Maradhi ya Moyo kwenye hospitali moja hapa Sarajevo, alikubali toleo la Amkeni! la Desemba 8, 1996, lenye jalada lililosema ‘Maradhi ya Moyo—Ni Nini Kinachoweza Kufanywa?’ Aliomba nakala zaidi kwa ajili ya madaktari wengine. Kisha Mashahidi wakapewa ruhusa ya kuwatembelea wagonjwa wote katika idara hiyo. Hivyo basi, kwa zaidi ya muda wa saa moja, magazeti zaidi ya 100 yalikuwa yametolewa kutoka kitanda hadi kitanda. Wagonjwa wengi walisema kwamba ilikuwa mara yao ya kwanza kutembelewa na mtu fulani ili awape kitia-moyo na tumaini.
“Katika pindi nyingine Mashahidi walizuru Idara ya Matibabu ya Watoto wakiwa na makala ya magazeti yanayofaa watoto. Tabibu mkuu wa Idara hii alikubali pia nakala chache za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia ili ziwekwe kwenye chumba cha kusomea. Sasa akina mama wanaowatembelea watoto wao katika hospitali hiyo huwasomea hadithi za Biblia kila siku. Mipango pia imefanywa ya kumtembelea huyo daktari nyumbani kwake.
“Kuna maelfu ya askari-jeshi kutoka mataifa mbalimbali wa Shirika la Kujihami la NATO katika nchi ya Sarajevo. Hawa pia wamepata ushahidi kamili. Nyakati nyingine sisi huhubiri kutoka gari moja la kivita hadi gari jingine la kivita tukitumia kijitabu Good News for All Nations pamoja na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika lugha mbalimbali. Magazeti zaidi ya 200 yalitolewa katika kambi ya askari-jeshi ya Waitalia. Jambo la kushangaza ni kwamba wengi wa askari-jeshi hawa Waitalia walisema hawajawahi kamwe kuzungumza na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, tulizungumza nao Sarajevo.
“Siku moja gari la kivita lilikuwa limeegeshwa kando ya barabara. Nilibisha kwenye gari hilo kwa mwavuli wangu, askari-jeshi mmoja akatoka. Nikamtolea gazeti Mnara wa Mlinzi lenye kichwa ‘Wajumbe wa Amani—Wao Ni Nani?’ Huyo askari alinitazama kisha akauliza, ‘Wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, sivyo?’ Alipotambua kwamba mimi ni mmoja wao, akajibu ‘Hata siamini; mko huku pia! Je, kuna sehemu yoyote duniani ambako hakuna Mashahidi wa Yehova?’”
Mtume Paulo alihimiza hivi: “Lihubiri neno, lifanye kwa hima katika majira yenye kufaa, katika majira yenye taabu.” (2 Timotheo 4:2) Kama waamini wenzao ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova katika Sarajevo wanafanya hivyo, hata kutoka kitanda hadi kitanda na gari la kivita hadi gari la kivita!