Wasaidie kwa Upendo Wale Wanaoonyesha Kupendezwa
1 Mwanafunzi Filipo alipoelekezwa na malaika wa Yehova kwa Mwethiopia aliyeonyesha kupendezwa halisi kwa Neno la Mungu la kweli, alijitolea kwa upendo kumsaidia aelewe alichokuwa akisoma. (Mdo. 8:26-39) Je, sisi hufanya jitihada za pekee kusaidia watu wanaoonyesha kupendezwa? Twapaswa kufanya hivyo, kwa kuwa agizo letu la kimungu latia ndani kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Twaweza kufanya nini ili tuwasaidie?
2 Weka kando wakati kila juma wa kufanya ziara za kurudia. Panga kuwarudia wale walioonyesha kupendezwa, na ujaribu kurudia mazungumzo ya Kimaandiko uliyoanzisha katika ziara yako ya kwanza. Weka akilini mradi wa kuanzisha funzo la Biblia. Rudi kwa ukawaida ili umtolee matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
3 Ikiwa uliongea juu ya thamani ya Biblia katika ziara yako ya kwanza, unaweza kurudia mazungumzo, ukitumia dokezo lililo kwenye kurasa 47-8 za kitabu “Kutoa Sababu” na kusema jambo kama hili:
◼ “Watu fulani huhisi kwamba ushauri wa Biblia hauna mafaa kwa ulimwengu wetu wa siku hizi. Wewe wahisije kuhusu hilo? [Ruhusu itikio.] Je, hutakubali kwamba kitabu kinachotoa shauri linalofaa linalotuwezesha kuwa na familia zenye furaha ni chenye kutumika? [Ruhusu itikio.] Maelezo na mazoea yanayohusu maisha ya familia yamebadilika, na matokeo tunayoona leo si mazuri. Lakini familia zinazotumia yale ambayo Biblia husema ziko imara na ni zenye furaha.” Soma Wakolosai 3:18-21. Toa trakti Sababu kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia, na ueleze kwamba sisi hutoa programu ya funzo la Biblia bila malipo.
4 Unaweza kuanzisha mazungumzo juu ya hali ya wafu kwa njia hii:
◼ “Kumekuwa na mazungumzo mengi juu ya hali ya wafu. Unafikiri ni nini hutokea tunapokufa? [Ruhusu itikio.] Dini zilizo nyingi hufundisha kwamba tunaendelea kuishi katika namna nyingine. Wengi wameshangaa kujifunza yale ambayo Biblia inasema juu ya jambo hilo. [Soma Mhubiri 9:5.] Ijapokuwa wafu hawako hai, hawajasahaulika. Mungu ameahidi kuwarudisha kwenye uhai chini ya utawala wa Ufalme wake.” Fungua ukurasa 162 katika kitabu Kuishi Milele, na uzungumzie maandiko na vielezi hivyo. Pangia ziara nyingine ya kurudi, ukiwa na lengo la kuanzisha funzo la Biblia.
5 Ikiwa unataka kutoa maelezo zaidi juu ya maoni ya Kikristo juu ya vita miongoni mwa mataifa, unaweza kusema jambo kama hili:
◼ “Watu fulani wanaamini kwamba kupigana ndiyo njia tu ya kutatua ugomvi. Wewe wahisije kuhusu hilo? [Ruhusu itikio.] Biblia huonyesha kwamba Mungu anataka watu waishi pamoja kwa amani. [Soma Warumi 12:17, 18.] Hilo litakuwa jambo halisi ulimwenguni pote chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.” Rejezea kwenye broshua Je! Kweli Mungu Anatujali?, kurasa 25-6. Jitolee kurudi ili ueleze ni kwa nini Yesu alitufundisha kusali ‘mapenzi ya Mungu yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni.’—Mt. 6:10.
6 Yule towashi Mwethiopia alitambua kutoweza kwake kuelewa bila mtu wa kumwongoza. (Mdo. 8:31) Filipo kwa upendo alimpa msaada uliohitajiwa. Sisi twaweza kuonyesha upendo wetu wa kweli kwa wengine kwa kuwasaidia kwa njia hiyohiyo.