Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w14 9/1 kur. 7-9
  • Je, Sheria ya Mungu kwa Waisraeli Ilikuwa ya Haki?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Sheria ya Mungu kwa Waisraeli Ilikuwa ya Haki?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WAAMUZI “WENYE HEKIMA NA BUSARA NA UZOEFU”
  • KANUNI ZILIZOTOKEZA MAAMUZI YA HAKI
  • WATU WALIOFAIDIKA NA HAKI YA KWELI
  • Yehova, “Hakimu wa Dunia Yote” Asiye na Upendeleo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jenga na Kufuata Imani Yako Pamoja na Waamuzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • “Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”
    Mkaribie Yehova
  • Wazee, Hukumuni kwa Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 9/1 kur. 7-9
Mwamuzi akisikiliza kesi katika taifa la kale la Israeli

Je, Sheria ya Mungu kwa Waisraeli Ilikuwa ya Haki?

MIAKA kadhaa iliyopita, mahakama fulani huko Ulaya zilikubali tuhuma za uwongo za mauaji dhidi ya wanaume wawili na kuwahukumu adhabu ya kifo. Ilipojulikana kwamba walishtakiwa kwa uwongo, wanasheria walijitahidi sana kutangua hukumu hiyo. Lakini walifanikiwa kumwokoa mshtakiwa mmoja tu kwa sababu tayari mwingine alikuwa ameuawa.

Kwa sababu makosa kama hayo yanaweza kutokea katika mfumo wowote wa kisheria, Biblia inahimiza hivi: “Haki—haki utaifuatilia.” (Kumbukumbu la Torati 16:20) Mahakimu wanapohukumu kwa haki, raia hunufaika. Sheria ya Mungu iliwapa Waisraeli mfumo wa sheria usio na ubaguzi na wenye haki. Acha tuchunguze Sheria hiyo ili tuone ikiwa “njia zake [Mungu] zote ni haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

WAAMUZI “WENYE HEKIMA NA BUSARA NA UZOEFU”

Watu hutendewa kwa haki ikiwa mahakimu ni wazoefu, si wabaguzi, wala wapenda-rushwa. Sheria ya Mungu ilikazia sana waamuzi wawe na sifa hizo. Mwanzoni mwa safari ya jangwani, Yehova alimwambia Musa achague “wanaume wenye uwezo, wanaomwogopa Mungu, wanaume wenye kutegemeka, wanaochukia faida isiyo ya haki,” ili wawe waamuzi. (Kutoka 18:21, 22) Miaka 40 baadaye, alikazia tena uhitaji wa kuwa na waamuzi “wenye hekima na busara na uzoefu.”—Kumbukumbu la Torati 1:13-17.

Miaka mingi baadaye, Mfalme Yehoshafatia wa Yuda aliwaambia waamuzi hivi: “Oneni mnalofanya, kwa sababu hamhukumu kwa ajili ya mwanadamu bali kwa ajili ya Yehova; naye yupo pamoja nanyi katika jambo la hukumu. Na sasa hofu ya Yehova na iwe juu yenu. Iweni waangalifu na mtende, kwa maana hakuna ukosefu wowote wa uadilifu wala ubaguzi wala kuchukua rushwa kwa upande wa Yehova Mungu wetu.” (2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7) Hivyo, mfalme aliwakumbusha kwamba wangewajibika kwa Mungu ikiwa wangefanya maamuzi wakiongozwa na ubaguzi au pupa.

Waisraeli walifaidika na kuhisi salama waamuzi walipofuata viwango hivyo vya juu. Sheria ya Mungu ilitoa pia kanuni zilizowasaidia waamuzi kuhukumu kwa haki hata katika kesi ngumu sana. Ni zipi baadhi ya kanuni hizo?

KANUNI ZILIZOTOKEZA MAAMUZI YA HAKI

Ijapokuwa waamuzi waliochaguliwa walikuwa wenye hekima na uwezo, hawakupaswa kufanya maamuzi kwa kutegemea uwezo au uzoefu wao. Yehova Mungu aliwapa kanuni na miongozo iliyowasaidia kufanya maamuzi sahihi. Zifuatazo ni baadhi ya kanuni walizopewa waamuzi Waisraeli.

