Ongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
1 Kuongoza wanafunzi wa Biblia hatua kwa hatua kufikia kuwa wanafunzi kunahitaji kufikiria kimbele na kupanga vizuri. Mafunzo yanapaswa kuanzishwa na kuongozwa tukiwa na kusudi lililo waziwazi akilini, lile la kusaidia mfunzwa awe mwanafunzi wa Kristo Yesu mwenye kuzaa matunda. (Mt. 13:23) Kwa hiyo, wafundishe washike mambo yote aliyoamuru Yesu. (Mt. 28:19, 20) Msaidie mwanafunzi aelewe kwamba funzo litaongozwa kila juma ili kumsaidia apate maarifa ya msingi ya Neno la Mungu. Pia, kwa fadhili onyesha uharaka wa kufanya maendeleo mazuri kupitia matumizi ya yale anayojifunza. (Mit. 22:17; Flp. 3:16) Lakini ni katika sehemu zipi hususa maendeleo yanapaswa kuonekana?
2 Pindi kwa pindi mhubiri anapaswa afikirie maendeleo yanayofanywa na mwanafunzi wa Biblia. Jiulize: Je! yeye anatayarisha somo lake kimbele, akisoma marejezo ya Maandiko ambayo yametajwa lakini hayakunukuliwa? (Mdo. 17:11; 1 The. 2:13) Je! anatoa maelezo yake kwa maneno yake mwenyewe na je! yanaonyesha uthamini wa kutoka moyoni kwa ajili ya kweli za Biblia anazojifunza? (Mit. 2:1-6) Je! lingekuwa jambo linalofaa kumtia moyo afanye usomaji zaidi wa Neno la Mungu na vichapo vya Sosaiti? Je! ameandikisha Amkeni! na Mnara wa Mlinzi? Je! yeye amefanya maendeleo kufikia kiwango cha kuthamini uandalizi wa andiko la kila siku?
3 Je! anaonyesha kupitia msemo wake, mwelekeo, na mwenendo kwamba anatumia kiwango cha Biblia kuhusu adili? (1 Kor. 6:9, 10) Je! yeye anafanya marekebisho katika utu? (Efe. 4:22-24) Je! uthamini wa kweli za Biblia unaotoka moyoni unamsukuma azungumze kivivi-hivi pamoja na watu wa ukoo, wafanya-kazi wenzi, au majirani kuhusu mambo anayojifunza? (Luka 6:45) Ikiwa anaweza kimwili na kulingana na hali, je! anafanyiza kigezo cha kawaida cha kuhudhuria mikutano ya kundi? (Ebr. 10:23-25) Kufikiria maendeleo ya mwanafunzi katika sehemu hizo kutasaidia kuamua kadiri ambayo yeye ‘anapokea kwa upole neno lile lililopandwa ndani.’—Yak. 1:21.
KUKOMESHA MAFUNZO YASIYOZAA MATUNDA
4 Ikiwa mwanafunzi hafanyi maendeleo yanayofaa baada ya wewe kumsaidia kwa saburi kwa muda fulani wa kutosha, huenda likawa jambo zuri kutumia wakati huo kwa faida nzuri kuwatafuta wanaostahili. (Mt. 10:11-13, NW) Kulingana na hali, huenda likawa jambo lenye hekima kukomesha funzo hilo. Msifu mwenye nyumba kikweli kwa maendeleo yaliyofanywa. Hata hivyo, onyesha kwamba jinsi kweli za Biblia zinavyofunzwa, zinapaswa kutumiwa. Ukitumia mfano wa maneno wa Yesu kuhusu mpandaji, unaweza kuzungumzia kila moja ya aina nne za udongo zinazorejezewa kisha uonyeshe jinsi kielezi hicho kinavyokazia uhitaji wa mwitikio chanya kwa ujumbe wa Ufalme. Huenda jambo hilo likamsaidia mwanafunzi ang’amue ni kitu gani ambacho kimemzuia asizidi kufanya maendeleo. Huenda ukawa na fursa ya kutoa maelezo kuhusu yale ambayo umeona. Uwe mwenye fadhili, lakini mwenye kusema mambo kwa unyofu na waziwazi. (1 Kor. 14:8, 9) Acha ajue kwamba funzo linaweza kurudiwa wakati marekebisho yanayohitajiwa yamefanywa. Kwa sasa, utakuwa ukimtembelea mara kwa mara ili kumtia moyo.—Ona Huduma ya Ufalme, Machi 1970, ukurasa 2.
5 Unapopata watu walio katika eneo ambao wamejifunza wakati uliopita, ni jambo la hekima kupata kujua walijifunza kwa muda gani na pamoja na nani. Kwa nini waliacha kujifunza? Ikiwa aliyeongoza funzo hilo wakati uliopita anajulikana, lingekuwa jambo zuri kuzungumza habari hiyo pamoja na yeye na mwangalizi wa utumishi kabla ya kuanza tena funzo hilo. Yaelekea kuna mambo fulani ya uhakika usiyoyajua. Watu fulani wamejifunza na wahubiri wengi tofauti tofauti kwa miaka iliyopita bila kufanya maendeleo yoyote. Tunahitaji kutumia wakati pamoja na wale wanaoonyesha kupendezwa kihalisi na ukweli.
6 Uwe unakomesha funzo la Biblia au unaanza tena lile lililokomeshwa wakati uliopita, huenda ukapenda kuzungumza pamoja na mwenye nyumba habari nzuri inayopatikana katika makala “Kungali Kuna Wakati wa ‘Kumgeukia Yehova’” kwenye kurasa 220-2 katika toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Aprili 1, 1976. Tunaponoa uwezo wetu wa kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo, huenda wengine wasiohesabika wakasaidiwa kujifunza, kukubali, na kuzoea ukweli. Jambo hilo linaweza kutokeza kupata kwao uhusiano wenye kibali pamoja na Yehova Mungu na, mwishowe uhai wa milele.—Flp. 4:9; Yn. 17:3.