Heshima na Staha Chini ya Utunzaji wa Mungu
ALIPOKUWA duniani, Yesu alionyesha kwa ukamili utu wa Baba yake na njia yake ya kufanya mambo. Alisema hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema . . . sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:28, 29; Wakolosai 1:15) Hivyo, kwa kuchunguza jinsi Yesu alivyowatendea wanawake na mtazamo wake kuwaelekea, tunaweza kuelewa maoni ya Mungu kuwahusu na mambo anayotazamia wafanye.
Kulingana na mambo yaliyoandikwa katika masimulizi ya Injili, wasomi fulani wamekubali kwamba maoni ya Yesu kuwaelekea wanawake yalikuwa tofauti sana na maoni ya watu wengi. Jinsi gani? Na jambo la muhimu zaidi ni, je, mafundisho yake bado yanawapa wanawake uhuru leo?
Jinsi Yesu Alivyowatendea Wanawake
Yesu hakuwaona tu kuwa vyombo vya kutosheleza tamaa za ngono. Kulingana na viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi, kushirikiana na watu wa jinsia tofauti kungetokeza tu tamaa zisizofaa. Kwa kuwa wanawake walionwa kuwa chanzo cha majaribu, hawakuruhusiwa kuzungumza na wanaume hadharani wala kutembea nje bila kuwa na ushungi. Kwa upande mwingine, Yesu aliwashauri wanaume wazuie tamaa zao wenyewe za kimwili na kuwatendea wanawake kwa heshima badala ya kuwatenga na watu wengine.—Mathayo 5:28.
Pia, Yesu alisema: “Yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine anafanya uzinzi dhidi [ya mke wake].” (Marko 10:11, 12) Hivyo, alipinga fundisho la kirabi lililofuatwa wakati huo ambalo liliwaruhusu wanaume wawataliki wake zao “kwa kila sababu.” (Mathayo 19:3, 9) Wayahudi wengi hawakuamini kwamba mtu angeweza kufanya uzinzi dhidi ya mke wake. Marabi wao walifundisha kwamba mume hangeweza kamwe kumtendea mke wake uzinzi, mwanamke tu ndiye angekosa kuwa mwaminifu! Kama vile kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinavyosema, “Yesu alipowawekea waume na wake matakwa yaleyale ya kimaadili, aliwastahi na kuwaheshimu wanawake.”
Matokeo ya mafundisho yake leo: Katika kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, wanawake hushirikiana kwa uhuru pamoja na wanaume kwenye mikutano. Hata hivyo, wanawake hawahitaji kuogopa kwamba wanaume watawaangalia na kuwatamani au kuwatongoza isivyofaa, kwa sababu wanaume Wakristo wanajitahidi kuwatendea “wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:2.
Yesu alitumia muda wake kuwafundisha wanawake. Kinyume na maoni ya kirabi ya kutowaelimisha wanawake yaliyoenea sana siku hizo, Yesu aliwafundisha na kuwatia moyo wajieleze. Kwa kutomnyima Maria shangwe ya kufundishwa, Yesu alionyesha kwamba mwanamke hapaswi tu kukaa jikoni. (Luka 10:38-42) Martha dada ya Maria, alifaidika pia kutokana na mafundisho ya Yesu, kama inavyoonyeshwa na jinsi alivyomjibu Yesu kwa hekima baada ya Lazaro kufa.—Yohana 11:21-27.
Yesu alisikiliza maoni ya wanawake. Nyakati hizo, wanawake wengi Wayahudi waliamini kwamba ili mtu apate furaha alipaswa kuwa na mwana mwenye kuheshimika, ikiwezekana mwana huyo awe nabii. Mwanamke fulani aliposema hivi kwa sauti: “Lenye furaha ni tumbo la uzazi lililokuchukua!” Yesu alitumia nafasi hiyo kumfundisha jambo bora zaidi. (Luka 11:27, 28) Kwa kumfundisha kwamba kumtii Mungu ni jambo muhimu zaidi, Yesu alimwonyesha jambo bora kuliko daraka la kidesturi ambalo wanawake walipewa.—Yohana 8:32.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Walimu katika kutaniko la Kikristo leo huwakaribisha wanawake watoe maelezo kwenye mikutano ya kutaniko. Wanawaheshimu wanawake wakomavu kwa kuwa “walimu wa yaliyo mema,” faraghani na kwa kuweka mfano mzuri. (Tito 2:3) Pia, wanawategemea wanawake hao katika kutangaza hadharani habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.—Zaburi 68:11; ona sanduku “Je, Mtume Paulo Aliwakataza Wanawake Kuzungumza?” kwenye ukurasa wa 9.
Yesu aliwajali wanawake. Katika nyakati za Biblia, wasichana hawakuthaminiwa sana kama wavulana. Talmud inaonyesha jambo hilo inaposema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye watoto wake ni wavulana, na ole kwake yule ambaye watoto wake ni wasichana.” Wazazi fulani walimwona msichana kuwa mzigo mkubwa sana, walilazimika kumtafutia mwenzi na kumlipia mahari, na hawangemtegemea awasaidie walipozeeka.
Yesu alionyesha kwamba uhai wa msichana mdogo ni muhimu kama vile tu uhai wa mvulana, alipomfufua binti ya Yairo, kama tu alivyomfufua mwana wa yule mjane wa Naini. (Marko 5:35, 41, 42; Luka 7:11-15) Baada ya kumponya mwanamke aliyekuwa akisumbuliwa na “roho ya udhaifu kwa miaka kumi na minane,” Yesu alimwita “binti ya Abrahamu,” usemi ambao inaelekea haukuwepo katika maandishi ya Kiyahudi. (Luka 13:10-16) Kwa kutumia usemi huo wenye kuheshimika na wa fadhili, hakumwona tu kuwa mshiriki kamili wa jamii, bali pia alitambua imani yake kubwa.—Luka 19:9; Wagalatia 3:7.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Msemo fulani wa huko Asia unasema hivi: “Kumlea binti ni kama kunyunyizia maji shamba la jirani.” Badala ya kuongozwa na mawazo kama hayo, kwa upendo akina baba Wakristo wanawatunza vizuri watoto wao wote, wa kiume na pia wa kike. Wazazi Wakristo wanahakikisha kwamba watoto wao wote wanapokea matibabu na elimu nzuri.
Yesu aliwaamini wanawake. Katika mahakama za Kiyahudi, ushahidi wa mwanamke ulionwa kuwa sawa na wa mtumwa. Yosefo, mwanahistoria wa karne ya kwanza alitoa ushauri huu: “Ushahidi wowote kutoka kwa mwanamke usikubaliwe, kwa sababu ya mwelekeo wao wa kutochukua mambo kwa uzito na ujasiri wao wa kike.”
Kinyume na hilo, Yesu aliwachagua wanawake watoe ushahidi kuhusu ufufuo wake. (Mathayo 28:1, 8-10) Ingawa wanawake hao waaminifu walijionea Bwana wao akiuawa na kuzikwa, ilikuwa vigumu kwa mitume kuamini maneno ya wanawake hao. (Mathayo 27:55, 56, 61; Luka 24:10, 11) Hata hivyo, kwa kuwatokea kwanza wanawake, Kristo aliyefufuliwa alionyesha kwamba walistahili kutoa ushahidi kama vile tu wanafunzi wake wengine walivyostahili.—Matendo 1:8, 14.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, wanaume wenye madaraka wanaonyesha kwamba wanawajali wanawake kwa kusikiliza maoni yao. Nao waume Wakristo ‘wanawapa heshima’ wake zao kwa kuwasikiliza kwa makini.—1 Petro 3:7; Mwanzo 21:12.
Kanuni za Biblia Huchangia Wanawake Kuwa na Furaha
Wanaume wanapomwiga Kristo, wanawake wanaheshimiwa na kupewa uhuru ambao Mungu alikusudia wawe nao mwanzoni. (Mwanzo 1:27, 28) Badala ya kuunga mkono tabia ya wanaume kuwadharau wanawake, waume Wakristo wanaruhusu waongozwe na kanuni za Biblia, na hivyo kuwaletea wake zao furaha.—Waefeso 5:28, 29.
Yelena alipoanza kujifunza Biblia, alikuwa akiumia kimyakimya kwa sababu ya kutendewa kikatili na mumewe. Mume huyo alikuwa amelelewa katika jamii yenye jeuri ambako ilikuwa jambo la kawaida kwa mtu kumteka nyara msichana ili awe mke wake na kumtendea vibaya. “Mambo niliyojifunza katika Biblia yalinitia nguvu,” anasema Yelena. “Nilielewa kwamba kuna mtu aliyenipenda sana na ambaye alinithamini na kunijali. Pia, nilielewa kwamba ikiwa mume wangu angejifunza Biblia, angebadili mtazamo wake kunielekea.” Mwishowe, matumaini yake yalitimia mume wake alipokubali kujifunza Biblia na akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Mume wangu akawa mfano mzuri wa kujizuia,” asema Yelena. “Tulijifunza kusameheana kwa hiari.” Yelena alifikia mkataa gani? “Kwa kweli kanuni za Biblia zimenisaidia nijihisi ninahitajiwa na kwamba niko salama katika ndoa yangu.”—Wakolosai 3:13, 18, 19.
Si Yelena tu aliyejionea jambo hilo. Mamilioni ya wanawake Wakristo wana furaha kwa sababu wao na waume zao wanajitahidi kufuata kanuni za Biblia katika ndoa zao. Wanaheshimiwa, wanafarijiwa, na kupata uhuru wanaposhirikiana na Wakristo wenzao.—Yohana 13:34, 35.
Wanaume na wanawake Wakristo wanatambua kwamba wakiwa wanadamu wenye dhambi na wasio wakamilifu, wao ni sehemu ya uumbaji wa Mungu ambao ‘umetiishwa chini ya ubatili.’ Hata hivyo, kwa kuwa na uhusiano wa karibu na Baba na Mungu wao mwenye upendo, Yehova, wanatumaini la ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ na kufurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Ni tumaini zuri kama nini kwa wanaume na wanawake chini ya utunzaji wa Mungu!—Waroma 8:20, 21.