Mnara wa Mlinzi na Amkeni!—Majarida ya Wakati Ufaao Yenye Kweli
“Umenikomboa, Ee BWANA [Yehova, NW], Mungu wa kweli.”—ZABURI 31:5.
1, 2. (a) Dada mmoja alihisije juu ya jambo fulani alilosoma katika Mnara wa Mlinzi? (b) Ni maswali gani yanayoulizwa juu ya majarida yetu?
“ASANTENI sana,” akaandika dada mmoja Mkristo, “kwa ajili ya habari ya ajabu katika makala ya Mnara wa Mlinzi ‘Wewe Waweza Kupata Faraja Katika Nyakati za Taabu.’a Habari nyingi sana mlizoeleza zilikuwa hasa hisia ambazo nimelazimika kushughulika nazo; ni kana kwamba makala hiyo iliandikwa kwangu moja kwa moja. Mara ya kwanza nilipoisoma, nilikuwa na machozi machoni pangu. Lilikuwa jambo la ajabu kung’amua kwamba kuna mtu mwingine ajuaye nihisivyo! Nashukuru sana kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ni wapi kwingineko tuwezako kupata ahadi za uhai wa milele katika Paradiso kwa wakati ujao ulio karibu na, kwa sasa, faraja kwa ajili ya nafsi zetu! Asanteni. Asanteni sana sana.”
2 Je! umepata kuhisi hivyo? Je! imepata kuonekana kama jambo fulani katika Mnara wa Mlinzi au jarida-jenzilo, Amkeni!, liliandikwa kwa ajili yako hasa? Ni mambo gani kuhusu magazeti yetu yanayovutia mioyo ya watu? Twaweza kusaidiaje wengine wanufaike na ule ujumbe wenye kuokoa uhai yaliyo nao?—1 Timotheo 4:16.
Magazeti Yateteayo Kweli
3. Ni kwa sababu gani nzuri magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yameathiri mioyo ya wasomaji wengi?
3 Yehova ni “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Neno lake, Biblia, ni kitabu cha kweli. (Yohana 17:17) Watu wenye mioyo yenye kufuatia haki huitikia kweli. (Linganisha Yohana 4:23, 24.) Sababu moja inayofanya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yaathiri mioyo ya mamilioni ya wasomaji ni kwamba hayo ni majarida yenye uaminifu-maadili na kweli. Kwa kweli, Mnara wa Mlinzi lilianza kuchapishwa kwa sababu ya suala la uaminifu-mshikamanifu dhidi ya kweli ya Biblia.
4, 5. (a) Ni hali zipi zilizomwongoza C. T. Russell atangaze Mnara wa Mlinzi? (b) Jarida Mnara wa Mlinzi hutumiwaje na “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?
4 Katika 1876, Charles T. Russell aliungana na Nelson H. Barbour, wa Rochester, New York. Russell aliandaa fedha ili kuanzisha upya uchapishaji wa gazeti la kidini la kawaida la Barbour Herald of the Morning, Barbour akiwa mhariri mkuu na Russell akiwa mhariri-msaidizi. Hata hivyo, karibu mwaka mmoja na nusu baadaye, katika toleo la Herald la Agosti 1878, Barbour aliandika makala iliyokanusha thamani ya ukombozi ya kifo cha Kristo. Katika toleo lifuatalo tu, Russell, aliyekuwa karibu miaka 30 mchanga zaidi ya Barbour, aliitikia kwa makala iliyounga mkono fidia, ambayo alirejezea kuwa “mojayapo mafundisho ya maana zaidi ya Neno la Mungu.” (Mathayo 20:28) Baada ya juhudi za mara kwa mara za kusababu na Barbour Kimaandiko, Russell aliamua hatimaye kukatiza mahusiano yote na Herald. Kuanzia na toleo la Juni 1879 la jarida hilo, jina la Russell halikutokea tena akiwa mhariri-msaidizi. Mwezi mmoja baadaye, Russell mwenye umri wa miaka 27 alianza kutangaza Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence (sasa likiitwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova), ambalo tangu mwanzo limeunga mkono kweli ya Kimaandiko, kama vile fidia.
