Kutoa Habari Njema—Kwa Kitabu Upeo wa Ufunuo
1 Wana wa Kora waliandika hivi juu ya Yehova: “Kwa kuwa Mungu huyu ni Mungu wetu kwa wakati usio dhahiri, hata milele. Yeye mwenyewe atatuongoza mpaka tufapo.” (Zab. 48:14, NW) Wanaume hao waaminifu waliweka tumaini lao kwa uhakika katika Yehova, wakaishi maisha yao yote kwa kulingana na maagizo ya kimungu. Ni vielelezo vizuri kama nini walivyotuwekea! Wale wanaoongozwa na Yehova leo wanapata burudiko na nuru ya elimu. (Isa. 58:11) Wanaepuka msiba wa wale wanaofuata “viongozi vipofu” wa mfumo huu mwovu, wanaoongoza wafuasi wao ndani ya “shimo” la huzuni kuu na mvurugo.—Mt. 15:14.
2 Hasa mwelekezo wa kimungu ni wa maana leo ulimwengu unaotuzunguka uzidipo kuwa wenye mvurugo na hatari. Watu wengi wanatatizwa nao wanatamani jawabu lenye kuridhisha. Basi, ni jambo lenye kufaa kama nini, kwamba twawatia moyo wasome kitabu Upeo wa Ufunuo! Kichapo hiki hutoa mwongozo wa kimungu kwa kueleza matukio yenye kutikisa dunia ya siku zetu kwa msaada wa unabii wa Ufunuo. Habari hiyo inaleta kitulizo na hutoa mwelekezo timamu juu ya jinsi watu leo wanavyoweza kuishi maisha yenye kumpendeza Mungu.
KUONYESHA KITABU UPEO WA UFUNUO
3 Jambo lenye kutokeza la kitabu Upeo wa Ufunuo ni vielezi vyacho, ambavyo ni misaada mikubwa katika kufundisha. Tumia vielezi hivyo kwa mafanikio unapotoa kitabu hicho katika utumishi wa shambani. Kwa mfano, kwenye ukurasa 302 kuna kielezi chenye kuonyesha waziwazi baraka za Ufalme. Hilo ni wazo la mchoraji picha la yale ambayo yamenenwa kwenye 2 Petro 3:13 na Ufunuo 21:4, maandiko mawili ya Kichwa cha Mazungumzo chetu.
4 Baada ya kujijulisha, tungeweza kuanza mazungumzo yetu kwa njia hii: “Tunawatembelea kuzungumza maana ya yale yanayotukia kutuzunguka katika ulimwengu leo. Baadhi ya viongozi wa ulimwengu wanahisi kwamba tuko karibu sana na enzi mpya ya amani. Je! wewe unahisi ndivyo ilivyo? [Ruhusu mwenye nyumba ajibu.] Ingawa huenda serikali zikaonekana kuwa zinatatua baadhi ya tofauti za kisiasa, mielekeo ya watu kuelekea mmoja na mwenzake na visa vya jeuri huonekana mara nyingi sana zikizuia jitihada za wanadamu za kuleta amani. Hata hivyo, kwenye 2 Petro 3:13 Biblia hutupa hakikisho juu ya jamii mpya ya kidunia ambayo itatenda ikiwa chini ya serikali ya kimbingu. [Soma andiko hilo na kufungua kitabu kwenye ukurasa 302.] Huu ni wonyesho wa mchoraji picha wa yale ambayo andiko hilo husema juu ya habari hiyo. Ni jambo gani linalokuvutia katika picha hii? [Ruhusu jibu.] Kuhusu hali zitakazokuwako duniani, Biblia husema pia kwenye Ufunuo 21:4 [soma andiko kutoka ukurasa 303, fungu la 6]. Hata kifo hakitaharibu amani ambayo Mungu atasimamisha.” Huenda ukapata matangulizi tofauti tofauti yanayofaa eneo lenu kwenye kurasa 9-15 za kitabu Kutoa Sababu.
5 Ijapokuwa twataka kuonyesha baraka za Ufalme katika kutoa habari njema, tunahitaji pia kusaidia watu wenye kupendezwa wathamini uharaka wa ujumbe ambao Yesu Kristo alijulisha wazi katika kitabu cha Ufunuo. Kwa hiyo, tungetaka kumalizia mazungumzo kwa sihi yenye uharaka na kujitolea tusaidie watu wenye mioyo myeupe wathamini kwamba hukumu dhidi ya mfumo huu na wale ambao huuunga mkono itakuja karibuni.
6 Unabii mbalimbali katika Ufunuo ni chanzo kikuu cha burudisho na shangwe. Yehova anatoa mwaliko kwa wote wenye mioyo minyoofu wafuate uongozi wake na kujinufaisha wenyewe. Acheni tutoe kitabu Upeo wa Ufunuo kwa bidii ili wote waweze kuongozwa na mwelekezo wa hekima wa Yehova.