Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 12/15 kur. 20-23
  • Jenga na Kufuata Imani Yako Pamoja na Waamuzi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jenga na Kufuata Imani Yako Pamoja na Waamuzi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Faidika na Mambo ya Msingi
  • Kutenda kwa Imani Yenye Nguvu Sana!
  • Angalia Uone Masomo ya Kujifunza
  • Kitabu Cha Biblia Namba 7—Waamuzi
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Waamuzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Waamuzi—Yaliyomo
    Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
  • “Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 12/15 kur. 20-23

Jenga na Kufuata Imani Yako Pamoja na Waamuzi

KAMA ungeulizwa utaje kikundi cha watu wa Kibiblia wenye imani ya kutokeza, ungetaja kikundi gani? Wale mitume 12? Wale wana 12 wa Yakobo? Pengine. Lakini ungekuwa na sababu ya kutosha ukitaja kikundi kingine cha watu 12 ambao imani yao inasifiwa kwetu katika Biblia.

Tunamaanisha wale wanaume 12 ambao matendo yao ya imani yanasimuliwa katika kitabu cha Waamuzi. Wengine wao wanatajwa katika Waebrania 11:32-34: “Wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha . . . ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni.”

Hapo wanne kati ya waamuzi hao wanatajwa. Unaweza kukumbuka waamuzi wengine waaminifu wangapi? Jaribu kukumbuka kabla hujaangalia orodha iliyo chini.a Inawezekana pia kwamba unakumbuka vitendo fulani vyenye kutokeza vilivyofanywa na waamuzi, kama vile Samsoni alipoangamiza wakuu na watu Wafilisti​—na yeye binafsi​—kwa kubomoa hekalu la Dagoni, au juu ya Gideoni kutumia mashujaa wa vita 300 tu kufagilia mbali majeshi ya Midiani. Watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo wamejua hadithi hizo katika Sunday school. Lakini je, wanapata mafunzo ya maana katika kitabu cha Waamuzi, mafunzo ambayo yanaweza kuwa na matokeo juu ya imani yao, kufanya maisha yao yawe bora sasa na kuwasaidia wafikie ‘uzima utakaokuwapo baadaye’? (1 Timotheo 4:8) Ikiwa unafikiri sivyo ilivyo, je, wewe ni tofauti? Je! wewe umekwisha kuruhusu kitabu cha Waamuzi kisaidie imani yako na maisha yako ya Kikristo?

Faidika na Mambo ya Msingi

Soma kitabu hicho. Utaona kwamba, hata ikiwa hiyo ndiyo mara yako ya kwanza kukisoma au ikiwa unakisoma mara nyingine, utavutwa sana na masimulizi mengi moto-moto. Yatakupa mambo mengi ya kuzungumza​—pamoja na watoto wako au vijana wengine, na pia na watu wakubwa wenye kufikiri. Lakini, unaposoma kumbuka mambo fulani makuu yanayotajwa katika masimulizi mengi. Kwa mfano mambo gani?

Moja ni kwamba ni rahisi sana kuruhusu imani yetu katika Mungu idhoofike au kusahau ambayo yeye amekufanyia. Mtu anayejifunza juu ya tumaini la Kikristo na juu ya kupata msamaha kupitia Kristo huenda akawa na bidii nyingi ya kwanza. Huenda akahudhuria mikutano kwa furaha na kushiriki katika huduma ya Kikristo. Anaweka mambo hayo kwanza maishani, wala hana wasiwasi juu ya vitu vya kimwili, kama kuwa na motokaa mpya, nyumba nzuri sana au vidude vya televisheni vya karibuni vyenye bei kubwa. Lakini baada ya miaka fulani, je, yeye atapoteza ‘upendo aliokuwa nao kwanza’? (Ufunuo 2:4) Historia ya Israeli inayofunuliwa katika Waamuzi inaonyesha jinsi jambo hilo linavyoweza kumpata ye yote wetu kwa urahisi.

Sura mbili za kwanza zinatoa utangulizi. Baada ya Waisraeli chini ya uongozi wa Yoshua kuitwaa Nchi ya Ahadi, hawakutii kwa kutofagilia mbali Wakanaani wenye kuabudu sanamu, wasio na adili. (Waamuzi 1:28-33) Kwa hiyo Yehova aliruhusu wageni hao na miungu yao wajaribu Israeli. (Waamuzi 2:19-23) Mara nyingi Israeli walishindwa na jaribu hilo. Kwa sababu hiyo kukawa uhitaji wa waamuzi.

Hali katika wakati wa mwamuzi wa kwanza, Othnieli, inaonyesha kawaida ya mambo yaliyotokea tena na tena. Waisraeli walikuwa wameshindwa na ibada chafu ya Baali, kwa hiyo Mungu akaruhusu mfalme mmoja wa Siria (Shamu) awaonee kwa miaka minane. Jambo hilo liliwasukuma ‘wamwitie Yehova na kumwomba msaada. Mungu akawainulia mwokozi, awaokoe, yaani, Othnieli. Roho ya Yehova ikamjilia juu yake, naye akawa mwamuzi wa Israeli; akatoka kwenenda vitani, naye Mungu akatia mfalme wa Siria mkononi mwake. Nayo nchi ikawa na amani muda wa miaka arobaini.’​—Waamuzi 3:7-11.

Jinsi Waisraeli hao walivyoshukuru walipokuwa huru, sawa na ambavyo sisi tulivyothamini kujifunza ukweli wa Kikristo na kuwa huru na dini ya uongo! Hata hivyo, miaka yenye kufuata ingetokeza nini? Mstari unaofuata unasema: “Basi wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu tena mbele za [ Yehova]; naye [Yehova] akamtia nguvu Egloni mfalme wa Moabu juu ya Israeli.” (Waamuzi 3:12) Hicho ni kielelezo na hatari ya mambo yanayoweza kutupata tukiruhusu masadikisho yetu yafifie. Lakini ili kututia moyo masimulizi hayo yanaendelea kusema hivi: Mara Waisraeli waliporudiwa na fahamu zao, Mungu akawainulia mwamuzi Ehudi mwenye kutumia mkono wa kushoto. Alimpa Mfalme Egloni aliyekuwa mnene ujumbe wenye kutaja mambo waziwazi, na kutokeza wokovu wa Israeli. Soma masimulizi hayo yenye kusisimua katika mistari inayobaki ya sura ya 3.

Kutenda kwa Imani Yenye Nguvu Sana!

Jambo jingine la msingi linalopaswa kukuvutia wewe ni kwamba Mungu anaweza kukutumia wewe utimize mambo yenye kutokeza sana ikiwa una imani yenye nguvu.​—Linganisha Mathayo 17:20; 21:21.

Mifano michache ni hii: Fikiria jinsi Gideoni akiwa na wanaume 300 tu wenye imani alivyofagilia mbali Wamidiani ambao walikuwa “mfano wa nzige kwa wingi.” (Waamuzi 7:1-25) Kwa kutiwa moyo na Debora, Baraka alitokeza ukombozi upande wa kaskazini kutokana na Wakanaani waliokuwa na magari ya vita yenye panga za chuma zenye kuogopesha sana, panga zilizokuwa zimechomoza kutoka kwa magurudumu yayo. Pia unapaswa kuangalia kwamba katika kisa hicho ni mwanamke aliyepiga pigo la mwisho la ushindi. (Waamuzi 4:—5;31) Nguvu za Samsoni zinajulikana sana. Kwa nguvu zake zisizo za kawaida, Samsoni aliweza kumrarua simba; akitumia taya ya punda aliwaua maadui elfu moja na akang’oa lango la mji wa Gaza, na kulibeba mpaka juu ya mlima.​—Waamuzi 14:5—16:3.

