Je, Wewe Huyasoma Magazeti?
1 Wenzi wa ndoa wamishonari katika Afrika walisema hivi kuhusu magazeti yetu: “Mnara wa Mlinzi hutusaidia tuwe chonjo kiroho katika eneo letu. Sisi hupata kitia-moyo na nguvu kutokana na kila toleo.” Je, wewe wayathamini sana majarida yetu kama wao? Na je, una hamu ya kuyasoma kama wao?
2 Huchukua wakati mwingi kutayarisha makala ziwezazo kusomwa kwa dakika chache tu. Ukijua hilo, je, utasoma makala hizo kijuujuu tu, ukitazama picha, au kusoma makala moja inayovuta uangalifu wako? Tutakuwa na hekima tukifanya mengi zaidi ya hayo. Twapaswa kuchukua wakati kusoma na kuchanganua makala zote katika kila toleo la magazeti yetu. Mnara wa Mlinzi ni jarida letu kuu la chakula cha kiroho cha wakati wake. Amkeni! huwa na makala zenye habari za kupendeza juu ya mambo mbalimbali. Tunayojifunza kwa kusoma magazeti haya kwatuimarisha kiroho na pia kututayarisha tushiriki kwa matokeo zaidi katika huduma. Tukishikilia usomaji wetu sisi wenyewe, tutakuwa wachangamfu kuyatoa magazeti hayo kwa wengine.
3 Jinsi ya Kuboresha Mazoea ya Kusoma: Je, waweza kuboresha usomaji wako wa magazeti? Hapa pana madokezo mawili ambayo husaidia wengi. (1) Panga ratiba ya kawaida ya usomaji. Kwa kuweka kando tu dakika 10 au 15 kila siku ili kusoma, utashangaa kadiri uwezavyo kusoma kwa juma moja. (2) Tumia utaratibu fulani wa kukusaidia kukumbuka yale ambayo umesoma. Labda waweza kutia alama mwanzoni mwa kila makala unayosoma. Bila hiyo, unaweza kukosa kusoma makala au hata gazeti lote. Ni jambo la maana kuwa na kawaida inayokufaa na kuishikilia.—Linganisha Wafilipi 3:16.
4 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameitikia kwa hekima nyakati zibadilikazo kwa kuchapisha makala ambazo hushughulika na mahitaji halisi ya watu. (Mt. 24:45) Kwa kweli, magazeti haya yameathiri maisha zetu. Kwa kiwango kikubwa, mwendo wa hali yetu ya kiroho wategemea ubora wa mazoea yetu ya kusoma ya kitheokrasi. Baraka nyingi za kiroho ziko akibani kwa wale wanaokomboa wakati wa kusoma magazeti yote.