Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 9/15 kur. 27-28
  • “Mmebadili Maoni Yangu Juu ya Mashahidi wa Yehova”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mmebadili Maoni Yangu Juu ya Mashahidi wa Yehova”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Habari Zinazolingana
  • Masimulizi ya Imani Kutoka Gereza Maarufu
    Amkeni!—2001
  • Sanduku La Swali
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Nilikuwa Mhalifu
    Amkeni!—1996
  • Je, Kweli Wahalifu Wanaweza Kurekebishwa?
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 9/15 kur. 27-28

“Mmebadili Maoni Yangu Juu ya Mashahidi wa Yehova”

NDIVYO alivyosema ofisa mmoja wa gereza huko Poland aliposoma makala juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova, kama ilivyoripotiwa katika toleo la Oktoba 15, 1998. Ile makala, “Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia,” ilitaja mafanikio ambayo Mashahidi wa Yehova wamepata kwa kuwahubiria wafungwa huko Wołów, Poland.

Kabla ya gazeti la Mnara wa Mlinzi lililotajwa juu kutolewa, mkutano wa pekee ulipangiwa Septemba 13, 1998, katika gereza la Wołów kwa minajili ya kuwapa wafungwa gazeti hilo. Miongoni mwa walioalikwa kuhudhuria walikuwemo Mashahidi wenyeji, wafungwa waliobatizwa na wenye kupendezwa, na maofisa kadhaa wa gereza. Yafuatayo ni baadhi ya mambo yaliyosemwa na wale waliohudhuria.

Jerzy, mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyebatiziwa gerezani zaidi ya miaka mitano iliyopita, alisema hivi: “Nina furaha sana, kwa kuwa naweza kusoma leo jinsi ambavyo ndugu zetu kutoka katika makutaniko jirani wamejitahidi sana ili kutusaidia.” Aliongeza kusema hivi: “Naendelea kujitahidi kufanya maendeleo, nami naweza kuona jinsi ambavyo Yehova amekuwa akinifinyanga.”

Mfungwa mwingine, aitwaye Zdzisław, alisema hivi kuhusu kazi ya kutoa ushahidi gerezani: “Kwa sasa, wafungwa wanne wanajitayarisha kubatizwa, na watu walioanza kupendezwa hivi majuzi wanaendelea kuhudhuria mikutano kwenye jumba letu. Makala hii yatuchochea kwa nguvu tuzidishe utendaji wetu katika shamba hili.” Ni mtazamo unaofaa kama nini, hasa kwa kuwa Zdzisław angali na miaka 19 ya kutumikia gerezani!

Baada ya kusoma makala hiyo inayohusu gereza la Wołów, ofisa mmoja wa gereza alisema hivi: “Tumepata heshima ya pekee. Sikuwahi kamwe kuwazia kwamba gereza hili lingeweza kupata kusemwa vizuri katika lugha 130 ulimwenguni. Nawapenda ninyi watu, nami nathamini jitihada zenu za kuwasaidia wafungwa.” Ofisa mwingine aliongeza kusema hivi: “Mmebadili maoni yangu juu ya Mashahidi wa Yehova. Hapo awali, niliwaona ninyi kuwa wanadini washikiliao mambo kupita kiasi. Sasa naona kwamba ninyi ni watu wenye maadili.”

Mkurugenzi wa gereza la Wołów, Marek Gajos, alitabasamu na kusema hivi: “Mwanzoni tulifikiri kwamba hamngetimiza mengi. Tulidhani kwamba ninyi ni sawa tu na zile dini nyingine zenye nia ya kubadili tabia za wafungwa kwa kutumia Biblia. Hata hivyo, tulipoona matokeo ya utendaji wenu wa mwanzoni, tuliamua kushirikiana nanyi. Mmekuwa mkija hapa bila kuchoka kwa miaka tisa sasa, nami nathamini sana mambo ambayo mmefanya kufikia sasa.”

Hata hivyo, makala hiyo ilipokewaje huko Wołów gerezani kwa jumla? Upendezi miongoni mwa wafungwa ulikuwa mkubwa sana hivi kwamba Mashahidi walio gerezani waliangusha magazeti yao yote. Maofisa wa gereza pia walionyesha upendezi kwa kuomba nakala 40 zaidi. Ili kupata magazeti hayo mengi yaliyotakikana, makutaniko ya huko yalisaidia kuandaa nakala nyingine 100 kwa ajili ya akina ndugu walio gerezani. Wakati huohuo, hudhurio la mikutano gerezani likaongezeka.

Piotr Choduń, ofisa wa gereza ambaye ameshirikiana na Mashahidi wa Yehova, alisema hivi: “Tuliamua makala hiyo iwekwe kwenye masanduku yote ya matangazo katika gereza letu. Twatumaini wafungwa wote ambao bado hawajaanza kujifunza Biblia watasoma gazeti hilo.”

Mashahidi wanaendelea kupata matokeo mazuri kwa sababu ya kielelezo chao kizuri na kuazimia kwao kujitahidi kuhubiri. Zaidi ya wale wafungwa 15 waliofanya maendeleo kiasi cha kubatizwa, maofisa 2 wa gereza wameweka maisha yao wakfu kwa Yehova na ofisa mwingine wa gereza ameomba funzo la Biblia. Bila shaka, akina ndugu wanaohubiri katika gereza la Wołów wanampa Yehova Mungu sifa zote kwa sababu ya mafanikio yao.—Linganisha 1 Wakorintho 3:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mashahidi watatu na mfungwa mmoja wakihudhuria kutolewa kwa gazeti hilo katika jumba la mihadhara la gereza hilo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki