Uhai wa Milele—Mradi Wetu
1 Maelfu ya watu waliofundishwa na Yesu walishuhudia ishara alizofanya. Lo, walishangilia pendeleo lililoje! Katika pindi moja yeye aliketisha mkutano, akatoa shukrani, kisha akawalisha mkate na samaki wengi. Walikuwa wanaume 5,000 hivi, bila kuhesabu wanawake na watoto. Ingawa Yesu aliyafikiria mahitaji ya kimwili ya watu, alihangaikia kwanza mahitaji yao ya kiroho. Kwa sababu hiyo, siku iliyofuata aliambia mkutano: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele.”—Yoh. 6:27.
2 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunataka kufuata shauri la Yesu na kutendea kazi manufaa za kiroho za milele. Hii inamaanisha kuweka vitu vya kimwili mahali pavyo na mradi wetu wa kwanza uwe kufanya penzi la Mungu. Basi, tunamwiga Yesu na kufanya kila jitihada ya maana kushiriki ukweli pamoja na wengine na kuwasaidia wathamini mambo ya kiroho, wakiwa na mradi wa uhai wa milele.
UTENDAJI KATIKA AGOSTI
3 Wakati wa Agosti, tutaendelea kutoa broshua zenye ukubwa wa gazeti Furahia Maisha Milele Duniani!, “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya,” Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, au Serikali Itakayoleta Paradiso.
4 Ni jambo jema kuwa na baadhi ya vichapo hivi vizuri. Hii inatuwezesha tuwe wenye kubadilikana, tujirekebishe kulingana na mapendezi ya mwenye nyumba, na kutoa broshua inayoonekana kufaa zaidi. Madokezo yenye msaada juu ya kutoa broshua yalitolewa katika “Kutangaza Habari Njema” katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Agosti 1988.
5 Ikiwa mwenye nyumba hachukui fasihi yoyote, tunaweza kumwachia trakti au handibili ili kuchochea kupendezwa kwa mtu huyu katika mambo ya kiroho. Au tunaweza kuliona kuwa jambo linalofaa kuzusha swali la Biblia na kudokeza mwenye nyumba alifikirie ili lizungumzwe baadaye tutakapozuru tena. Unaweza kuchagua maswali kama vile “Je! binadamu waliumbwa waishi kwa miaka michache tu kisha wafe?” (Reasoning ukurasa 245 au Vichwa vya Mazungumzo 51B) “Je! kuna ushuhuda wowote kuhusu umbo la mwili wa binadamu unaoonyesha kwamba mwili ulikusudiwa uishi milele?” (Reasoning ukurasa 247, au Kuishi Milele ukurasa 7.)
6 Ili tuwe wenye matokeo katika kushiriki habari njema na wengine, tunahitaji kujitayarisha vizuri. Hii inahitaji kujitayarisha mapema. Je! tumezoelea sana Kichwa cha Mazungumzo, na tuna mambo hususa ya kutaja kutoka fasihi? Kwa kufanya usomaji wetu wa Biblia kila juma na kuzungumza andiko kila siku, hali yetu ya kiroho itakua, nasi tutakuwa na mambo mengi mazuri ya kuzungumza katika huduma yetu.—Linganisha Yeremia 20:9.
7 Wakati wa Agosti, huenda ukawa na fursa ya kufanya kazi pamoja na wahubiri tofauti tofauti. Hii inaweza kukufanya ufahamiane na wengi na kufanya urafiki na wengine. Kutakuwezesha pia uone jinsi wengine wanavyotoa habari njema, jambo ambalo huenda ukakosa ikiwa unafanya kazi na mtu yule yule. Ndiyo, mradi wetu ni utumishi wa uaminifu kwa Yehova tukifikiria uhai wa milele. Na tuonyeshe uthamini kwa mambo ya kiroho kwa utendaji wetu tunapowachochea wengine kwenye upendo na kazi nzuri.—Ebr. 10:24.