Kuvuna kwa Kulingana na Kadiri ya Jitihada Yetu ya Binafsi
1 Yehova Mungu ameonyesha upendo wake kwa aina ya kibinadamu kwa njia nyingi. Yesu alikazia upendo wa Mungu usiolinganika, akitaja kwa umati uliokusanyika kwamba Mungu “huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mt. 5:43-48) Katika pindi nyingine, Yesu alitambulisha wonyesho wa upendo wa Baba yake wenye kutokeza kupita mwingine wowote—dhabihu ya Mwana wake mzaliwa-pekee, ambaye Mungu alimtoa kwa ajili ya wokovu wetu. (Yn. 3:16) Yesu aliwaonya wasikilizaji wake kwa upole waitikie kwa uthamini upendo wa Yehova. Je! sisi tunajaribu kufanya hivyo?
2 Ili sisi tuweze kuonyesha uthamini kamili na kupata manufaa za milele kutokana na upendo wa Yehova, lazima tupate kumjua. (Yn. 17:3) Twahitaji shauri na mwelekezo kwa habari ya jinsi tuwezavyo kumtumikia kwa kukubalika. Yehova ameonyesha hangaikio lake lenye upendo kwa kutupatia Biblia, Neno lake lenye kupuliziwa lililoandikwa kwa uongozi wa roho, na kwa kusimamisha tengenezo lake zuri ajabu, ambalo kupitia kwalo twapokea shauri na maagizo. (Mt. 24:45-47; 2 Tim. 3:16, 17) Tukiwa watu wa Yehova walio wakfu, tumefundishwa katika njia zake. Lakini je! sisi tunaonyesha kwa jitihada zetu za binafsi kwamba twathamini upendo wa Yehova? Je! sisi tunatii shauri lake ili tumpendeze na hivyo tujinufaishe? (Isa. 48:17; Yak. 1:22) Mtume Paulo aliandika hivi kwenye 1 Wakorintho 3:8: “Basi yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe.”
3 Ndiyo, lazima tujitahidi kufanya yale ambayo Mungu atutaka tufanye. Si kila mtu hufanya maendeleo ya kiroho kwa mwendo ule ule. Kuna mambo mengi yanayohusika katika kufanya maendeleo kwetu, na lingekuwa jambo lisilo la hekima kufanya ulinganisho wenye kuvunja moyo. Hata hivyo, jambo muhimu sana ni jitihada za kila mtu mmoja mmoja tufanyazo. Twaweza kufanya nini ili tukaribie zaidi tengenezo? Je! kuna maeneo ambamo twaweza kufanya maendeleo kwa kukubali madaraka yetu ya binafsi tukiwa Wakristo? Ni jitihada gani itatakwa ili kuupa utendaji wa kundi utegemezo bora zaidi? Je! kuna mambo tunayohitaji kutumia kuhusu maagizo tunayopewa na tengenezo?—1 Tim. 4:16.
WAIGE WAAMINIFU
4 Habari njema za Ufalme zimehubiriwa kwa makumi ya miaka na ndugu na dada waaminifu. Waaminifu hao, kama Paulo, wanastahiki kuigwa. (1 Kor. 11:1) Wameitikia upendo wa Mungu nao wamevuna manufaa nyingi kwa sababu ya kazi yao ya bidii na jitihada zao binafsi za kufuata shauri la Biblia. Wanafanyiza kiini imara cha wafanyakazi wenye bidii katika kundi, bila kupuuza daraka lao binafsi. Twaweza kuona tunda la kujitaabisha kwao binafsi.—Rum. 1:13; 2 Kor. 3:1-3.
5 Sasa, makumi ya maelfu ya wapya wanamiminika kuingia ndani ya tengenezo kila mwaka. (Isa. 60:8) Wao pia wanachukua kwa uzito uhitaji wa kujitaabisha ili wawe watu wa kiroho wakomavu, na bidii yao katika kazi ya kuhubiri inastahiki kusifiwa. Wananufaishwa kwa kuona jinsi Yehova hubariki wale ambao hufanya kazi kwa bidii katika utumishi wake. Kielelezo cha ndugu na dada wakomavu husaidia wapya kuthamini kwamba huu sio wakati wa kulegeza mkono au kuacha utumishi wetu kwa Mungu. Tuwe wahubiri wapya au wenye ujuzi, je! sisi tunaendelea kukua kiroho, tukikubali madaraka yetu binafsi ya Kikristo na kujinufaisha na maandalizi yote ya kitheokrasi?
KUTUMIA TUNAYOJIFUNZA
6 Muda mrefu kabla Yakobo hajaandika kwamba yatupasa kuwa ‘watendaji wa kazi,’ Musa alisema hivi kwa Wayahudi: “Ni lazima nyinyi mtumie maneno haya.” (Yak. 1:25; Kum. 11:18, NW) Hivyo maarifa yenyewe hayakutosha. Wayahudi walihitaji kutumia maneno ya Sheria katika utii kwa Yehova. Kanuni hii ya msingi ingali iko ivyo hivyo. Hakika Yesu, Mwana wa Mungu, alijua umaana wa kutii. (Yn. 8:28) Alisema kwenye Mathayo 7:24: “Kila asikiaye maneno haya yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili.”
7 Je! sisi tunatumia yale tunayojifunza kwenye makusanyiko ya mzunguko? Je! sisi tunathamini kwa nini ni jambo muhimu sana wakati huu kukaa tukikesha na kubaki tukiwa na akili zetu? Je! sisi tunakuwa chonjo kuona mashambulio na mitego yenye hila anayotega Ibilisi? Je! sisi tunathamini shauri na maonyo tunayopewa na tengenezo kwa kurudiwa-rudiwa kuhusu uhitaji wa usafi wa kiadili na kiroho katika kundi? Ni kwa kadiri gani sisi watu mmoja mmoja tunatumia yale tusikiayo?—Yak. 1:23-25.
8 Programu itakayofuata ya siku ya kusanyiko la pekee inakazia uhitaji wetu wa kuwa watakatifu, kama Yehova alivyo mtakatifu. (1 Pet. 1:14-16) Utakatifu humaanisha usafi wa kidini au utakato, hali ya kuwa wakfu kwa Mungu. Huonyesha hali ya kutengwa kwa ajili ya utumishi wa Mungu. Sisi tumekabidhiwa huduma ya habari njema. Kwa sababu hiyo, lazima sisi tuwe safi kiroho, kiadili, na kimwili ili tustahili kuchukua lile Neno takatifu la kweli. Hilo lataka kwamba sisi tujiangalie zaidi ya ilivyo kawaida. (Ebr. 2:1) Tunapofanya hivyo, tutavuna baraka kwa kulingana na jitihada zetu binafsi.
NUFAISHWA NA FUNZO LA KIBINAFSI
9 Funzo la kibinafsi hutusaidia kujenga imani yenye nguvu, na kuongeza uthamini wetu kwa ajili ya kweli. Hutupa uhakika na kututayarisha kusema kwa mamlaka. Hutupatia ufahamu wa ndani na utambuzi na kutusaidia kuvaa ule utu mpya. (Kol. 1:9-11) Hata hivyo, funzo lenye matokeo huhitaji wakati na jitihada, na hakuna njia ya mkato ya kupata maarifa sahihi na kina cha kiroho. Tutavuna faida kutoka funzo kulingana na jitihada tunayotia katika funzo.—2 Kor. 9:6, 7; Gal. 6:7.
10 Je! sisi tunatenga wakati wa kutosha kila juma ili kutayarisha mikutano yetu ya kundi? Hiyo ni njia moja ambayo kwayo twaweza kuonyesha uthamini kwa ajili ya mlo wa kiroho anaoandaa Yehova kupitia mtumwa mwaminifu na mwenye akili. Utayarishaji ufaao wa mikutano hutusaidia kushikamana na ratiba ya kusoma na kujifunza Neno la Mungu. Je! sisi tunatenga wakati kila juma kwa ajili ya usomaji wetu wa Biblia kama ilivyoratibiwa katika programu kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Inataka dakika chache tu kila siku kusoma na kutafakari juu ya habari hiyo. Mkutano wa Utumishi husaidia kutuweka chonjo kuona njia ambazo katika hizo twaweza kufanya huduma yetu ya hadhara iwe yenye mafanikio. Je! sisi hutayarisha, tukifikiria kipekee jinsi tunavyoweza kutumia habari hiyo katika huduma? Na je! sisi hufanya jitihada kuitumia mara hiyo? Mipango mahususi yapasa kufanywa ili kutayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi na kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kundi. Je! tunafanya hivyo?
SHIRIKI MIKUTANONI
11 Twaweza kunufaishwa zaidi na mikutano tunapoishiriki. Kutayarishia mikutano na kisha kufanya jitihada kushiriki hutufanya tuwe wasikivu wakati wa mikutano na hufanya iwe rahisi zaidi kwetu kunufaishwa na maelezo ya wengine. Wengi wangali wakumbuka kazi yenye bidii waliyofanya ili watoe elezo lao la kwanza kwenye mkutano au hotuba yao ya kwanza ya wanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Ijapokuwa kadiri kubwa ya wasiwasi yapasa iwe imepungua, je! sisi huendelea kufanya bidii ili maendeleo yetu ya kiroho yadhihirike kwa wote? (1 Tim. 4:15) Wengine hunufaishwa na kutiwa moyo na maelezo yetu. Tukijitayarisha vizuri, tukiwa tumekwisha jifunza habari itakayozungumzwa mikutanoni, ushiriki wetu wenye kujaa maana katika mikutano utachochea wengine katika upendo na kazi njema.—Ebr. 10:23-25.
12 Maelezo yetu hayapasi kuwa marefu na yenye kutatiza. Kwa kawaida ni vizuri zaidi kutoa maelelzo mafupi ambayo hujibu moja kwa moja maswali yanayoulizwa au kusaidia kuonyesha waziwazi matumizi ya andiko fulani. Ikiwa tumetayarisha vizuri, tutaweza kutoa maelezo kwa maneno yetu wenyewe. Tunapofanya hivyo, manufaa kwetu sisi wenyewe na kwa wengine ni nyingi zaidi. Kwa nini? Kwa sababu inatutaka tufikiri juu ya yale tunayosema na kueleza jambo kama tunavyolielewa. Huenda hilo likafanya iwe rahisi zaidi kwa wengine kuelewa habari hiyo. Pia, itatusaidia kukumbuka habari hiyo ili kuitumia katika pindi nyingine.
PANDA KWA UKARIMU SHAMBANI
13 Huduma yetu ya Kikristo ni hazina ya utumishi. (2 Kor. 4:7) Je! wewe huiona hivyo? Kupitia kwa huduma, tuna pendeleo la kuwaeleza wengine imani yetu. Yesu alisema kwamba kinywa hunena yale yaujazayo moyo. (Luka 6:45) Jitihada ya kibinafsi tunayofanya ili kuwa na ushiriki kamili katika huduma huturuhusu tuvune manufaa nyingi. Uelewevu wetu wa kweli unanolewa, nasi twasitawisha uwezo mwingi zaidi wa kutumia Biblia. Tunapata shangwe ya kuletea wengine kweli na kuwasaidia wajifunze juu ya Muumba wao Mkuu. Twasimama tukiwa mashahidi kwa ufaaji wa utawala wa Mungu na enzi kuu yake. Tunafurahi kwa sababu twajua kwamba sisi tunampendeza Yehova, tukigeuzwa tuwe na mfano wake na kufanya mapenzi yake.—Mt. 5:48.
14 Ikiwa twaendelea kupima jitihada yetu ya binafsi, ibada yetu kwa Yehova haitapata kamwe kuwa utumishi wa vivi hivi tu. Hiyo yamaanisha nini? Yamaanisha kwamba hatutakuwa wenye moyo nusu-nusu katika kutii mapenzi ya Mungu, tukitoa tu kile kinachofanana na utumishi kwake au kiasi kilicho cha chini zaidi bila ujitoaji na jitihada halisi yenye kuhisiwa moyoni. Utumishi wetu kwa Yehova lazima uwe wa moyo wote. Tuna wajibu wa Kimaandiko wa kutoa vyote tulivyo navyo katika utumishi wake. (Kol. 3:23, 24) Ni kweli, hali hutofautiana, na Yehova hataki kutoka kwetu zaidi ya yale tuwezayo kufanya. Hata hivyo, yale tuwezayo kufanya, yeye hututarajia tuyafanye! (Mt. 22:37) Kwa kuwa asili ya kibinadamu yenye dhambi huelekea kutotaka kujitumikisha, inafaa tujichunguze wenyewe mara kwa mara na kuona maeneo ambamo twaweza kufanya maendeleo katika utumishi wetu kwa Mungu. Je! sisi tumezoea kufanya hivyo?
15 Ni lazima tutumie hadhari ikiwa tutaepuka kuruhusu mafuatio na tamaa za kibinafsi zituzuie kutoa kilicho bora zaidi katika utumishi wa Yehova. Anasa, utendaji wa kupisha wakati, na tafrija lazima ziwekwe mahali pazo. Pia, lazima tujitahadhari dhidi ya mwelekeo wa kujihusisha kupita kiasi katika utendaji wa vitu vya kimwili. Kwa kutii shauri la Yesu kwenye Mathayo 6:22, 23, bila shaka tutaweza kufanya jitihada zaidi katika kufuatia masilahi ya kiroho na kuvuna kulingana na jitihada hiyo.
16 Tuendeleapo kufanya kazi kwa bidii ili kuvaa utu mpya, tutakubali daraka letu wenyewe la kutumia shauri na madokezo ambayo twapokea kwenye mikutano ya kundi, makusanyiko, mikusanyiko, na kupitia vichapo. Kila mmoja wetu na ajifunze kwa bidii yenye kuendelea, ashiriki kwa bidii katika mikutano, na kushiriki katika kazi hii kubwa ya kufanya wanafunzi kwa kadiri hali zetu binafsi zitaturuhusu. Kwa kuitikia hivyo kwa kuthamini upendo wa Mungu, twaweza kuwa na hakika ya kuvuna kwa wingi thawabu za kiroho sasa na kudumisha tumaini imara la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova.