Waangalizi Wanaoongoza—Mwandishi
1 Mwandishi wa kutaniko hutimiza fungu muhimu katika kuhakikisha kwamba ‘mambo yote yanatukia kwa adabu na kwa mpango.’ (1 Kor. 14:40) Akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, yeye hushughulikia mawasiliano na rekodi za maana za kutaniko. Ijapokuwa huenda wajibu wake mbalimbali usionekane na kila mtu kama ule wa wazee wale wengine, utumishi wake wahitajiwa sana na kuthaminiwa sana.
2 Barua ipokewapo kutoka kwa Sosaiti au kwa wengine, mwandishi huishughulikia na kuhakikisha kwamba yajibiwa inapohitajika. Yeye huhakikisha kwamba barua zinazopokewa zapitishwa miongoni mwa wazee kisha aziweka kwenye faili kwa ajili ya marejezeo. Huangalia fomu za maagizo ya magazeti na fasihi na kuzipelekea Sosaiti. Yeye husimamia moja kwa moja wale wanaoshughulikia hesabu na maandikisho na vilevile mambo yanayohusiana na kusanyiko.
3 Kwa kuwa lazima mwandishi apeleke ripoti ya kutaniko ya utumishi wa shambani ya kila mwezi kwa Sosaiti kufikia tarehe sita ya mwezi, yatulazimu sisi sote tutoe ripoti ya utendaji wetu wa shambani bila kukawia mwishoni mwa mwezi. Kisha hujaza ripoti za utumishi kwenye kadi za Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Mhubiri yeyote anaweza kuomba aone rekodi yake ya kibinafsi ya utendaji.
4 Mhubiri anapohamia kutanikoni au kulihama, mwandishi huomba au kupelekea wazee wa kutaniko lile jingine barua ya kumjulisha pamoja na kadi zake za Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri.—Huduma Yetu, uku. 104-105.
5 Mwandishi hupitia utendaji wa mapainia, akiwajulisha wazee, na hasa mwangalizi wa utumishi, matatizo yoyote ambayo huenda ikawa mapainia wanapatwa nayo. Yeye hujulisha viongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko wahubiri ambao si wa kawaida katika utumishi wa shambani. Mwandishi na vilevile mwangalizi wa utumishi huchukua uongozi katika kusimamia jitihada za kutunza wasiotenda.—Huduma ya Ufalme Yetu, Novemba 1987, uku. 1.
6 Tukiwa na uthamini unaofaa wa wajibu mbalimbali wa mwandishi, na tufanye yale tuwezayo kusaidia usimamizi wake uwe rahisi kwake kuutimiza.—1 Kor. 4:2.