Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w09 5/1 uku. 18
  • Yehova Alipofunua Sifa Zake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Alipofunua Sifa Zake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Habari Zinazolingana
  • Kuzijua Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Sifa za Yehova Zinazovutia
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2020
  • Mungu wa Kweli Ni Nani?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Musa—Jinsi Maisha Yake Yanavyokuhusu
    Amkeni!—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
w09 5/1 uku. 18

Mkaribie Mungu

Yehova Alipofunua Sifa Zake

Kutoka 34:6, 7

UNGEELEZA sifa na matendo ya Mungu jinsi gani? Wazia kwamba ungeweza kumuuliza Mungu kuhusu sifa zake na kusikiliza anapokueleza. Nabii Musa alipata pendeleo hilo, na jambo la kufurahisha ni kwamba Mungu alimwongoza kuandika yaliyotukia.

Akiwa kwenye Mlima Sinai, Musa alimsihi Yehova hivi: “Nionyeshe, tafadhali, utukufu wako.” (Kutoka 33:18) Siku iliyofuata, nabii huyo alipata pendeleo la kuuona utukufu wa Mungu.a Musa hakueleza kwa undani mambo aliyoona kwenye maono hayo yenye kuvutia. Badala yake, aliandika maneno ambayo Mungu alisema, ambayo ni muhimu sana. Hebu tuchunguze mambo ambayo Yehova alisema yanayotajwa katika Kutoka 34:6, 7.

Jambo la kwanza ambalo Mungu anafunua kujihusu ni kwamba yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema.” (Mstari wa 6) Kulingana na msomi mmoja, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “rehema” linaonyesha “huruma nyororo [za Mungu], kama huruma za baba kwa watoto wake.” Neno linalotafsiriwa “neema” linahusiana na kitenzi “kinachomhusu mtu anayesukumwa na moyo kumsaidia mtu mwenye uhitaji.” Ni wazi kwamba Yehova anataka tujue kuwa anawatunza waabudu wake kama vile wazazi wanavyowatunza watoto wao—kwa kuwaonyesha upendo mwororo na kuhangaikia sana mahitaji yao.—Zaburi 103:8, 13.

Halafu, Yehova anasema kwamba yeye “si mwepesi wa hasira.” (Mstari wa 6) Hawakasirikii upesi watumishi wake duniani. Badala yake yeye anawaonyesha subira na kuvumilia makosa yao huku akiwapa nafasi ya kubadili mwenendo wao wenye dhambi.—2 Petro 3:9.

Mungu anaendelea kuzungumza na Musa, akisema kwamba yeye “ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” (Mstari wa 6) Fadhili zenye upendo, au upendo mshikamanifu, ni sifa nzuri ambayo Yehova anatumia kujenga uhusiano thabiti kati yake na watu wake. (Kumbukumbu la Torati 7:9) Yehova pia ni chanzo cha ukweli. Hawezi kudanganya wala kudanganywa. Kwa kuwa yeye ni “Mungu wa ukweli,” tunaamini kabisa yote anayosema, kutia ndani ahadi zake kuhusu wakati ujao.—Zaburi 31:5.

Ukweli mwingine muhimu ambao Yehova anataka tujue kumhusu ni kwamba yeye anasamehe “kosa na ubaya na dhambi.” (Mstari wa 7) Yeye yuko “tayari kusamehe” wakosaji wanaotubu. (Zaburi 86:5) Lakini Yehova hapuuzi ubaya. Anaeleza kwamba “kwa vyovyote hatakosa kuadhibu.” (Mstari wa 7) Mungu ni mtakatifu na mwenye haki na hatakosa kuwaadhibu watenda-dhambi. Siku moja watapatwa na matokeo ya dhambi zao.

Yehova ameonyesha wazi kwamba anataka tumjue na tujue sifa na njia zake kwa kutueleza kuzihusu. Bila shaka umechochewa kujifunza zaidi kuhusu sifa zake nzuri.

[Maelezo ya chini]

a Musa hakumwona Yehova moja kwa moja, kwa kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kumwona Mungu na kuishi. (Kutoka 33:20) Yaelekea Yehova alimwonyesha Musa maono kuhusu utukufu Wake na alizungumza naye kupitia malaika.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki