Tumaini Zuri Zaidi kwa Ajili ya Nafsi
ASKARI-JESHI Waroma hawakuwa wametazamia tokeo hili. Walipokuwa wakishambulia ngome ya mlimani ya Masada, ngome ya mwisho ya majeshi ya uasi ya Wayahudi, walijitayarisha kwa ajili ya shambulio la maadui wao, kwa ajili ya makelele ya askari, kwa ajili ya vilio vya wanawake na watoto. Badala ya hivyo walisikia mialiko ya miali ya moto. Walipokuwa wakiichunguza hiyo ngome iliyokuwa ikichomeka, hao Waroma walipata kujua ule ukweli mbaya sana: maadui wao—watu wapatao 960—walikuwa wamekufa tayari! Kwa utaratibu, wale askari Wayahudi walikuwa wameua familia zao wenyewe, kisha wakauana. Mtu wa mwisho akajiua mwenyewe.a Ni jambo gani lililokuwa limewaongoza kwenye uuaji huo wa kimakusudi wa watu wengi sana na kule kujiua?
Kulingana na mwanahistoria Yosefo aliyeishi wakati huohuo, kisababishi cha maana kilikuwa ile itikadi katika nafsi isiyoweza kufa. Eleazar Ben Jair, yule kiongozi wa Wazeloti katika Masada, mwanzoni alikuwa amejaribu kuwashawishi wanaume wake kwamba kujiua kungekuwa jambo la kuheshimika zaidi kuliko kifo au utumwa mikononi mwa Waroma. Alipowaona wakisitasita, alianza kutoa hotuba ya kutoka moyoni juu ya nafsi. Aliwaambia kwamba mwili ulikuwa kizuizi tu, gereza la nafsi. “Lakini inapowekwa huru na uzito unaoivuta hadi duniani na unaoizingira,” yeye akaendelea, “nafsi inarudi mahali payo yenyewe, ndipo kwa kweli inaposhiriki nguvu zenye baraka na uweza usio na kikomo hata kidogo, ikiendelea kutoonekana kwa macho ya kibinadamu kama Mungu Mwenyewe.”
Itikio lilikuwa nini? Yosefo aripoti kwamba baada ya Eleazar kusema kuhusu jambo hilo kwa muda mrefu, “wasikilizaji wake wote walimkatiza na wakiwa wamejaa idili isiyodhibitika walifanya haraka kutimiza hilo tendo.” Yosefo aongeza hivi: “Kana kwamba walikuwa wamepagawa walienda mbio, kila mtu akiwa na hamu sana ya kufanya haraka zaidi kuliko yule mtu mwingine, . . . walikuwa wamenaswa na tamaa kubwa sana ya kuwaua wake zao, watoto wao, na wao wenyewe.”
Kielelezo hicho kibaya sana chatoa kielezi cha jinsi fundisho la kutokufa kwa nafsi liwezavyo kubadili maoni ya kawaida ya wanadamu juu ya kifo. Wale wanaoamini hivyo wanafundishwa kuona kifo, si kuwa adui mbaya zaidi wa binadamu, bali kuwa njia tu iwekayo huru nafsi ili ifurahie kuwako bora zaidi. Lakini kwa nini Wazeloti hao Wayahudi waliamini hivyo? Wengi wangedhani kwamba maandishi yao matakatifu, Maandiko ya Kiebrania, hufundisha kwamba binadamu ana roho yenye ufahamu ndani yake, nafsi inayoponyoka ili kuendelea kuishi baada ya kifo. Je, ndivyo ilivyo kweli?
Nafsi Katika Maandiko ya Kiebrania
Kwa neno moja, la. Mlemle katika kitabu cha kwanza chenyewe cha Biblia, Mwanzo, tunaambiwa kwamba nafsi si kitu fulani ulicho nacho, hiyo ni wewe mwenyewe. Twasoma hivi juu ya uumbaji wa Adamu, yule binadamu wa kwanza: “Mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7, italiki ni zetu.) Neno la Kiebrania linalotumiwa hapa kwa nafsi, neʹphesh, huonekana zaidi ya mara 700 katika Maandiko ya Kiebrania, bila kuonyesha kamwe hata mara moja wazo la kwamba kuna sehemu ya kiroho ya mwanadamu, iliyotengwa, iliyo ya kimbingu. Kinyume cha hilo, nafsi ni ya kugusika, ya kushikika, halisi.
Fungua katika nakala yako mwenyewe ya Biblia, maandiko yafuatayo yaliyotajwa, kwani neno la Kiebrania neʹphesh linapatikana katika kila moja yayo. Yanaonyesha kwa wazi kwamba nafsi yaweza kukabili tisho, hatari, na hata kutekwa nyara (Kumbukumbu la Torati 24:7; Waamuzi 9:17; 1 Samweli 19:11); kugusa vitu (Ayubu 6:7); kutiwa katika minyororo ya chuma (Zaburi 105:18); kutamani kula, kuteswa kwa kufunga, na kuzimia kwa sababu ya njaa na kiu; na kupatwa na ugonjwa wenye kudhoofisha au hata hali ya kukosa usingizi kwa sababu ya huzuni. (Kumbukumbu la Torati 12:20; Zaburi 35:13; 69:10; 106:15; 107:9; 119:28) Yaani, kwa sababu nafsi yako ni wewe, wewe binafsi, nafsi yako yaweza kupatwa na jambo lolote uwezalo kupatwa nalo.b
Lakini je, hilo lamaanisha kwamba kwa kweli nafsi yaweza kufa? Ndiyo. Kinyume sana cha kuwa na hali ya kutokufa, katika Maandiko ya Kiebrania nafsi za kibinadamu husemwa kuwa ‘zimekataliwa mbali,’ au kuuawa, kwa sababu ya kufanya kosa, kupigwa hata kufa, kuuawa kimakusudi, kuharibiwa, na kuraruliwa vipande-vipande. (Kutoka 31:14; Kumbukumbu la Torati 19:6; 22:26; Zaburi 7:2) “Nafusi ya mtu ifanyayo dhambi ndiyo itakayokufa,” lasema Ezekieli 18:4, The Old Testament in Swahili (Mombasa). Kwa wazi, kifo ndicho mwisho wa kawaida wa nafsi za kibinadamu, kwa kuwa sisi sote hufanya dhambi. (Zaburi 51:5) Binadamu wa kwanza, Adamu, aliambiwa kwamba adhabu ya dhambi ilikuwa kifo—si uhamisho hadi makao ya roho na hali ya kutokufa. (Mwanzo 2:17) Na alipofanya dhambi, hukumu hii ilitamkwa: “Kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Adamu na Hawa walipokufa, walikuwa tu kile ambacho Biblia hurejezea mara nyingi kuwa ‘nafsi zilizokufa.’—Hesabu 5:2; 6:6, NW.
Si ajabu sana kwamba The Encyclopedia Americana husema hivi juu ya nafsi katika Maandiko ya Kiebrania: “Dhana juu ya binadamu iliyo katika Agano la Kale ni ile ya muungano, si kufungamana kwa nafsi na mwili.” Yaongeza hivi: “Nefesh . . . haionwi kamwe kuwa yenye kutenda kazi kando ya mwili.”
Kwa hiyo, Wayahudi waaminifu waliamini kifo kuwa nini? Kusema kwa usahili, wao waliamini kwamba kifo ni kinyume cha uhai. Zaburi 146:4 husimulia lile linalotendeka wakati roho, au kani ya uhai, inapomwondoka binadamu: “Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”c Vivyo hivyo, Mfalme Sulemani aliandika kwamba wafu “hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5.
Basi, kwa nini Wayahudi wengi wa karne ya kwanza, kama wale Wazeloti katika Masada, walisadiki sana juu ya kutokufa kwa nafsi?
Uvutano wa Kigiriki
Wayahudi hawakupata wazo hili kutoka katika Biblia, bali kutoka kwa Wagiriki. Yaonekana hiyo dhana ilitoka katika madhehebu ya kidini yenye mafumbo ya Kigiriki na kuingia falsafa ya Kigiriki, kati ya karne ya saba na tano K.W.K. Wazo la kuwako kwa uhai baada ya kifo ambako nafsi mbaya zingepokea malipo yenye maumivu lilikuwa limewavutia watu wengi kwa muda mrefu, na hiyo dhana ikaimarika na kuenea. Wanafalsafa walibishana daima juu ya hali hususa ya nafsi. Homer alidai kwamba nafsi ilihama upesi wakati wa kifo, ikifanya sauti yenye kusikika ya kuvuma, mlio mwembamba mkali, au ya mchakacho. Epicurus alisema kwamba kwa kweli nafsi ilikuwa na uzani na basi ilikuwa na mwili mdogo mno.d
Lakini yule ambaye labda ndiye mwenye kuunga mkono zaidi kutokufa kwa nafsi alikuwa Plato, mwanafalsafa Mgiriki wa karne ya nne K.W.K. Ufafanuzi wake wa kifo cha mwalimu wake, Socrates, wafunua masadikisho yaliyofanana sana na yale ya Wazeloti wa Masada karne kadhaa baadaye. Kama vile msomi Oscar Cullmann aelezavyo, “Plato atuonyesha jinsi Socrates anavyokufa katika hali ya amani na utulivu kamili. Kifo cha Socrates ni kifo kizuri sana. Tisho la kifo halionekani hata kidogo. Socrates hawezi kuhofu kifo, kwa maana hicho kwa kweli hutuweka huru na mwili. . . . Kifo ni rafiki mkubwa wa nafsi. Ndivyo [Socrates] afundishavyo; na ndivyo anavyokufa, kwa kupatana vizuri ajabu na fundisho lake.”
Yaonekana ni katika kipindi cha Kimakabayo, katika karne ya pili kabla ya Kristo, kwamba Wayahudi walianza kutwaa fundisho hili kutoka kwa Wagiriki. Katika karne ya kwanza W.K., Yosefo atuambia kwamba Mafarisayo na Waesene—vikundi vya kidini vya Kiyahudi vyenye mamlaka—walifuata fundisho hilo. Ushairi fulani ambao labda ulitungwa katika muhula huo huonyesha itikadi hiyohiyo.
Lakini, namna gani Yesu Kristo? Je, yeye na wafuasi wake walifundisha pia wazo hili kutoka katika dini ya Kigiriki?
Maoni ya Wakristo wa Mapema Juu ya Nafsi
Wakristo wa karne ya kwanza hawakuiona nafsi sawa na vile Wagiriki walivyoiona. Kwa kielelezo, fikiria kifo cha Lazaro, rafiki ya Yesu. Ikiwa Lazaro angalikuwa na nafsi isiyoweza kufa iliyohama upesi, ikiwa uhuru na yenye furaha, wakati wa kifo, je, hilo simulizi katika Yohana sura ya 11 lisingalikuwa tofauti kabisa? Kwa hakika Yesu angaliwaambia wafuasi wake ikiwa Lazaro alikuwa hai na mzima na mwenye ufahamu huko mbinguni; kinyume cha hilo, yeye alisema kwa kupatana na Maandiko ya Kiebrania akawaambia kwamba Lazaro alikuwa amelala, bila ufahamu. (Mstari wa 11) Kwa hakika Yesu angalishangilia ikiwa rafiki yake alikuwa akifurahia kuwako kupya kuzuri ajabu; badala ya hivyo, twamwona akilia machozi hadharani juu ya kifo hicho. (Mstari wa 35) Kwa hakika, ikiwa nafsi ya Lazaro ingalikuwa mbinguni, ikifurahia hali ya kutokufa yenye raha, Yesu asingalikuwa kamwe mkatili sana hivi kwamba amwite ili arudi kuishi miaka mingine michache katika “gereza” la mwili wa nyama usio mkamilifu miongoni mwa wanadamu wagonjwa na wanaokufa.
Je, Lazaro alirudi kutoka kifo akiwa na masimulizi matukufu juu ya siku zake nne nzuri ajabu akiwa kiumbe cha roho kisicho na mwili? La, hakufanya hivyo. Waaminio kuwa nafsi haiwezi kufa wataitikia kwamba ilikuwa hivyo kwa sababu ono la mtu huyo lilikuwa lenye kutisha sana lisiweze kufafanuliwa kwa maneno. Lakini hoja hiyo yashindwa kusadikisha; kwani, je, Lazaro asingaliweza bado kuwaambia wapendwa wake angalau hivyo—yaani kwamba alikuwa amekuwa na ono zuri ajabu mno lisiweze kufafanuliwa? Badala ya hivyo, Lazaro hakusema lolote kuhusu maono yoyote aliyokuwa amekuwa nayo akiwa mfu. Ebu fikiria hili—mtu kutosema lolote juu ya habari ambayo wanadamu huchunguza zaidi kuliko nyingine yoyote: jinsi kifo kilivyo! Unyamavu huo waweza kuelezwa kwa njia moja pekee. Hakukuwa na jambo la kusimulia. Wafu wamelala, hawana ufahamu.
Kwa hiyo, je, Biblia huonyesha kifo kuwa rafiki ya nafsi, njia tu kati ya hatua mbili za kuwako? La! Kwa Wakristo wa kweli kama mtume Paulo, kifo hakikuwa rafiki; kilikuwa “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Wakristo hawaoni kifo kuwa jambo la asili, bali hukiona kuwa jambo baya sana, lisilo la asili, kwani ni tokeo la moja kwa moja la dhambi na uasi dhidi ya Mungu. (Warumi 5:12; 6:23) Hicho hakikuwa kamwe sehemu ya kusudi la Mungu la awali kwa ajili ya wanadamu.
Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawako bila tumaini kwa habari ya kifo cha nafsi. Ufufuo wa Lazaro ni mojapo masimulizi mengi ya Biblia yanayotuonyesha waziwazi tumaini la kweli, la Kimaandiko kwa ajili ya nafsi zilizokufa—ufufuo. Biblia hufundisha juu ya aina mbili tofauti za ufufuo. Kwa wanadamu walio wengi sana wanaolala kaburini, wawe ni waadilifu au wasio waadilifu, kuna tumaini la ufufuo kwenye uhai wa milele katika Paradiso hapa duniani. (Luka 23:43; Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Kwa kikundi kidogo ambacho Yesu alirejezea kuwa “kundi [lake] dogo,” kuna ufufuo kwenye uhai usioweza kufa wakiwa viumbe wa roho mbinguni. Hao, wanaotia ndani mitume wa Kristo, watatawala pamoja na Kristo Yesu juu ya wanadamu na kuwarudisha kwenye ukamilifu.—Luka 12:32; 1 Wakorintho 15:53, 54; Ufunuo 20:6.
Basi, ni kwa nini twaona makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yakifundisha kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu badala ya ufufuo? Fikiria hili jibu lililoandaliwa na mwanatheolojia Werner Jaeger katika The Harvard Theological Review huko nyuma katika 1959: “Jambo la hakika la maana zaidi katika historia ya mafundisho ya Kikristo lilikuwa kwamba yule baba wa theolojia ya Kikristo, Origen, alikuwa mwanafalsafa wa Kiplato kwenye shule ya Alexandria. Aliongezea mafundisho ya Kikristo yale mafundisho mengi kuhusu kutokufa kwa nafsi, aliyotwaa kutoka kwa Plato.” Kwa hiyo kanisa lilifanya sawa tu na vile Wayahudi walivyokuwa wamefanya karne kadhaa mapema! Yalipuuza mafundisho ya Kibiblia kwa kupendelea falsafa ya Kigiriki.
Machimbuko Halisi ya Hilo Fundisho
Sasa huenda watu fulani wakauliza, katika kutetea hili fundisho la nafsi isiyoweza kufa, Kwa nini dini nyingi sana za ulimwengu hufundisha jambo hilohilo, katika njia moja au nyingine? Maandiko hutoa sababu dhahiri kwa nini fundisho hilo limeenea sana katika jumuiya za kidini za ulimwengu huu.
Biblia hutuambia kwamba “ulimwengu wote unatawaliwa na yule mwovu” na humtambulisha kimahususi Shetani kuwa “mtawala wa ulimwengu huu.” (1 Yohana 5:19; Yohana 12:31, linganisha Habari Njema kwa Watu Wote.) Bila shaka, dini za ulimwengu haziepuki uvutano wa Shetani. Kinyume cha hivyo, zimechangia sana matatizo na ugomvi katika ulimwengu wa leo. Na kwa habari ya nafsi, yaonekana zinaonyesha fikira za Shetani kwa wazi sana. Jinsi gani?
Kumbuka ule uwongo wa kwanza kabisa kupata kusemwa. Mungu alikuwa amewaambia Adamu na Hawa kwamba tokeo lingekuwa kifo ikiwa wangefanya dhambi dhidi yake. Lakini Shetani alimhakikishia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4) Bila shaka, Adamu na Hawa walikufa; walirudi mavumbini sawa na vile Mungu alivyokuwa amesema. Shetani, “baba wa uwongo,” hakuuacha kamwe uwongo wake wa kwanza. (Yohana 8:44, HNWW) Katika dini zisizohesabika ambazo hukosa kufuata mafundisho ya Biblia au ambazo huyapuuza waziwazi, wazo hilihili huenezwa bado: ‘Hakika hutakufa. Huenda mwili wako ukaangamia, lakini nafsi yako itaendelea kuishi, milele—sawa na Mungu!’ Lakupendeza, Shetani alikuwa pia amemwambia Hawa kwamba yeye angekuwa “kama Mungu”!—Mwanzo 3:5.
Ni afadhali kama nini kuwa na tumaini linalotegemea kweli, badala ya uwongo au falsafa za kibinadamu. Ni afadhali kama nini kuwa na uhakika kwamba wapendwa wetu waliokufa wamo kaburini bila ufahamu badala ya kuhangaikia mahali ambapo nafsi isiyoweza kufa imeenda! Kulala huko kwa wafu hakupaswi kutuhofisha au kutushusha moyo. Kwa njia fulani, twaweza kuona wafu kuwa katika mahali salama pa kupumzikia. Kwa nini salama? Kwa sababu Biblia hutuhakikishia kwamba wafu wanaopendwa na Yehova wako hai katika maana ya pekee. (Luka 20:38) Wako hai katika kumbukumbu lake. Hilo ni wazo lenye kufariji sana kwa sababu kumbukumbu lake halina mipaka. Ana hamu ya kurudisha kwenye uhai mamilioni yasiyohesabika ya wanadamu wapendwa na kuyapa fursa ya kuishi milele juu ya dunia iliyo paradiso.—Linganisha Ayubu 14:14, 15.
Ile siku tukufu ya ufufuo itakuja, kwa kuwa ni lazima ahadi zote za Yehova zitimizwe. (Isaya 55:10, 11) Ebu fikiria unabii huu ukitimizwa: “Lakini wafu wako waishi, miili yao itainuka tena. Wale walalao katika dunia wataamka na kupiga kelele kwa shangwe; kwa kuwa umande wako ni umande wa nuru ya kumetameta, na dunia itawazaa tena wale waliokufa zamani.” (Isaya 26:19, The New English Bible) Kwa hiyo wafu wanaolala kaburini wako salama sawa na kitoto kilicho katika tumbo la uzazi la mama yacho. Wako karibu ‘kuzaliwa,’ kurudishwa kwenye uhai juu ya dunia iliyo paradiso!
Ni tumaini gani ambalo lingeweza kuwa zuri zaidi kuliko hilo?
[Maelezo ya Chini]
a Imeripotiwa kwamba wanawake wawili na watoto watano waliokoka kwa kujificha. Baadaye hao wanawake walisimulia mambo yote kwa Waroma waliowateka.
b Bila shaka, sawa na maneno mengi yawezayo kutumiwa kwa njia nyingi sana, neno neʹphesh pia lina maana mbalimbali. Kwa mfano, yaweza kurejezea mtu wa ndani, hasa katika kurejezea hisia zenye kina. (1 Samweli 18:1) Yaweza kurejezea pia maisha ambayo mtu hufurahia akiwa nafsi.—1 Wafalme 17:21-23.
c Neno la Kiebrania kwa “roho,” ruʹach, lamaanisha “pumzi” au “upepo.” Kuhusiana na wanadamu, hairejezei roho yenye ufahamu, bali, kama The New International Dictionary of New Testament Theology ielezavyo, yarejezea “kani ya uhai ya mtu.”
d Yeye hakuwa wa mwisho kuwa na fikira hizo za kigeni sana. Mapema karne hii, mwanasayansi fulani alidai kwa kweli kuwa alipima uzani wa nafsi za watu kadhaa kwa kupata tofauti ya uzani wao mara tu baada ya kifo na kabla tu ya kifo.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wazeloti Wayahudi katika Masada waliamini kwamba kifo kingeweka huru nafsi zao