5 Kwa miaka 114 iliyopita, Mnara wa Mlinzi, kama vile wakili stadi, limejithibitisha lenyewe kuwa mteteaji wa kweli na mafundisho ya Biblia. Katika kufanya hivyo, limejishindia uhakika wa mamilioni ya wasomaji wenye uthamini. Bado latetea fidia kwa nguvu. (Kwa kielelezo, ona toleo la Februari 15, 1991.) Na laendelea likiwa chombo kikubwa cha “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na Baraza Linaloongoza lake cha kutangazia kuanzishwa kwa Ufalme wa Yehova na kugawanya chakula cha kiroho “kwa wakati wake.”—Mathayo 24:14, 45.
6, 7. Ni nini lililosemwa kuwa kusudi la The Golden Age, na nini kionyeshacho kwamba watu wenye kufikiri waliitikia ujumbe walo?
6 Namna gani gazeti Amkeni!? Tangu mwanzo walo, Amkeni! pia limetetea kweli. Likiitwa The Golden Age hapo awali, gazeti hilo lilikusudiwa kugawiwa umma. Kuhusu kusudi lalo, toleo la kwanza la tarehe, Oktoba 1, 1919, lilisema hivi: “Kusudi lalo ni kueleza kwa maoni ya hekima ya Kimungu maana ya kweli ya matukio makubwa ya siku ya leo na kuthibitishia akili zenye kufikiri kwa ithibati isiyokanika na yenye kusadikisha kwamba wakati wa baraka kubwa zaidi kwa ainabinadamu uko karibu sasa.” Watu wenye kufikiri waliitikia ujumbe wa The Golden Age. Kwa miaka kadhaa, mwenezo walo hata ulikuwa mkubwa zaidi ya ule wa Mnara wa Mlinzi.b
7 Hata hivyo, uvutio wa Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, si kwa sababu tu hayo huchapisha mafundisho ya kweli na kueleza umaana wa kiunabii wa hali za ulimwengu. Hasa katika mwongo mmoja au miwili iliyopita, magazeti yetu yameinasa mioyo ya watu kwa sababu nyinginezo pia.
Makala za Wakati Ufaao Zinazoathiri Maisha za Watu
8. Yuda alifanya badiliko jipi katika habari ya kuandikwa, akiwahimiza wasomaji wake wakinze mivutano gani iliyo ndani ya kutaniko?
8 Karibu miaka 30 baada ya kifo na ufufuo wa Yesu Kristo, mwandikaji wa Biblia Yuda alikabili hali ngumu. Watu wasio na adili, walio kama wanyama walikuwa wamepenya ndani miongoni mwa Wakristo. Yuda alikuwa amekusudia kuwaandikia Wakristo wenzake juu ya habari ya kimafundisho—wokovu ambao Wakristo wapakwa hushiriki. Badala ya hivyo, akielekezwa na roho takatifu, aliona ni lazima awahimize wasomaji wake wakinze mivutano yenye kufisidi iliyo ndani ya kutaniko. (Yuda 3, 4, 19-23) Yuda alibadili habari kulingana na hali akaandaa shauri la wakati ufaao uliotimiza mahitaji ya ndugu zake Wakristo.
9. Ni nini kihusikacho katika kuandaa makala ya wakati ufaao kwa ajili ya majarida yetu?
9 Vivyo hivyo, kutayarisha makala za wakati ufaao kwa ajili ya majarida yetu ni daraka gumu. Nyakati hubadilika, na ndivyo na watu—mahitaji yao na mapendezi yao si jinsi yalivyokuwa hata mwongo mmoja au miwili iliyopita. Mwangalizi mmoja asafiriye alionelea hivi karibuni: “Nilipokuwa Shahidi huko nyuma katika miaka ya 1950, njia tuliyojifunza Biblia pamoja na wengine ilikuwa ya kimafundisho hasa—tukiwafundisha kweli juu ya Utatu, moto wa helo, nafsi, na kadhalika. Lakini sasa, yaonekana, kuna matatizo na magumu mengi sana katika maisha za watu hivi kwamba ni lazima tuwafundishe jinsi ya kuishi.” Kwa nini ni hivyo?
10. Kwa nini isitushangaze kwamba kumekuwa mzoroto wenye kuendelea kwa uthabiti katika shughuli za kibinadamu tangu 1914?
10 Kuhusu “siku za mwisho,” Biblia ilitabiri hivi: “Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.” (2 Timotheo 3:1, 13) Kwa hiyo, isitushangaze kwamba kumekuwa mzoroto wenye kuendelea kwa uthabiti katika shughuli za kibinadamu tangu wakati wa mwisho ulipoanza katika 1914. Shetani, ambaye wakati wake unaobaki ni mfupi zaidi ya wakati wowote, anatoa hasira yake juu ya jamii ya kibinadamu kuliko wakati mwingine wowote. (Ufunuo 12:9, 12) Likiwa tokeo, kanuni za kiadili na za familia ni tofauti sana na jinsi zilivyokuwa miaka 30 au 40 tu iliyopita. Watu kwa ujumla hawana mwelekeo wa kidini kama walivyokuwa nao katika miongo iliyopita. Uhalifu umeenea sana hivi kwamba watu wanajitahadhari kwa njia ambazo hazikujulikana miaka 20 au 30 tu iliyopita.—Mathayo 24:12.
11. (a) Ni habari za aina gani zilizomo akilini mwa watu, na jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili imeitikiaje mahitaji? (b) Toa kielelezo cha makala ya Mnara wa Mlinzi au ya Amkeni! ambayo imeathiri maisha yako.
11 Basi, si ajabu kwamba masuala ya kihisiamoyo, ya kijamii, na ya familia yamo akilini mwa watu wengi. Mtumwa mwaminifu mwenye akili ameitikia kwa moyo mkuu katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa kuchapisha makala za wakati ufaao ambazo zimeshughulikia mahitaji halisi ya watu na ambazo kwa kweli zimeathiri maisha zao. Fikiria vielelezo kadhaa.
12. (a) Kwa nini makala juu ya familia zenye mzazi mmoja zilitayarishwa kwa ajili ya Mnara wa Mlinzi katika 1981? (b) Dada mmoja alielezaje uthamini wake kwa ajili ya makala juu ya familia zenye mzazi mmoja?
12 Masuala ya Familia. Wakati ripoti za ulimwenguni pote zilipoonyesha ongezeko la haraka katika idadi ya familia zenye mzazi mmoja, makala zisizo na kifani juu ya kichwa “Jamaa Zenye Mzazi Mmoja—Zinashindana na Matatizo” zilitayarishwa kwa ajili ya toleo la Machi 1, 1981, la Mnara wa Mlinzi. Makala hizo zilikuwa na kusudi lenye sehemu mbili: (1) kusaidia wazazi wasio na wenzi wakabiliane na matatizo ya pekee wanaokabili na (2) kusaidia wengine waarifiwe vizuri zaidi ili waweze kuonyesha “hisia-mwenzi” na ‘kutunza’ kikweli familia zenye mzazi mmoja. (1 Petro 3:8; Yakobo 1:27, NW) Wasomaji wengi waliandika ili kueleza uthamini wao kwa ajili ya makala hizo. “Nilipoona jalada hilo kwa kweli lilileta machozi machoni pangu,” akaandika mzazi mmoja asiye na mwenzi, “na nilipofungua gazeti na kusoma habari, moyo wangu ulifurika kwa shukrani kuelekea Yehova kwa ajili ya kuandaa habari ya jinsi hiyo kwa wakati uliohitajiwa.”
13. Ni habari gani juu ya mshuko wa moyo iliyochapishwa katika Amkeni! mwaka wa 1981, na msomaji mmoja alikuwa na nini lakusema juu yayo?
13 Masuala ya kihisiamoyo. Habari juu ya mshuko wa moyo imezungumziwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! tangu miaka ya 1960. (1 Wathesalonike 5:14) Lakini kulikuwa na mtazamo mpya na ufaao juu ya habari hiyo katika mifululizo ya makala juu ya kichwa cha jalada “Waweza Kupiga Vita Dhidi ya Mshuko wa Moyo!” katika toleo la Amkeni! la Septemba 8, 1981 (Kiingereza). Upesi barua za kueleza uthamini zilitiririka kwenye Watch Tower Society kutoka sehemu zote za ulimwengu. “Naweza kuelezaje kwenye karatasi hisia zilizomo moyoni mwangu?” akaandika dada mmoja. “Nina umri wa miaka 24, na katika muda wa miaka kumi iliyopita, nimekuwa na vipindi vingi vya mshuko wa moyo. Lakini sasa nahisi nikiwa karibu zaidi na Yehova na nashukuru kwamba aliitikia mahitaji ya watu walioshuka moyo kwa makala hizo zenye upendo, na nilitaka kuwaambia hivyo.”
14, 15. (a) Habari juu ya kutendwa vibaya kwa watoto imeshughulikiwaje katika majarida yetu? (b) Ni makala zipi za magazeti zilizomvutia mpanda-farasi mmoja wa mashindano katika Australia?
14 Masuala ya kijamii. Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho” watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio wapenda wa kwao, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema.” (2 Timotheo 3:1-3) Kwa hiyo, haipasi itushangaze kwamba kutendwa vibaya kwa watoto kunazoewa na wengi leo. Habari hiyo ilishughulikiwa waziwazi katika makala “Msaada kwa Wenye Kutendwa Ugoni wa Maharimu” katika Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1983 (Kiingereza). Miaka minane baadaye, mifululizo ya makala juu ya kichwa cha jalada “Kuponya Majeraha ya Kutendwa Vibaya kwa Watoto” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 8, 1991, (Kiingereza) ilitayarishwa kwa uangalifu ili kuandaa uelewevu na tumaini kwa wale waliotendwa vibaya na pia kuelimisha wengine ili waweze kutoa msaada wenye kusaidia. Mifululizo hiyo ya makala ilivutia itikio kubwa zaidi kutoka kwa wasomaji katika historia ya majarida yetu. Msomaji mmoja aliandika hivi: “Jambo ambalo limeathiri zaidi kupona kwangu ni yale mawazo ya kufariji na marejezeo ya Kimaandiko katika makala hizo. Kujua kwamba Yehova hakuniona kuwa mwenye umaana mdogo zaidi kulinipa kitulizo kikubwa sana. Kujua kwamba sikuwa peke yangu kulinifariji vilevile.”
15 Mpanda-farasi mmoja wa mashindano katika Melbourne, Australia, alipiga simu ya mbali kwenye ofisi ya Watch Tower Society ya Sydney, akieleza jinsi alivyochukia mazingira ya mashindano ya farasi. Alisema kwamba alikuwa ametoka tu kusoma Amkeni! la Machi 8 juu ya “Kunajisiwa—Hofu Kuu ya Wanawake” na hakuweza kuamini hata kidogo kwamba gazeti lenye thamani jinsi hiyo lilikuwako. Aliuliza maswali kwa muda wa dakika 30 na alifurahi kusikia majibu yaliyotolewa.
16. Waweza kuonyesha uthamini wako kwa ajili ya majarida yetu katika njia zipi?
16 Namna gani wewe? Je! maisha yako yameathiriwa na makala hususa iliyochapishwa katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni!? Ikiwa ndivyo, bila shaka washukuru sana kwa ajili ya majarida yetu. Waweza kuonyeshaje uthamini wako? Kwa hakika ni kwa kusoma kila toleo wewe mwenyewe. Pia waweza kushiriki katika kuyagawa majarida hayo kwa kadiri kubwa iwezekanavyo. Hilo laweza kufanywaje?
Yashiriki Pamoja na Wengine!
17. Makutaniko yaweza kufanya nini ili kuongeza ugawaji wa magazeti?
17 Kwanza, kuna jambo fulani ambalo kila kutaniko laweza kufanya. Toleo la Oktoba 1952 la Informant (sasa Huduma ya Ufalme Yetu) lilisema hivi: “Njia yenye matokeo zaidi ya kugawa magazeti ni nyumba kwa nyumba na duka kwa duka. Kwa hiyo Sosaiti yapendekeza kwamba sehemu hizo za ugawaji wa magazeti ziwe sehemu ya kawaida ya utendaji wa Siku ya Magazeti.” Shauri hilo bado lafaa leo. Makutaniko yaweza kuratibu Siku ya Magazeti ya kawaida, siku iliyowekwa kando kwa sababu hasa ya kutoa ushahidi wa magazeti. Kwa makutaniko yaliyo mengi, Jumamosi hususa bila shaka zitakuwa wakati mzuri. Ndiyo, acha kila kutaniko liweke kando siku au jioni za pekee kwa ajili ya kutoa ushahidi wa magazeti—nyumba kwa nyumba, duka kwa duka, barabarani, na kwa watu wanaopelekewa magazeti kikawaida. Kwa kuongezea, wewe uliye mhubiri wa Ufalme, waweza kufanya nini kusaidia kuongeza ugawaji wa magazeti?
