Yatumie Magazeti Kuishiriki Kweli
1 Thamani ya habari za kweli na zilizo hakika hushushwa sana katika jamii ya watu wa leo kwa sababu ya utangazaji uliotiwa chumvi, ahadi za kisiasa zenye kupotosha, na madai ya udanganyifu kati ya mataifa. Mnara wa Mlinzi na Amkeni! hayana kifani kwa sababu ni hayo tu yatangazayo kweli juu ya Ufalme wa Mungu na kueleza mambo ambayo lazima watu wote wafanye ili kufurahia baraka za milele utakazozileta.
2 Katika nchi moja ofisa wa wizara ya habari aliyethamini ubora wa magazeti mawili haya alisaidia kwa hiari ili yapate kibali cha kugawanywa. Alitaarifu hivi: “Mimi naona Mnara wa Mlinzi kuwa moja la magazeti yaliyo bora zaidi; nafurahia sana kusaidia.” Ni pendeleo letu kusaidia wengine kwa kugawanya majarida haya yawezayo kutoa ujuzi wenye kupa uhai. (Yn. 17:3) Wewe utatoaje magazeti haya yenye thamani wakati wa Mei? Labda madokezo yafuatayo yatasaidia.
3 Ikiwa unakazia makala ya “Mnara wa Mlinzi,” la Aprili 15, ungeweza kusema hivi:
◼ “Tunaongea na watu juu ya kitabu kiuzwacho kwa wingi zaidi ulimwenguni. Je! wajua kitabu hicho? [Ruhusu jibu.] Tunaongea juu ya Biblia. Ni lazima kuwe na sababu nzuri sana ambayo imefanya watu wengi hivyo wainunue Biblia. Sababu yapatikana kwenye 2 Timotheo 3:16.” Baada ya kusoma andiko hilo, kazia mambo yafaayo kutoka kurasa 6, 7 za makala “Waweza Kupata Wapi Mwongozo Wenye Kutumainika?” Halafu toa andikisho. Toleo la kawaida lisipokubaliwa waweza kutoa yale magazeti mawili na broshua kwa mchango wa kawaida.
4 Au baada ya utangulizi mfupi, ungeweza kusema jambo kama hili ukikazia makala ya Aprili 1:
◼ “Je! wafikiri itawezekana wakati fulani watu waishi katika hali zile zilizoonyeshwa katika ukurasa wa 7 wa toleo hili la Mnara wa Mlinzi?” (Ruhusu mwenye nyumba ajibu.) Halafu vuta fikira na usome kwenye habari zilizo chini ya picha na uzungumze maandiko yaliyo katika fungu la 1 katika ukurasa wa 7. Kazia thamani ya magazeti kuwa yakija nyumbani kwa ukawaida wakati ufanyapo toleo la andikisho.
5 Katika maandishi yako ya ziara za kurudia, yaelekea una orodha ya wale walioonyesha upendezi fulani hapo kwanza, lakini hakukuwa na matokeo. Kwa kuwa itikio lilikuwa dogo tu, huenda ikawa wewe huhisi uhitaji wa kurudirudi. Lakini huenda ukaweza kutumia orodha hiyo ili kukuza kawaida ya kupelekea watu hao magazeti. Ukiona makala ambayo wahisi ingeweza kuvutia mtu fulani hususa, hakikisha kuzuru mtu huyo na kumtolea gazeti hilo.
6 Kutoa Ushahidi wa Kivivihivi: Hii ni njia nzuri kabisa ya kusababisha mtu apendezwe na magazeti. Kuweka kwa busara majalada ya magazeti yenye kuvuta macho yakionekana wazi huenda kukatosha ili kuanzisha mazungumzo. Dada mmoja aliweka matoleo fulani juu ya dawati lake hivi kwamba wafanyakazi wenzake wangeweza kuyaona walipopita; aliweza kuangusha kadhaa. Hakikisha unaenda na nakala chache, na uchukue hatua ya kwanza kuyatoa mwezi huu uendapo dukani, shuleni, usafiripo kwa basi, au ukutanapo na wengine kwingineko.
7 Kwa msaada wa Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, sisi tumepata majibu kwa maswali muhimu juu ya Yehova na ibada yake. Twataka kutumia majarida haya kwa kila njia iwezekanayo ili kusaidia wengine wapate kumjua Yehova “Mungu wa kweli.”—Zab. 31:5.