Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 9/1 kur. 25-29
  • Yehova Amekuwa Jabali Langu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Amekuwa Jabali Langu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupata Familia ya Kiroho
  • Painia Aliye Peke Yake
  • Kuvumilia Mnyanyaso na Uhamisho
  • Ongezeko Licha ya Mnyanyaso
  • Yehova, “Mwokozi”
  • Nilipata Majaribu Makali Sana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Yatima Aliyeachwa Ampata Baba Mwenye Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kumpa Yehova Kile Anachostahili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 9/1 kur. 25-29

Yehova Amekuwa Jabali Langu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA EMMANUEL LIONOUDAKIS

Mama yangu alikunja uso na kuniambia: “Ukishikilia uamuzi wako, basi itakubidi uondoke katika nyumba hii.” Nilikuwa nimeamua kuhubiri Ufalme wa Mungu wakati wote. Hata hivyo, familia yetu haingeweza kuvumilia aibu iliyowapata kwa sababu ya kukamatwa kwangu mara kwa mara.

WAZAZI wangu walikuwa wanyenyekevu na wenye kumhofu Mungu. Waliishi katika kijiji cha Douliana, magharibi mwa kisiwa cha Ugiriki cha Krete, nilikozaliwa mwaka wa 1908. Tangu nilipokuwa kijana, walinifundisha kumhofu na kumstahi Mungu. Nilipenda Neno la Mungu, ingawa sikuwa nimepata kuona walimu au makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki wakiwa na Biblia.

Baada ya jirani fulani kusoma mabuku sita ya Studies in the Scriptures, yaliyoandikwa na C. T. Russell, na kitabu The Harp of God, alinieleza kwa shauku habari za Maandiko zenye kuelimisha zilizokuwa katika vitabu hivyo. Vitabu hivyo vilichapishwa na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Nilifurahi kupata Biblia na nakala za vitabu kutoka ofisi ya Watch Tower Society jijini Athene. Bado naweza kukumbuka tukikaa hadi usiku sana pamoja na jirani huyo, huku tukisali kwa Yehova, na kwa mwangaza wa mshumaa, kusoma Maandiko kwa bidii tukisaidiwa na vichapo hivyo.

Nilipoanza kuwaeleza wengine ujuzi wa Biblia niliokuwa nimepata karibuni, nilikuwa na umri wa miaka 20 nami nilikuwa mwalimu kwenye shule moja katika kijiji kilichokuwa karibu. Muda si muda, sisi tukiwa wanne tukaanza kufanya mikutano ya kujifunza Biblia kwa ukawaida huko Douliana. Pia, tuligawanya trakti, vijitabu, vitabu, na Biblia ili kuwasaidia wengine wajifunze tumaini pekee kwa wanadamu, Ufalme wa Mungu.

Katika mwaka wa 1931 tulikuwa kati ya maelfu ulimwenguni kote waliokubali jina Mashahidi wa Yehova, linalotegemea Biblia. (Isaya 43:10) Katika mwaka uliofuata, tulishiriki katika kampeni ya kuupasha umma habari, tukiwafafanulia wenye mamlaka jina letu jipya na umuhimu wake. Hilo lilitia ndani kugawanya kijitabu kilichokuwa na habari ifaayo kwa kila kasisi, hakimu, ofisa wa polisi, na mfanyabiashara katika eneo letu.

Kama ilivyotarajiwa, makasisi wakachochea mnyanyaso mwingi. Nilipokamatwa mara ya kwanza, nilihukumiwa kifungo cha siku 20 gerezani. Mara baada ya kuachiliwa, nikakamatwa tena na kuhukumiwa kifungo cha mwezi mmoja gerezani. Hakimu alipotaka tuache kuhubiri, tulijibu kwa maneno ya Matendo 5:29: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Baadaye, mwaka wa 1932, mwakilishi wa Watch Tower alikitembelea kikundi chetu kidogo huko Douliana, na sote wanne tukabatizwa.