18, 19. (a) Kuwa mwenye utambuzi juu ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwaweza kukusaidiaje kuangusha magazeti? (b) Ni nini faida ya utoaji mfupi, unaolenga jambo kuu wakati wa kutoa magazeti? (c) Ni nini kionyeshacho thamani ya kuyaangusha magazeti nyumbani mwa watu?
18 Kuwa mwenye utambuzi juu ya “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!” ni hatua ya kwanza. Yasome magazeti kimbele. Usomapo kila makala jiulize, ‘Makala hii ingekuwa yenye kupendeza kwa nani?’ Fikiria maneno machache ambayo ungeweza kusema ili kuchochea kupendezwa katika makala hiyo. Zaidi ya kuunga mkono Siku ya Magazeti ya kawaida, kwa nini usichukue nakala ili uweze kutumia kwa faida kila fursa kuzishiriki na wengine—unaposafiri au kununua vitu na unapoongea na wafanyakazi wenzako, majirani, wanafunzi wenzako, au walimu?
19 Kufanya utoaji wako uwe sahili ni dokezo la pili. Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1956, (Kiingereza) lilisema hivi: “Utoaji mfupi unaolenga jambo kuu, wafaa zaidi wakati wa kutoa magazeti. Kusudi ni kuangusha nakala nyingi. Hizo ‘zitajisemea’ zenyewe.” Wahubiri wengine wamepata matokeo kwa kuchagua wazo moja kutoka makala moja, kulisema kwa maneno machache, na kuyatoa magazeti. Mara yakiwa ndani ya nyumba, magazeti yaweza ‘kusema’ na wengine zaidi ya yule mtu aliyeyakubali kutoka kwako. Katika Ailandi mwanafunzi mchanga wa chuo kikuu alisoma toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1991, ambalo baba yake alikuwa amekubali kutoka kwa Shahidi mmoja. Makala juu ya uwasiliano na habari nyinginezo ziliamsha kupendezwa kwake. Mara alipokuwa amelisoma gazeti hilo, aliwapigia Mashahidi simu, akitumia nambari iliyoorodheshwa katika kitabu cha nambari za simu. Funzo la Biblia lilianzishwa upesi, na mwanamke huyo mchanga alibatizwa kwenye “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya katika Julai 1993. Kwa hakika, acheni tuangushe magazeti hayo nyumbani mwa watu, ambamo yaweza ‘kusema’ na watu! Mwangalizi mmoja asafiriye alitoa dokezo jingine sahili: “Toa magazeti mkobani mwako wa vitabu.”[15a] Kwa kweli, ikiwa lile usemalo halichochei kupendezwa kwa mwenye nyumba, basi labda picha zenye kuvutia za majalada yayo zitakuangushia magazeti hayo.
20, 21. (a) Waweza kuwaje mwenye kunyumbulika unaposhiriki katika kazi ya magazeti? (b) Waweza kufanya nini ili kuangusha magazeti zaidi kila mwezi?
20 Dokezo la tatu ni kuwa mwenye kunyumbulika. (Linganisha 1 Wakorintho 9:19-23.) Tayarisha utoaji mbalimbali mfupi mchache. Uwe na makala moja akilini ambalo litawavutia wanaume, nyingine wanawake. Kwa vijana, waweza kutumia makala “Vijana Huuliza . . . ” Uwe mwenye kunyumbulika pia, kuhusu wakati unaposhiriki katika kazi ya magazeti. Kuongezea Siku ya Magazeti, huenda ukaona kwamba ushahidi wa jioni hutoa fursa bora zaidi ya kutoa magazeti nyumba kwa nyumba.
21 Dokezo la nne ni kuweka mradi wa kibinafsi. Nyongeza yenye kichwa “Magazeti Yanaonyesha Njia Inayoelekeza Kwenye Uzima,” iliyotokea katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Aprili 1984, ilisema hivi: “Kama dokezo, wahubiri wanaweza kuwa na mradi wa magazeti 10 hivi kila mwezi, ikitegemea hali zao; huenda mapaina wakajitahidi kufikia 90. Bila shaka, wahubiri wengine huenda wakaweza kuangusha magazeti zaidi kwa mwezi na kwa hiyo watajiwekea mradi wa kibinafsi wa juu zaidi. Hata hivyo, kwa sababu ya afya mbaya, aina ya eneo, au sababu nyingine nzuri mradi wa wengine huenda ukawa chini. Lakini bado utumishi wao kwa Yehova ni wenye kustahili. (Mt. 13:23; Luka 21:3, 4) Jambo la maana ni kuwa na mradi wa kibinafsi.”
22. Twaweza kuonyesha katika njia gani kwamba twamshukuru Yehova kwa ajili ya majarida yetu yenye kweli ya wakati ufaao?
22 Twashukuru kama nini kwamba Yehova, “Mungu wa kweli,” ametumia jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili na Baraza Linaloongoza lake kutuandalia majarida hayo ya wakati ufaao! (Zaburi 31:5) Maadamu ni mapenzi ya Yehova, magazeti hayo yataendelea kushughulikia mahitaji halisi ya watu. Yataendelea kuunga mkono viwango vya juu vya kiadili vya Yehova. Havitaacha kuendeleza mafundisho yafaayo. Na yataendelea kuvuta fikira kwenye utimizo wa unabii unaotia alama siku zetu kuwa wakati ambapo Ufalme wa Mungu unatawala na mapenzi ya Mungu yanafanywa duniani kadiri yasivyopata kufanywa wakati mwingine na idadi yenye kuongezeka ya waabudu wa kweli wa Yehova. (Mathayo 6:10; Ufunuo 11:15) Tuna hazina yenye thamani kubwa kama nini katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Acheni tutumie kwa faida yetu kila fursa ya kushiriki pamoja na wale wenye moyo msikivu majarida hayo ya maana yanayoathiri maisha za watu na kutetea kweli za Ufalme.
[Maelezo ya Chini]
a Julai 15, 1992, kurasa 19-22.
b Kwa miaka mingi Mnara wa Mlinzi lilionwa kuwa gazeti ya Wakristo wapakwa hasa. Hata hivyo, kuanzia 1935, mkazo wenye kuongezeka uliwekwa juu ya kutia moyo ule “umati mkubwa,” ambao tumaini lao ni uhai wa milele duniani, upokee na kusoma Mnara wa Mlinzi. (Ufunuo 7:9, NW) Miaka michache baadaye, katika 1940, Mnara wa Mlinzi lilitolewa kwa ukawaida kwa watu barabarani. Baadaye, mwenezo uliongezeka kwa haraka.
Jibu Lako Ni Nini?
◻ Ni nini kionyeshacho kwamba Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ni majarida yenye kweli?
◻ Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yameathirije maisha za watu?
◻ Makutaniko yaweza kufanya nini ili kuongeza ugawaji wa magazeti?
◻ Ni madokezo gani yawezayo kukusaidia kuangusha magazeti zaidi?
[Sanduku katika ukurasa wa 22]
Baadhi ya Makala Ambazo Zimeathiri Maisha za Watu
Kwa muda wa miaka iliyopita wasomaji wengi wameandika kueleza uthamini kwa ajili ya makala hususa zilizochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Chache tu kati ya zile habari nyingi zilizowaathiri wasomaji wetu zimeorodheshwa chini. Je! hizi au makala nyingine zimebadili maisha yako?
Mnara wa Mlinzi
“Kubali Msaada wa Mungu Ili Kushinda Makosa ya Siri” (Aprili 15, 1985, Kiingereza)
“Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee” (Juni 1, 1987)
“Elimu Yenye Kusudi” (Novemba 1, 1992)
Amkeni!
“Waweza Kupiga Vita Dhidi ya Mshuko wa Moyo!” (Septemba 8, 1981, Kiingereza)
“Wakati Mtu Unayependa Anapokufa . . .” (Juni 1986)
“Linda Watoto Wako!” (Oktoba 8, 1993)
[Picha katika ukurasa wa 23]
Katika Kanada—kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kutumia magazeti
[Picha katika ukurasa wa 24]
Katika Myanmari—kutoa magazeti yaelekezayo kwenye njia ya uhai