Gileadi Yatuma Mishonari “Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia”
KWA zaidi ya nusu karne sasa, Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower imekuwa ikituma mishonari. Mnamo Septemba 11, 1999, darasa la 107 la Gileadi lilihitimu. Lilikuwa na wanafunzi 48 kutoka nchi 11, nao walipewa mgawo wa kutumikia katika nchi 24. Watajiunga na maelfu ya mishonari wengine, ambao wamechangia sana kutimiza maneno ya mwisho ya Yesu kabla ya yeye kupaa mbinguni. Alitabiri kwamba wanafunzi wake “[wa]takuwa mashahidi [wake] . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.
Programu ya kuhitimu, iliyofanywa katika Kituo cha Elimu cha Watchtower kule Patterson, New York, ilikuwa pindi tukufu katika mazingira maridadi. Wanafunzi waliokuwa wakihitimu walifurahi sana kwa sababu jamaa zao, rafiki zao wa karibu, na wageni wao walihudhuria. Wote waliohudhuria walikuwa watu 4,992 kutia ndani wale waliounganishwa kupitia simu na vidio katika Brooklyn na Wallkill.
Tumikia Yehova na Jirani kwa Uaminifu
“Ni Nani Aliye Upande wa Yehova?” Hicho kilikuwa ndicho kichwa cha habari ya ufunguzi ya Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza aliyekuwa mwenyekiti wa programu hiyo ya kuhitimu. Alieleza kwamba Waisraeli walikabili suala hilo wakati wa Musa. Wanafunzi waliokuwa wakihitimu pamoja na wale waliohudhuria walikumbushwa kwamba Waisraeli wengi walipoteza uhai nyikani kwa sababu hawakushikamana na Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Baada ya kuabudu sanamu, “wakaketi kula na kunywa, wakaondoka wacheze.” (Kutoka 32:1-29) Yesu aliwaonya Wakristo dhidi ya hatari iyo hiyo: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe kwamba mioyo yenu isiwe kamwe yenye kulemewa na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara hiyo.”—Luka 21:34-36.
Msemaji aliyefuata, Gene Smalley, wa Idara ya Uandikaji, aliwauliza hivi wanafunzi wenye kuhitimu: “Je, Mtathibitisha Kwamba Nyinyi Ni Kitulizo?” Alieleza kwamba neno la Kigiriki pa·re·go·riʹa lilianza kutumiwa katika Kiingereza kurejezea dawa fulani yenye kutuliza maumivu. Lakini, mtume Paulo alitumia neno hili la Kigiriki lenye kufafanua mambo sana kwenye Wakolosai 4:11 kurejezea wafanyakazi wenzake. Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, neno hili limetafsiriwa “msaada wenye kutia nguvu.”
Wakiwa katika migawo yao mishonari hao waliokuwa wakihitimu wanaweza kuwa kitulizo wakati huu kwa njia ya unyenyekevu kabisa kwa kuwa msaada wenye kutia nguvu ndugu na dada wenyeji na kwa kuonyesha roho ya kushirikiana na yenye upendo wanaposhirikiana na mishonari wenzao.
Daniel Sydlik, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akafuatia kuzungumzia “Ile Kanuni Bora ya Kufuata Maishani.” Alieleza kwamba ile kanuni bora iliyotajwa na Yesu kwenye Mathayo 7:12, “mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo,” yatia ndani kufanyia watu wengine mema, si kuepuka tu kufanya madhara.
Ili kufanikiwa, mambo matatu yanahitajika: macho yenye utambuzi, moyo wenye kusikitikia, na msaada. Akimalizia, alisema: “Tukiwa na tamaa ya kusaidia, twapasa kusaidia mara moja. Ni lazima tujitahidi sana kuwafanyia wengine mambo ambayo tungependa watufanyie.” Hivyo ndivyo inavyopasa kuwa hasa kwa mishonari wa kweli wanaoenda nchi nyinginezo kuwasaidia watu kufuata Ukristo wa kweli.
Wafunzi Watoa Vikumbusha Vyenye Upendo
Mfunzi wa Gileadi Karl Adams aliwatia moyo mishonari wenye kuhitimu ‘Waendelee Kukua.’ Katika njia zipi? Kwanza, katika ujuzi na uwezo wa kutumia ujuzi huo vizuri. Wakiwa Gileadi, wanafunzi walijifunza jinsi ya kufanya utafiti ili kujua muktadha wa masimulizi ya Biblia. Walitiwa moyo wafikirie jinsi kila simulizi linavyohusu maisha yao. Walihimizwa kuendelea kufanya hivyo.
“Pili, endeleeni kukua katika upendo. Upendo hukua unapokuzwa. Upendo unaweza kufa unapopuuzwa,” Ndugu Adams akasema. (Wafilipi 1:9) Sasa, wakiwa mishonari, wao watahitaji kukua katika upendo katika hali tofauti-tofauti. Na jambo la tatu: “Endeleeni kukua katika fadhili isiyostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 3:18) “Hiyo ndiyo fadhili nzuri ajabu ambayo Yehova ameonyesha kupitia Mwana wake,” msemaji akasema. “Tuzidipo kukuza uthamini wetu kwa fadhili hiyo isiyostahiliwa, sisi huzidi kufurahia kufanya mapenzi ya Mungu na kutekeleza migawo ambayo ametupa.”
Mfunzi mwingine wa Gileadi, Mark Noumair, alizungumzia habari yenye kichwa “Unaweza Kuvumilia Majaribu Unapoyakabili kwa Upendo.” Aliwaonya kwa upole hivi: “Jifunze kukabili magumu katika maisha ya mishonari kwa upendo, na utaweza kuvumilia. Yehova huwatia nidhamu wale tu anaowapenda. Hata ukihisi kwamba shauri fulani halifai, ni la kukuonea, au halikustahili, upendo wako kwa Yehova na uhusiano wako pamoja naye utakusaidia kuvumilia.”
Ndugu Noumair alisema kwamba utumishi wa mishonari una kazi nyingi. “Lakini kazi bila upendo itakufanya ukose uradhi. Bila upendo, kazi zako za nyumbani—kama vile kupika, kununua vitu, kusafisha matunda, kuchemsha maji—zaweza kukuhuzunisha sana. Ni lazima utue ukajiulize, ‘Mbona ninafanya kazi hizi?’ Ukijiambia, ‘Jitihada zangu zinachangia afya na furaha ya mishonari wenzangu,’ basi itakuwa rahisi kuvumilia.” Akimalizia, aliwatia moyo: “Iwe ni kukubali nidhamu, kutimiza wajibu wako wa mishonari, au kushughulikia kutoelewana, kufanya hayo kwa upendo kutakuwezesha uvumilie katika mgawo wako. ‘Upendo haushindwi kamwe.’”—1 Wakorintho 13:8.
Mfunzi wa Gileadi Wallace Liverance akafuatia kwa kuongoza maigizo ya mambo kadhaa yenye kupendeza yaliyoonwa na wanafunzi walipokuwa wakishirikiana na makutaniko ya huko. Mbali na kwenda nyumba hadi nyumba, wao walitumia mazoezi ya mishonari kutafuta watu kwenye vituo vya lori, mahali pa umma pa kujifulia nguo, vituo vya gari-moshi, na sehemu nyinginezo.
Mishonari Wenye Ujuzi Wawapa Uhakikisho
Mishonari wapya wanapoenda katika nchi ya kigeni, je, wanapaswa kuhangaika? Je, wanaweza kukabili magumu katika mgawo wao wa kigeni? Ofisi za tawi hufanya nini ili kuwasaidia mishonari hao wapya wafanikiwe? Ili kujibu maswali hayo na mengineyo, Steven Lett, wa Idara ya Utumishi, na David Splane, wa Idara ya Uandikaji, waliwahoji ndugu ambao wakati huo walikuwa wakihudhuria shule ya wasimamizi wa tawi katika Kituo cha Elimu cha Watchtower. Ndugu waliohojiwa wanatumikia katika halmashauri za tawi katika Hispania, Hong Kong, Liberia, Benin, Madagaska, Brazili, na Japani.
Watumishi hao wa Yehova wenye uzoefu mwingi, ambao wengi wao wametumikia wakiwa mishonari kwa miongo mingi, waliwapa uhakikisho wanafunzi waliokuwa wakihitimu pamoja na wazazi wao na jamaa zao waliohudhuria. Kwa kutegemea mambo waliyojionea wenyewe na mambo yaliyoonwa na mishonari wenzao, wao walionyesha kwamba matatizo na mahangaiko yanaweza kushughulikiwa kwa mafanikio. Huenda wakakabili tatizo kubwa, “lakini linaweza kusuluhishwa, na Sosaiti hutusaidia,” akasema Raimo Kuokkanen, ambaye ni mishonari nchini Madagaska. “Hatukuchagua mgawo wetu, tuliupokea,” akasema Östen Gustavsson, ambaye wakati huu anatumikia nchini Brazili. “Basi tuliamua kufanya yote tuwezayo kubaki kwenye mgawo wetu.” James Linton, ambaye anatumikia nchini Japani, alisema kwamba jambo lililomsaidia ni “kuwapo kwa ndugu ambao tayari walikuwa wakitumikia katika mgawo wa mishonari.” Utumishi wa mishonari ni njia yenye furaha na yenye kuridhisha ya kumtumikia Yehova na kutunza kondoo zake.
Kuepuka Tauni Inayoua Hali ya Kiroho
Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ambaye mwenyewe alihitimu katika darasa la saba la Gileadi mwaka wa 1946, alitoa hotuba ya mwisho, yenye kichwa “Ugumu wa Kudumu Ukiwa Hai Kiroho.” Akitaja kwanza misiba mibaya sana inayoendelea kukumba sehemu mbalimbali za ulimwengu, alitaja pia kwamba kwa kweli misiba mibaya hata zaidi inapata wanadamu.
Akirejezea Zaburi 91, Ndugu Jaracz alitambulisha “tauni” na “uele” ambao umetokeza ugonjwa na kuua mamilioni ya watu kotekote kwa njia ya kiroho. Ibilisi na mfumo wake mwovu ametumia propaganda yake iliyo kama tauni, inayotegemea maarifa ya akili pekee na kufuatia vitu vya kimwili, ili kudhoofisha na kuua hali ya kiroho, lakini Yehova atuhakikishia kwamba tauni hii haitamkaribia “aketiye mahali pa siri pake aliye juu.”—Zaburi 91:1-7.
“Ugumu,” asema Ndugu Jaracz, “ni kudumisha imani yenye nguvu, kubaki mahali pa usalama. Hatuwezi kuwa kama wadhihaki ‘wasio na ukiroho.’ Na hilo ni tatizo leo. Ni tatizo linalotukabili sisi sote katika tengenezo. Na unaweza kulikabili katika mgawo wako wa mishonari.” (Yuda 18, 19) Lakini mishonari hao waliokuwa wakihitimu waliambiwa kwamba wanaweza kudumisha hali yao ya kiroho katika migawo yao. Kwa mfano, walihimizwa wafikirie jinsi ndugu zetu wanavyovumilia katika Urusi, Asia, na katika nchi za Afrika—japo marufuku, upinzani mkali, dhihaka, propaganda za kutoamini Mungu, na mashtaka ya uwongo. Na katika hali nyingi, pia kuna matatizo halisi yanayotokezwa na vita vya kikabila na uhaba wa bidhaa muhimu.
Hali ya kiroho inapokuwa dhaifu, “ni lazima ujitahidi kuona chanzo cha tatizo kisha ujaribu kukirekebisha, ukitumia shauri la Neno la Mungu.” Mifano ya Biblia ilitolewa. Yoshua alitiwa moyo kusoma nakala ya Sheria kwa sauti ya chini kila siku. (Yoshua 1:8) Kitabu cha Sheria kilipopatikana katika siku za Yosia, Yehova alibariki jinsi walivyofuata kwa uaminifu maagizo yake. (2 Wafalme 23:2, 3) Timotheo aliyajua maandiko matakatifu tangu utotoni. (2 Timotheo 3:14, 15) Waberoya walikuwa wasikivu sana; walionwa kuwa “wenye akili ya uelekevu” kwa sababu walichunguza Maandiko kila siku. (Matendo 17:10, 11) Na Yesu Kristo ndiye kielelezo bora cha mtu aliyejua Neno la Mungu na kulitumia.—Mathayo 4:1-11.
Kwa kumalizia, Ndugu Jaracz aliwahimiza hivi kwa uchangamfu mishonari hao wapya: “Sasa mko tayari kutimiza mgawo wenu wa mishonari. Na mtaenda ng’ambo, na kihalisi, katika sehemu tofauti-tofauti za dunia. Tukikabili ugumu wa kuendelea kuwa hai kiroho, basi hatutaacha chochote kitukengeushe tusitekeleze yale ambayo tumeazimia kufanya. Mnaenda kuhubiri kwa bidii, kuwachochea wengine kuiga imani yenu, na tutasali pamoja nanyi kwamba wale mnaowafundisha, Yehova atawafanya kuwa hai kama ambavyo ametufanya. Na basi, wengi zaidi wataponyoka msiba wa kiroho ambao sasa unaendelea kukumba ulimwengu wote. Watazidi kujiunga nasi ili kufanya mapenzi ya Yehova. Yehova na awabariki kwa jambo hilo.”
Baada ya mwenyekiti kusoma salamu kutoka nchi mbalimbali ulimwenguni, wakati ukafika wa kuwapa diploma wanafunzi wenye kuhitimu. Kisha barua changamfu iliyoandikwa na wanafunzi hao ikasomwa. Walimshukuru Yehova na tengenezo lake kama nini kwa ajili ya mazoezi ya kipekee ambayo walipokea na kwa sababu ya migawo yao wakiwa mishonari wanaoenda “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
Takwimu za Darasa
Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 11
Idadi ya nchi walikogawiwa: 24
Idadi ya wanafunzi: 48
Idadi ya wenzi wa ndoa: 24
Wastani wa umri: 34
Wastani wa miaka katika kweli: 17
Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12
[Picha katika ukurasa wa 26]
Darasa la 107 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower
Katika orodha ifuatayo, nambari za safu zaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.
1. Peralta, C.; Hollenbeck, B.; Shaw, R.; Hassan, N.; Martin, D.; Hutchinson, A. 2. Edwards, L.; Vezer, T.; Ceruti, Q.; Entzminger, G.; D’Aloise, L.; Baglieri, L. 3. Knight, P.; Krause, A.; Kasuske, D.; Rose, M.; Friedl, K.; Nieto, R. 4. Rose, E.; Backus, T.; Talley, S.; Humbert, D.; Bernhardt, A.; Peralta, M. 5. D’Aloise, A.; Humbert, D.; Dunn, H.; Gatling, G.; Shaw, J.; Ceruti, M. 6. Baglieri, S.; Krause, J.; Hollenbeck, T.; Martin, M.; Bernhardt, J.; Hutchinson, M. 7. Backus, A.; Dunn, O.; Gatling, T.; Vezer, R.; Knight, P.; Hassan, O. 8. Nieto, C.; Talley, M.; Friedl, D.; Kasuske, A.; Edwards, J.; Entzminger, M.