Je, Biblia Ni Neno la Mungu?
“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 TIMOTHEO 3:16, 17.
MTUME Paulo alisema maneno yenye nguvu kama nini kuhusu thamani kubwa ya Biblia! Bila shaka, alikuwa akizungumzia hasa sehemu ya Biblia ambayo alikuwa nayo wakati huo, yaani, maandishi ambayo nyakati nyingine wengine wanayaita Agano la Kale. Lakini maneno yake yanahusu pia vitabu vyote 66 vya Biblia, kutia ndani vile vilivyoandikwa na wanafunzi waaminifu wa Yesu katika karne ya kwanza W.K.
Je, unaiheshimu sana Biblia kama Paulo alivyoiheshimu? Je, unafikiri kwamba kwa kweli waandikaji wa Biblia waliongozwa na roho ya Mungu? Wakristo wa karne ya kwanza waliamini hivyo. Sikuzote Wakristo wa kweli wameamini hivyo. Kwa mfano, kasisi Mwingereza wa karne ya 14, John Wycliffe, aliiona Biblia kuwa “sheria isiyokosea ya kweli.” Kikieleza kuhusu maneno ya Paulo yaliyo hapo juu, kitabu kimoja (The New Bible Dictionary) kinasema kwamba ‘kwa kuwa Biblia imeongozwa na roho ya Mungu basi ni hakika kwamba mambo yote ambayo inasema ni ya kweli.’
Mitazamo ya Watu Kuelekea Biblia Yabadilika
Hata hivyo, katika nyakati za hivi karibuni, watu wengi wameacha kuitegemea Biblia. Kitabu kimoja (The World’s Religions) kinasema hivi: “Wakristo wote [bado] wanakubali kwa maneno tu kwamba Biblia inategemeka katika kuongoza matendo yao na kujenga imani yao.” Hata hivyo, kwa matendo, mambo yamebadilika kabisa. Watu wengi sasa wanaiona Biblia kuwa “mapokeo ya wanadamu ambayo hayategemeki.” Ingawa wanatambua kwamba waandikaji wa Biblia walikuwa watu wenye imani kubwa, wanawaona kuwa watu wasio wakamilifu ambao walijitahidi sana kueleza kweli nzito za kiroho, lakini hawakuwa na ujuzi na elimu tuliyo nayo leo.
Kwa kweli, ni watu wachache sana leo ambao wanaacha Biblia iongoze mawazo na matendo yao. Kwa mfano, ni mara ngapi unapowasikia watu wakisema kwamba viwango vya Biblia vya maadili vimepitwa na wakati na havitegemeki? Watu wengi wanaona ni sawa kupunguza uzito wa sheria na kanuni za Biblia au hata wanazipuuza kabisa ili kufanya yale wanayotaka. Watu fulani wanaodai kuwa Wakristo wanapuuza kimakusudi yale ambayo Biblia inasema kuhusu uasherati, uzinzi, ukosefu wa unyoofu, na ulevi.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Kwa nini wanatenda hivyo? Mwanzoni mwa karne ya 20, mchunguzi wa vitu vya kale Sir Charles Marston alitaja katika kitabu chake (The Bible Is True) sababu moja inayowafanya watu watende hivyo. Alisema kwamba watu walikuwa tayari sana “kukubali bila kupinga mawazo mengi yasiyo na maana ya waandikaji wa kisasa” ambao walipinga kabisa wazo la kwamba Biblia ni ya kweli. Je, bado wanafanya hivyo leo? Unapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mawazo na mafundisho ya wasomi ambao wanawachochea watu wasiamini Biblia? Ona jinsi habari inayofuata inavyosema kuhusu hilo.