Kutoweza Kufa kwa Nafsi—Chanzo cha Fundisho Hilo
“Hakuna kichwa cha mazungumzo ambacho, kwa kulinganisha na uhai wake wenye chanzo cha kiroho, kimevuta akili ya mwanadamu sana kama kile cha hali yake ya baada ya kifo.”—“ENCYCLOPÆDIA OF RELIGION AND ETHICS.”
1-3. Namna gani Socrates na Plato waliendeleza wazo la kwamba nafsi ni isiyoweza kufa?
MTAALAMU na mwalimu mwenye umri wa miaka 70 alishtakiwa ukosefu wa heshima kwa Mungu na uharibifu wa mawazo ya vijana kwa fundisho lake. Ingawa alijitetea kwa akili sana wakati wa kusambishwa, baraza la waamzi wenye upendeleo lilimpata na kosa na hivyo akahukumiwa kifo. Saa chache kabla ya kuuawa, mwalimu huyu mzee atolea wanafunzi waliokusanyika kumzunguka mfululizo wa sababu ili kuhakikisha kwamba nafsi ni isiyoweza kufa na kwamba kifo si jambo la kuogopa.
2 Mwanaume huyu aliyehukumiwa kifo ni Socrates, mwanafalsafa Mgiriki mwenye sifa sana wa karne ya tano K.W.K.a Mwanafunzi wake Plato aliandika matukio haya katika vitabu Apologie na Phaedo. Socrates na Plato ni wenye kusifiwa kuwa kati ya watu wa kwanza walioendeleza mbele wazo la kwamba nafsi ni isiyoweza kufa. Lakini si wao walio vyanzo vya fundisho hilo.
3 Kama tutakavyoona, vyanzo vya wazo hilo la kutoweza kufa kwa nafsi ya binadamu ni tangu nyakati za mapema zaidi. Lakini Socrates na Plato, ndio waliolikuza sana wazo hili na kulifanya kuwa fundisho la kifalsafa, hivyo kulifanya livutie zaidi jamii za watu wenye elimu wa siku zao na kuendelea.
Kutoka Pythagoras mpaka Mapiramidi
4. Kabla ya Socrates, maoni ya Wagiriki yalikuwa nini kuhusu maisha ya baadaye?
4 Wagiriki walioishi kabla ya Socrates na Plato pia waliamini kwamba nafsi inaendelea kuishi baada ya kifo. Pythagoras, Mgiriki mwenye elimu ya hesabu ajulikanaye sana wa karne ya sita K.W.K., alishikilia kwamba nafsi ni isiyoweza kufa na hivyo yapaswa kugeuka na kuingia mwili mwingine. Kabla yake, Thales wa Miletus, aliyefikiriwa kuwa mwanafalsafa Mgiriki aliyejulikana mapema zaidi, alifikiri kwamba nafsi isiyoweza kufa inapatikana si tu katika watu, wanyama na mimea lakini pia imo katika vitu kama smaku, kwa kuwa inaweza kusogeza chuma. Wagiriki wa kale walidai kwamba nafsi za wafu zilikuwa zikichukuliwa kwa mashua ndogo kuvuka mto Styx mpaka kwenye nchi kubwa chini ya ardhi iitwayo Ulimwengu wa chini. Huko, waamuzi wahukumia zile nafsi kuingia ama kwenye mateso katika gereza lenye kuzungukwa na kuta ndefu sana, ama kwenye raha kamili katika makao ya waliobarikiwa baada ya kifo.
5, 6. Waajemi waliiona nafsi namna gani?
5 Katika Irani, au Uajemi, kuelekea mashariki, nabii aitwaye Zoroastre alitokea katika karne ya saba K.W.K. Yeye aliingiza namna ya ibada iliyojulikana baadaye kuwa Kizoroastriani. Hiyo ilikuwa dini ya Milki ya Uajemi, iliyoutawala ulimwengu kabla ya Ugiriki kuwa nguvu kubwa ya ulimwengu. Maandishi ya Kizoroastriani yasema: “Nafsi ya Mwadilifu itakuwa milele katika shangwe ikiwa isiyoweza kufa, lakini nafsi ya Mwongo hakika itakuwa yenye kuteswa. Na hizi amri Ahura Mazda [maana yake mungu mwenye hekima] ameziamuru kupitia enzi Yake yenye mamlaka.”
6 Lile fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi lilikuwa pia sehemu ya dini ya Kiirani ya kabla ya Kizoroatriani. Kwa mfano, makabila ya zamani ya Irani yalishugulikia nafsi za waliokufa kwa kuwatolea chakula na mavazi ili kuwafaidi hao walio katika ulimwengu wa chini.
7, 8. Wamisri wa kale waliamini nini kuhusu kuokoka kifo cha mwili kwa nafsi?
7 Imani katika uhai baada ya kifo ilikuwa fundisho la maana sana katika dini ya Misri. Wamisri walishikilia kwamba ile nafsi ya mtu aliyekufa ingeweza kuhukumiwa na Osiris, mungu mkuu katika ulimwengu wa chini. Kwa mfano, maandishi ya funjo (papyrus) yanayodaiwa kuwa ya kutoka karne ya 14 K.W.K. yaonyesha Anubis, mungu wa wafu, akiongoza nafsi ya yule mwandishi Hunefer mbele ya Osiris. Moyo wa mwandishi ukiwakilishwa na dhamiri yake, unapimwa juu ya mizani dhidi ya nyoya ambayo mungu mke wa ukweli na haki huvaa kwenye kichwa chake. Thoth, mungu mwingine, hurekodi matokeo. Kwa kuwa moyo wa Hunefer si mzito kwa kulemewa na kosa, wapima uzito ulio chini ya lile nyoya, naye Hunefer aruhusiwa kuingia nchi ya Osiris na kupata kutoweza kufa. Funjo hilo huonyesha pia dubwana wa kike akisimama pembeni ya mizani, tayari kumla mtu aliyekufa ikiwa moyo wake unashindwa jaribio. Wamisri pia walikuwa wakimumiani wafu wao ili wasioze na kulinda miili ya mafarao katika mapiramidi yenye kustaajabisha kwa kuwa walifikiri kwamba kuokoka kwa nafsi kulitegemea kulindwa kwa mwili.
8 Kwa hiyo, ustaarabu mbalimbali wa kale ulishikilia kwa umoja fundisho moja—kule kutoweza kufa kwa nafsi. Je! walipata fundisho hili kutoka chanzo kilekile kimoja?
Chanzo-Asili
9. Ni dini gani iliyokuwa na uvutano juu ya ulimwengu wa kale wa Misri, Uajemi na Ugiriki?
9 Kitabu The Religion of Babylonia and Assyria chasema: “Katika ulimwengu wa zamani, Misri, Uajemi, na Ugiriki zilihisi uvutano wa dini ya Kibabuloni.” Kitabu hiki kinaendelea kufasiria: “Katika mwono wa muungano wa mapema kati ya Misri na Babuloni, kama ilivyofunuliwa na vibao vya kuandikia vya El-Amarna, bila shaka kulikuwa uwezekano mwingi wa kuingia kwa maoni na desturi za Kibabuloni katika ibada za Misri. Katika Uajemi, ibada ya Mithra hufunua uvutano ulio wazi wa mawazo ya Kibabuloni . . . Mchanganyiko wenye nguvu wa sehemu ya Kisemiti katika hadithi za kwanza za Kigiriki na pia katika madhehebu ya kwanza ya Kigiriki sasa unakubaliwa kwa ujumla na wanachuo kuwa hauhitaji maelezo zaidi. Sehemu hizo za Kisemiti kwa kadiri kubwa ni za Kibabuloni hasa.”b
10, 11. Maoni ya Wababuloni kuhusu uhai baada ya kifo yalikuwa nini?
10 Lakini, je! maoni ya Kibabuloni kuhusu jambo linalotukia baada ya kifo hayatofautiani kabisa na yale ya Kimisri, Kiajemi na Kigiriki? Kwa mfano, fikiria Utungo wa Kishairi wa Gilgamesh. Mwanamume shujaa mzee, Gilgamesh, akisumbuliwa mara kwa mara na kuwapo kwa kifo, ashika njia akitafuta kutoweza kufa lakini ashindwa kukupata. Katika safari akutana na kijana mwanamke mchuuza-mvinyo ambaye pia humsadikisha apate faida yote ya maisha aliyo nayo sasa, kwa kuwa hatapata uhai usiokuwa na mwisho autafutao. Ujumbe wa utungo mzima wa shairi ni kwamba kifo hakiepukiki na tumaini la kutoweza kufa ni ndoto tu. Je! hili laonyesha sasa kwamba Wababuloni hawakuamini katika maisha ya kisha kufa?
11 Profesa Morris Jastrow, Jr., wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania, Shirikisho la Amerika, aliandika: “Wala watu wala viongozi wa kidini [wa Babuloni] hawakufikiria kamwe uwezekano wa kutoweka kabisa kwa kile ambacho wakati moja kilikuja kwenye uhai. Kifo [katika maoni yao] kilikuwa mpito wa kuingia katika aina nyingine ya uhai, na kukana kutokufa kwa mtu ni kutilia tu mkazo kwamba mtu hawezi kuepuka kifo ambacho, kulingana na imani yao, humpeleka mtu kwenye aina nyingine ya uhai.” Ndiyo, Wababuloni waliamini pia kwamba uhai wa aina nyingine, katika umbo lingine, uliendelea kuwako baada ya kifo. Walionyesha wazo hilo kwa kuzika vitu fulani pamoja na mfu ili aendelee kuvitumia baadaye.
12-14. (a) Kisha Garika, chanzo cha fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi kilikuwa wapi? (b) Namna gani fundisho hili lilisambaa juu ya dunia?
12 Bila shaka, lile fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi larudi nyuma huko Babuloni wa kale. Kulingana na Biblia, kitabu chenye kutia alama historia sahihi, jiji la Babeli au Babuloni liliwekewa msingi na Nimrodi, mjukuu mkubwa wa Noa.c Kisha Garika ya ulimwenguni pote katika siku za Noa, kulikuwako lugha moja na dini moja tu. Kwa kuanzisha jiji na kuujenga mnara wake hapo, Nimrodi alianzisha dini nyingine. Maandishi ya Biblia huonyesha kwamba kisha mvurugo wa lugha huko Babeli, wajenzi wa mnara ambao hawakufanikiwa walisambaa na kufanyiza mianzo mipya, wakichukua pamoja nao dini yao. (Mwanzo 10:6-10; 11:4-9) Hivyo mafundisho ya kidini ya Kibabuloni yalisambaa juu ya uso wa dunia.
13 Kulingana na mapokeo, Nimrodi alikufa kifo chenye jeuri. Kisha kifo chake Wababuloni kwa sababu zenye kusikika wangelikuwa na mwelekeo wa kumheshimu sana kama mwanzilishi, mjenzi na mfalme wa kwanza wa jiji lao. Kwa kuwa mungu Marduku (Merodak) alifikiriwa kuwa mwanzilishi wa Babuloni, wasomi wengine wamependekeza kwamba Marduku awakilisha Nimrodi aliyefanywa kuwa mungu. Ikiwa ni hivyo, basi lile wazo la kwamba mtu anayo nafsi ambayo huendelea kuishi baada ya kufa lilikubaliwa na wengi haikosi wakati wa kifo cha Nimrodi. Kwa vyovyote, kurasa zenye kuandikwa za historia hufunua kwamba kufuatia Garika, chanzo cha fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi kilikuwa ni Babuloni.
14 Basi, namna gani fundisho hilo lilikuja kuwa la lazima sana katika dini nyingi za wakati wetu? Sehemu ifuatayo itachunguza kuingia kwa fundisho hili katika dini za Mashariki.
[Maelezo ya Chini]
a K.W.K. humaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.” W.K. huonyesha “Wakati wa Kawaida,” ambao mara nyingi huitwa A.D., kwa Anno Domini, ikimaanisha “katika mwaka wa Bwana wetu.”
b El-Amarna ni uwanja wenye magofu wa mji Akhetaton wa Misri, unaodaiwa kuwa ulijengwa katika karne ya 14 K.W.K.
c Tazama Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kurusa 37-54, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Maoni ya Wamisri juu ya nafsi zilizo katika ulimwengu wa chini
[Picha katika ukurasa wa 7]
Socrates alijadili kwamba nafsi ni isiyokufa