Matangulizi Yenye Matokeo
1 Tunaposhiriki kwenye kazi ya nyumba kwa nyumba, daima tunaelekewa na swali hili, “Mwanzoni nitasema nini?” Wahubiri wenye ujuzi wanaopata matokeo mazuri katika utumishi wa shambani wanatoa madokezo kadhaa yenye kusaidia. Baadhi yayo ni gani?
2 Kwanza, ni jambo la maana kupendezwa kwa moyo mweupe na watu tunaosema nao. Kupendezwa huko kwa kibinafsi kunaonyeshwa kwa maneno na vitendo. Ni jambo la maana kufikiria maoni ya mwenye nyumba. Uliza maswali yanayofaa na kisha usikilize kwa uangalifu jibu lake. Kwa vyovyote vile, ni lazima tujaribu kumsaidia mwenye nyumba aone jinsi anavyoweza kufaidika kibinafsi kwa kufikiria habari tunayozungumza.
YAFIKIRIE MAONI YAO
3 Yesu alipokuwa akitolea ushahidi mwanamke Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na Sikari, nyingine za semi zake zilisikika kuwa ngeni kwake. Hazikupatana na kufikiri kwake wala na njia ambayo yeye aliabudu. Kwa uangalifu, Yesu alisikiliza, na mwanamke huyo alipokuwa akijibu, Yesu alifikiria yale aliyosema. Yeye alitaka kumsaidia mwanamke huyo. (Yohana 4:13, 14, 19-26) Je! sisi tunajitahidi kufuata kielelezo cha Yesu katika jambo hilo tunaposhiriki katika kazi ya kutoa ushahidi?
4 Ikiwa watu katika eneo lenu wanaitikia maneno yako ya utangulizi kwa kusema, “Mimi nina dini yangu mwenyewe,” ungeweza kufanya nini? Mwandikaji wa Biblia alisema: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.” (Mit. 15:28) Je! wewe hufanya hivyo? Je! umepata kufikiria habari kwenye kurasa 18-19 za kitabu Reasoning ukiwa unakumbuka kanuni ya andiko hilo? Pia waweza kufanya kazi na wahubiri wenye matokeo katika utumishi wa shambani kusudi ujifunze jinsi ya kufanya matangulizi yako yawe yenye matokeo zaidi.
5 Katika maeneo ambayo watu wengi hutumia kipingamizi cha kwamba wana dini yao wenyewe, huenda ukaona inafaidi kutazamia maelezo yao na kutokeza jambo hilo kwanza. Kwa kielelezo, baada ya salamu ya kwanza, huenda ukasema: “Je! una dini yako mwenyewe [Sikiliza jibu lao.] Nilijua unayo kwa sababu wengi katika eneo hili wanayo. Hata hivyo, sababu ya ziara yangu asubuhi hii ni . . . ” Halafu endelea na habari unayotaka kuzungumza.
6 Kama wenye nyumba wengi wanasema, “Nina shughuli nyingi,” ungeweza kuchagua wazo moja au mawili yanayosemwa kwenye kurasa 19-20 za kitabu Reasoning na kuyarekebisha kulingana na mahitaji ya eneo lako. Namna namna za semi hizo zaweza kutumiwa katika kutazamia vipingamizi vinavyosikiwa mara nyingi.
KUTUMIA MATANGULIZI KUTOKA KITABU REASONING
7 Wengi wanafaulu sana katika kutumia matangulizi kwenye kurasa 9-15 za kitabu Reasoning. Utaona kwamba zinahusu habari ambazo kwa ujumla watu huhangaikia, kama vile matukio ya karibuni, usalama wa kibinafsi, kazi ya kuajiriwa, makao, maisha ya jamaa, na wakati ujao. Hata hivyo, ona pia kwamba mpangilio wa maneno ya matangulizi yaliyodokezwa katika kitabu Reasoning unamwalika mwenye nyumba atoe maoni yake. Unamsaidia aone umaana wa habari inayotolewa na kwamba inamhusu yeye binafsi. Matumizi yenye matokeo ya matangulizi hayo yaweza kuzuia wenye nyumba wasitumie baadhi ya vipingamizi vilivyo vya kawaida zaidi.
8 Fikiria kwa uangalifu matangulizi unayosadiki yatakuwa yenye matokeo zaidi katika eneo lenu. Jifunze kutumia matangulizi katika kitabu Reasoning. Nufaika na ujuzi wa wahubiri wengine. Sali kwa ajili ya baraka ya Yehova juu ya jitihada zako. Kwa jitihada kubwa na baraka ya Yehova, huenda ikawa kwamba watu wengi zaidi katika eneo lenu wataitikia vizuri habari njema za wokovu.