Hakuna shaka kwamba imani yenye kutokeza ilionyeshwa na waamuzi hao, na kwa hakika ikawastahilisha waandikwe katika orodha ya kitabu cha Waebrania kuwa wao ni mifano kwa ajili yetu. Mifano katika njia gani? Bila shaka hungetazamia kumrarua simba kwa mikono yako tu, sivyo? Lakini utakabili matatizo makali kwa imani yako ukijaribu kuishi kila siku kama Mkristo aliye mshikamanifu kwa Yehova.

Pengine ukiwa kijana shuleni unakabili mkazo mkubwa sana ujaribu dawa za kulevya au ngono, au kufuatia ufundi fulani wa kikazi ukiwa mtaalamu mwenye kulipwa mshahara mnono. Ukiwa mtu binafsi, au pamoja na jamaa yako, labda umejinyima sana mambo ya kimwili ili utumikie ukiwa mhudumu wa wakati wote au kuishi mahali ambako kuna uhitaji mkubwa wa wahudumu wa namna hiyo, lakini unaona Wakristo wengine ambao inaonekana wanafanya utajiri na maisha ya juu kuwa mambo ya kwanza maishani. Au huenda imani yako ikatatizwa kwa sababu mtu mwingine amekukatisha sana tamaa. Huenda ikawa ni mtu ambaye alikuwa mashuhuri kati ya Wakristo lakini ambaye kiburi chake kilimwongoza ageuke na kupinga ndugu zake. Kwa upande mwingine, ingeweza kuwa ni mtu wa ukoo wa karibu ambaye upendo wake umekuwa baridi na ambaye ameacha kumtumikia Yehova.

Katika cho chote cha visa hivyo, je, utapata kitia-moyo kwa imani ya waamuzi? Imani yao waliyopewa na Mungu iliwawezesha mambo ambayo yangaliweza kuonekana kuwa hayawezekani. Mungu uyo huyo anaweza kukupa wewe imani ukiendelea kuitafuta kupitia sala na kuendelea katika njia ya Kikristo. Imani ni tunda la roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Kuhusu roho iyo hiyo iliyomfanya Samsoni awe mwenye nguvu, Yesu alisema, “Baba aliye mbinguni [atazidi] sana kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao!” Kwa sababu hiyo, katika sura iyo hiyo ya Waebrania ambayo imeorodhesha waamuzi kuwa mifano ya imani tunahakikishwa kwamba Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao.” (Luka 11:13; Waebrania 11:6) Yeye pia anaweza kuthawabisha imani yako.

Angalia Uone Masomo ya Kujifunza

Tumekwisha elekeza fikira kwenye masomo kadha unayoweza kupata katika Waamuzi. Lakini bila shaka bado utaona faida ya ziada kutokana na kisehemu hiki cha Maandiko ‘yaliyoongozwa na Mungu na yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.’​—2 Timotheo 3:16, NW.

Kwa mfano, utaona kwamba kwa njia ya kiasi Gideoni hakutaka kufuata mwendo fulani mpaka alipokuwa na uhakika kwamba ulikuwa ni mapenzi ya Mungu. Baadaye, kiasi icho hicho kilimsaidia aepuke kuringa kwa sababu ya kufanikiwa na mashuhuri. Huenda ukaweza kufaidika kwa hilo. Kumbuka kwamba kwa msaada wa Mungu jeshi dogo la Gideoni lilifagilia mbali kabisa umati wa Wamidiani. Ebu wazia jinsi jambo hilo linavyoweza kuwa lilimletea Gideoni sifa. Kwa kulinganisha, huenda ukapata sifa kwa ajili ya karama fulani yenye kutokeza, kama vile kuwa msemaji wa watu wote mwenye uwezo mzuri au mpangaji-mambo mzuri sana. Kwa habari ya Gideoni, “watu wa Israeli wakamwambia Gideoni, Tawala wewe juu yetu, wewe, na mwanao, na mjukuu wako pia; kwa kuwa wewe umetuokoa na mikono ya Midiani.” Mtu aitikieje sifa ya jinsi hiyo? Gideoni alisema: “Mimi sitatawala juu yenu, wala mwanangu hatatawala juu yenu; yeye [Yehova] atatawala juu yenu.” (Waamuzi 8:22, 23) Vivyo hivyo sisi na tujaribu sana kudumisha kiasi, tukitambua kwamba karama zetu zote​—na kupitia hizo mambo ambayo tunatimiza​—zinatokana na uweza mbalimbali ambao Mungu aliwapa wanadamu.

