Kuonyesha Mungu na Jirani Upendo
1 Alipokuwa akijibu mmoja aliyeuliza: “Mwalimu, katika torati ni amri ipi iliyo kuu?” Yesu alisema: “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho [nafsi, NW] yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako [wewe mwenyewe, NW].”—Mt. 22:36-39.
2 Upendo wa kina kirefu wa Yesu kwa Mungu ulidhihirishwa katika njia aliyoishi maisha yake. Yeye alisema: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yoh. 4:34) Upendo wake wa kweli kwa jirani ulimsukuma ahubiri habari njema za Ufalme wa Yehova kwa bidii. Pia yeye alifanya matendo ya kuponya. Na ni wonyesho bora wa upendo kama nini ulioonwa kwa kutoa uhai wake uwe dhabihu kwa ajili ya aina ya binadamu! Tunaweza kumwigaje Yesu katika kuonyesha Mungu na jirani upendo?
JINSI YA KUONYESHA UPENDO
3 Kuwaambia wengine habari njema za Ufalme ni njia kubwa ya kufanya hivyo. Watu wanahitaji kupewa msingi wa tumaini na habari za kuwasaidia wakabiliane na nyakati hizi zenye hatari. (2 Tim. 3:1) Imani yetu katika Ufalme wa Mungu yapaswa itusukume tuseme juu yao kwa hamu yenye bidii ili tuwape wote fursa ya kusikia ukweli. Kusema ukweli juu ya Ufalme wa Mungu na kusudi lake kuelekea dunia kunamheshimu yeye. Je! sisi tuna upendo wa jinsi hiyo kwa ajili ya Mungu na jirani? Je! sisi tunashiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri Ufalme? Je! sisi tunatumia fursa za kuwatolea ushuhuda kivivi-hivi watu wa ukoo, majirani na wengine? Sisi sote lazima tutoe ithibati halisi kama hiyo ya upendo wetu kwa Mungu na jirani.
4 Huenda watu fulani wakawa wamehisi kwamba ni wale tu walio stadi au wenye elimu nzuri ndio wanaostahili kuchukua ujumbe kama huo wa maana sana. Zaidi, utegemeo wetu kwa Yehova ndio unaohitajiwa. (Luka 11:13; 1 Kor. 1:26, 29, 31) Upendo kwa Mungu na jirani utatuwezesha tushinde hisia hasi na kupata shangwe ya kweli katika huduma. Tunapong’amua kwamba tunasaidia watu wanaosemwa kuwa “wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji,” hatujihangaikii sisi wenyewe kupita kiasi.—Mt. 9:35, 36.
JINSI YA KUSHIRIKI KATIKA FEBRUARI
5 Wakati wa mwezi Februari, tuna fursa nzuri ya kuonyesha Yehova na jirani upendo wetu kwa kutoa vichapo vya zamani vya Sosaiti kwa nusu ya mchango wa kawaida. Vichapo hivi vya zamani vinaonyesha habari mbalimbali, nyingine zazo bila shaka zitavutia watu mbalimbali katika eneo letu. Tayari vichapo hivyo vimethibitisha ubora wavyo kwa kuwasaidia watu wengi waitikie habari njema. Kwa hiyo ikiwa tuna vyovyote vya vitabu hivi vinavyobaki akibani, tunatiwa moyo tujitahidi kwa umoja ili tuvitie mikononi mwa watu wanaopendezwa wanaoweza kusaidiwa waje kwenye njia ya uhai.
6 Makundi ambayo hayana vitabu vya zamani akibani yatatoa kitabu chochote chenye kurasa 192. Jitihada ya kipekee inapaswa ifanywe ili kutumia vitabu vyote vya zamani ambavyo vimo akibani kundini.
7 Hakikisheni kwamba mnatunza maandishi mazuri ya nyumba kwa nyumba. Tunapoeneza eneo letu mara nyingi zaidi, jambo hili linahitajiwa zaidi. Upendezi unapopatikana, jaribu kuuliza jina la mtu huyo. Andika vyote vilivyoangushwa na pia kupendezwa kulikoonyeshwa wakati toleo la fasihi halikukubaliwa. Andika lile mlilozungumzia, jambo lililoonekana kumpendeza mtu huyo, na wakati ambao huenda akapatikana nyumbani. Pia, tunza kwa uangalifu maandishi ya anwani za watu ambao hawakupatikana nyumbani. Kupanga mambo kitengenezo katika jambo hili kutachangia kuwa wenye matokeo zaidi katika huduma.
8 Kushika zile amri kubwa mbili ni jambo linalohitajiwa sana kwa Wakristo leo kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Na tujitahidi kuonyesha Mungu na jirani upendo wetu kwa kutangaza Ufalme wa Yehova katika kila fursa wakati wa mwezi Februari!