Kwa Nini Kuna Ubishi Mwingi Kuhusu Roho Takatifu
ROHO takatifu ni nini? Huenda swali hilo likaonekana rahisi lakini huenda ikawa vigumu kupata jibu lake. Papa Benedikto wa 16 aliuambia hivi umati uliokuwa umekusanyika huko Australia: “Ni kana kwamba hatuwezi kuelewa Roho ni nini hasa.”
Bila shaka, watu hawana uhakika na hutoa maoni mengi kuhusu swali, Roho takatifu ni nini? Yafuatayo ni baadhi ya majibu yanayotolewa:
• Ni mtu halisi anayeishi ndani ya wanafunzi wa Kristo.
• Sayansi ya kimungu, sheria ya Mungu ikitenda.
• Mungu akitenda katika ulimwengu.
• Mtu wa tatu katika Utatu.
Kwa nini kuna ubishi mwingi hivyo? Ubishi huo ulianza katika karne ya nne W.K. ambapo wanatheolojia fulani walidai kwamba roho takatifu ni mtu ambaye kwa njia fulani analingana na Mungu. Hata hivyo, jambo hilo halipatikani katika Maandiko wala wafuasi wa mapema wa Kristo hawakufundisha hivyo. Kitabu fulani (New Catholic Encyclopedia) kinaeleza hivi: “Kwa wazi Agano la Kale halionyeshi kuwa roho ya Mungu ni mtu . . . Roho ya Mungu ni nguvu za Mungu.” Kitabu hichohicho kilisema hivi: “Maandiko mengi ya Agano Jipya huonyesha roho ya Mungu kuwa kitu, wala si mtu; jambo hilo linaonekana hasa kutokana na ulinganifu uliopo kati ya roho na nguvu za Mungu.”
Inaeleweka kwamba watu huona vigumu kufikiria nguvu kuwa mtu. Hivyo, uchunguzi uliofanywa karibuni nchini Marekani ulionyesha kwamba watu wengi wanapinga wazo la kwamba roho takatifu ni mtu. Je, wako sahihi? Au je, tunapaswa kuwaamini wanatheolojia ambao husisitiza kwamba “Roho Mtakatifu ni Mtu tofauti na Baba na Mwana”?
Ili kupata jibu linalotegemeka, tunahitaji kuchunguza Neno la Mungu, Biblia, ambalo hufafanua roho takatifu kwa undani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa katika kufundishia ukweli, . . . kusahihisha makosa.”—2 Timotheo 3:16, Biblia Habari Njema.
Kwa nini utafute ukweli kuhusu roho takatifu? Kwa sababu kujua kweli kunaweza kukufungulia njia ya kupata msaada kutoka kwa Mungu. Je, nyakati nyingine wewe huona kwamba huna nguvu za kuvumilia hali ngumu? Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa . . . Ikiwa ninyi . . . mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:9, 13.
Katika habari zinazofuata, Maandiko yatatufafanulia roho takatifu ni nini. Na tutajifunza jinsi ambavyo inaweza kutunufaisha maishani.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Maandiko yanatufafanulia roho takatifu ni nini