Wasaidie Wale Wanaohudhuria Mikutano
1 Daudi alikuwa akionyesha tamaa ya kutoka moyoni aliposema: “Miongoni mwa umayamaya wenye makundi makundi mimi nitambariki Yehova.” (Zab. 26:12, NW) Daudi alitambulisha umayamaya wenye makundi makundi kuwa waabudu wa Yehova. Je! tamaa yetu ya kutoka moyoni ni kame ile ya Daudi? Tunaweza kuonyesha kwamba ndivyo ilivyo kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ambapo tunaweza kumbariki Yehova na kuwatia wengine moyo wafanye hivyo.—Ebr. 10:24, 25.
2 Yaelekea kwamba kuna hesabu kubwa ya watu mmoja mmoja wanaohudhuria mikutano katika kundi lako lakini bado si wahubiri wa habari njema. Tarakwimu za karibuni za hadhirina ya mikutano zinaonyesha kwamba watu wanaokaribia hesabu maradufu ya wahubiri wanaoshiriki wanahudhuria hotuba ya watu wote. Tunaweza kufanya nini tuwasaidie watu hao wastahili kushiriki katika huduma? Wengine ni watoto wa waabudu wa Yehova, lakini walio wengi ni watu wapya wanaopendezwa. Je! sisi tunaweza kuwa wenye msaada kwa wenye kupendezwa hawa? Huenda wengine wao wakawa watu ambao bado hawajaanza kujifunza. Unapozungumza nao mikutanoni, huenda ukapata kwamba wengine wao watafurahi ukiongoza funzo la Biblia pamoja nao.
3 Upendo wa akina ndugu kwa mmoja na mwenzake na kwa watu wapya haukosi kuonwa. Kama alivyosema mwanamume mmoja kijana baada ya kuhudhuria mkutano mara ya kwanza: “Mimi nilishangaa kwamba wote walifahamiana na kwamba jumba lilikuwa na uchangamfu wa mazungumzo ya kirafiki.” Jambo hilo lilimfanya ataka kuendelea kuhudhuria. Yeye angeweza kuona kwamba upendo ambao akina ndugu walikuwa nao mmoja kwa mwenzake ulikuwa wa kweli.
NJIA ZA KUSAIDIA
4 Upendo wetu na hangaiko letu kwa wengine linaweza kuonyeshwa kwa kuzungumza nao kabla na baada ya mikutano. Kupendezwa sana huko na hali njema ya wengine kulionyeshwa na Paulo. Katika Warumi sura ya 16, yeye alipeleka salamu kwa watu wengi mmoja mmoja, akionyesha kwamba aliwafahamu vizuri na alihangaikia hali yao njema ya kimwili na kiroho. (Rum. 16:1-16, NW) Yeye alipeleka salamu kwa wengine ambao walikuwa wamekuwa “katika muungano pamoja na Kristo” kwa muda mrefu zaidi ya yeye, likionyesha kupendezwa kwake na watu walio katika madaraja yote ya ukuzi wa kiroho. Maelezo yake kuwahusu yanaonyesha kwamba yeye alikuwa amechukua wakati na kuonyesha kupendezwa ili apate kuwafahamu. Yeye alielewa matatizo yao naye angeweza kuwasaidia kiroho. Kuja kwenye mikutano mapema kunaandaa nafasi nzuri ya kufahamiana vizuri zaidi na wengine na kuwatia moyo. Mbona usijaribu kwa bidii kufika dakika 15 au 20 kabla mkutano haujaanza na kubaki kidogo baadaye ili ushiriki kikamili zaidi katika kuwatia wengine moyo.
5 Tunaweza kuwatia moyo wahudhuriaji wapya wa mikutano kwa kuwaonyesha jinsi ya kutayarisha kwa ajili ya mikutano. Wanaweza kutiwa moyo kujibu maswali mikutanoni na kujiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wanapostahili. Madokezo machache yanayofaa kutoka kwa mhubiri mwenye ujuzi yanaweza kuwasaidia wapya katika kutayarisha hotuba na kutoa maelezo yenye maana katika maneno yao wenyewe.—Ona Kiongozi cha Shule, somo 4, 7, na 18.
6 Tukiwa sehemu ya umayamaya wenye makundi makundi wa Yehova tukionyesha upendo wa kweli mmoja na mwenzake, tunakua kiroho, na kifungo cha umoja chenye nguvu zaidi kinatokea. (Gal. 6:10) Tamaa yetu ya kuhusika katika utendaji wa kundi inakuwa yenye kina kirefu, nasi tunatafuta kuwa na ushirika mkubwa katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Basi, acheni sisi, tuendeleze jitihada yetu yenye upendo ya kuwasaidia wapya wasifu na kuheshimu Yehova.