Kutoka Kuwa Wanafunzi Wenye Mafanikio Hadi Kuwa Wamishonari Wenye Mafanikio
“BADO siwezi kuamini kwamba tumekuwa na pendeleo hili!” Will akasema kwa mshangao, akirejezea mazoezi ambayo yeye na mke wake Patsy, walikuwa wametoka tu kukamilisha wakiwa wanafunzi wa darasa la 103 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Zahid na Jeni walikubaliana nao. “Twahisi kwamba tumependelewa kuwa hapa,” wakasema. Wanafunzi wote walikuwa wamejifunza kwa bidii yenye kuendelea shuleni. Sasa walikuwa na hamu ya kuanza kazi-maisha yao wakiwa wamishonari. Lakini kwanza, kwenye programu ya uhitimu katika Septemba 6, 1997, walipokea shauri lenye upendo ambalo lingewasaidia kufanikiwa katika migawo yao ya mishonari.
Mwenyekiti wa hiyo programu alikuwa Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alitaja kwamba—pamoja na familia ya Betheli na wawakilishi wa ofisi za tawi 48 za Watch Tower Soceity—marafiki na jamaa kutoka Kanada, Ulaya, Puerto Riko, na Marekani walikuwapo ili kuwahakikishia wanafunzi tegemezo na upendo wao. Ndugu Jaracz alioenelea kwamba wamishonari ambao hutumwa na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo mara nyingi wamekengeushwa kutoka katika kazi ya mishonari, wakaanza kufuatia miradi ya kisomi au hata wakanaswa katika siasa. Tofauti nao, wahitimu wa Gileadi hufanya yale ambayo wamezoezwa kufanya. Wao hufundisha watu Biblia.
Kisha Robert Butler kutoka katika ofisi ya Brooklyn ya Sosaiti akazungumza juu ya kichwa “Ifanikishe Njia Yako.” Alieleza kwamba wakati ambapo wanadamu wanapima mafanikio kwa kutegemea mapato ya kifedha au mengine ya kibinafsi, jambo la maana kwa kweli ni jinsi ambavyo Mungu hupima mafanikio. Huduma ya Yesu ilifanikiwa, si kwa sababu aligeuza imani ya idadi kubwa ya watu, bali kwa sababu alikuwa mwaminifu katika mgawo wake. Yesu alimletea Yehova utukufu, naye alibaki bila kuchafuliwa na ulimwengu. (Yohana 16:33; 17:4) Hayo ndiyo mambo ambayo kila Mkristo aweza kufanya.
“Iweni Watumwa kwa Watu Wote,” akashauri Robert Pevy, aliyekuwa mishonari hapo awali katika nchi za Mashariki. Mtume Paulo alikuwa mishonari mwenye mafanikio. Siri yake ilikuwa nini? Alijifanya kuwa mtumwa kwa wote. (1 Wakorintho 9:19-23) Msemaji alifafanua hivi: “Mhitimu wa Gileadi mwenye mtazamo huo hatauona utumishi wa mishonari kuwa aina fulani ya kupanda cheo katika kazi-maisha, njia ya kufikia nyadhifa za maana zaidi katika tengenezo. Mishonari huenda katika mgawo wake akiwa na nia moja tu—kutumikia, kwa kuwa hilo ndilo watumwa hufanya.”
Akitegemeza shauri lake hasa kwenye 2 Wakorintho sura ya 3 na ya 4, Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza aliwahimiza wanafunzi ‘Wafanye Mrudisho wa Utukufu wa Yehova Kama Vioo.’ Aliwakumbusha kwamba ujuzi juu ya Mungu ni kama nuru ambayo huangazia Mkristo afunguapo moyo wake ili aupokee. Twarudisha nuru hiyo kwa kuhubiri habari njema na kwa kudumisha mwenendo bora. “Nyakati nyingine huenda mkahisi hamfai,” akakubali. “Wakati hisia hizo zizukapo, mtegemeeni Yehova, ‘ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu.’” (2 Wakorintho 4:7) Akirudia maneno ya Paulo yaliyorekodiwa kwenye 2 Wakorintho 4:1, Ndugu Lösch aliwaomba wanafunzi hivi: “Msife moyo katika mgawo wenu wa mishonari. Dumisheni kioo chenu kikiwa kimeng’ara!”
Karl Adams, mshiriki wa kitivo cha Gileadi, alizungumza juu ya kichwa chenye kuvutia “Yehova Yuko Wapi?” Hilo swali halirejezei mahali alipo Mungu katika ulimwengu wote mzima, bali larejezea ule uhitaji wa kufikiria maoni ya Yehova na maonyesho ya mwelekezo wake. “Chini ya mkazo,” akasema, “huenda hata mtu aliye na rekodi ndefu katika utumishi wa Yehova akasahau maoni ya Yehova.” (Ayubu 35:10) Vipi juu ya siku yetu ya kisasa? Mwaka wa 1942, watu wa Mungu walihitaji mwongozo. Je, kazi ya kuhubiri ilikuwa ikiisha, au kulikuwa na kazi zaidi ya kufanywa? Mapenzi ya Yehova kwa watu wake yalikuwa nini? Walipokuwa wakijifunza Neno la Mungu, jibu likapata kuwa wazi. “Kabla ya mwaka huo kumalizika,” Ndugu Adams akajulisha wazi, “mipango ya Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower ilikuwa tayari.” Bila shaka Yehova amebariki kazi ya wamishonari ambao hutumwa na shule hiyo.
Mark Noumair alikuwa mfunzi wa pili kuzungumza. Katika hotuba yake, yenye kichwa “Utaitumiaje Talanta Yako?,” aliwatia moyo wanafunzi kutumia mazoezi waliyokuwa wamepokea Gileadi mara tu wafikapo katika migawo yao mipya. “Jitahidi kupendezwa na wengine,” akasema. “Pata kujihusisha. Uwe na hamu ya kujifunza desturi, historia, ucheshi wa hiyo nchi. Kadiri ujifunzavyo lugha haraka, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwako kubadilikana ili kufaana na mgawo wako.”
Wanafunzi Wenye Bidii Wapata Shangwe Katika Huduma
Kwa kuongezea kujifunza wenyewe wakiwa Gileadi, wanafunzi walipewa mgawo wa kushirikiana na makutaniko 11 ya mahali hapo. Kwenye miisho-juma, walishiriki kwa bidii katika utendaji wa kuhubiri. Wallace Liverance wa kitivo cha Gileadi aliwakaribisha wanafunzi kadhaa ili washiriki na wasikilizaji baadhi ya mambo waliyoona. Shangwe yao ilidhihirika walipokuwa wakisimulia mambo waliyojionea walipokuwa wakitoa ushahidi mahali penye maduka mengi, katika maegesho ya magari, katika eneo la kibiashara, barabarani, na kutoka nyumba hadi nyumba. Baadhi yao walitafuta njia za kuwafikia watu wenye kusema lugha za kigeni ambao waliishi na kufanya kazi katika eneo la kutaniko lao. Angalau mafunzo ya Biblia kumi yalianzishwa na kuongozwa na washiriki wa darasa la 103 wakati wa ile miezi mitano ya kuzoezwa kwao.
Wamishonari wa Muda Mrefu Washiriki Siri za Mafanikio
Kufuatia sehemu hii ya programu yenye kuonewa shangwe, Patrick Lafranca na William Van de Wall waliwakaribisha washiriki saba wa Halmashauri ya Tawi ili waeleze masomo waliyokuwa wamejifunza katika kazi-maisha zao za mishonari kwa manufaa ya hilo darasa. Waliwaonya kwa upole wahitimu waione migawo yao ya mishonari kuwa yatoka kwa Yehova na waazimie kushikamana na hiyo migawo. Walizungumza juu ya matokeo chanya ambayo wamishonari waliozoezwa katika Gileadi wamekuwa nayo katika kazi ya nchi nyinginezo.
Ni nini kilichowasaidia washiriki hao wa Halmashauri ya Tawi watumikie kwa miongo mingi wakiwa wamishonari wenye furaha, wenye matokeo? Walifanya kazi karibu-karibu na ndugu wenyeji, wakajifunza kutoka kwao. Walijikaza kujifunza lugha mara tu walipofika katika migawo yao. Walijifunza kuwa wenye kubadilikana na kufaana na desturi za kienyeji. Charles Eisenhower, mhitimu wa darasa la kwanza la Gileadi na ambaye amekuwa mishonari kwa miaka 54, alishiriki “siri” tano ambazo wamishonari wenye mafanikio wamejifunza: (1) Jifunze Biblia kwa ukawaida, (2) jifunze lugha, (3) uwe mtendaji katika huduma, (4) fanyia kazi amani katika makao ya mishonari, na (5) sali kwa Yehova kwa ukawaida. Hao wanafunzi walivutiwa sana na shauri lenye kutumika walilopokea na pia shangwe ya wazi ambayo wamishonari hao wenye uzoefu wanayo katika utumishi wa Yehova. Kama vile Armando na Lupe walivyosema, “wana furaha wasemapo juu ya maisha zao.”
Baada ya mahojiano, hotuba moja ilisalia. Albert Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alichagua kichwa “Usimamizi-Nyumba Mwaminifu wa Neno la Mungu Hufunua Vito Vyenye Thamani vya Kweli,” kuwa kichwa cha habari yake. Kwa kuwa Biblia ndicho kitabu kikuu cha mafundisho cha Shule ya Gileadi, wanafunzi walipendezwa katika yale aliyokuwa nayo ya kusema. Ndugu Schroeder alionyesha kwamba New World Translation of the Holy Scriptures ilipoanza kufanyiwa kazi miaka 50 iliyopita, washiriki watiwa-mafuta wa Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya Ulimwengu Mpya hawakutafuta kibali cha watu bali walitegemea mwongozo wa roho takatifu. (Yeremia 17:5-8) Ingawa hivyo, majuzi watu fulani wenye mamlaka wametambua kiwango cha juu kilichowekwa na New World Translation. Katika barua iliyoandikiwa Sosaiti, msomi mmoja aliandika hivi: “Mimi najua kichapo bora nionapo kimoja, na ‘Halmashauri ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya’ yenu imefanya kazi yake vizuri.”
Baada ya hotuba hiyo, wanafunzi walipokea shahada zao, na migawo yao ikatangazwa kwa wasikilizaji. Ilikuwa pindi yenye kuchochea hisia kwa washiriki wa hilo darasa. Mwakilishi wa darasa alipokuwa akisoma barua ya uthamini, wengi walihisi shukrani zenye kuhisiwa moyoni na walitokwa na machozi. Baadhi ya wanafunzi walikuwa wamejitayarishia kazi ya mishonari kwa miaka kadhaa. Waking’amua kwamba mtaala wa Gileadi ungeongozwa katika Kiingereza, wachache kati yao walikuwa wamehamia makutaniko yenye kusema Kiingereza ili kuboresha matumizi yao ya hiyo lugha. Wengine walikuwa wamehamia mahali ambapo palikuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa mapainia, ama katika nchi yao wenyewe ama ng’ambo. Na bado wengine walikuwa wamejitayarisha kwa kusoma mambo yaliyoonwa, kufanya utafiti, au kutazama tena na tena vidiokaseti ya Sosaiti To the Ends of the Earth.
Will na Patsy, waliotajwa mwanzoni, walizidiwa na hisia kwa sababu ya upendezi wa kibinafsi ambao hao wanafunzi walionyeshwa. “Hata watu ambao hawakutujua walikuwa wakitukumbatia na kutupiga picha. Mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitusalimu na kusema, ‘Twawaonea fahari!’” Bila shaka, wanafunzi wa darasa la 103 wapendwa sana. Wamezoezwa vizuri. Mazoezi ambayo wamepokea katika Gileadi yatawawezesha kufanya badiliko kutoka kuwa wanafunzi wenye mafanikio hadi kuwa wamishonari wenye mafanikio.
[Sanduku katika ukurasa wa 22]
Takwimu za Darasa
Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 9
Idadi ya nchi walikogawiwa: 18
Idadi ya wanafunzi: 48
Idadi ya wenzi wa ndoa: 24
Wastani wa umri: 33
Wastani wa miaka katika kweli: 16
Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12
[Picha katika ukurasa wa 23]
Darasa la 103 Linalohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower
Katika orodha iliyo chini, safu zimepewa nambari kutoka mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.
(1) Bunn, A.; Dahlstedt, M.; Campaña, Z.; Boyacioglu, R.; Ogando, G.; Nikonchuk, T.; Melvin, S. (2) May, M.; Mapula, M.; Lwin, J.; Hietamaa, D.; Hernandez, C.; Boyacioglu, N.; Sturm, A.; Melvin, K. (3) Thom, J.; Mapula, E.; Nault, M.; Teasdale, P.; Wright, P.; Pérez, L.; Shenefelt, M.; Pak, H. (4) Murphy, M.; Campaña, J.; Stewart, S.; Cereda, M.; Reed, M.; Pérez, A.; Teasdale, W.; Pak, J. (5) Stewart, D.; Wright, A.; Cereda, P.; Nikonchuk, F.; Reed, J.; Hietamaa, K.; Ogando, C.; Shenefelt, R. (6) Murphy, T.; Hernandez, J.; Nault, M.; Bunn, B.; Thom, R.; Dahlstedt, T.; Lwin, Z.; May, R.; Sturm, A.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Twaenda wapi?