Mungu Hasahau “Pendo Lile Mlilolidhihirisha kwa Jina Lake”
“MUNGU si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.” (Waebrania 6:10) Maneno hayo ya mtume Paulo ni ya kweli kwa Mashahidi wa Yehova katika Ulaya ya Mashariki. Wakitumikia kwa uaminifu masilahi ya jina la Mungu, kwa miongo kadhaa wamefanya kazi kwa muda mrefu na kwa bidii sana chini ya vizuizi vilivyowekwa na serikali zilizodhibitiwa na ile iliyokuwa Sovieti. Yehova hukumbuka matendo yao mazuri na huwapa baraka nyingi za Ufalme. Kwa mfano, acha tutazame ripoti ya utumishi ya mwaka uliopita kutoka maeneo haya matatu tu.
Maeneo ya Ile Iliyokuwa Muungano wa Sovieti
Maeneo ya ile iliyokuwa Muungano wa Sovieti yanaripoti kwamba katika mwaka wa utumishi wa 1992, kilele cha idadi ya wahubiri wa Ufalme kiliongezeka kwa asilimia 35—kutoka 49,171 hadi 66,211! Lakini si hayo tu, kwani wahubiri hao wamekuwa wenye bidii sana, kama vile iwezavyo kuonwa kwa maongezeko mazuri katika maangusho ya fasihi ya Biblia, kutia na magazeti. Wametumia vema broshua na vijitabu pia, wakiangusha 1,654,559. Hiyo ni zaidi ya mara tatu ya tarakimu ya mwaka jana ya 477,235! Itikio limekuwa nini kwa maangusho yote hayo? Kuongezeka maradufu kwa idadi ya mafunzo ya Biblia nyumbani. Sasa mafunzo ya Biblia 38,484 yanaongozwa.
Pia, kushiriki katika utumishi wa upainia msaidizi kuliongezeka kwa asilimia 94. Hilo bila shaka lilichangia ile idadi yenye kutokeza ya wanafunzi waliobatizwa karibuni, 26,986, kwa kulinganishwa na idadi ya mwaka jana ya 6,570, ongezeko la kushangaza la asilimia 311!
Baadhi ya wale waliobatizwa karibuni walikujaje kupendezwa na habari njema? Nyakati nyingine hangaiko lenye kina la Shahidi aliyekuwa akiongoza funzo lilikuwa ndiyo sababu moja. Mwangalizi-msimamizi kutoka Moldova asimulia hivi:
“Mke wangu na mimi tulimtembelea mwanamke aliyekuwa ameonyesha kupendezwa na kweli ya Biblia hapo awali. Funzo la Biblia lilianzwa naye. Hata hivyo, mume wake hakuonyesha kupendezwa hata kidogo. Siku moja tulipokuwa njiani kwenda kumtembelea mwanamke huyo ili kuendelea na funzo, hali-hewa ilikuwa yenye baridi nyingi na yenye theluji. Watu wachache sana walikuwa barabarani, lakini tulifika nyumbani kwake wakati uliowekwa barabara. Alimwambia mume wake hivi: ‘Je! waona kadiri ambavyo watu hawa wanatujali sisi? Wanafika kwa wakati barabara ijapokuwa theluji.’ Tukio hilo lilimsababisha mume wake afikiri. Alibadili nia yake akajiunga katika funzo, na sasa yeye na mke wake ni Mashahidi waliobatizwa.”
Nyakati nyingine adabu nzuri ya Shahidi huenda ikachochea kupendezwa na habari njema. Mzee mmoja, kutoka Moldova pia, alikuwa na ono hili:
“Mwanamume mmoja niliyemtembelea katika eneo langu la kuhubiri hakupendezwa na Mashahidi wa Yehova. Alisema kwamba alikuwa wa dini ya Orthodoksi, sawa na baba na babu yake. Kwa hiyo aliniomba niondoke kwenye makao yake. Hata hivyo, kabla ya mimi kuondoka, alinipa nafasi ya kumwambia sababu ya ziara yangu. Nilielekeza kwenye Mathayo 28:19, linalotaarifu hivi: ‘Enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].’ Kisha nikampa anwani ya mahali petu pa kukutania na kuondoka. Kwa mshangao wangu, juma moja baadaye mwanamume huyo alikuja kwenye mkutano wetu! Alikaa mpaka programu ilipokwisha. Alieleza kwamba muda wote wa juma hilo, alikuwa amehisi majuto kwa sababu ya kunitenda kwa njia isiyo ya kirafiki. Funzo la Biblia lilianzishwa mara hiyo, na sasa yeye ni mmoja wa ndugu zetu.”
Sehemu nyingine yenye kutokeza ya mwaka wa utumishi imekuwa lile itikio jingine kwa mahitaji ya ndugu zetu katika eneo hilo. Katika kipindi cha baridi cha 1991/92, tani 400 hivi za vyakula na kiasi kikubwa cha nguo za wanaume, wanawake, na watoto vilipelekwa kwa wale wenye uhitaji. Maandalizi hayo yaligawanywa kwa kweli katika kila pande za eneo la ile iliyokuwa Muungano wa Sovieti, hata mbali kufikia Irkutsk katika Siberia na Khabarovsk, karibu na Japani. Wonyesho wenye kuvutia kwelikweli wa kwamba Yehova hakusahau upendo ule ambao ndugu zetu wameonyesha kwa jina lake! Uthibitisho huo wa upendo wa kidugu unaochochewa na roho ya Yehova umekuwa pia na tokeo la kuwaunganisha na familia ya ulimwenguni pote. Kwa mfano, dada mmoja katika Ukrainia aliandikia ofisi ya tawi hivi:
“Msaada mliotupa sisi uligusa sana mioyo yetu. Tulichochewa hadi kutokwa na machozi na tukamshukuru Yehova Mungu kwa ajili ya kutotusahau. Ni kweli, tuna magumu mengi ya kimwili sasa, lakini kwa sababu ya msaada uliowasili kutoka kwa ndugu katika Magharibi, tulipona kimwili. Sasa, kwa sababu ya msaada wenu, familia yetu itaweza kutumia wakati mwingi zaidi katika utumishi wa Yehova. Yehova akipenda, binti yangu na mimi tutafanya upainia msaidizi katika miezi ya kiangazi.”
Kuongezea, ile jitihada ya kutoa msaada ilitolea ushahidi watu wasio Mashahidi kwa sababu watazamaji waliweza kuona kwamba Mashahidi huonyesha upendo kwa matendo yao. Familia moja kutoka kundi jingine iliandika hivi: “Tulipokea msaada wa kimwili wa chakula na nguo. Ni vingi sana! Utegemezo na kitia-moyo chenu ni somo kwetu kwamba sisi pia twapaswa kuwafanyia wengine mema. Tendo hilo la upendo halikupita bila kuonwa na wasioamini, pamoja na watu wenye kupendezwa na familia zao; limetoa ushahidi mkubwa sana juu ya udugu wa kweli.”
Mikusanyiko ya wilaya mitano na mkusanyiko wa kimataifa mmoja wenye kichwa “Wachukuaji Nuru,” uliofanywa miezi ya Juni na Julai iliyopita, ilikuwa uthibitisho mwingine wa baraka ya Yehova juu ya kazi ngumu ya Mashahidi wake na upendo ambao wameonyesha kwa kujulisha jina lake. Mikusanyiko hiyo ilihudhuriwa na watu 91,673, na 8,562 wakabatizwa. Hudhurio lililokuwa kubwa zaidi lilikuwa katika St. Petersburg, mahali pa mkusanyiko wa kimataifa, ambapo 46,214—kutia na wajumbe kutoka nchi 30 kuzunguka ulimwengu—walikusanyika kwenye Stediamu ya Kirov.
Katika Siberia mwanamume mmoja mwenye miaka 60 hivi alikuja penye mkusanyiko katika Irkutsk ili kuchunguza tu. Alisema hivi: “Wahudhuriaji wote wamejivalia vema, ni wenye nyuso zenye kutabasamu, na ni wenye fadhili mmoja kwa mwenzake. Watu hawa ni kama familia moja yenye umoja. Mmoja aweza kuhisi kwamba wao ni marafiki si kwenye stediamu tu bali pia katika utendaji wa kila siku. Nilipokea fasihi ya Biblia iliyo bora sana na kujifunza vema zaidi hili ni tengenezo la aina gani. Ninataka kuendelea kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova na kujifunza Biblia pamoja nao.”
Kwenye mkusanyiko uo huo katika Irkutsk, ambako 5,051 walihudhuria, mwanamke mmoja mwenye kupendezwa kutoka Jamhuri ya Yakut, Siberia, alisema hivi: “Mimi huwatazama watu hao, na kutaka kulia kwa shangwe. Ninamshukuru Yehova sana kwamba alinisaidia kuwajua watu wa jinsi hiyo. Hapa kwenye mkusanyiko, nimepokea fasihi, na ninataka kuongea na wengine juu yayo. Nataka sana kuwa mwabudu wa Yehova.”
Mkurugenzi wa Stediamu Kuu katika Alma Ata, Kazakhstan, ambako 6,605 walihudhuria mkusanyiko, alisema yafuatayo: “Nimesisimuliwa na mtazamo wenu. Sasa nimesadikishwa kwamba nyinyi nyote, vijana kwa wazee, ni watu wenye kustahika. Siwezi kusema kwamba ninaamini katika Mungu, lakini ninaamini katika mambo matakatifu yanayowasilishwa na udugu wenu, katika mtazamo wenu kuelekea thamani za kiroho na za kimwili.”
Ofisa mmoja wa polisi kwenye mkusanyiko wa Alma Ata alionelea hivi: “Nimekutana na nyinyi watu mara mbili, kila mara ikiwa kwenye mkusanyiko. Ni jambo lenye kupendeza sana kufanya kazi pamoja na Mashahidi wa Yehova.”
Romania
Yehova hakusahau pia upendo ule ambao ndugu katika Romania wameonyesha kwa jina lake. Mwaka wa utumishi huo uliopita ulikuwa na matukio mengi ya furaha kwa Mashahidi. Kwanza, ofisi ya tawi ilianzishwa mara nyingine tena katika Bucharest. Utendaji halali wa mwisho ulikoma katika 1949. Ofisi hiyo ina ndugu na dada karibu 20 wakifanya kazi kwenye vifaa hivyo vipya. Ofisi hiyo ya tawi inatumikia wahubiri 24,752—kilele chenye kupita vyote kinachowakilisha ongezeko la asilimia 21 kupita wastani wa mwaka jana.
Baada ya miaka kadhaa ya kuhubiri kwa siri, wahubiri wanazoea vema zaidi kazi ya kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba peupe. Jambo lililoonwa kutoka Jimbo la Mureş laonyesha jinsi Mashahidi wengine wanavyotumia vizuri nafasi yoyote ya kuwahubiri wengine, hata wakati wanaposafiri. Ofisi ya tawi yaandika hivi:
“Mhubiri mmoja aliamua kuhubiri kutoka behewa moja la gari moshi hadi jingine. Itikio la watu lilikuwa lenye upendeleo kwa ujumla, lakini katika behewa la mwisho, matatizo yalitokea. Hakuna hata abiria mmoja aliyetaka kuchukua nakala ya magazeti yetu. Mwishowe, mwanamume mmoja, akiwa ameudhika sana, akasimama na kupaaza sauti: ‘Nitayatupa magazeti yako yote nje! Kwa nini watusumbua sana na dini yako?’ Mhubiri huyo akajibu kwa fadhili kwamba hata kama angeyatupa magazeti hayo nje, mtu mwingine angenufaishwa na tendo lake—wale ambao wangeyaokota magazeti hayo. Akiona utulivu wa mhubiri, huyo mwanamume alivutiwa sana hivi kwamba aliyachukua magazeti hayo na kuanza kuyagawanya yeye mwenyewe kwa maabiria wengine katika behewa hilo. Kwa kushangaza, wote walichukua kila mtu gazeti. Baada ya kuyagawanya, mwanamume huyo hakuwa na nakala ya kujipatia. Kwa hiyo, mhubiri alimwuliza: ‘Bwana, hutaki kujipatia nakala zozote?’ Ndipo mwanamume huyo akatwaa gazeti moja kutoka kwa abiria mmoja aliyekuwa na nakala mbili na kusema: ‘Sasa nakala moja imenifikia mimi pia!’”
Katika nchi nyingi kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova nyakati nyingine imechochea upinzani wa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Katika Romania, makasisi wa Kanisa la Orthodoksi mara nyingi hukasirika na Mashahidi. Lakini hilo haliwezi kumzuia Yehova asiwabariki watu wake kwa upendo ule ambao wameonyesha kwa jina lake. Mwangalizi mmoja wa mzunguko aandika hivi:
“Tulienda kwenye utumishi mashambani, pamoja na kundi la huko. Kulikuwako ndugu mia moja. Tulikodi basi lililotupeleka karibu kilometa 50 ndani ya eneo la mashambani, kwenye mji mdogo. Tuliwaalika wengi kwenye hotuba ya watu wote ambayo ingetolewa katika Jumba la Kitamaduni. Mara mkutano ulipoanza, kasisi wa Kanisa la Orthodoksi aliwasili kuuvuruga mkutano wetu. Maofisa wa polisi walijaribu kumzuia kasisi huyo. Hata hivyo, alikataa kutulia. Alifanikiwa kuusimamisha mkutano alipovunja kioo cha mlango mkuu wa kuingilia. Hata hivyo, wakazi wengi wa hapo hawakukubaliana hata kidogo na tabia ya kasisi huyo. Ushahidi kamili ungeweza sasa kutolewa kwa wote waliohudhuria, na kiasi kikubwa cha fasihi kiligawanywa.”
Kwa kusikitisha, katika sehemu nyinginezo za nchi, kuna Mashahidi wachache sana. Painia mmoja wa kawaida alipowasili jimbo la Olt kwa mara ya kwanza, alipata ndugu tisa tu katika jimbo zima na eneo kubwa la kuhubiri. Baada ya mwaka mmoja idadi ya Mashahidi iliongezeka hadi 27, ambao tano kati yao walikuwa wahubiri walioanzishwa kutenda tena. Painia huyo alipata makao katika jiji la Korabia, ambako hakukuwa Mashahidi wowote. Baada ya Mashahidi kuwa huko siku 45 tu, kasisi wa huko aliteta dhidi ya kazi yao kupitia redio ya Kraiova. Alisema kwamba Mashahidi walikuwa “wamelivamia” jiji la Korabia na mafundisho yao, wakijaribu kufanya watu wabadili dini yao. Mashambulio hayo yaliendelea, kwa kusudi la kukomesha kazi hiyo na kuharibu sifa nzuri ya Mashahidi katika eneo hilo. Upeo wa hayo yote ulifika wakati ndugu wa hapo walipokuwa Bucharest kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya. Kasisi wa Kanisa la Orthodoksi wa Korabia alitangaza hivi kwa uthabiti baada ya mahubiri yake ya kanisa: “Sote twapaswa kufanya mwandamano wa kuteta barabarani ili kuwachochea polisi wachukue hatua dhidi ya Mashahidi, ambao wamejaza eneo zima na vichapo vyao na kuwapotosha watu.” Lakini usiku uleule kabla ya mkutano huo kufanywa, jambo lisilo la kawaida lilitukia. Kikundi cha waharabu kiliharibu Kathedro na Jumba la Kitamaduni la Mji. Kwa hiyo, mkutano wa kuteta haukufanywa kamwe!
Maeneo ya Ile Iliyokuwa Yugoslavia
Mwaka wa utumishi wa 1992 umekuwa mwaka mgumu zaidi kwa ndugu katika eneo la Yugoslavia. Hata hivyo, wakati huohuo, wamekuwa na maono yenye shangwe. Kwa shukrani, Yehova hasahau kazi yao na upendo walioonyesha kwa jina lake.
Vita ilianza kwanza katika Slovenia, halafu katika Kroatia, na baadaye katika Bosnia na Herzegovina. Katika mwaka mmoja tu, kutoka jamhuri moja, Serikali tano mpya zilikuwa zikijaribu kuweka mipaka, sheria, na fedha zazo zenyewe. Mamia ya Mashahidi walilazimika waondoke makao yao na kupata himaya pamoja na ndugu zao katika sehemu nyinginezo. Kama vile katika nchi nyinginezo katika Ulaya ya Mashariki, halmashauri za dharura ziliwekwa rasmi katika majiji makubwa zaidi, zikishughulikia makao, chakula, na mavazi kwa ajili ya ndugu zetu wenye uhitaji. Katika mwaka wa utumishi, karibu tani 55 za chakula ziligawanywa kwa akina ndugu katika makundi ndani ya maeneo yenye shida. Barua nyingi za shukrani zimepokewa.
Akina ndugu katika Dubrovnik walisimulia jinsi walivyokuwa na shukrani kwa ajili ya msaada uliotolewa. Dada mmoja alipokuwa akiwenda nyumbani akiwa na kifurushi cha chakula, jirani yake alimwuliza alikoyanunua mayai hayo. Dada alimwambia kwamba ndugu zake wa kiroho katika sehemu nyingine walikuwa wamempelekea. Jirani huyo alistaajabu. Katika kisa kingine mtu asiyejulikana kutoka Slovenia alimpigia simu mzee mmoja na kusema hivi: “Nimesikia ya kwamba Mashahidi wa Yehova wanagawanya chakula wanachopokea kutoka kwa ndugu zao katika njia inayofaa. Nimewapelekea watu vifurushi kadhaa; hata hivyo, havikufikia vituo vyavyo. Je! naweza kuwapelekea vifaa vya misaada, na mvigawanye?” Pia, magazeti ya habari na redio viliripoti kwa upendeleo juu ya kazi yetu ya kutoa msaada.
Ndugu mmoja aliyebatizwa kwenye mkusanyiko wa kimataifa katika Zagreb katika 1991 alikuwa ametambua magumu yaliyokuwa yakitokea na hivyo akanunua duka zima la chakula. Alichukua chakula hicho nyumbani kwake karibu na eneo la vita. Upungufu wa chakula ulipokuwa mbaya zaidi, ugavi huo ulithibitika kuwa baraka ya kweli kwa akina ndugu.
Iliwezekana kupata cheti cha ruhusa kwa ajili ya lori kubwa ya kupeleka chakula cha kawaida kwa akina ndugu waliokuwa wamezingiwa katika Sarajevo. Twafurahi kusema kwamba kiliweza kupelekwa kwa mafanikio.
Mapigano yamewadhuru raia. Kwa huzuni, kufikia mwisho wa mwaka wa utumishi, ndugu na dada zetu sita na watu wawili wenye kupendezwa walikuwa wamekufa, na wengine walikuwa wamejeruhiwa.
Hata hivyo, maono mengi yanaonyesha kwa ujumla, kwamba ni ulinzi kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Katika kisa kimoja akina ndugu walikuwa wakisafiri kwenda kwenye mkusanyiko wa wilaya katika Belgrade wakati basi liliposimamishwa na wanajeshi, wakiuliza kama kulikuwako washiriki wa dini fulani miongoni mwao. Akina ndugu walijibu kwamba hakukuwa wowote. Walilazimika waonyeshe vitambulisho vyao, na baadhi yao walikuwa na majina yaliyoonyesha kwamba wangeweza kuwa wa dini hiyo. Wanajeshi hao waliwashtaki juu ya kusema uwongo, lakini ndugu hao walikuwa na barua zao za kuarifu kanisa kwamba walikuwa wameliacha; hata ingawa walikuwa wamezaliwa katika dini hiyo, walitaarifu kwamba sasa walikuwa Mashahidi wa Yehova, wakisafiri kwenda kwenye mkusanyiko wao. Baada ya hiyo wanajeshi hao waliwaacha waendelee na safari.
Mapainia wanaendelea na utumishi wao kwa bidii isiyopungua, na hilo limethibitika kuwa kichocheo cha kweli kwa kazi hiyo. Mnara wa Mlinzi, lenye majalada yalo yanayochangamsha ya rangi kamili, linatafsiriwa sawia katika lugha zote kuu za mkoa huo. Linawaandalia kwa kawaida wapendao kweli na uadilifu “posho kwa wakati wake.” (Luka 12:42) Katika mwaka wa utumishi wa 1992, ndugu na dada wapya 674 walibatizwa.
Kwa hakika, Mungu hakusahau kazi ya akina ndugu katika Ulaya ya Mashariki na upendo ambao wameonyesha kwa jina lake. Zaidi ya hayo, anatamani kwamba waabudu wake wote, haidhuru wanakoishi, wafuate lile shauri zuri ambalo Paulo alitoa baadaye, kwenye Waebrania 6:11, linalosema hivi: “Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho.”