Historia ya Gideoni na waamuzi wengine inatuonyesha sisi, pia, kwamba wao ni wanadamu wasiokamilika, kama sisi. Tunaweza kupata masomo fulani kutokana na makosa yao.

Kwa hiyo, wakati Gideoni alipowaruhusu Waisraeli washiriki nyara zake pamoja naye, alitengeneza naivera yenye bei kubwa sana, vazi lililo kama aproni, labda likiwa limepambwa kwa mawe ya thamani. Ingawa huenda ikawa alikuwa amechochewa afanye hivyo kwa kusudi zuri, Waisraeli wengine waliitendea kama kwamba ni sanamu ya kuabudiwa, wakaelekeza kwingine ibada ya Yehova kutoka patakatifu.​—Waamuzi 8:24-27.

Roho ya Yehova ilitenda kwa nguvu sana juu ya Samsoni, ikamwezesha afanye matendo yenye kupita nguvu za kibinadamu. (Waamuzi 14:5, 6, 19; 15:14, 15; 16:3, 28-30) Pia ilikuwa “kutoka kwa Yehova” akaomba mwanamke fulani Mfilisti awe mke wake, kwa maana Samsoni ‘alikuwa akitafuta nafasi dhidi ya Wafilisti.’ (Waamuzi 14:4, NW) Jambo hilo lilielekeza kwenye mapambano yaliyoua wengi wa Wafilisti wenye kuonea. Pia bila shaka ilikuwa ni kwa ajili ya mwelekezo wa Yehova kwamba Samsoni akaenda mpaka Gaza na kukaa kwenye nyumba ya kahaba mmoja, kwa maana hilo liliongoza kwenye tendo jingine kuu la kuaibisha Wafilisti wasio na adili hata kidogo.b Hata hivyo, inaonekana kwamba uhusiano wa Samsoni na wanawake hao huenda ukawa ulimvuta atende kipumbavu alipompenda Delila, yaelekea mwanamke Mwisraeli ambaye Wafilisti wangeweza kumpa rushwa.​—Waamuzi 16:1-21.

Masimulizi kama hayo yanapaswa kutufundisha kwamba sikuzote ni lazima tujihadhari na mashambulizi yenye hila ya adui wetu. Kwa mfano, huenda Mkristo akawa na kusudi zuri la kumtembelea mwabudu mwenzake wa jinsia tofauti, kama vile kumfariji au kumtia moyo wakati wa msiba. Hata hivyo kwa kawaida si jambo la hekima kufanya hivyo wakati hao wawili wangekuwa peke yao. Kutokamilika kwa kibinadamu kungeweza kuwaingiza katika mwenendo usiofaa, au hali hiyo ingeweza kuwasukuma majirani waseme kwamba Wakristo wana adili zilizoshuka kama za walio wengi katika ujamii.

Kwa upande mwingine, tafakari juu ya imani na bidii ya kujitoa kwa Yehova ya binti bikira wa Yeftha. Huenda Wakristo fulani walio waseja wakawa na maoni kwamba hali zinazofaa zikitokea ili waweze kupata wenzi wenye kupenda walio washikamanifu, huenda wakafunga ndoa. Hata hivyo maadamu wao ni waseja wanaweza kukumbuka kwamba ingawa binti ya Yeftha alikuwa na pindi ambazo alijisikia amekosa jambo fulani kwa sababu ya kuwa katika hali ya kutoweza kuolewa au kuzaa watoto, yeye alidumisha imani ya kusifika katika mgawo wa pekee ambao hali yake ya useja ilimruhusu kuwa nao.​—Waamuzi 11:30-40.

Hayo ni baadhi tu ya masomo mengi yenye faida utakayoweza kupata katika kitabu cha Waamuzi chenye kusisimua na kutia imani. Ukimaliza kusoma kitabu hicho unapaswa uwe na usadikisho ulioongezeka kwamba Yehova ndiye Mwokozi mkuu wa wale wanaomwabudu yeye. Ikiwa wewe ni mmoja wa Waabudu wake, tafuta kuwa na imani yenye nguvu inayochochea, kama inavyoonyeshwa vizuri sana katika waamuzi.

[Maelezo ya Chini]

a Othnieli, Ehudi, Shamgari, Tola, Yairi, Ibzani, Eloni, Abdoni. Ingawa pia walihukumu Israeli, Yoshua na Samweli kwa kawaida hawatiwi katika kikundi kinachotajwa katika kitabu cha Waamuzi.

b Ni jambo la akili kukata maneno kwamba, akiwa mgeni, Samsoni alitaka tu mahali pa kulala usiku kucha, wala hakuenda kwenye nyumba ya kahaba kwa sababu zisizo za adili. Masimulizi yanasema kwamba “akalala hata usiku wa manane” wala hayasemi kwamba “akalala na mwanamke huyo mpaka usiku wa manane.”

[Chati katika ukurasa wa 20, 21]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mistari iliyolala ina weusi unaotofautiana ili kutofautisha vipindi mbalimbali.

Chati hii imepangwa ionyeshe njia moja kati ya nyingi ambayo katika hiyo wakati wa vipindi vinavyotajwa katika kitabu cha Waamuzi ungeweza kuingia katika urefu wa wakati unaoonyeshwa kwingine. Kwa habari zaidi, ona kitabu Aid to Bible Understanding, kurasa 335-8.

1473 K.W.K.

KUSHINDWA kwa Kanaani (6)

Kipindi cha katikati (35[?])

SIRIA chini ya Kushanrishathaimu yaonea Israeli (8)

OTHNIEL ashinda Siria

“Nchi ikawa na amani” (40)

MOABU chini ya Egloni yaonea Israeli (18)

EHUDI ashinda Moabu

“Nchi ikawa na amani” (80)

KANAANI chini ya Yabini wa Hazori yaonea Israeli (20)

SHAMGARI ‘aokoa Israeli’ kutokana na Wafilisti. Kipindi chenyewe hakitajwi

BARAKA ashinda Kanaani

“Nchi ikawa na amani” (40)

MIDIANI yaonea Israeli (7)

GIDEONI ashinda Midiani

“Nchi ikawa na amani. . . katika siku za Gideoni” (40)

ABIMELEKI atawala (3)

TOLA (wa Isakari) ahukumu Israeli (23)

YAIRI (wa Gileadi) ahukumu Israeli (22)

AMONI yaonea Israeli (18)

Miaka 300 tangu kuanza kwa ushindi wa Israeli. (Waamuzi 11:26-33)

YEFTHA ashinda Amoni; ahukumu (6)

IBZANI (wa Bethlehemu) ahukumu (7)

FILISTIA yaonea Israeli (40)

ELONI (wa Zebuluni) ahukumu (10)

ABDONI (wa Efraimu) ahukumu (8)

SAMSONI (wa Dani) ahukumu (20)

Sanduku la agano katika Kiriath-yearimu miaka 20

ELI Kuhani mkuu (40)

Filistia yashinda Israeli

Kipindi cha katikati (5 [?])

SAMWELI nabii, mwamuzi

Samweli aongoza Israeli mpaka kwenye ushindi juu ya Filistia (1 Samweli 7:7-14)

1117 B.C.E.

SAULI Mfalme (40) Utawala waanza miaka 356 tangu mwanzo wa ushindi wa Kanaani. (1 Wafalme 6:1; Kumbukumbu la Torati 2:7; Matendo 13:21; 2 Samweli 5:4)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki