Kuwapata Wenye Kupendezwa Kupitia Kutoa Ushahidi wa Barabarani Wenye Matokeo
1 Yesu aliagiza wanafunzi wake watafute wale waliostahili kusikia zile habari njema za Ufalme. (Mt. 10:11) Lakini, katika maeneo mengi leo, inakuwa vigumu zaidi na zaidi kuwapata watu nyumbani mwao. Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kufanywa ili kuwafikia wenye kustahili ambao huenda wakakosekana?
2 Ushahidi wa barabarani waweza kuwa njia yenye matokeo ya kuwapata watu wanaokosekana katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Twaweza kutoa ushahidi wa barabarani kwenye vituo vya basi, karibu na majengo yenye ulinzi mkali, katika bustani za umma, na mahali kwingineko ambako watu hujihusisha na shughuli za kila siku.
3 Ushahidi wa barabarani unapotajwa, watu fulani wana hisi za wasiwasi. Huenda wakasitasita kushiriki mahubiri hayo kwa sababu wanaelekea kuona haya au wanaogopa kuchambuliwa na watu wanaokataa ujumbe wa Ufalme. Mahangaiko haya kwa kawaida si ya msingi ufaao. Wale ambao wana ujuzi wa utendaji huu waripoti kwamba si mgumu kuliko ushahidi wa mlango kwa mlango. Kwa kweli, wameona kwamba watu walio wengi wanazoea kufikiwa barabarani kwa sababu mbalimbali, na watu fulani huenda wakawa na mwelekeo wa kuzungumza au kusikiliza kuliko vile wangekuwa ikiwa tungebisha mlango wao. Kwa hiyo ‘tukijipa ujasiri,’ tunaweza kupata matokeo yenye kupendeza sana.—1 The. 2:2, NW.
4 Mahubiri ya barabarani yaweza kufanywaje kwa matokeo zaidi? Ni muhimu kujitayarisha vema. Soma magazeti mapema, na uchague jambo moja au mawili ya kuzungumza ambayo wahisi yatapendeza watu unaokutana nao. Utoaji wa sekunde 30 wafaa. Kwa kuwa lengo ni kuonana na wengine kibinafsi, chagua mahali ambapo watu wengi hupitia kwa ukawaida. Ijapokuwa huenda ikafaa kuwa na mhubiri mwingine karibu nawe, kwa kawaida ni vema kuwa mbalimbali. Wahubiri wanaosimama pamoja huenda wakaelekea kutumia wakati wakiongea pamoja nao wasitoe uangalifu kwa wale wa umma ambao huenda wakawa na mwelekeo wa kusikiliza ujumbe wa Ufalme.
5 Kusimama mahali pamoja na kuonyesha magazeti tu hakuna matokeo kama vile kuchukua hatua ya kuwafikia watu mmoja-mmoja. Jaribu kusitawisha uwasiliano wa macho. Uwe mchangamfu, mwenye urafiki, na mwenye mfikio wa moja kwa moja unapojitahidi kuanzisha mazungumzo. Katika visa vingine, huenda ukahitaji kutembea hatua chache na mtu huyo unapoongea naye. Akikubali, mtolee magazeti. Magazeti yakikataliwa, unaweza kutoa trakti.
6 Kwa kawaida inafaa kutayarisha utoaji mfupi ambao hutokeza swali au elezo litakaloamsha kupendezwa. Ikiwa kuna itikio lenye kupendeza, jaribu kupata jina la mtu huyo, anwani yake, na labda hata nambari yake ya simu ili uweze kufuatia kupendezwa huko. Unaweza kusema: “Ikiwa utapenda kujifunza mengi, nitafurahi kukutembelea nyumbani mwako au kupanga Shahidi mwingine afanye hivyo.”
7 Mzee mmoja aliyekuwa akitoa ushahidi wa barabarani alimfikia mwanamke naye akapata kujua kwamba hakuwa amepata kamwe pindi ya kuongea na Mashahidi nyumbani mwake. Alikubali kitabu na akaridhia dada amtembelee nyumbani mwake kwa wakati unaofaa. Wengi wenye kustahili wanaweza kupatikana kwa hakika na wasaidiwe tukiwa wenye matokeo katika ushahidi wa barabarani.—Mdo. 17:17.