Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w15 10/1 kur. 6-8
  • Sala​—Ina Umuhimu Gani Kwako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala​—Ina Umuhimu Gani Kwako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Amani ya akili.
  • Inatufariji na kutupatia nguvu tunapopatwa na majaribu.
  • Hekima kutoka kwa Mungu.
  • Sala Zinaweza Kukusaidiaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Kwa Nini Tusali Bila Kukoma?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Jinsi ya Kusali—Je, Kukariri Sala ya Bwana Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kusali?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
w15 10/1 kur. 6-8
Mwanamke anasali huku akikumbuka hali ya mama yake aliye mgonjwa

HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

Sala Ina Umuhimu Gani Kwako?

Kabla ya kufanya jambo lolote, ni kawaida kujiuliza hivi: ‘Lina umuhimu gani kwangu?’ Je, tunaonyesha ubinafsi kwa kujiuliza hivyo kuhusu sala? Hapana. Si ajabu kwamba tunataka kujua ikiwa sala ina faida yoyote. Hata mwanamume mwaminifu Ayubu aliuliza hivi: “Kama ningemwita, je, angenijibu?”—Ayubu 9:16.

Katika makala zilizotangulia, tulichunguza uthibitisho unaoonyesha kwamba sala ni zaidi ya desturi ya kidini au aina fulani ya tiba ya akili. Mungu wa kweli husikiliza sala. Atatusikiliza tukisali kwa njia inayofaa na kuhusu mambo yanayofaa. Anatuhimiza tumkaribie. (Yakobo 4:8) Hivyo, tutarajie nini tukisali kwa ukawaida? Acheni tuchunguze baadhi ya faida tutakazopata.

Amani ya akili.

Unapopata matatizo au changamoto maishani, je, wewe huwa na wasiwasi mwingi? Katika nyakati kama hizo, Biblia inatutia moyo ‘tusali bila kuacha’ na kuacha “maombi yenu yajulishwe Mungu.” (1 Wathesalonike 5:17; Wafilipi 4:6) Biblia hutuhakikishia kwamba tukisali kwa Mungu, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:7) Tutapata amani tukimweleza Baba yetu wa mbinguni mahangaiko yetu. Kwa kweli, anatutia moyo tufanye hivyo. “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza,” inasema Zaburi 55:22.

“Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” —Zaburi 55:22

Watu wengi ulimwenguni wamepata amani hiyo. Hee Ran, kutoka Korea Kusini, anasema: “Hata ninapokuwa na matatizo makubwa sana, nikisali, ninahisi kama mzigo umepungua na ninahisi nimepata nguvu za kuendelea kuvumilia.” Cecilia, kutoka Ufilipino, anaeleza hivi: “Nikiwa mama, ninahangaikia sana hali ya binti zangu na mama yangu, ambaye sasa hawezi kunitambua. Sala imenisaidia niendelee na shughuli zangu za kila siku bila kuwa na wasiwasi mwingi. Ninajua kwamba Yehova atanisaidia kuwatunza.”

Inatufariji na kutupatia nguvu tunapopatwa na majaribu.

Je, unakabili hali ngumu sana, labda inayohatarisha uhai wako au inayohuzunisha sana? Kusali kwa “Mungu wa faraja yote” kunaweza kukupa kitulizo kwa kiasi kikubwa. Biblia inasema kwamba yeye “hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Kwa mfano, pindi moja Yesu alipokuwa amefadhaika sana, ‘alipiga magoti na kuanza kusali.’ Matokeo yalikuwa nini? “Ndipo malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.” (Luka 22:41, 43) Mwanamume mwingine mwaminifu, Nehemia, alitishwa na watu waovu waliojaribu kumzuia asifanye kazi aliyopewa na Mungu. Alisali hivi: “Itie mikono yangu nguvu.” Mambo yaliyotendeka baada ya hapo yanaonyesha kwamba kwa kweli Mungu alimsaidia kushinda woga na kumaliza kazi yake. (Nehemia 6:9-16) Reginald, kutoka Ghana, anaeleza hivi kuhusu sala: “Ninaposali, hasa ninapolemewa na hali ngumu, ninahisi kama nimemwambia mtu anayeweza kunisaidia na ambaye amenihakikishia kwamba sina haja ya kuwa na wasiwasi.” Bila shaka, Mungu anaweza kutufariji tunaposali kwake.

Hekima kutoka kwa Mungu.

Baadhi ya maamuzi tunayofanya yanaweza kutuathiri sisi na wale tunaowapenda. Tunawezaje kufanya maamuzi ya hekima? Biblia inasema hivi: “Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, [hasa ya kushughulika na majaribu] na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Ikiwa tutasali ili tupate hekima, Mungu atatumia roho yake takatifu kutuongoza tufanye maamuzi ya hekima. Tunaweza hasa kusali ili tupewe roho takatifu kwa sababu Yesu alituhakikishia hivi: “Baba aliye mbinguni [atawapa] roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:13.

Mwanamume akisali

“Mara zote nilisali kwa Yehova ili nipate mwongozo wa kufanya uamuzi unaofaa.”—Kwabena, Ghana

Hata Yesu alitambua umuhimu wa kusali kwa Baba yake alipotaka kufanya maamuzi mazito. Biblia inatuambia kwamba alipotaka kuwachagua wanaume 12 ambao wangekuwa mitume wake, ‘alisali kwa Mungu usiku wote.’—Luka 6:12.

Kama ilivyokuwa kwa Yesu, watu wengi leo wamepata amani ya akili wanapoona jinsi Mungu anavyojibu wanapomwomba awasaidie kufanya maamuzi ya hekima. Regina, kutoka Ufilipino, anakabili matatizo ya aina mbalimbali, kama vile kujiruzuku yeye mwenyewe na familia yake baada ya kufiwa na mume, kupoteza kazi, na ugumu wa kulea watoto. Ni nini kilichomsaidia kufanya maamuzi ya hekima? Anasema hivi: “Ninategemea msaada wa Yehova kupitia sala.” Kwabena, kutoka Ghana, anaeleza kwa nini alimwomba Mungu msaada: “Nilipoteza kazi ya ujenzi yenye mshahara mnono.” Anapofikiria maamuzi aliyohitaji kufanya, anasema hivi: “Mara zote nilisali kwa Yehova ili nipate mwongozo wa kufanya uamuzi unaofaa.” Anaongezea hivi: “Nina hakika kwamba Yehova alinisaidia kuchagua kazi inayoniwezesha kutimiza mahitaji yangu ya kiroho na kimwili.” Wewe pia unaweza kupata mwongozo wa Mungu ukisali kuhusu mambo yanayoweza kuathiri uhusiano wako pamoja naye.

Tumetaja faida chache unazoweza kupata ukisali. (Kwa mifano zaidi, tazama sanduku “Faida za Sala.”) Hata hivyo, ili upate faida hizo unahitaji kwanza kumjua Mungu na mapenzi yake. Ikiwa ungependa jambo hilo, tunakutia moyo waombe Mashahidi wa Yehova wakufundishe Biblia.a Hiyo inaweza kuwa hatua ya kwanza ya kumkaribia “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.

a Ili upate habari zaidi wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au tembelea tovuti yetu ya www.jw.org/sw.

Faida za Sala

Amani ya akili “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

Faraja kutoka kwa Mungu “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

Mwongozo wa kufanya maamuzi ya hekima “Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.”—Yakobo 1:5.

Msaada wa kuepuka kishawishi “Salini, ili msiingie katika jaribu.”—Luka 22:40.

Msamaha wa dhambi “Watu wangu ambao jina langu limeitwa juu yao wajinyenyekeze na kusali na kuutafuta uso wangu na wageuke kutoka katika njia zao mbaya, basi mimi nitasikia nikiwa mbinguni na kusamehe dhambi yao.”—2 Mambo ya Nyakati 7:14.

Njia ya kuwasaidia wengine “Dua ya mtu mwadilifu, inapofanya kazi, ina nguvu nyingi.”—Yakobo 5:16.

Tunatiwa moyo sala zinapojibiwa “Yehova akaendelea kumwambia [Sulemani]: ‘Nimeisikia sala yako na ombi lako la kutaka kibali ambalo uliomba kibali mbele zangu.’”—1 Wafalme 9:3.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki