Wanafunzi Wenye Kuhitimu wa Neno la Mungu
KATIKA kuwaiga Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa kuhubiri kwao nyumba hadi nyumba. Kazi hiyo ilikaziwa katika maneno ya ufunguzi kwenye programu ya kuhitimu ya darasa la 102 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower.
Machi 1, 1997, Albert Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alivuta fikira kwenye makala ya juzi katika jarida Le Point la Kifaransa. Liliandika juu ya mipango ya Katoliki ya Kiroma ya kuanza kuhubiri nyumba hadi nyumba katika Italia. “Ili [wamishonari wa Vatikani] wasiwasili mikono mitupu wanaposhindania eneo la Mashahidi wa Yehova,” hiyo makala ikasema, “Vatikani hata imepanga kuchapisha nakala milioni moja za Gospeli ya Mtakatifu Marko, wajumbe wao wanapokabili wastadi [Mashahidi] katika ‘kuangusha’ habari njema nyumba hadi nyumba.”
Wahitimu hao 48 ni miongoni mwa wale ambao wameiga njia za Yesu za kuhubiri zenye ustadi katika kueneza Neno la Mungu. Walikuwa wametoka nchi nane kuja kwenye Watchtower Educational Center katika Patterson, New York. Katika miezi mitano ya mafunzo yao, walijifunza Biblia nzima. Mtaala wao ulitia ndani pia historia ya tengenezo la Mungu, pande zenye kutumika za maisha ya umishonari, na matunda ya roho ya Mungu. Hayo yote yalifanywa kukiwa na mradi mmoja akilini—kuwatayarisha kwa ajili ya utumishi wa umishonari katika nchi za kigeni 17 ambako walikuwa wakitumwa. Walipokuwa wakihitimu, wasikilizaji 5,015 wa kimataifa walishiriki shangwe ya hiyo pindi. Ni shauri gani la mwisho lenye kutumika ambalo hao wanafunzi wa Gileadi walipokea?
Kitia-Moyo cha Wakati Ufaao kwa Wamishonari Wapya
Baada ya maneno ya ufunguzi ya mwenyekiti, msaidiaji wa Halmashauri ya Wafanyakazi ya Baraza Linaloongoza, Ralph Walls, aliwatolea hao wamishonari wapya hotuba fupi ya kwanza yenye ushauri wenye kutumika. Kichwa cha hotuba yake kilikuwa “Kumbukeni Kupenda.” Alionyesha kwamba Biblia, katika 2 Timotheo sura ya 3, ilivyotabiri kwamba ulimwengu ungezidi kuwa bila upendo. Aliwatolea hao wamishonari wapya kikumbusha hiki cha wakati ufaao, kwa kupatana na ufafanuzi wa upendo upatikanao kwenye 1 Wakorintho 13:1-7: “Huenda nyinyi, mkiwa wamishonari, mkapita kiwango kilichowekwa cha saa. Huenda mkawa na ujuzi mwingi kutokana na mazoezi yenu ya Gileadi. Au huenda sisi tukafanya kazi kwa bidii saa za ziada kwenye migawo yetu katika ofisi ya tawi. Lakini jitihada na dhabihu zetu zinakuwa si kitu tukisahau kupenda.”
Aliyefuata kwenye programu alikuwa Carey Barber, wa Baraza Linaloongoza, aliyezungumza juu ya kichwa “Yehova Anatuongoza Hadi Ushindi.” Tangu mianzo yao midogo baada ya Vita ya Ulimwengu ya 1, Yehova Mungu amewaongoza watumishi wake waaminifu kwenye ushindi katika upigaji-mbiu wa habari njema ya Ufalme wake, licha ya mnyanyaso. Katika mwaka wa 1931 Wanafunzi wa Biblia, kama walivyojulikana wakati huo, walikubali kirasmi kutumia jina Mashahidi wa Yehova, jambo lililowatia uchungu wa moyo makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. “Darasa la 102 la wamishonari waliozoezwa Gileadi sasa lina pendeleo tukufu la kuwa na fungu kubwa katika kazi yenye utukufu ya kuwatolea watu wengi iwezekanavyo fursa ya kujifunza jina hilo takatifu,” akasema Ndugu Barber. Wanajiunga na orodha ndefu ya wamishonari 7,131 ambao wamezoezwa kwenye Shule ya Gileadi na ambao wamesaidia kupanua kuhubiriwa kwa Neno la Mungu kutoka nchi 54 katika mwaka wa 1943 hadi nchi 233 leo.
Msemaji aliyefuata, Lloyd Barry, ambaye pia ni wa Baraza Linaloongoza, alikuwa mhitimu wa darasa la 11 la Gileadi na alitumikia akiwa mishonari katika Japani kwa muda wa miaka 25. Aliandaa kitia-moyo kwa hotuba yake yenye kichwa, “Kaa Katika Mambo Haya.” “Shangwe yenu iliyo nyingi itapatikana katika kuvumilia,” akawaambia wanafunzi. Ni thawabu gani ambazo hutokana na kuvumilia katika kazi ya umishonari au katika mgawo wowote wa kitheokrasi? “Zaidi ya yote, uvumilivu wetu hufanya moyo wa Yehova ushangilie . . . Kuna uradhi mkubwa unaopatikana katika kushika uaminifu-maadili chini ya mtihani . . . Ufanye utumishi wako wa umishonari kuwa kazi ya maisha . . . Thawabu yako italeta pongezi yenye kuchangamsha moyo kuambiwa ‘vema.’” (Mathayo 25:21; Mithali 27:11) Katika kumalizia utoaji wake, Ndugu Barry alipendekeza kwa ukunjufu wa moyo kwamba wamishonari hao wapya ‘wakae katika mambo haya’ kwa kuazimia hivi kwamba shamba la umishonari linakuwa maisha yao wenyewe.—1 Timotheo 4:16.
“Ni Nini Utakachoona?” lilikuwa swali lililoulizwa na Karl Adams, ambaye amepata kushiriki katika kufunza madarasa mengi ya Gileadi. Alieleza kwamba kile ambacho wamishonari wapya wangeona katika migawo yao chategemea si uwezo wao wa kuona kimwili tu bali pia macho yao ya moyo. (Waefeso 1:18) Hilo lilitolewa kielezi na yale wapelelezi Waisraeli waliyoyaona walipokagua Bara Lililoahidiwa. Wapelelezi wote 12 waliona mambo yaleyale kwa maoni ya kimwili, lakini wawili tu ndio walioona Bara Lililoahidiwa kwa maoni ya Mungu. Wamishonari waweza pia kuona mambo katika njia zilizo tofauti. Katika nchi fulani ambako watakuwa wakitumikia, huenda wakaona umaskini, kuteseka, na hali ya kukosa tumaini. Lakini hawapaswi kuitikia isivyofaa na kuacha mgawo wao. Ndugu Adams alizungumza juu ya mishonari mmoja kutoka darasa fulani la juzi aliyesema hivi: “Mambo haya yaliyoonwa yalinifanya ning’amue kwamba yanibidi nikae hapa. Watu hawa wanahitaji tumaini la wakati ujao. Ninataka kuboresha maisha yao.” Ndugu Adams alimalizia kwa kuwatia moyo wamishonari wapya kuziona nchi walikotumwa kuwa maeneo ambayo Yehova ameazimia kuyafanya sehemu ya Paradiso Yake ya tufeni pote na kuwaona watu huko kuwa wanaotazamiwa kuwa washiriki wa jamii mpya ya ulimwengu.
Hotuba ya mwisho katika sehemu hii ya programu ilitolewa na Wallace Liverance, aliyetumikia kwa miaka kadhaa katika shamba la umishonari kabla ya kuwa mfunzi wa Gileadi. “Tendeni kwa Ufahamu Wenye Kina Katika Kazi za Ajabu za Mungu” ndicho kilichokuwa kichwa cha hotuba yake. Kutenda kwa ufahamu wenye kina huhusisha kutenda kwa busara, hadhari, na kwa akili ya kawaida. Hilo lilikuwa jambo ambalo Mfalme Sauli wa Israeli alishindwa kufanya.—1 Samweli 13:9-13; 15:1-22.
Njia moja ya kutenda kwa ufahamu wenye kina ni kwa kukubali magumu ya kuzoeleana na njia mpya ya maisha, kutia ndani kujifunza lugha mpya na kupata kujua watu. Mambo ambayo huwapata wamishonari katika kukabili magumu na kushinda vizuizi yaweza kuwaimarisha kiroho katika njia ile ambayo Yoshua na Kalebu walitiwa nguvu waliposhinda ile nchi ambayo Mungu alikuwa amewagawia.
Mahojiano
Sehemu inayofuata ya programu ilitia ndani mfululizo wa mahojiano. Harold Jackson alimhoji Ulysses Glass, msajili na mfunzi wa muda mrefu wa Shule ya Gileadi, ambaye sasa ana umri wa miaka 85. Wamishonari wengi ambao bado wako shambani wanakumbuka vizuri miaka yake ya ufundishaji na uzoezaji wenye uaminifu. Kisha akaja Mark Noumair, mfunzi wa Gileadi aliyetumia miaka 11 akiwa mishonari katika Afrika kabla ya kujiunga na wafanyakazi wa Shule ya Gileadi. Aliwahoji wanafunzi juu ya utumishi wao wakati wa miezi mitano ya mafunzo. Mambo waliyoona yalionyesha waziwazi kwamba kuna watu wanaopendezwa na Neno la Mungu katika eneo la pale.
Kisha Robert Ciranko na Charles Molohan wakazungumza na wanaume wenye uzoefu waliokuwa wakihudhuria shule nyingine kwenye hayo majengo, shule kwa ajili ya wafanyakazi wa ofisi za tawi. Ushauri wao kwa darasa hilo lenye kuhitimu ulitia ndani uhitaji wa kuwa wanyenyekevu na kuchangia muungano wa kutaniko. Walidokeza kwamba hao wahitimu hawapaswi kuwa na mawazo ya kimbele juu ya yale yatakayotukia katika kazi ya umishonari lakini, badala ya hivyo, wawe tu tayari kukubali hali yoyote ile. Kutumia ushauri huo bila shaka kutawasaidia hao wamishonari wapya kutimiza migawo yao wakiwa walimu wa Neno la Mungu.
Hatimaye, Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliwahutubia wasikilizaji juu ya kichwa “Ni Nini Kinachomvuta Nani?” Alieleza kwamba tunapoonyesha matunda ya roho tukiwa Wakristo, twaweza kuwa na uvutano mzuri juu ya watu wengine. “Wamishonari wanaotumwa na tengenezo la Yehova wametokeza rekodi istahiliyo sifa ya kuvutia watu katika njia ya kiroho ifaayo,” akasema. Kisha akataja maelezo fulani yaliyotolewa na watu mmoja-mmoja ambao wamesaidiwa kumtumikia Mungu kwa sababu ya vielelezo vizuri vilivyowekwa na wamishonari. “Dumisheni sifa ambayo watu wa Yehova wamepata na mwendelee kubisha milango hiyo katika migawo yenu ya nchi za kigeni katika kutafuta wanaostahili . . . Pia, kwa mwenendo wenu mnyoofu, na safi, kinzeni roho ya ulimwengu huu, na iweni uvutano wenye faida kwa sifa na staha ya Yehova,” akamalizia.
Katika kukamilisha programu, mwenyekiti alishiriki salamu kutoka sehemu za karibu na za mbali na kisha akatoa diploma na kutangaza migawo ya umishonari. Baada ya hayo, mmoja wa wahitimu alisoma azimio la darasa akitoa shukrani kwa mafunzo yaliyoandaliwa. Kwa wazi, programu hiyo ya kuhitimu ya darasa la 102 iliwafanya wote waliohudhuria wawe wenye kuazimia zaidi kusonga mbele katika kulitangaza Neno la Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Darasa la 102 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower
Katika orodha iliyo chini, safu zimepewa nambari kutoka mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.
(1) Duffy, C.; Alexis, D.; Harff, R.; Lee, J.; Corey, V.; Nortum, T.; Mora, N.; Journet, F. (2) Djupvik, L.; Singh, K.; Hart, B.; Kirkoryan, M.; Lee, S.; Rastall, S.; Zoulin, K.; Kollat, K. (3) Singh, D.; Pitteloud, J.; Pitteloud, F.; Bokoch, N.; Torma, C.; Muxlow, A.; Richardson, C.; Nortum, D. (4) Harff, J.; Journet, K.; Barber, A.; Loberto, J.; Loberto, R.; Muxlow, M.; Mora, R.; Hart, M. (5) Torma, S.; Rastall, A.; Diaz, R.; Diaz, H.; Weiser, M.; Weiser, J.; Kirkoryan, G.; Zoulin, A. (6) Alexis, R.; Barber, D.; Djupvik, H.; Duffy, C.; Kollat, T.; Richardson, M.; Bokoch, S.; Corey, G.