Kupata Familia ya Kiroho

Kwa sababu ya tamaa yangu ya kutaka kufanya mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri, niliacha kazi ya ualimu. Mama yangu hakuweza kuvumilia jambo hilo. Akanitaka niondoke nyumbani. Kwa kibali cha ofisi ya tawi ya Watch Tower jijini Athene, nilikaribishwa kwa furaha nyumbani kwa ndugu Mkristo mkarimu wa jiji la Iráklion, Krete. Hivyo, katika Agosti 1933, ndugu kutoka katika kijiji changu cha nyumbani, pamoja na watu fulani wenye kupendezwa, wakaja kwenye kituo cha basi kuniaga. Huo ulikuwa wakati wenye kuhuzunisha sana, na sote tulilia, kwa kuwa hatukuwa na hakika juu ya wakati ambapo tungeonana tena.

Jijini Iráklion nilijiunga na familia moja ya kiroho yenye upendo. Kulikuwa na ndugu wengine watatu Wakristo na dada mmoja, tuliokutana nao kikawaida kwa ajili ya kujifunza na ibada. Ningeweza kuona moja kwa moja utimizo wa ahadi ya Yesu: “Hakuna ambaye ameacha nyumba au akina ndugu au akina dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati, nyumba na akina ndugu na akina dada na akina mama.” (Marko 10:29, 30) Niligawiwa kuhubiri katika jiji hilo na vijiji jirani. Nilipomaliza jiji, nilienda kuhubiri katika maeneo ya utawala ya Iráklion na Lasithion.

Painia Aliye Peke Yake

Nilitumia wakati mwingi nikitembea kijiji hadi kijiji. Isitoshe, ilinibidi kubeba kilogramu kadhaa za vichapo, kwa kuwa tulipokea fasihi mara chache. Kwa kuwa sikuwa na mahali pa kulala, nilikuwa nikienda katika mkahawa fulani kijijini na kungoja hadi mteja wa mwisho alipoondoka—kwa kawaida baada ya saa sita usiku—kisha nikalala kochini na kuamka mapema asubuhi iliyofuata kabla mwenye mkahawa hajaanza kuandaa vinywaji. Kochi hizo zilikuwa na viroboto wengi sana.

Ingawa watu walikuwa wenye ubaridi, nilifurahi kumtumikia Yehova kwa nguvu zangu za ujana. Nilipokuta mtu anayependezwa na kweli ya Biblia, hilo liliimarisha tena azimio langu la kuendelea na huduma hiyo ya kuokoa uhai. Iliburudisha pia kushirikiana na ndugu zangu wa kiroho. Nilikuwa nikikutana nao baada ya kutokuwepo kwa siku 20 hadi 50, ikitegemea umbali wa mahali nilipokuwa nikihubiri kutoka jiji la Iráklion.

Ningali nakumbuka vizuri sana jinsi nilivyoona upweke alasiri moja, hasa nilipokumbuka kwamba ndugu zangu na dada zangu Wakristo jijini Iráklion wangefanya mikutano yao ya kawaida jioni hiyo. Nilitamani sana kuwaona hivi kwamba niliamua kutembea kilometa 25 ili kufika walipokuwa. Sijawahi kutembea haraka hivyo. Ilifariji kama nini kufurahia ushirika mzuri pamoja na ndugu zangu jioni hiyo na kuimarishwa tena kiroho!

Muda si muda, jitihada zangu ngumu za kuhubiri zikaanza kuzaa matunda. Kama vile wakati wa mitume, ‘Yehova akaendelea kuongeza kwetu wale wenye kuokolewa.’ (Matendo 2:47) Idadi ya waabudu wa Yehova ikaanza kuongezeka kisiwani Krete. Wengine walipojiunga nami katika huduma, sikuona upweke tena. Tulivumilia shida za kimwili na mnyanyaso mkali. Tulikula mkate kila siku, na kuongezea mayai, zeituni, au mboga zozote tulizopata kwa kubadilishana na fasihi iliyochukuliwa na wale tuliowahubiria.

Mjini Ierápetra, kusini-mashariki mwa Krete, nilimhubiria muuza-nguo aliyeitwa Minos Kokkinakis. Licha ya jitihada zangu nyingi za kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye, hakuwa na wakati kwa sababu ya maisha yake yenye shughuli nyingi. Hata hivyo, hatimaye alipoamua kuchukua funzo lake la Biblia kwa uzito, alifanya mabadiliko makubwa maishani. Alipata pia kuwa mhubiri mwenye bidii zaidi wa habari njema. Emmanuel Paterakis mwenye umri wa miaka 18 ambaye alikuwa ameajiriwa na Kokkinakis, alivutiwa na mabadiliko hayo, na muda si muda, yeye pia akaomba fasihi ya Biblia. Nilifurahi kama nini kumwona akifanya maendeleo thabiti ya kiroho na hatimaye kuwa mishonari!a

Wakati huohuo, kutaniko kijijini mwangu liliendelea kukua na sasa lilikuwa na wahubiri 14. Sitasahau kamwe siku niliposoma barua kutoka kwa Despina, dada yangu wa kimwili, akinifahamisha kwamba yeye na wazazi wangu wamekubali kweli na sasa ni waabudu wa Yehova waliobatizwa!