Chunguza kwa makini. Kupitia Musa, Yehova aliwaagiza waamuzi Waisraeli hivi: “Mnaposikiliza kesi kati ya ndugu zenu, hukumuni kwa uadilifu.” (Kumbukumbu la Torati 1:16) Mahakimu wanaweza kuhukumu kwa haki ikiwa tu wanajua mambo yote yanayohusika. Kwa hiyo Yehova aliwaagiza waamuzi watafute na “kupeleleza na kuuliza habari kabisa.” Walipaswa kuhakikisha kwamba shtaka “limethibitishwa kuwa kweli” kabla ya kuhukumu.—Kumbukumbu la Torati 13:14; 17:4.

Kuwasikiliza mashahidi. Mashahidi walikuwa muhimu sana katika uchunguzi. Sheria ya Mungu ilisema: “Shahidi mmoja asiinuke juu ya mtu kuhusu kosa au dhambi yoyote, kuhusu dhambi yoyote ambayo huenda akafanya. Kwa kinywa cha mashahidi wawili au kwa kinywa cha mashahidi watatu jambo hilo litathibitishwa vizuri.” (Kumbukumbu la Torati 19:15) Pia, Sheria ya Mungu iliwaamuru mashahidi hivi: “Usieneze habari isiyo ya kweli. Usishirikiane na mtu mwovu kwa kuwa shahidi anayepanga jeuri.”—Kutoka 23:1.

Mashahidi walipaswa kusema kweli. Adhabu ya kudanganya mahakamani ilikuwa onyo kali kwa wote: “Waamuzi watatafuta kabisa, na ikiwa shahidi huyo ni shahidi wa uwongo naye ameleta shtaka la uwongo juu ya ndugu yake, ndipo mtakapomfanyia kama vile alivyompangia ndugu yake hila, nawe utaondolea mbali kilicho kibaya kutoka katikati yako.” (Kumbukumbu la Torati 19:18, 19) Hivyo, kama mtu angedanganya mahakamani ili achukue urithi wa mwenzake, angelipa gharama inayolingana na urithi huo. Ikiwa angedanganya ili mtu asiye na hatia auawe, basi angeuawa yeye mwenyewe. Miongozo hiyo iliwachochea sana watu waseme ukweli.

Hukumu isiyo na ubaguzi. Baada ya kusikiliza mashahidi wote, waamuzi walipaswa kutoa hukumu. Katika hatua hiyo, walipaswa kufikiria agizo hili la Mungu: “Usiwatendee watu wa hali ya chini kwa njia ya ubaguzi, wala usimpendelee mtu mkuu. Utamhukumu mwenzako kwa haki.” (Mambo ya Walawi 19:15) Katika kesi zote, waamuzi walipaswa kuhukumu kwa haki badala ya kuangalia sura au cheo cha mtu.

Kanuni hizo zilizotolewa miaka mingi iliyopita katika Sheria ya Mungu kwa Waisraeli, bado zinaweza kutumika mahakamani leo. Zinapofuatwa, zinaweza kuwasaidia mahakimu kutenda kwa haki.

Hakimu akisikiliza wanaume wawili wakibishana kortini

Kanuni za Sheria ya Mungu zinapofuatwa, zinaweza kuwasaidia mahakimu kutenda kwa haki

WATU WALIOFAIDIKA NA HAKI YA KWELI

Musa aliwauliza Waisraeli hivi: “Kuna taifa gani kubwa lenye masharti na maamuzi ya hukumu ya uadilifu kama sheria yote hii ninayoweka mbele yenu leo?” (Kumbukumbu la Torati 4:8) Kwa kweli, hakuna taifa lingine lililofaidika na sheria kama hiyo. Wakati wa utawala wa Mfalme Sulemani, aliyejitahidi kufuata sheria za Mungu akiwa kijana, watu ‘waliendelea kukaa salama’ na kufurahia amani na ufanisi, “wakila na kunywa na kushangilia.”—1 Wafalme 4:20, 25.

Kwa kusikitisha, baadaye Waisraeli walipuuza sheria za Mungu. Kupitia nabii Yeremia, Mungu alisema hivi: “Tazama! Wamelikataa neno la Yehova, nao wana hekima gani?” (Yeremia 8:9) Matokeo ni kwamba Yerusalemu likawa “jiji lenye hatia ya damu” lililojaa “machukizo.” Mwishowe, liliharibiwa na kuachwa ukiwa kwa miaka 70.—Ezekieli 22:2; Yeremia 25:11.

Nabii Isaya aliishi kipindi chenye misukosuko katika Israeli. Alipofikiria kipindi hicho, alisema hivi kumhusu Yehova Mungu na Sheria yake: “Kunapokuwa na hukumu kutoka kwako kwa ajili ya dunia, wakaaji wa nchi yenye kuzaa hakika watajifunza uadilifu.”—Isaya 26:9.

Isaya aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri hivi kumhusu Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo: “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isaya 11:3, 4) Hilo ni tumaini zuri kama nini kwa wale watakaokuwa raia wa Mfalme wa Kimasihi chini ya Ufalme wa Mungu!—Mathayo 6:10.

a Jina Yehoshafati linamaanisha “Yehova ni Mwamuzi.”

Je, Sheria ya Mungu Iliruhusu Kulipiza Kisasi?

Maneno “jicho kwa jicho, jino kwa jino,” yaliyo kwenye Biblia yamewatatiza wengi. (Kutoka 21:24) Watu fulani wanaamini yanaonyesha kwamba Mungu anaruhusu kulipiza kisasi. Hata hivyo, maoni hayo yanapingana na sheria hii ya Mungu: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Hivyo basi, tunapaswa kuyaelewaje maneno hayo ya kitabu cha Kutoka?

Andiko la Kutoka 21:22 linazungumzia wanaume wawili wanaopigana na mmoja wao anamuumiza mwanamke mwenye mimba, hivi kwamba anazaa mtoto wake kabla ya wakati. Ikiwa mama huyo na mtoto hawangekufa, basi mume wa mwanamke huyo hakupaswa kulipiza kisasi. Badala yake, mwanamume aliyemuumiza mama huyo alipaswa ‘alipie hasara kulingana na kile ambacho mume wa mwanamke huyo angemdai; naye angekitoa kupitia kwa waamuzi.’ Yaani, waamuzi wangemwamuru mwanamume aliyemuumiza mama huyo amlipe mume wake. Ikiwa mama au mtoto angekufa kwa sababu ya majeraha, basi waamuzi wangeamuru mkosaji auawe.

Katika kisa hiki, waamuzi ndio wangefuata amri ya “nafsi kwa nafsi, jicho kwa jicho, jino kwa jino” bali si mtu aliyekosewa. (Kutoka 21:23, 24) Kanuni hiyo iliwakumbusha waamuzi kwamba adhabu ilipaswa kulingana kabisa na kosa. Msomi wa Biblia Richard Elliott Friedman anasema: “Kanuni ya msingi ni kwamba adhabu inapaswa kulingana na hatia na haipaswi kuzidi hatia hiyo.”

Mwanamume akimpiga mwenzake kofi

Maoni ya kwamba Sheria ya Mungu iliruhusu watu walipize kisasi yalitoka wapi? Inapendeza kwamba katika andiko la Mathayo 5:38, 39, Yesu alisema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Jicho kwa jicho na jino kwa jino.’ Hata hivyo, mimi ninawaambia ninyi: Msimpinge yeye aliye mwovu; bali yeyote anayekupiga kofi kwenye shavu lako la kuume, mgeuzie lile lingine pia.” Huenda katika siku za Yesu, baadhi ya viongozi wa kidini walifundisha ‘sheria ya kulipiza kisasi’ katika mapokeo yao na hivyo kuruhusu watu walipize kisasi. Hata hivyo, Yesu alionyesha waziwazi kwamba fundisho hilo halikuungwa mkono na Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki