Sanduku La Swali
◼ Ni tahadhari gani tunazopaswa kuzingatia tunapowahubiria wafungwa gerezani?
Kuna wafungwa takriban milioni nane ulimwenguni pote, na baadhi yao hupendezwa na habari njema. (1 Tim. 2:4) Ofisi moja ya tawi hupokea barua 1,400 hivi kila mwezi kutoka kwa wafungwa na jamaa zao wakiomba vichapo au kutembelewa. Ingawa wafungwa wengi hupendezwa kikweli, imeonekana kwamba wengine hujifanya wanapendezwa ili wajifaidi kibinafsi kutokana na watu wa Mungu. Kwa sababu hiyo, wahubiri wote wanapaswa kuzingatia tahadhari zifuatazo kuhusu kuwahubiria wafungwa gerezani.
Katika visa vingi, wafungwa huhubiriwa kupitia barua. Haipendekezwi kamwe akina dada wawaandikie wafungwa wanaume barua, hata kama wana lengo la kuwasaidia kiroho. Akina ndugu wanaostahili peke yao ndio wanaopaswa kufanya hivyo. Akina dada wanaostahili wanaweza kupewa mgawo wa kuwaandikia barua wafungwa wa kike wanaopendezwa kabisa na kweli ya Biblia. Wafungwa hawapaswi kutumiwa pesa au zawadi nyingine, hata wakiomba vitu hivyo.
Mfungwa anapopendezwa, kutaniko la eneo hilo lapasa kupewa jina na anwani yake. Kwa kawaida ndugu wanaostahili wa kutaniko hilo wanajua jinsi ya kushughulikia hali mbalimbali zinazoweza kutokea. Ikiwa mhubiri hajui kutaniko la eneo hilo, anapaswa kutuma habari hiyo kwa ofisi ya tawi.
Si kosa kwa ndugu waliopewa mgawo huo kufanya mikutano na wafungwa ikiwa inaruhusiwa ili wafungwa kadhaa wajifunze pamoja. Hata hivyo, sherehe za pekee hazipasi kufanywa gerezani ambapo wahubiri wanachangamana kwa uhuru pamoja na wafungwa. Zaidi ya hayo, si jambo la hekima kwa wahubiri kuwatembelea wafungwa wakati wowote na kushirikiana nao kwa ukaribu.
Na tuwe ‘wenye hadhari kama nyoka na wasio na hatia kama njiwa’ tunapowahubiria wafungwa habari njema.—Mt. 10:16.