Kuvumilia Mnyanyaso na Uhamisho

Kanisa Othodoksi la Ugiriki lilianza kuiona shughuli yetu ya kuhubiri kama pigo la nzige wenye kuangamiza, nao wakaazimia kutuangamiza kabisa. Katika Machi 1938, nilipelekwa mbele ya mwendesha mashtaka wa umma, aliyetaka niondoke katika eneo hilo mara moja. Nilimjibu kwamba shughuli yetu ya kuhubiri ilinufaisha kwa kweli na kwamba amri ya kufanya kazi yetu ilitoka kwa Mfalme wetu Yesu Kristo, mwenye mamlaka ya juu zaidi.—Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8.

Siku iliyofuata, niliitwa kwenye kituo cha polisi cha huko. Hapo nilijulishwa kwamba mimi ni mtu hatari kwa umma nami nikahukumiwa kwenda uhamishoni kwa mwaka mmoja katika kisiwa cha Amorgos cha Aegea. Baada ya siku kadhaa nikasafirishwa, pingu mikononi, kwa mashua kwenda kisiwani humo. Hakukuwa na Mashahidi wa Yehova wengine huko Amorgos. Ebu wazia jinsi nilivyoshangaa pale nilipojua, baada ya miezi sita, kwamba Shahidi mwingine alikuwa amehamishwa kuja kisiwani humo! Yeye alikuwa nani? Minos Kokkinakis, niliyejifunza naye Biblia huko Krete. Nilifurahi kama nini kuwa na mwenzi wa kiroho! Baadaye, nilipata pendeleo la kumbatiza katika maji ya Amorgos.b

Punde baada ya kurudi Krete, nikakamatwa tena, na wakati huu nilipelekwa uhamishoni kwa miezi sita katika mji mdogo wa Neapolisi ulio kisiwani humo. Baada ya uhamisho wangu wa miezi sita kwisha, nikakamatwa, nikatiwa gerezani kwa siku kumi, kisha nikapelekwa kwenye kisiwa kilichotengewa Wakomunisti waliohamishwa ambapo nilikaa kwa miezi minne. Niling’amua ukweli wa maneno ya mtume Paulo: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.”—2 Timotheo 3:12.

Ongezeko Licha ya Mnyanyaso

Ugiriki ilipotekwa na Ujerumani katika miaka ya 1940-1944, karibu shughuli yetu ya kuhubiri ikome kabisa. Hata hivyo, watu wa Yehova nchini Ugiriki walijipanga tena haraka na tukaanza upya shughuli yetu ya kuhubiri. Ili kufidia muda uliopotea, tuliendelea na kazi ya Ufalme kwa bidii nyingi.

Kama ilivyotarajiwa, upinzani wa kidini ukazuka tena. Mara nyingi, makasisi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki wangejichukulia sheria mkononi. Katika kijiji kimoja, kasisi alichochea kikundi chenye ghasia kitushambulie. Kasisi mwenyewe alianza kunipiga huku mwanawe akinipiga upande wa nyuma. Nilikimbilia nyumba iliyokuwa karibu ili kujikinga, huku mwenzangu katika mahubiri akiburutwa hadi kwenye uwanja wa umma wa kijiji hicho. Huko, kikundi hicho kilirarua fasihi zake, na mwanamke mmoja akafuliza kusema kwa sauti kubwa kutoka roshani mwake, “Muueni!” Hatimaye tukaokolewa na daktari mmoja na polisi aliyekuwa akipita.

Baadaye, mwaka wa 1952, nikakamatwa tena na kuhukumiwa kwenda uhamishoni huko Kastelli Kissamos, Krete, kwa miezi minne. Muda mfupi baadaye, nikazoezwa ili kuzuru makutaniko na kuyaimarisha kiroho. Baada ya kufanya kazi hiyo ya kusafiri kwa miaka miwili, nilimwoa dada Mkristo mwaminifu aitwaye Despina, somo ya dada yangu wa kimwili, naye amethibitika kuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova tangu wakati huo. Baada ya arusi, nilipewa mgawo wa painia wa pekee mjini Hania, Krete, ambako ningali natumikia.

Kwa karibu miaka 70 ya utumishi wa wakati wote, nimehubiri karibu Krete yote—kisiwa chenye ukubwa wa kilometa mraba 8,300 na urefu wa kilometa 250. Nimefurahi zaidi kuona Mashahidi wachache katika kisiwa hiki katika miaka ya 1930, wakikua na kufikia wahubiri watendaji wa Ufalme wa Mungu 1,100, leo. Namshukuru Yehova kwa kunipa fursa ya kuwa na fungu katika kuwasaidia wengi wa wahubiri hao wapate ujuzi sahihi kutoka kwa Biblia na tumaini la ajabu kwa wakati ujao.

Yehova, “Mwokozi”

Mambo yaliyonipata yamenifundisha kwamba yahitaji uvumilivu na subira ili kusaidia watu wamjue Mungu wa kweli. Yehova huandaa kwa wingi sifa hizi zenye kuhitajika sana. Wakati wa utumishi wangu wa wakati wote wa miaka 67, nimetafakari mara nyingi maneno haya ya mtume Paulo: “Katika kila njia twajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu, kwa uvumilivu wa mengi, kwa dhiki nyingi, kwa visa vya uhitaji, kwa magumu, kwa mapigo, kwa magereza, kwa mivurugo, kwa kazi za jasho, kwa masiku ya kukosa usingizi, kwa nyakati za kuwa bila chakula.” (2 Wakorintho 6:4, 5) Hasa wakati wa miaka ya mapema ya utumishi, hali yangu ya kifedha ilikuwa mbaya sana. Hata hivyo, Yehova hakuniacha wala kuacha familia yangu kamwe. Amethibitika kuwa Msaidiaji mwaminifu na mwenye nguvu. (Waebrania 13:5, 6) Sikuzote tuliona msaada wake wa upendo katika kazi ya kukusanya kondoo na pia kukidhi mahitaji yetu.

Ninapokumbuka hayo na kuona kwamba, katika maana ya kiroho, jangwa limechanua maua, nina hakika kwamba kazi yangu haikuwa ya bure. Nilitumia nguvu zangu za ujana kwa njia inayonufaisha zaidi. Kazi-maisha yangu ya huduma ya wakati wote imekuwa yenye maana zaidi kuliko kazi nyingine yoyote. Sasa nikiwa nimezeeka, naweza kwa moyo wote kuwahimiza vijana ‘wamkumbuke Muumba wao siku za ujana wao.’—Mhubiri 12:1.

Ingawa nina umri wa miaka 91, bado naweza kutumia muda wa saa 120 katika kazi ya kuhubiri kila mwezi. Kila siku, mimi huamka saa 1:30 asubuhi na kuwatolea watu ushahidi barabarani, dukani, au katika maegesho ya magari. Mimi huangusha magazeti 150 kwa wastani kila mwezi. Uwezo wa kusikia na matatizo ya kukumbuka sasa hufanya maisha yangu yawe magumu, lakini ndugu na dada zangu wa kiroho wenye upendo—familia yangu kubwa ya kiroho—na pia familia za binti zangu wawili, wamenitegemeza kwelikweli.

Zaidi ya yote, nimejifunza kumtumaini Yehova. Sikuzote amethibitika kuwa “jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu.”—Zaburi 18:2.

[Maelezo ya Chini]

a Ili kupata masimulizi ya maisha ya Emmanuel Paterakis, ona Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1996, ukurasa wa 22-27.

b Ili kupata habari kuhusu ushindi wa kisheria wa Minos Kokkinakis, ona Mnara wa Mlinzi, la Septemba 1, 1993, ukurasa wa 27-31. Minos Kokkinakis alikufa Januari 1999.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Chini: Nikiwa na mke wangu; kushoto: mwaka wa 1927; kwenye ukurasa unaoelekeana na huu: nikiwa na Minos Kokkinakis (kushoto) na Shahidi mwingine huko Acropolis, mwaka wa 1939, punde baada ya kurudi kutoka uhamishoni

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki